Search This Blog

Wednesday, November 18, 2020

DAPHINE SEHEMU YA 2/10

 

 


DAPHINE
MTUNZI….EMMANUEL F.KWAY(THE STORY MASTER)
AGE…(18+)
Watchstrap…+255718 862176
SEHEMU YA 2 KATI YA 10

 


“Kama nilivyokwambia Mwanangu inabidi uende jeshini kama ulivyoambiwa mimi nina amini yupo sahihi kabisa”

Kila walipojaribu kumuimbisha Daphine kuhusu swala la kwenda jeshini alikatakaa katakata,Mr.Vital Kamere alikasirishwa ndiyo maana akaamua kuwashirikisha Hans na Beatrice ili waingilie kati.Siku zote waliamini mzee huyu tajiri yupo sahihi mbali na hapo alikuwa ni msaada mkubwa sana kwao,kukataa matakwa yake kulimaanisha kumkosea adabu ndiyo maana walimuunga mkono hata bila kuhoji ni kwanini alitoa maamuzi hayo ya kutaka Daphine aende jeshini tena nchini Urusi.

“Mimi siwezi nataka kusoma form five Mama”

Daphine bado alikazia msimamo wake.

“Sawa utaendelea na masomo ukirudi,nakuomba mwanangu.Kumbuka huyu ndiye aliyekusaidia umesahau!”

“Hata kama Mama,mimi sipendi kuwa mwanajeshi”

“Daphine tafadhali,wazazi wako tumefunga safari kutokea Morogoro kisa wewe,Kamere amekasirika sana”

“Mama”

“Abee mwanangu”

“Kwahiyo nikirudi nitaendelea na kidato cha tano?”

“Kabisa,hilo ondoa shaka”

“Sawa nimekubali”

“Naomba pia ukubali kwa moyo mmoja Daphine”

“Usijali Mama”

Taarifa za kukubali kwa Daphine kwenda jeshini alivyofikishiwa Mr.Vital Kamere alizipokea kwa furaha sana na kwa kuwa Hans na Beatrice walikuwa wafanyakazi wake siku hiyohiyo aliwapandisha vyeo mishahara yao ikaongezeka,moyo wa Vital Kamere ulifurahi na mara moja akaanza mipango ya safari,ilielekea aliyekuwa akisubiriwa ni Daphine akubali .Ndani ya siku saba viza ya Daphine ilikuwa tayari imetoka na taratibu za safari ndiyo zilikuwa zinapangwa.

“Daphine”

“Yes Dad”

Alimuita hivyo ingawa hakuwa baba yake,Mr.Vital Kamere ndiye alipenda aitwe hivyo.

“Utaanza safari wiki ijayo,upo tayari?”

“Ndio,kwani hatuendi wote?”

Daphine aliuliza huku akiwa mwenye wasiwasi usoni.

“Hapana mimi nina shughuli nyingi lakini usijali kuna watanzania wenzako wengine watakupokea”

“Dad,nimekuzoea sana”

“Usijali Daphine,mimi nipo nitakuwa nakuja kukusalimia”

Ilikuwa ni vigumu sana kwa swala hilo kumuingia Daphine akilini lakini hakuwa na jinsi ilikuwa ni lazima afuate aliyoambiwa ingawa moyo wake ulikuwa mzito,katika vitu ambavyo alivichukia na katika maisha yake hakuwahi kuvifikiria ni swala la kwenda jeshini alichukia jeshini sababu alijua nini maana yake,alielewa ni mateso gani ataenda kukumbana nayo mbeleni akiwa depo.

Mr.Vital Kamere ndiye aliyemsaidia na kumsomesha hivyo aliapia kuwa hatomuangusha.

“Sikuwahi kukuangusha Dad hata darasani,na huko jeshini sitokuangusha pia”

“Nashukuru kusikia hivyo”

“Ahsante kwa kila kitu”

Kila kitu kilikuwa nyuma ya pazia hakuelewa ndani ya moyo wa Mr.Vital Kamere kuna kitu gani.Kutokana na jinsi alivyosaidiwa na alivyopendwa hakuwa na sababu yoyote ya kuhoji maswali akiamini kuwa hiyo itamfanya Mr.Vital Kamere akasirike pengine asitishe huduma zake.

***

Hakuna siku ambayo Daphine alimwaga machozi kama siku hiyo ya Alhamisi saa tatu ya usiku uwanja wa kimataifa Mwl.Julius Nyerere.Macho yake yalikuwa mekundu kwa kulia na yalivimba mno,hakupenda safari hiyo lakini ilibidi awaridhishe wazazi wake,Mr.Vital Kamere,Hans pamoja na Beatrice walim-bembeleza Daphine bila mafanikio!

“Usilie mwanangu,sisi wazazi wako utatukuta”

“Ma…ma Ba..ba nina..wapenda sa..ana sijazoea kukaa mbali nanyinyi Da..d”

Daphine alilia kwa kwikwi mpaka baadhi ya wasafiri wakaanza kuwatizama,machozi yalimbubujika kupita kiasi ingawa alipewa moyo lakini wapi, ilikuwa ndiyo kama wanamchochea.Kilichowashtua ni kipaza sauti kuwa ndege tayari imetuwa na abiria walitakiwa kuanza kujiandaa.

“South African Airways hiyo,Daphine safari njema mwanangu.Ukifika Tambo international Airport utaona kibao kimeandikwa jina lako.Kama nilivyokupa maelekezo”

Mr.Vital Kamere aliongea na kumuangalia Daphine ambaye bado alikuwa akilia machozi ya kwikwi,ilikuwa ni ngumu sana kwake kuamini anawaacha wazazi wake na nchi ya Tanzania anayoipenda na kwenda ugenini tena jeshini,jambo ambalo wakati wote alitamani liwe ndoto,ashtuke!


Aliweka begi dogo mgongoni vizuri na jingine kubwa akaanza kuliburuza kuelekea langoni ambapo aliungana na abiria wengine,akageuka nyuma,akawapungia mikono huku bado machozi yakimchuruzika mashavuni,mpaka alipoingia ndani na kuonesha tiketi pamoja na passport yake.

“Pita”

Alivyoruhusiwa akaingia ndani ya chumba cha ukaguzi ambacho abiria ndiyo waliruhusiwa kuingia tu,ukaguzi ukaendelea akavua kila kitu cha chuma na kupita chini ya kimlango kidogo ambapo mbele alichukuwa mabegi yake na kuzidi kufuata taratibu zote,ndani ya dakika ishirini kila kitu kilikuwa sawa.Akakaa chini ya geti namba kumi na nane ili asubiri taratibu nyingine,ingawa ilikuwa ni mara yake ya pili kusafiri ama kupanda ndege alijitahidi kukariri,alihofia kupotea sababu alikuwa peke yake.

“Abiria wa South African Airways namba 206K ndege ipo tayari hivyo mnaombwa muingie ndani kwa ajili ya safari”

Ilisikika sauti nyororo kutokea kwenye spika ikijirudia kwa lugha tofauti tofauti,Daphine akatizama tiketi yake kama ndiyo yenyewe,akaweka begi lake mgongoni vizuri akaungana na abiria wenzake na kupita kwenye geti ambalo tayari lilikuwa wazi.

Vitu vingi vilipita ndani ya akili yake alitafakari mambo mengi hususani maisha mapya atakayoenda kuanza,habari za jeshi alizijua na alielewa ni jinsi gani ataenda kuteseka akiwa mafunzoni mbali na hapo hakuelewa kwanini Mr.Vital Kamere alifanya uamuzi huo wa kumpeleka jeshini.

Aliingia ndani ya ndege na kuanza kutafuta kiti alichopangiwa,alivyopata siti yake akaketi na kujitupa kwenye mawazo.Alichukuwa muda mfupi kutafakari maisha yake yaliyopita,akakumbuka jinsi alivyowagonganisha wanaume,alikumbuka maisha yake alivyokuwa akiishi maisha ya kuteseka na baadaye akataka kufungwa kwa kosa la kusingiziwa kuuwa,akatokea Mr.Vital Kamere kumsaidia.Vitu vingi vilimiminika kichwani mwake akawa kama anatizama mkanda wa kusisimua.Hakuelewa maisha yake yangekuwaje kama asingetokea Mzee Kamere kuyakomboa.Taratibu akafunga mkanda baada ya maelekezo kutolewa na baada ya dakika tano ndege ilianza kutembea huku maelekezo ya hapa na pale yakitolewa,Daphine alikuwa mbali kifikra lakini mwili wake ulikuwepo,bila kutegemea alihisi mashavu yake yanalowana.Hakuelewa ni kwa wakati gani machozi yalianza kumtoka,moyo wake bado ulimuuma kupita kiasi kwenda mbali na alipopazoea.

“Dada mbona unalia?”

Ilikuwa ni sauti iliyomshtua kutoka pembeni yake lakini hakujibu badala yake alitoa kitambaa na kujifuta machozi.

****

“KARIBU SANA DAPHINE HANS”

Hicho ndicho kibao kilichokuwa kinamtizama Daphine aliyekuwa anatokeza nje ya lango.Mwanamke aliyevalia koti jeusi, mrefu kiasi ndiye aliyekuwa ameshika bango hilo kama alama ya kumpokea mgeni wake.Hapohapo akashikwa bega.

“Mimi ndiyo Daphine Hans”

Daphine akasema.

“Karibu sana,mimi naitwa Asha”

“Nashukuru kukufahamu”

“Mimi pia,tafadhali nifuate”

Asha na Daphine waliongozana,mpaka upande wa pili ambapo huko utaratibu mwingine ulianza wa kukata tiketi.

“wewe ni Mtanzania pia?”

Lilikuwa ni swali lililoulizwa na Daphine.

“Ndio”

“sasa hivi tunaelekea wapi?”

“Urusi”

“Nawewe pia unaenda?”

Lilikuwa ni swali lingine kutoka kwa Daphine na ilionekana Asha hakupendezwa na maswali ndiyo maana hakujibu tena akabaki kimnya.Kwa jinsi alivyotembea Asha ilionekana alikuwa ni mtu wa mazoezi mbali na hapo mwili wake ulikuwa umekomaa kiasi,tiketi zilikuwa zimekatwa tayari mbili kumaanisha kuwa wote walitakiwa wasafiri.

Yalikuwa yamebaki masaa mawili ili wapande ndege nyingine ya shirika la urusi ambayo itakayowapeleka jijini Moscow.Wakiwa wanasubiri ndege,simu ya Asha ikaita.Akaitoa kutoka ndani ya koti lake kubwa.

“Halloo”

“Unaongea na Vital Kamere,usitaje jina langu.Upo na Daphine?Jibu ndio au hapana”

“Ndio”

Daphine ingawa alikuwa pembeni ya simu lakini hakuelewa ni nani aliyepiga simu hiyo,Asha hakutaka kuweka swala hilo wazi sababu alifuata maelekezo.

“Sasa nisikilize,fanya kama nilivyokwambia mkifika Moscow usipoteze muda,mambo yanatakiwa yaende harakaharaka”

“Sawa”

“Ukifika Moscow nipigie simu”

“Okay”

“Safari njema”

Asha alikata simu na kumtizama Daphine aliyekuwa pembeni yake,alimsikitikia sana msichana huyu mdogo kwa mambo aliyoambiwa amfanyie na Vital KAMERE!



Bado moyo wake ulikuwa ukidunda kupita kiasi,Daphine alikuwa mwenye wasiwasi muda wote, aliliogopa swala la jeshi,alielewa nini maana yake kwamba mafunzo ya jeshi hayakuwa lelemama yaliihitaji uvumilivu wa hali ya juu sana.Katika maisha yake hakuwahi hata kuota kama atakuja kuwa mwanajeshi sababu alichukia,alikuwa na mawazo chungumzima kichwani mwake kama ingekuwa ni hiyari yake basi angekataa katukatu.Bado walikuwa uwanja wa ndege wanasubiri ndege itakayowapeleka moja kwa moja nchini Urusi wakitokea Afrika kusini.Walisubiri kwa takribani masaa mawili ndipo walisikia kipaza sauti.

“Simama twende”

Ilikuwa ni kauli ya kibabe na yenye amri iliyosindikizwa na ukali,Daphine akazidi kuingiwa na hofu akainuka wakaongozana mpaka kwenye lango kubwa la abiria wanaosafiri,taratibu za ukaguzi zikaanza hapohapo.Dakika arobaini baadaye wote walikuwa ndani ya ndege kubwa wakisubiri safari ambayo ingewachukuwa masaa mengi sana angani.Daphine hakuacha kuwaza hakuelewa nini mwisho wa maisha yake baada ya kutoka jeshini.Alipenda kuwa mwanasayansi mkubwa duniani lakini aliona kama ndoto zake zinaenda kuzimika.

“Tutafika saa ngapi?”

Lilikuwa ni swali kutoka kwa Daphine huku akimwangalia Asha usoni.Lakini hakujibiwa Asha alimtizama na kugeuza shingo yake dirishani.Taratibu ndege ikaanza kujigeuza na kukaa sawa kwenye barabara yake na kuanza kuserereka adoado,kila ilipozidi kwenda ndipo ilipozidi kuchanganya mwendo mpaka ilipofika kwenye barabara yake ya kuruka,hapo ikasimama ili kusubiri ndege nyingi ziruke.Marubani walikuwa makini na waliendelea kufanya mawasiliano makao makuu,hatimaye ndege ikaruhusiwa kuingia kwenye barabara yake,ikaanza kutembea kwa kasi ya risasi huku injini zikizidi kupiga kelele sana,ikaanza kuinuka kwa mbele kisha matairi mengine taratibu yakafuatia na kupaa angani,ikazidi kwenda juu zaidi mpaka kuingia katikati ya mawingu hapo ilikaa sawa na abiria wakaruhusiwa kufungua mikanda yao.

***

“Kuna mtu alinipigia simu majuzi,sijui hii namba kaipata wapi.Naomba ufuatilie ujue ni nani”

“Alafu tufanye nini Mh.Raisi?”

“Nitawaambia cha kufanya mkimpata,alinipigia simu sijui ni kwanini watu wanakuwa hivi nataka awe wa mfano”

“Sawa Mh.Raisi”

Raisi Leslie Benjamin alikuwa katika mazungumzo mazito na msaidizi wake siku hiyo wakiwa ofisini wawili,alitaka mtu aliyempigia simu na kumtisha awekwe chini ya ulinzi mara moja hicho ndicho kitu kilichoenda kufanyika.

“Mugolozi”

Raisi Leslie alimuita Mfanyakazi wake kabla ya kutoka mlangoni.

“Naam”

“Mtafute Mr.Ndomba ndiyo itakuwa raisi kumpata huyo kijana.Mkabidhi tu namba za simu yeye atajua ni wapi pa kuanzia”

“Okay”

Harakati za kumsaka Ngesa zilianza dakika hiyohiyo.Mr Mugolozi alivyoingia ndani ya ofisi yake akainua mkonga wa simu na kubonyeza namba fulanifulani simu ya upande wa pili ikaanza kusikika ikiita.

“Unaongea na Mugolozi Baitani kutoka Ikulu,habari za wakati huu Mr.Ndomba”

Mugolozi alianza kujitambulisha.

“Ndio muheshimwa,habari za majukumu ya ujenzi wa taifa?”

“Nzuri tu,sasa sitaki kupoteza muda.Kuna namba nitakupa naomba ufanye kama ulivyofanya mara ya mwisho”

“Hilo halina shaka,nipe namba”

“0750 322432”

“Okay ndani ya dakika ishirini nitakupa jibu”

Mr.Ndomba alitegemewa katika mitandao yote katika maswala ya I.T.Kijana huyu mdogo mwenye umri wa miaka ishirini na mbili aliweza kujizolea umaarufu na kugombaniwa na karibia mitandao yote ya simu kama IMACOM,TIGO,HAJREYMER,M&KCOM wote walipanda dau ili kumtaka kwa pesa ndefu,kichwa chake kilitisha sio utani,hakuna kitu chochote kilichomshinda kuhusu kompyuta, aliweza kuichambua yote kama aliitengeneza yeye.

Mbali na kufanya kazi mitandaoni hata serikali ilimtafuta ili kutatua mambo yao mbalimbali kama kutafuta wahalifu kisiri.Na siku hiyo alipewa kazi nyingine na Mugolozi Baitani,haraka akaingia kwenye kompyuta yake akaifungua na kuingiza namba za simu.Ndani ya dakika mbili akawa kapata jibu kamili.Akainua mkonga wa simu ili kutoa jibu.

“Hallo,jina lake anaitwa Derick Ngesa,anaishi Arusha Sakina nyumba namba kumi na tisa”

“Sawa Ahsante”

“Karibu tena”

Kazi ya kumsaka Ngesa ikaanza mara moja,shushushu walimwagwa Arusha siku hiyo hiyo na walifanikiwa kuijuwa nyumba ya tajiri yake,Jimmy Magembe.Kwa maana hiyo walipaki magari yao nje ya geti wakimsubiri Ngesa wamuweke chini ya Ulinzi wakiwa na picha yake mikononi mwao.

“Sindo yule pale”

Mmoja wa wapelelezi kutoka usalama wa taifa alimuuliza mwenzake,akiwa kama hana uhakika.

“Embu subiri”

Mwingine akajibu huku akitizama picha iliyokuwa mkononi mwake.

“Ndiyo mwenyewe”

Kutokana na Nissan Patrol aliyokuwa anaendesha Ngesa kuwa na vioo vyeusi ilifanya sura yake ionekane akiwa nyuma ya usukani anaendesha gari hana wasiwasi analitoa nje ya geti.Wapelelezi wakashuka na kusimama mbele ya gari.

“Habari za wakati huu?”

Mmoja wa wapelelezi alitoa salamu huku akigonga kioo cha gari,Ngesa akateremsha ili kumsikiliza.

“Nzuri tu”

“Unaweza ukaongozana na sisi?”

“Hapana siwezi nina kazi nyingi”

Ngesa alijibu na kuweka gia akitaka kuliondosha gari.

“Acha kujibu jeuri.Upo chini ya ulinzi shuka ndani ya gari tuongozane”

Ilikuwa ni kauli iliyomfanya Ngesa awatizame watu hawa watano waliokuwa wamezingira gari wanaongea kwa kujiamini.

“Kwa kosa gani?”

“Ebwana weka gari ndani au tuongozane usifanye mambo yawe magumu.Turahisishe zoezi”

“Mnanipeleka wapi?”

Kilichowafanya wapelelezi wageuke ni baada ya geti kubwa kufunguliwa,akatokeza mzee aliyevaa suti nyeusi kanyonga tai kohoni.

“Kuna nini hapa?”

Ndani ya dakika moja kila mtu alijitambulisha na kuhitimisha kuwa Ngesa yupo chini ya ulinzi.

“Huyu ni kijana wangu,amefanya kosa gani?”

“Hatuwezi kuongea hapa.Yupo chini ya ulinzi”

“Sawa,naomba niongee na mkuu wenu”

“Mzee hatuna huo muda,naomba utuelewe”

Wapelelezi hawakuelewa somo,walichoagizwa ni kumtia Ngesa mikononi mwao kisha wamuweke chini ya Ulinzi.Hicho ndicho kilichotokea, hapohapo wakamtoa ndani ya gari na kumuweka chini ya ulinzi na kuingia naye ndani ya gari.

***

Meli kubwa iliyobeba mizigo ilikuwa inatokea Dubai kupitia bahari ya Hindi,ilibeba makontena mia nane.Ilitembea baharini kwa takribani siku nane kutokana na kusimama na kutia nanga nchi nyingi tofauti tofauti.Wafanyabiashara mbalimbali waliagiza mali zao kama magari na vifaa vingi kutokea nchi za ughaibuni.Miongoni mwa wafanyabiashara walioagiza magari ni mfanyabiashara tajiri Mr.Vital Kamere alitumia magari kama mwavuli wa kubebea mabomu hatari ya Nuclear,aliungana mkono na Brigedia Karanje.

Siku hiyo usiku ilikuwa inasubiriwa kwa hamu kubwa kupita kiasi,ilikuwa ni lazima mabomu hayo yapitishwe bandari ya posta kimagendo.Haikuwa kazi rahisi kufanya hivyo kutokana na ukaguzi uliokuwepo.Swala hilo ndilo lilimuumiza sana akili Brigedia Karanje,kukamatwa kwa silaha zake kulimaanisha mipango yake kukwama,hakutaka kuruhusu jambo hilo litokee kamwe ndio maana aliumiza kichwa chake mchana na usiku bila kulala.

Siku iliyofuata asubuhi na mapema alichukuwa simu yake na kuanza mazungumzo na Mr.Kamongo mkaguzi mkuu wa bandari.

“Unaongea na Brigedia Karanje”

Ilikuwa ni sauti nzito ya kukwaruza tena bila ya kujuliana hali,Kamongo alimfahamu mwanajeshi huyo na habari zake za kutisha alizijua pia.

“Ndio mkuu habari za asubuhi”

“Kuna mizigo ya jeshi itaingia leo usiku saa tano nitakuja mwenyewe kuichukuwa sitotaka kupotezewa muda”

“Lakini mkuu kuna utaratibu wa…”

“Nimekwambia sitotaka kupotezewa muda,umenielewa?”

Brigedia Karanje akachimba mkwara.

“Sawa hakuna shida”

“Vizuri”

Zoezi la kuongea na simu lilivyokamilika,akabonyeza namba nyingine na kuiweka simu sikioni tena.

“Mwanguku”

“Naam mkuu”

“Ikifika saa nne usiku nataka uzime umeme jiji zima la Dar es salaam”

“Leo?”

“Ndio…Zima umeme”

“Sawa mkuu”

Mipango tayari ilisukwa na TANESCO walijuwa hizo ni taratibu za jeshi pindi wanapoingiza silaha za moto,ilitakiwa jiji zima la Dar es salaam umeme uzimwe.

***

Ni kweli saa nne ya usiku juu ya alama ilivyotimia umeme ukazimwa, jiji zima likawa giza,Ngesa alikuwa yupo kituo cha Polisi Msimbazi ‘centre’ nyuma ya nondo akiwa chini ya ulinzi mkali bila kujua nini kosa lake.Akili yake ilimtuma ajiokoe na kujitoa maabusu kwa njia moja ama nyingine,lakini jinsi alivyothibitiwa haikuwa rahisi kujinasua hata kidogo,kuna vitu vilivyokuwa vinaendelea chini kwa chini alivisikia japokuwa hakutaka kuyapa mawazo yake kipaumbele.


******

“Unamfahamu huyu?”

“Ndio!ni raisi wangu.Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh.Leslie Benjamin”

“Umejibu vizuri”

“Tazama hizi picha”

Ilikuwa ndani ya chumba kidogo kilichofananishwa na selo, pembeni kulikuwa kuna silaha nzito za moto tena za kutisha.Daphine alitandwa na hofu sababu mambo kama hayo hakuwahi kuyaona katika maisha yake.

“Tazama hizi picha”

Daphine alizinduliwa baada ya kuonekana na uwoga wa kukagua chumba kilichokuwa na mitutu,alivyoangalia mezani aliona picha za maiti, wanaume kwa wanawake walikuwa wamekatwakatwa vibaya sana,matumbo yao yalikuwa wazi na wengine walikuwa wamepigwa risasi.Ilikuwa ni picha mbaya sana kwa Daphine ambaye bado alikuwa mdogo kutizama mambo ya kinyama kama hayo,bado hakuelewa ni kwanini anaoneshwa vitu kama hivyo.

“Hapa ni Tanzania,kagera. Mwaka 1991 hawa ni watanzania wenzako”

“Kwanini?Ilikuwaje?nani alifanya hivi?”

Daphine aliuliza maswali ya mfululizo akionesha sura ya ukali kidogo,iliyochanganyika na hasira ndani yake.

“Raisi wako ndiyo kafanya haya,Raisi Leslie Benjamin ndiyo alifanya huu unyama”

Maneno hayo yalimfanya Daphine amtizame Asha machoni.




Bado haikumuingia akilini kuwa Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Mh.Leslie Benjamin kwamba angeweza kufanya ukatili kama huo,juu ya picha alizidi kuona ukatili wa kinyama kupita kiasi.Kumbukumbu zake zikarudi nyuma kwa kasi ya mwewe akamuona jinsi Raisi Leslie alivyowapokea ikulu wakala naye chakula na kupiga picha mbalimbali hiyo ilitosha kabisa kudhihirisha kuwa Raisi wake hakuwa mtu mbaya.

“Raisi Leslie ndiyo kafanya hivi?Kwanini?”

Lilikuwa ni swali lingine kutoka kwa Daphine huku akichukuwa moja ya picha zilizokuwa mezani,akatizama maiti zilizochanwachanwa vibaya sana.Akazidi kuchukuwa picha nyingine akaona wakina mama walivyofumuliwa matumbo yao na risasi.

“Najua mpaka sasa hivi hauamini lakini ndiyo hivyo,huo ndiyo ukweli halisi”

“Kwanini asishikiliwe au kushtakiwa?”

“Ndiyo maana tupo hapa”

“Kivipi?”

“Ipo siku utaelewa”

Kichwa cha Daphine kilijaa msongo wa mawazo,alimfikiria Raisi wake na bado hakuamini kama ndiye yeye alifanya unyama alioambiwa na Asha,akiwa katika bahari ya mawazo mlango wa chumba walichokuwepo ungafunguliwa.Akaingia mwanaume mrefu mwenye misuli mingi kiunoni ana bastola.

“Twendeni”

Kauli hiyo ilimfanya Asha asimame pamoja na Daphine wote wakatoka nje,siku nzima waliitumia kumuonesha Daphine mazingira ya kambi,ilikuwa ni kambi yenye eneo kubwa iliyokuwa katika jiji la Moscow katikati ya visiwa vya Bahamas,hakuna mtu aliyefahamu nini kinaendelea ndani ya kisiwa hicho ilikuwa ni siri kubwa sana.

Mazoezi yalikuwa yakiendelea chini kwa chini ili baadaye nchi ya Tanzania ije kupinduliwa kimabavu,kutokana na maneno ya chuki waliyokuwa wakipewa na kupandikizwa kila mtu alimchukia Rais Leslie Benjamin,nchi ya Tanzania haikupaniwa kupinduliwa peke yake bali Raisi Leslie Benjamin atekwe nyara auliwe.Ndiyo maana mazoezi yalitolewa usiku na machana,kwa maana hiyo lilihitajika jeshi kakamavu.Hata Daphine alivyofika hakupewa nafasi ya kupumzika siku hiyo hiyo aliingia mazoezini akikimbia mchakamchaka umbali wa kama kilomita tano kwenda na kurudi,alichoka kupita kiasi.Kilichomfanya azoee mazingira ni kwasababu wengi wao walikuwa watanzania wenzake hiyo ilimfanya ajisikie yupo nyumbani ingawa alikuwa nchini Urusi.

“Wake up,wake up!”

Saa tisa za usiku ndoo za maji zilimwagwa kwenye kila kitanda,Daphine alikurupuka baada ya kumwagiwa maji akiwa kitandani katikati ya usiku ndani ya bweni walilolala wanawake na wanaume.

“Dakika mbili za kujiandaa jogging,dakika mbili natoa”

Haikuwa ombi bali ni amri, mzee aliyevalia mavazi ya kijeshi ndiye aliyetoa kauli hiyo akaondoka akiwaacha wakijiandaa.Daphine alihisi mwili wake umechoka kila kiungo chake cha mwili kina muuma kutokana na kukimbia siku iliyopita,katika kujitafakari kwake dakika mbili zikawa zimekatika tayari.Mlango wa bweni ukafunguliwa tena Mzee wa bweni akazama ndani.

“Dakika mbili zimepita tokeni nje”

Watu walianza kutoka nje lakini Daphine alikuwa bado amesimama haelewi ni kitu gani akifanye.

“Vipi?”

“Bado sijajiandaa”

“Kuja hapa”

Daphine akasogea kwa uwoga jinsi mzee huyo alivyomuangalia ilimuogopesha,sura yake ilitisha kupita kiasi na ilikuwa na makunyanzi usoni.

“Muda wote ulikuwa wapi?”

“Samahaa..”

“Lazima nikupe adhabu ili siku nyingine uwahi”

Haikuwa utani kosa dogo kama hilo Daphine alipewa adhabu, alitolewa nje mpaka katikati ya uwanja mkubwa ambapo kulikuwa na kijumba kidogo chenye machuma juu kimefunikwa na mfuko mkubwa mweupe wa nailoni,humo ndipo Daphine alipoingizwa kama adhabu ya kuchelewa kutoka bwenini.

“Ukae kwanza humo”

Kwa mara ya kwanza Daphine hakuelewa nini maana ya adhabu hiyo sababu ilikuwa ni asubuhi,jua lilivyoanza kuwaka ndipo alipoanza kuhisi maumivu makali mwilini,jua liliwaka likawa linapenya katikati ya nailoni likafanya joto kali la kuchoma,Daphine alihisi kuunguwa mwili,machozi yakaanza kumtoka yalikuwa ni mateso makali mno kwake.

Bado aliendelea kumtupia lawama zote Mr.Vital Kamere aliyemshauri aingie jeshini.Mateso kama hayo alijuwa ni lazima yangekuwepo,jua lilimchoma mwilini mithili ya pasi,akahisi kama anaunguzwa na moto mkali,alilia bila kupata msaada wowote ule wala kuingiza kitu chochote mdomoni, kiu ilimkaba usiseme mate yakamkauka mdomoni,akiwa amekaa chini jua linawaka na kumchoma akahisi kishindo cha mtu kinakuja,alivyogeuza kichwa chake alishindwa kumuona vizuri sababu ya mwanga mkali wa jua.

“Simama utoke nje,adhabu yako imeisha”

Daphine alitolewa akarudishwa bwenini,kichwa kilianza kumuuma mno akahisi kama kuna mtu ndani yake anakipiga na nyundo.

“Vipi mambo mimi naitwa Zaitun,mwenzangu unaitwa nani?”

Sauti hiyo ilimshtua Daphine aliyekuwa amekaa kitandani anaugulia maumivu ya kichwa chake.

“Daphi..ne”

“Pole sana kwa yaliyokukuta leo,vipi unaumwa?”

“Ndio”

“Nini tatizo?”

“Kichwa”

“Ngoja nikupe dawa lakini usimwambie mtu yoyote kuwa nimekupa”

“Sawa”

Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kujenga urafiki na msichana mdogo aliyeitwa Zaitun,kuanzia siku hiyo wakawa wanakula wote wanafanya kila kitu pamoja mpaka mazoezi,kadri siku zilivyokwenda mbele ndipo Daphine alipozidi kuzoea wakati mwingine hakulala usiku, aliweza kukaa macho bila kulala kwa takribani siku tatu,hiyo iliwashangaza zaidi wakuu wa jeshi.Kadri siku zilivyozidi kwenda ndipo mazoezi yalivyozidi kuwa makali mno.

***

Juma lililofuata tangu Daphine awasili walianza mazoezi mengine ya kuogelea ndani ya maji,ilikuwa kila asubuhi ni lazima wakakimbie kandokando ya bahari kisha baadaye kupiga mbizi,mazoezi yakazidi kukolea na Daphine akaanza kuzoea kadri siku zilivyokwenda mbele.

“Nani kachafua choo?”

“Nauliza tena nani kachafua choo,alafu hajasafisha kaweka mzigo wake?”

Sauti hiyo ilienea ndani ya bweni zima na ilikuwa ya kutisha,alikuwa ni mwanaume aliyekomaa mweusi tii,kama mkurya!

“Wewe hapo,nilikusikia usiku unaenda chooni simama”

Daphine aliogopa mno,kidole kilikuwa kwake nayeye ndiye aliambiwa asimame, bweni zima macho yalikuwa kwake.Ilikuwa ni siku ya Jumapili mapumziko kila mtu alikuwa bwenini.

“Kodendee sikil..”

“Siongei nawewe”

Zaitun alivyotaka kuingilia alitulizwa,Kodende alifananishwa na nyapara ndiyo maana aliogopeka kupita kiasi ndani ya kambi hiyo ya jeshi.Alimfikia Daphine bila kuuliza akamkwida t shirt na kumsimamisha juu.

“Sio Mimi”

“Kelele,unanifahamu mimi?”

“Hapan..Ndio ni..”

Kabla ya Daphine kumalizia sentensi yake alisukumizwa mbali akadondoka chali sakafuni na kupigwa teke la mbavu,kabla ya kuugulia maumivu ya mbavu alipigwa tena teke la mgongo hakuelewa kosa lake lilikuwa nini mpaka apigwe kiasi hicho,kilichomuuma zaidi hakuna hata mtu aliyeweza kumsaidia zaidi tu waliweka duara na wengine kuanza kushangilia.


Kuendelea kubaki chini bila kujitetea kulimaanisha kuendelea kupokea kipondo mpaka kuumizwa, hakutaka swala hilo liendelee ilikuwa ni lazima nayeye angalau ajitetee.Alivyokuwa chini alizidi kushindiliwa mateke, hapo ndipo aliukamata mguu wa Kodende,akauvuta kwa nguvu.Kodende alidondoka chini mzima mzima kama embe mtini,Daphine hakutaka kumuachia.Akasimama haraka na kumrukia kooni kama chui ambapo alimkaba kwa nguvu zake zote shingoni bila kumuacha,Kodende alitapatapa chini akijaribu kuutoa mkono wa Daphine shingoni mwake lakini wapi,Jinsi Daphine alivyozungusha mkono wake haikuwa rahisi kwa mtu yoyote kumtoa alimkaba kwa hasira huku akilia machozi,hiyo ilifanya bweni zima lipige kelele nyingi wakimshangilia Daphine.

Hapohapo wanajeshi waliingia ndani ya bweni kelele ziliwafikia nje,wakamtoa Daphine aliyekuwa juu ya Kodende na kutoka naye.

“Kwanini unapigana?”

Daphine aliulizwa na kusindikizwa na kibao kikali cha shavu ambacho kilimuangusha chini,hakukaa sawa akapigwa na kitako cha mtutu kichwani akapasuka vibaya sana damu zikaanza kumvuja.Wakamburuza na kuondoka naye ambapo huko alipewa adhabu kali kuliko kawaida.

Alipelekwa ndani ya kichumba kidogo ambapo huko alivuliwa nguo zake zote akabakiwa na chupi peke yake juu akiwa na blazia tu,mikono yake imefungwa kwa juu kama nyama buchani.Wakatokeza wanaume watatu wenye miraba minne wakiwa na mikanda ya jeshi mikononi mwao.

“Nadhani mnajuwa cha kufanya”

Ilikuwa ni kauli kutoka kwa Luteni Kibaigwa akiwa anawatizama vijana wa kazi,ungekuwa kambini na kuulizwa mwanajeshi yupi ana roho mbaya basi ungemtaja Luteni Kibaigwa.Alikuwa na mdomo mkubwa na macho yake yalikuwa yana makengeza,wanafunzi waliokuwa depo walimpachika jina na kumuita ‘Black Mamba’ kutokana na mdomo wake kuwa mkubwa kama mamba na siku zote waliomba Mungu wasiingie mikononi mwa Luteni Kibaigwa.

“Hakikisheni hizo kamba mmezikaza,Mwambie Mujuni alete lile dumu lenye maji ya pilipili”

Daphine machozi yalianza kumlenga kabla ya mateso kuanza,hakustaili kupewa adhabu kama hiyo.Hakuelewa ana mkosi gani,hiyo ilikuwa ni adhabu ya pili kwake kupata ndani ya siku chache tangu aingie depo.

Akiwa anakazwa kamba vizuri mikononi madumu makubwa matano ya lita ishirini yaliyokuwa yana maji ya pilipili yukawekwa mbele yake.Kilichofuata hapo ni kuchalazwa mikanda mwilini,watu hawa waliokuwa wamebobea kutesa watu depo walifanya kazi yao ipasavyo.

“Ahhhhhh aaaaaaaaaah”

Daphine alikuwa akilia machozi maumivu aliyokuwa anayasikia hayakuwa na kipimo,wanajeshi walipokezana kumchapa mikanda ikawa inamtoa alama,ndani ya dakika tatu akaanza kuvuja damu mgongoni na tumboni,hapo ndipo dumu moja wapo lililokuwa na maji ya pilipili likachukuliwa,Daphine akaanza kumiminiwa yakapita mpaka juu ya vidonda vilivyokuwa vinatoa damu.

Kelele za maumivu alizokuwa anapiga zilipaa na kuenea kambi nzima ya jeshi!



Daphine alikuwa akilia machozi maumivu aliyokuwa anayasikia hayakuwa na kipimo,wanajeshi walipokezana kumchapa mikanda ikawa inamtoa alama,ndani ya dakika tatu akaanza kuvuja damu mgongoni na tumboni,hapo ndipo dumu moja wapo lililokuwa na maji ya pilipili likachukuliwa,Daphine akaanza kumiminiwa yakapita mpaka juu ya vidonda vilivyokuwa vinatoa damu.

SONGA NAYO.


Maumivu aliyohisi mwilini mwake hayakuwa na kipimo chake,Daphine alilia machozi ya uchungu na kupiga kelele nyingi lakini wapi.Wanajeshi waliobobea kutesa binadamu wenzao walizidi kufanya kazi yao waliendelea kumchalaza Daphine mikanda mwilini mwake bila huruma.Walivyochoka walinyanyua madumu ya maji yenye pilipili na kum-miminia.Hapo ndipo Daphine alipokuwa akihisi kama anachanwa chanwa na viwembe,vidonda alivyokuwa navyo vilipoingia maji ndipo alipohisi uchungu ajabu.Kama angekuwa na uwezo wa kujitowesha duniani basi angefanya hivyo mateso aliyokuwa anapata yalizidi kipimo chake.


Mpaka kunapambazuka asubuhi Daphine alikuwa hajiwezi tena mwili mzima una alama za mikanda na vidonda,amelegea hawezi hata kujigusa kabisa.Akahisi kuna watu wanafungua mlango wa chumba alichokuwa amening’inizwa kama nyama.Akaelewa tayari mateso yanaanza upya,kwa hali ya kuchoka akanyanyua kichwa chake juu.

“Mtoeni”

Luteni Kibaigwa alitoa amri hiyo,Daphine akafunguliwa akashikwa huku na kule na watu wawili akawa anaburuzwa kutolewa nje ambapo aliwaona wenzake wapo gwaride tayari.Akapelekwa mpaka bwenini.

“Una dakika tatu za kujiandaa uwende gwaride”

Bila kujali ni kiasi gani Daphine alikuwa kwenye mateso Luteni kubaigwa alitoa amri hiyo.

“Umenisikia”

“Nd..io”

“Nadhani unajua nini maana yake usipokuwepo gwaride ndani ya dakika tatu”

Luteni Kibaigwa alitoka nje.

Daphine alitamani angalau apumzike ama apewe chakula ale lakini haikuwezekana ilikuwa ni lazima awepo gwaride ndani ya dakika tatu,asingetokea ili maanisha kurudishwa upya kwenye mateso ambayo hakutaka kurudi tena.Ki uvivu akajikaza na kutembea mpaka kwenye begi lake,akatoa nguo akavaa na kuanza kutembea kutoka nje,akafanikiwa kuwahi na kusikiliza maelekezo ambapo baada ya dakika tano mazoezi yalianza.Kikosi kilielekea baharini ili kukimbia.Daphine alikuwa amechoka lakini alijikaza,alijipa moyo kuwa ipo siku kila kitu kitakwisha kwani hakuna lenye mwanzo lisilokuwa na mwisho wake.

“Daphine pole sana”

Rafiki yake wa karibu Zaituni alimfariji wakiwa kandokando ya fukwe za bahari.

“Ahsante”

“Inabidi uvumilie tu”

“Sawa”

Mazoezi yalivyoisha,wakapewa dakika ishirini ili wale chakula cha mchana.Zaitun hakula chakula alichukuwa akamkabidhi rafiki yake, Daphine.

“Kula na hiki”

“Hapana”

“Kula Daphine”

Hivyo ndivyo ilivyokuwa,Zaituni na Daphine wakawa maswaiba wakubwa na kila kitu walifanya pamoja.

Hata lilivyokuja swala la jinsi ya kulenga shabaha walikuwa bega kwa bega.

Kadri siku zilivyozidi kwenda mbele ndipo Daphine alipozidi kuzoea na kuwa mkakamavu, akaelewa jinsi ya kushika mtutu na kutumia silaha zote za kivita,mazoezi yalimkomaza na hata lilipokuja swala la mazoezi ya kupambana na adui Daphine aliweza kuelewa kwa haraka, kichwa chake kilinasa mambo kama sumaku,hata alivyopewa watu wawili kupambana naye aliwachakaza vibaya sana.Daphine alijuwa kukunja ngumi na alikuwa mwepesi kurusha mateke ya hewani yaani ‘round kick’.

“Daphine,ingia kati….Kenny,Mudi,Mussa,Suka”

Mkuu wa kikosi Captain Mkabi alisema,Daphine akasimama na wanaume wengine wanne walioenda hewani futi nyingi.

“Ingieni katikati”

Walitengeneza kama duara na katikati kulikuwa kuna uwazi mkubwa,Daphine akaingia katikati akiwa amevaa vest nyeusi chini suruali ya jeshi na mabuti marefu ya jeshi pia,aliwatizama wanaume hawa wanne waliomzunguka,akawaangalia kwa zamu kila mmoja wapo,akakunja ngumi.Yalikuwa ni mazoezi ya kupimana nguvu kwa njia ya kupambana.Sekunde mbili zilivyokatika ngumi ilirushwa kutokea nyuma ikamfikia Daphine kwenye mbavu akajikunja,kabla ya kuugulia maumivu akatulizwa na ngumi ya uso akayumba alivyokaa sawa akasimama wima,ngumi nyingine ilivyorushwa aliiona na kuinama chini ikapita hewani alivyoibuka juu alikuwa tayari amekunja ngumi akamchimbua Kenny ngumi ya kidevu,akadondoka chali,akageuka nyuma haraka na kuruka ‘round kick’,teke likamfikia Mudi usoni akamvuta na kumtwanga kichwa cha pua akampasua vibaya sana,akahisi amekabwa na mtu wa nyuma yake,akampiga kipepsi akajivuta na kupeleka mikono yake kwa nyuma akainama na kumrusha Mussa kwa mbele,akabinuka na kulala chali,hapo Daphine hakuchelewa akaanza kumshambulia ngumi za pua na mdomo.Suka alivyotaka kumvaa akatulizwa na teke.Tayari akawa amewadondosha wanaume wanne,ilikuwa ni kama filamu ya kuigiza.

Captain Mkabi akabaki kinywa wazi,alishindwa kumuelewa mwanamke huyu anayepambana na kuwadondosha wanaume aliowategemea jeshini.

“Inatosha”

Daphine alizidi kupewa mafunzo akapikwa na kupipika,hakuna mtu yoyote aliyeweza kumshinda likija katika swala la kupambana,wakati mwingine aliweza kupiga hata watu nane mpaka kumi jambo hilo likawa tishio kubwa,kila kiongozi akawa anamzungumzia yeye.

Na sio hivyo tu Daphine alikuwa hodari wa kulenga shabaha akitumia bastola,alijuwa kutumia silaha zote,AK 47,Rivolver,Mark 4 mpaka Sub machice gun.

“Zaitun,hii inashikwa hivi.Huu mkanda unauvaa begani,mkono wa kushoto unauweka hapa alafu huu unashika hapa chini”

Daphine alikuwa akimuelekeza Zaituni jinsi ya kushika mtutu siku hiyo walivyokuwa wanafanya mazoezi katikati ya msitu.Risasi ndizo zilikuwa zinarindima,wakiwa mazoezini.

***

“Mkuu anakuja leo saa kumi ya jioni,saa tisa muwe katika gwaride.Sawa”

Yalikuwa ni maagizo mafupi waliyoachiwa siku hiyo ya Jumapili asubuhi sana na siku hiyo uwanja ulisafishwa kwa ajili ya mapokezi.Wanafunzi wote kambini wakawa mkao wa kumpokea mtu waliyeambiwa ni mkubwa wao katika jeshi.

“Nani anakuja?wewe unamfahamu?”

Daphine alimuuliza rafiki yake Zaituni baada ya maagizo hayo kutolewa,walikuwa wamekaa wote kitandani.

“Hapana,simjui”

“Anaitwa Brigedia Karanje”

Sauti ya mtu wa nyuma yao iliwashtua,ilielekea hawakujua kama kuna mtu anawasikiliza.

“Brigedia Karanje?”

Daphine akauliza kwa hamaki na kugeuka!

“Ndiyo,anaitwa Brigedia Karanje ni komandoo sasa hivi.Ndiyo mkubwa wa majeshi nchini Tanzania”

Hivyo ndivyo ilivyokuwa Brigedia Karanje alitakiwa kufika nchini Urusi,jijini Moscow saa kumi ya Jioni akitokea nchini Tanzania,ilikuwa ni lazima akawaangalie vijana wake.Sababu tayari alishaingiza mabomu ya Nuclear nchini Tanzania kumaanisha kuwa mambo tayari yalikuwa yamekwiva.

*****

“Tuku! Tuku! Tuku! Tuku! Tuku!”

Ulisikika mlio mkubwa wa helkopta ikitokea angani saa kumi ya jioni,vumbi lilitimka ilikuwa ni helkopta kubwa ya jeshi iliyokuwa mita chache angani kumaanisha kuwa ilitaka kutuwa juu ya uwanja huo wa kambi,wanafunzi na viongozi wote wa jeshi walikuwa gwaride vumbi likiwapuliza lakini hawakujigusa wala kutingishika.

Taratibu Helkopta ikaanza kushuka chini kisha kuweka machuma yake juu ya ardhi,mmoja wa wanajeshi akashuka kutokea ndani ya helkopta akafungua mlango na kuchapa mguu wake mmoja chini na kupiga saluti, ilionekana aliyekuwa anashuka alikuwa ni mkubwa wake.


Ni kweli ndani ya Helkopta alishuka Brigedia Karanje,wanajeshi wote wakachapa miguu chini na kupiga saluti.Daphine alimshangaa Mwanajeshi huyo aliyekuwa mrefu sana aliyejazia mikononi usoni ana mabaka kama kenge,ukubwa wa mwili wa Brigedia Karanje ulifananishwa na Goliath.Bila kusema chochote kazi yake ikawa ni kupita na kukagua gwaride,hakuna mtu aliyejigusa.

“Vijana wameiva?”

Bridegia Karanje akamuuliza Luteni Kibaigwa aliyekuwa nyuma yake.

“Ndio mkuu”

“Una uhakika?”

“Ndio mkuu”

“Wewe njoo hapa”

Moyo wa Daphine ukapiga kwa nguvu kidole kilimlenga yeye.Akawa anatetemeka kwa hofu alihisi kinyesi kinampenya kwenye nguo yake ya ndani hakuelewa kwanini hali hiyo imemtokea,alivyotaka kutoka kwenye gwaride akatulizwa.

“Sio wewe huyo mwenzako”

Kumbe hakuwa yeye ni jirani yake upande wa kulia ndiye aliyeitwa,Brigedia Karanje akatembea mpaka katikati ili apimane naye nguvu mwanaume huyo aliyemchangua.Akamuita kwa kutumia mkono wake,kila ngumi iliyorushwa ilidunda kifuani mwa Brigedia huyu,akakunja ngumi moja,na alivyoitupa hakufanya makosa kijana aliyefahamika kwa jina la Mkavinja,alitupwa mbali na alikuwa amepasuka mdomo,damu zinamchuluzika.

“Vijana bado kabisa,Wewe hapo kuja hapa”

Safari hiyo aliitwa Daphine na ndivyo ilivyokuwa alitembea mpaka kwa Brigedia Karanje akainua kichwa juu sababu ya urefu wake kama Goliath,alivyorusha ngumi ikadunda kifuani.Brigedia Karanje akamtizama Daphine kwa dharau,akarusha ngumi Daphine akahepa kushoto ngumi ikapita hewani akakaa sawa,Brigedia Karanje alivyorusha ngumi nyingine ikawa vilevile.

Daphine alikuwa mwepesi na mwanamke makini mno,aliamini kwamba mwanaume anayepambana naye hakuwa wa kawaida alikuwa ana nguvu na mkakamavu hivyo ilihitajika akili ya ziada ilibidi ajiongeze.Hata hivyo haikuwa kazi rahisi.Kila mtu alikuwa makini kuangalia mpambano huo,sababu walimuelewa Daphine,Kosa alilofanya Daphine ni kurudi nyuma,hapo ndipo alipopigwa teke la Kifua akadondoka chali,Brigedia alivyotaka kumkanyaga tumboni akabiringika na kuinuka haraka,akasimama wima.

Kwa kasi ya mwewe akakimbia mpaka kwenye mlingoti wa Bendera,ilikuwa kosa kubwa sana kwa Brigedia Karanje kumfuata kwa nyuma kwani Daphine aliushika mlingoti wa chuma kwa mikono miwili na kujizungusha kwa nguvu, kabla ya Brigedia Karanje kumfikia alipokea mateke mawili makali ya uso,akayumba kidogo hapo hapo Daphine akaruka ‘Round kick’ hewani,mateke yakamfikia Brigedia Karanje shingoni,akapepesuka Daphine hakuchelewa alivyotua chini akamkata ngwala,Puuu! Brigedia Karanje akadondoka chini,wanajeshi wote wakabaki vinywa wazi,wakakodoa macho yao kumshangaa mwanamke huyu jasiri!



Ilikuwa ni aibu kubwa sana kwake kuangushwa chini na mwanafunzi tena mwanamke,hakuelewa ni kitu gani akifanye lakini hasira zilimpanda lilikuwa ni jambo la kudhalilishwa kupita kiasi kwa upande wake.

Aliona ni kama kavuliwa nguo zote yu uchi wa mnyama,ki utaalaam akiwa chali aliweka mikono kwa nyuma juu ya ardhi akasimama wima,sura yake ilionesha kujawa na hasira,akavimba.Daphine aliogopa mno akaanza kurudi nyuma,kabla hajafika nyuma zaidi akarushiwa teke ambalo aliliona na kuinama chini likapita hewani,alivyoinuka alikumbana na ngumi nzito ya puani,ikamyumbisha kabla hajakaa sawa akapigwa teke zito la kifua.Brigedia Karanje alijawa na hasira ajabu, akamfuata na kumkaba kohoni kwa mkono mmoja akamuinua juu,miguu ya Daphine ikawa inaning’inia chini,akazidi kukabwa.Daphine alihisi maumivu makali kohoni alivyojaribu kujitoa ilishindikana Brigedia Karanje alikuwa ana misuli,akamrusha kando, hakuishia hapo alimsogelea na kuanza kumpiga mateke ya mbavu na tumbo, akamkanyaga kifuani kwa nguvu.Daphine alikuwa akihema juu juu huku akiugulia maumivu mwilini mwake.Brigedia Karanje alikuwa akimtizama Daphine aliyekuwa chini ya miguu yake,alimuangalia kwa kama sekunde tano bila kufanya chochote.

“Nahitaji mtu mwingine”

Brigedia kazi yake ilikuwa ni kuteua wanafunzi na kuanza kupambana nao,kuna kitu alijifunza baada ya zoezi hilo kuisha kuwa Mwanamke aliyeitwa Daphine alikuwa ana uwezo wa ajabu sana kwenye mpambano,hilo alilijuwa waziwazi hata hivyo hakutaka kuliweka swala hilo bayana.

***

Mazoezi yalizidi kuendelea na kadri siku zilivyozidi kusogea mbele ndipo Daphine alipozidi kukomazwa,kila mwanajeshi alikuwa akimtegemea yeye na wakati mwingine akawa mwalimu kwa wanafunzi wenzake,alikuwa ni mwanamke aliyekuwa anajiamini kuliko mtu yoyote yule,kifupi aliogopeka kambi nzima ingawa alikuwa mpole mno,Daphine hakuwa mkorofi. Kama ungemuangalia usingeweza kuamini kwamba mwanamke huyu ana balaa!

***

“Nahitaji niondoke na yule binti,jina lake nani?”

Brigedia Karanje alisema siku hiyo usiku baada ya kumuangalia Daphine mchana kwenye mpambano,hakushindwa hata mmoja hiyo ilimfanya Brigedia huyu atake kurudi naye Tanzania.

“Unamsemea Daphine?”

“Ndiyo”

“Hakuna shaka”

Huo ndiyo utaratibu uliokuwa unaandaliwa na Brigedia Karanje,ilikuwa ni lazima amtumie akirudi Tanzania kwa njia yoyote ile.

***

Ni kweli,Daphine siku hiyo alifurahi sana alivyoambiwa kwamba alihitajika kuongozana na Brigredia Karanje.Alipanga vitu vyake harakaharaka ndani ya begi lake dogo kwa ajiri ya safari ambayo aliambiwa anarejea nchini Tanzania, mtu wa kwanza kumkumbuka ni Vital Kamere na wazazi wake,maisha aliyokuwa analelewa yalimfanya atamani kufika haraka sana nyumbani.Alivyomaliza kila kitu akatembea mpaka kwa Zaitun akamshika bega.

“Nitakumisi sana”

Daphine alizungumza huku machozi yakianza kumlenga,moyo ulimuuma kuachana na rafiki yake kipenzi aliyemzoea lakini hakuwa na jinsi ilikuwa ni lazima arudi nyumbani, Tanzania.

“Hata Mimi Daphine usinisahau lakini”

“Nina Imani ipo siku tutakutana”

“Kila la kheri”

“Ahsante”

Wote wakakumbatiana, ilikuwa ni picha ya uzuni mno kwa watu hawa wawili waliozoeana,Zaitun alishindwa kuelewa angeishi vipi bila ya Daphine, alimzoea!Alivyomaliza kuagana na Zaitun akapita kuwaaga baadhi ya marafiki zake.

“Daphine”

Kauli hiyo kutoka mlangoni ilimshtua alivyokuwa akiwaaga wenzake,alikuwa ni mwanajeshi na nje mlio wa Helkopta ulisikika kumaanisha kuwa anahitajika kuondoka muda huohuo.Hivyo ndivyo ilivyokuwa,akatembea taratibu na kutoka nje ya bweni ambapo Helkopta ilikuwa tayari iko umbali wa mita tano inazungusha mapanga boi yake.

“Inamisha kichwa chini”

Daphine akainama kidogo na kuingia ndani ya helkopta ambapo alimkuta Brigedia Karanje tayari yupo ndani,alivyokaa vizuri mlango ukafungwa helkopta ikaanza taratibu kuinuka juu,Daphine akawa anaangalia chini anazidi kuuacha uwanja,bado hakuamini kuwa hatorudi tena eneo hilo.

***

Ngesa alikaa kituoni nyuma ya nondo wiki nzima,bila kuelewa nini hatma yake.Kilichomchanganya zaidi hakusikilizwa hata kidogo mbali na hapo hakuelewa kosa lake,bosi wake Jimmy Magembe alijaribu kumkinga akijaribu kumtetea lakini wapi,askari walichachamaa.

“Mzee huwezi kumuona tushasema”

“Kwanini nisimuone?ni kijana wangu”

“Ndiyo hivyo haya ni mambo ya usalama wa taifa”

“Naomba niongee na bosi wenu”

“Sawa”

Afande aliyefahamika kwa jina la Kibwe aliinua simu na kuwasiliana na mkubwa wake wa kazi.Alivyokata simu akamgeukia Jimmy Magembe.

“Yupo ndani pita”

Jimmy Magembe akanyoosha mpaka kwa mkuu wa kituo cha polisi ambapo mlangoni kuliandikwa IGP, akagonga na kuingia ndani.

“Karibu”

“Ahsante sana”

“Nakusikiliza”

“Mimi naitwa Jimmy Magembe,Derick Ngesa ni dereva wangu.Nahitaji kujuwa amefanya kosa gani?”

“Derick Ngesa?”

“Ndiyo”

“Hayo mambo yapo nje ya uwezo wangu,ni mambo ya usalama wa taifa.Hapa tumemuhifadhi kidogo.Ngoja nikwambie juu juu,anataka kufanya machafuzi ya nchi”

“Kivipi?”

“Sina cha kukwambia kingine”

“Nahitaji kujuwa”

“Nimeshakwambia ninachokijuwa,Ahsante!”

IGP Sajo Kabogoza aliongea kwa ukali kidogo ilionekana hakutaka maswali mengine zaidi,yeye alipewa maagizo kutoka ngazi za juu kuwa Ngesa ashikiliwe na asitoke mpaka apewe ruksa, hivyo ndivyo alivyofanya hakutaka kwenda kinyume na miiko ya kazi yake.Aliogopa kibarua chake kuota nyasi,bado alitamani kula pesa za uma ndiyo maana alikuwa na kitambi kikubwa.IGP Sajo alipenda sana rushwa lakini aliapia hata kama angepewa kiasi gani cha pesa ili Ngesa apewe dhamana angegoma.

“Nadhani tumemalizana naomba nipishe”

Mr.Jimmy Magembe alisimama akafungua mlango na kuondoka zake,hakuwa na sababu za kuendelea kubaki eneo hilo,alishakata tamaa akayaacha mambo yalivyo ingawa alitamani sana kumuweka Ngesa huru.

****

“Wuwuwu wuwuwu wuwuwu”

Mbwa walikuwa wakibweka mno ndani ya jumba kubwa, kelele zao zikazidi hiyo ilimaanisha kuna kitu kibaya wameona.

“Baba Hamisa,mbwa wanabweka hao unawasikia?”

“Ndiyo,walinzi si wapo lakini”

“Hata kama nahisi kuna kitu”

Ingawa kulikuwa na walinzi hiyo haikufanya Baba Hamisa aendelee kuuchapa usingizi,akapapasa chini ya mto na kuchomoa bastola.

“Nisubiri hapo usitoke”Akamwambia mkewe.

Baba Hamisa,akachomoa magazine ili kuhakikisha kama ina risasi alivyoridhika akarudisha.

“Kacha kacha”Akaikoki chemba ikafunguka.

Akatoka na kufunga mlango,akatembea mpaka Seblen,akafungua pazia.Akatumbua macho yake na kuogopa baada ya kuona walinzi wote wapo chini.

“Tulia hivyo hivyo,weka hiyo bastola yako chini”

Alihisi mkojo unataka kumpenya,kilichomchanganya zaidi sauti aliyoisikia ilikuwa ya mwanamke.

“Weka bastola hiyo chini,sasa hivi”

Kichuma kilivyomgusa kisogoni ndipo alihisi kinyesi kinataka kumtoka,taratibu akaweka bastola juu ya kochi bila kugeuka nyuma,moyo wa Baba Hamisa ulikuwa unapiga kwa nguvu,alihofia uhai wake ingawa hakuelewa kwanini alivamiwa ndani ya nyumba yake usiku huo.

“Pesa ninazo,zipo ndani ya kabati nitakupa ta…”

“Kimnya,sina shida na pesa zako”

“Sasa una shida gani na mimi?”

“Nataka kumtumia ujumbe kaka yako Leslie Benjamin kwa ukatili wote alioufanya”

“Mbo..na si..kuelewi”

Bastola ilikuwa kwenye utosi wa baba Hamisa na mwanamke aliyeishika hakuonesha masihara hata kidogo ingawa alikuwa ameziba sura kama ninja,alionekana macho na alikuwa amevaa mavazi meusi juu mpaka chini.

“Baba Hamisa…pyuu pyuuuu”

Ni bora Mke wake angekaa kimya kuliko kutokeza na kuropoka kwa sauti, bastola yenye kiwambo mbele kinachozuia mlio wa bastola ilichomoa risasi.Zikamfikia Mama Hamisa kichwani akadondoka chini,damu zikatapakaa.

“Mama Hami..sa..pyuuuuu”

Ubongo wa Baba Hamisa ukachenguliwa na risasi na huo ndiyo ukawa mwisho wa maisha yao duniani.Hapohapo mwanamke huyo akatoa simu mfukoni na kuiweka sikioni.

“Tayari kazi imekwisha”

“vizuri sana Daphine,weka hiyo karatasi mezani.Rudi nyumbani”

Brigedia Karanje,kwa mara ya kwanza alitabasamu baada ya kupokea taarifa kuwa mdogo wake raisi wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Tonny Leslie Benjamin tayari amefariki dunia,alielewa ni kiasi gani ingekuwa pigo kwa Raisi Leslie Benjamin.Kama sinema kwake ilikuwa ni trela bado ‘movie’ kamili haijaanza!Ilikuwa ni lazima Raisi Leslie Benjamin alie na kusaga meno!




Ilikuwa ndiyo mara yake ya pili kuuwa katika maisha yake, mbegu aliyopandikizwa ilimfanya atake kumuuwa siku hiyohiyo Raisi Leslie Benjamin.Alikuwa ana usongo naye kupita kiasi.Aliziangalia maiti mbili zilizokuwa mbele yake na kuacha karatasi juu ya meza kama alivyopewa maagizo na Brigedia Karanje.Akaruka na kutoka nje ambapo pia kulikuwa na maiti nyingine za walinzi.Mwenyewe aliwapiga risasi ili kazi yake iwe rahisi.Akavuta mlango na kutoka nje ambapo aliingia ndani ya gari akawasha na kulitoa mbio,ulikuwa ni usiku sana kwa maana hiyo barabara ilikuwa haina magari mengi.Brigedia Karanje alimpangia nyumba kubwa maeneo ya Magomeni mapipa,ilikuwa ni nyumba iliyojificha,kubwa kiasi.Alivyofika aliweka gari nje ya nyumba na kushuka.Akatoa funguo zake na kufunga mlango ambapo aliingia na kunyoosha mpaka chumbani kwake,akajitupa kitandani na kujikita kwenye mawazo.Aliwaza vitu vingi sana siku hiyo hususani nchi yake ya Tanzania.

****

Difenda kumi na moja za polisi zilikuwa nje ya nyumba ya Marehemu Tonny Benjamin,kila kitu kilichotokea kilifanya jeshi la polisi lipigwe na butwaa,askari saba walikuwa chini wameuwawa kwa kupigwa risasi na Tonny Benjamin pamoja na mke wake walikutwa ndani wameuwawa vilevile.Kutokana na uzito wa mauaji hayo ilifanya mpaka Inspector Christopher Mlaba aingilie kati.Askari wote waliizunguka nyumba hiyo wakijaribu kutafuta vitu ambavyo vingekuwa kama ushahidi.

“Piga maiti picha huyu mtu aliyefanya hivi itakuwa ni mtu wa karibu”

Inspector Christopher aliongea kwa masikitiko makubwa sana.

“Mh Raisi anajuwa?”

Lilikuwa ni swali kutoka kwa Kamishna wa jeshi la polisi wilaya ya Ilala Afande Omari Dudu.

“Hapana”

“Inabidi aambiwe,huyu ni mdogo wake wa damu”

“Naelewa lakini jambo hili sio la kukurupuka na….”

Inspector Christopher kabla ya kumalizia sentensi alikatishwa na Sirgent Mujo alikuwa ametokea ndani akiwa kama ana kitu cha dharura anataka kukisema,mkononi alikuwa ameshika karatasi nyeupe.

“Mkuu,kuna kitu hapa”

“Kitu gani?”

“Kuna ujumbe umeachwa”

“Unasemaje huo ujumbe”

Wote wakamsogelea Sirgent Mujo,akatoa karatasi macho yao yakawa yanapita juu ya mwandiko.

‘HUU NI MWANZO TU SALAMU HIZI MUMFIKISHIE RAISI WENU LESLIE BENJAMIN NIMEANZA NA MDOGO WAKE KAMA JARIBIO NA YOYOTE ATAKAYE JARIBU KUFUATILIA NITAANZA NAYE NI MIMI FRANK MAN’SAI’

“Mh!”

Askari mmoja aliguna baada ya kusoma barua hiyo iliyokuwa na maneno ya kuogopesha,jina lililoandikwa chini ndilo liliwafanya waangaliane usoni.

“Mheshimiwa Frank Man’sai?”

Askari mmoja aliwauliza wenzake ingawa jibu la swali lilikuwa wazi sababu kila mtu alisoma barua.

“Ndiyo”

“Ndiyo amehusika hapa?”

“Sijui, lakini inabidi tuanze naye kwanza kama mtuhumiwa namba moja.Mpigie simu Mheshimiwa Raisi”

“Nimwambie nini?”

“Mwambie ukweli”

“Sasa nitaanzia wapi?”

“Unamuogopa?”

“Hapana”

“Basi mpigie simu,au wacha mimi nitaenda ikulu leo”

Hakuna hata askari mmoja aliyeamini kuwa Mh.Frank Man’sai waziri wa nishati na madini ndiyo kafanya mambo hayo ya mauaji lakini hawakuwa na la kufanya ilibidi wamuweke chini ya ulinzi kama mtuhumiwa wao namba moja.Hilo ndilo lilienda kufanyika.Inspector Christoper na dereva wake waliingia ndani ya gari na safari ya kuelekea Magogoni ikulu kuanza mara moja.

***

“No Tony amefariki?”

“Ndio Mheshimiwa Raisi”

“Ilikuwaje?”

Inspector Christopher alieleza kila kitu kinagaubaga na mwisho akaitimisha barua aliyoikuta.

Tangu awahi kumjua Raisi wake hakuwahi kumuona akilia machozi kama mtoto.Uchungu alioupata Mh.Raisi haukuelezeka,alimpenda sana mdogo wake na licha ya yote walizaliwa wawili tu ndiyo maana alimwaga machozi,akainamisha kichwa chake chini,alivyokiinua baada ya sekunde mbili macho yake yalikuwa mekundu,akatoa kitambaa na kukiweka machoni.

“Hiyo barua inasemaje?”Aliuliza na kuvuta kamasi.

Inpsector Christopher akamuangalia Raisi wake,hakuelewa aanzie wapi sababu alijuwa ni kitu gani kingetokea baada ya kumwambia kilichoonekana ndani ya barua.

“Mh.Frank Man’sai”

“Kafanya nini?”

“Ndiyo kafanya haya yote”

“Sio kweli”

“Ndiyo ivyo,yeye ndiye kaandika barua”

Hasira za Raisi Leslie zilifanya achukuwe maamuzi ya harakaharaka,hapohapo akatoa kauli kuwa Mh.Frank Man’sai awekwe ndani mara moja tena kabla ya lisaa limoja.

“Sawa Mh.Raisi”

“Sasa hivi”

Inspector Christopher alisimama wima na kutoka nje ambapo alikuta difenda inaunguruma,akatoa redio upepo na kuanza kufanya mawasiliano na kituo cha polisi staki shari.

“Afande Mocha,upo kituoni?”

“Ndio Mkuu”

“Naomba uchukuwe vijana kumi muende kwenye nyumba ya Mh.Frank Man’sai”

“Alafu baada ya hapo?”

“Mumuweke chini ya ulinzi”

“Unasema?”

Sio kwamba Afande Mocha hakusikia amri aliyopewa na mkuu wake wa kazi,mtu aliyetakiwa kwenda kumuweka chini ya ulinzi alikuwa ni kiongozi mkubwa sana serikalini ndiyo maana akashtuka alidhani wenda mkuu wake amekosea jina na angeenda kinyume wenda kibao kingemgeukia yeye mwenyewe.

“Nasema hivi,tafuta vijana kumi muende kwa Mh.Man’sai mumuweke chini ya ulinzi.Ni amri kutoka kwa Raisi Leslie”

“Sawa mkuu”

Hakukuwa na haja ya kupoteza muda,askari kumi wakatafutwa wakaingia ndani ya Deffender safari ikaanza ya kwenda nyumbani kwa Mh.Frank Man’sai.Licha ya kuwahi kufika ndani ya dakika kumi lakini hawakumkuta.

“Mh.Anasafiri leo ninavyoongea na nyie yupo njiani anaelekea uwanja wa ndege”

Hapohapo afande Mocha akatoa redio upepo na kumtaarifu mkuu wake wa kazi,ambaye hata yeye alitoa taarifa hiyo kama ilivyo kwa Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Kwahiyo anataka kutoroka?”

Hilo ndilo lilikuwa swali la kwanza kulitupa Mh.Raisi baada ya kupewa taarifa hizo,kutaka kusafiri ghafla kwa Mh.Frank Man’sai kulimpa jibu hilo moja kwa moja.

“Akamatwe mara moja,sasa hivi tuma vijana wako”

Hapohapo Mh.Rais akainua mkonga wa simu na kumtafuta Mkurugenzi wa kitengo cha usafiri wa anga,Mr.Alex Pondamaji.

“Naomba Frank Man’sai awekwe chini ya ulinzi mara moja,endapo akifika hapo”

“Mh.Raisi una..”

“Nimesema nataka mtu huyo awekwe chini ya ulinzi kabla hajaondoka hapa nchini haraka iwezekanavyo hata kama keshapanda ndege fuatilieni”

Ilikuwa ndiyo mara ya kwanza kwa Raisi Leslie kuongea kwa sauti ya kufoka,alizungumza kwa hasira za waziwazi.Hakuelewa amfanye nini Mh.Frank Man’sai endapo atawekwa chini ya ulinzi na vyombo vya dola.

****

Landcruser Vx aliyokuwa anatumia waziri wa nishati na Madini Mh.Frank Man’sai ilikuwa ipo uwanja wa ndege Mwl.Julius Nyerere akiwa viti vya nyuma, tiketi yake mkononi pamoja na hati yake ya kusafiria,alikuwa akielekea nchini Marekani.Dereva wake akashuka na kumfungulia mlango, Mh.Frank Man’sai akateremka.

“Mh.Nakutakia safari njema”

“Ubaki salama nashukuru sana,nikifika tutawasiliana”

“sawa”

Mh.Frank Man’sai akageuka ili kuelekea lango la wasafiri kabla ya kupiga hatua ya tano lundo la maaskari lilitokeza wakamzunguka.

“Mheshimiwa upo chini ya ulinzi”

Afande Mkono Sagasa ndiye aliyetamka huku akimuangalia Mh.Frank Man’sai usoni.Hakukuwa na muda wa kujitetea Mh.Frank Man’sai aliwekwa chini ya ulinzi akaingizwa ndani ya diffenda hapohapo.

***

“Afande,afande niambie ukweli.Tonny Benjamin amefariki?”

Habari za Tonny Benjamin kufariki dunia zilikuwa bado hazijatangazwa rasmi kwenye vyombo vya habari,ni jeshi la polisi tu na baadhi ya viongozi ndiyo walikuwa wanajuwa kifo hicho.

“Afande,afande”

Ngesa akazidi kuita,habari hizo zilimshtua hata yeye sababu uhusiano wake na Tonny ulikuwa wa karibu kupita kiasi licha ya hivyo walishirikiana katika mambo mengi tofautitofauti,haikuwa rahisi kwa Ngesa kuzipitisha habari hizo ndani ya kichwa chake ndiyo maana akauliza.

“Ndio amefariki usiku wa kuamkia leo”

“Aliumwa?”

“Hapana”

“Ilikuwaje afande?”

“Alivamiwa na watu wasiojulikana wakapigwa risasi yeye na mkewe”

“Mshawapata wahalifu?”

“Hapana lakini tushapata pa kuanzia”

“Wapi?”

Ngesa alihoji maswali mengi kupita kiasi,kutokana na Afande aliyekuwa zamu siku hiyo walizoeana ndiyo maana Ngesa alidiriki kuuliza maswali chungumzima!

“Kuna barua iliokotwa nyumbani kwa Marehemu kwamba Mh.Frank Man’sai amehusika”

“Mh.Frank Man’sai?”

“Ndiyo”

“Hapana sio kweli”

“Ndiyo hivyo,kila mtu haamini lakini ukweli ndiyo huo”

“Raisi yeye amesemaje?”

“Ametoa kauli kuwa awekwe chini ya ulinzi”

Kuna kitu Ngesa alijifunza kutoka katika maelezo ya Afande aliyekuwa ana muhoji,roho yake ilikataa kabisa kukubali kwamba Mh.Frank Man’sai alifanya mauaji hayo.Ilikuwa ni lazima afanye kitu ili awatafute wahalifu,kuanzia hapo akawa amekaa kimnya anatafakari kitu cha kufanya.

“Kwahiyo watampeleka kituo gani?”

“Nadhani staki shari”

“Okay”

Moyo wa Ngesa uliuma ajabu,Tonny Benjamin alikuwa ni zaidi ya ndugu kwake.Kila sekunde ilivyosogea ndipo hasira zilimkaba mno,alitamani kuzipinda nondo na kuzivunja ili aondoke na kuwasaka watu waliofanya mambo hayo ya kinyama.

“Lazima nitoke humu ndani”

Ngesa aliwaza na kukaa kitako akitafakari njia za kutoroka kituo cha polisi,haikuwa kazi rahisi hata kidogo ilikuwa ni lazima atumie akili ya ziada ndiyo maana alitafakari kiundani zaidi,akatizama juu akaona kidirisha kidogo.Akapiga hesabu zake za harakaharaka akakosa jibu,masaa yalikuwa yanasogea mbele,hatimaye ikafika usiku.

“Afandee tumbooo,tumboooo”

Sauti ya Ngesa ilisikika akiwa ndani ya nondo analalamika,ikafika mpaka mapokezi.

“Embu kaa kimnya wewe kunguni”

Afande aliyeingia zamu usiku alifoka kwa hasira.

“Tumbooo tumboooo”

“Subiri nije kukupa dawa”

Afande akasimama na kirungu kwa nia ya kwenda kumpiga navyo Ngesa ili atulie,ilikuwa kosa kubwa sana kwake kuzikaribia nondo kwani Ngesa alitoa mkono wake nje akamvuta na kuzungusha mkono shingoni mwake akamkandamiza kwenye nondo,ilikuwa ni roba kali,haikuwa rahisi kwa afande huyu kumzidi Ngesa nguvu hata kidogo,taratibu akawa anaishiwa nguvu mpaka akapoteza fahamu,Ngesa akamvuta karibu kabisa.

Akapitisha mkono wake katikati ya nondo na kutoa funguo.Akauchomeka kwenye kufuli,likaachia.Hapohapo akatoka nje,akamburuza askari na kumuweka kando.Akachomoa bastola yake na kuiweka kiuno,akamvua nguo zake zote akavaa yeye.Ngesa akawa ndani ya sare za polisi akawa kama mmoja wao.Alivyopita mapokezi akachukuwa funguo za gari na kutoka nje,akaingia ndani ya Diffender na kulitia moto.Safari yake ilikuwa ni kwenda Staki shari kumkomboa Mh.Frank Man’sai.

***

“Mimi sijui chochote”

“Mheshimiwa hatutaki kupeleka haya mambo mbali tafadhali naomba utueleze sababu utaozea jela”

“Mnapoteza muda wenu bure mimi sielewi chochote,Tonny mara ya mwisho kuonana naye ilikuwa last week nashangaa mnavyoniambia ameuwawa”

“Ulikuwa una safiri,kwanini?”

“Nilikuwa naenda kumtembelea mwanangu shule,Marekani”

“Unataka sisi tukuamini?”

Mh.Frank Man’sai alikuwa ndani ya chumba cha mahojiano ndani ya kituo cha polisi staki shari,hapo ndipo alipokuwa anafanyiwa usaili,tangia asubuhi mpaka usiku unafika lakini jibu lake lilikuwa lilelile kuwa hajui lolote.

“Hii barua kaandika nani?”

Hiyo ndiyo ilimfanya Mh.Man’sai atumbue macho kama mjusi aliyebanwa na mlango.Muandiko uliokuwa juu ya karatasi ulimuogopesha kwa sababu ulifanana na wake ingawa katika kumbukumbuku zake kichwani hakuwahi kufanya kitu kama hicho,aliogopa!

“Huu mwandiko wa nani?”

Lilikuwa ni swali kutoka kwa afande Solo huyu ndiye aliyekuwa akimsaili Waziri wa nishati na madini Mh.Frank Man’sai.Karatasi nyingine zikaletwa ili kuufananisha mwandiko.

“Huu ni mwandiko wako Mheshimiwa,tushajuwa tayari wewe ndiye umefanya mauaji.Tunachotaka kujuwa kingine,umeshirikiana na nani.Nina amini haupo peke yako”

****

Diffenda ilipiga msele nje ya kituo cha polisi staki shari baada ya Ngesa kupiga breki,vumbi likatimka ingawa ilikuwa usiku.Alidhamiria kuuwa endapo polisi wangeenda kinyume na anachohitaji,Ngesa alikuwa ni mtu mwenye hasira mbaya,alivimba kama chura siku hiyo.Akateremka kutoka kwenye gari na kunyoosha mpaka mapokezi.

“Habari afande”

Ilikuwa ni salamu kutoka kwa askari aliyekuwa mapokezi.

“Nzuri,namuhitaji Mh.Man’sai.Nimetumwa kuja kumchukuwa,yuko wapi?”

“Umetokea kituo gani?”

“Msimbazi”

“Mbona hatuna taarifa hizo”

“Frank yuko wapi?”

Swali hilo liliambata na sauti ya ukali.

“Sitokuuliza tena mara nyingine”

Hapohapo akachomoa bastola na kumlenga askari usawa wa kichwani.

“Mh.Man’sai yuko wapi,moja..mbili..tat..”

“Yupo yupo chumba kinachofuata”

“Ongoza mbele”

Afande aliyetambulika kwa jina la Oswadi kinyesi kilimbana kichuma cha bastola kilikuwa nyuma ya kisogo chake anatetemeka kama mgonjwa wa kifafa,alielewa mwanaume aliyekuwa nyuma yake hakuwa na masihara na endapo ataenda kinyume ubongo wake ungesambaratishwa vibaya sana,alikiogopa kifo hiko kibaya cha kupigwa risasi.Kitendo cha kuingia ndani Ngesa akamuweka chini ya ulinzi afande Solo.

“Kimnya hivyo hivyo,wewe mfunge mwenzako pingu.Fanya upesi simameni juu”

Hicho ndicho kilichofanyika,wote wakafungana pingu,wakasimama na kufungiwa ‘lock up’

“Mh.Frank naomba tuongozane”

Ngesa nyuma Mh.Frank Man’sai mbele,wakatoka mpaka nje na kuingia ndani ya diffenda.

“Wewe ni nani?”

Mh.Frank akauliza baada ya safari kuanza.

“Naitwa Ngesa, naelewa wewe haukufanya mauaji”

Maneno ya Ngesa yalimfanya Mh.Frank amtizame Mwanaume huyu mdogo aliyeongea kwa kujiamini.

****

Ndani ya kambi ya Jeshi sherehe ya chini kwa chini iliendelea baada ya zoezi la Kuumuwa Tonny Benjamin kukamilika,badala ya kuuzunika.Brigedia Karanje na wenzake waliaandaa tafrija ndogo ya kumpongeza Daphine siku hiyo usiku.

“Kwahiyo wanajuwa Mh.Frank Man’sai ndio kafanya mauaji?”

“Ndio na sasa hivi ninavyoongea nawewe yupo staki shari kituoni pale”

“Safi sana,nataka kwanza wauwane wenyewe kwa wenyewe.Ili waturahisishie kazi”

Hapo hapo waligonga ‘cheers’ na kufurahia ushindi,pembeni alikuwa amesimama Daphine na mzinga mkubwa wa pombe kali.



Ndani walikuwa wanajeshi ishirini na saba,ilikuwa ni sherehe ndogo ndani ya kambi ya Lugalo na iliongozwa na Brigedia Karanje,moyoni alikuwa ana furaha ajabu sababu alijuwa ni kiasi gani Raisi Leslie Benjamin ameumia moyo licha ya yote hakutaka kuishia hapo.Kabla ya kumuuwa ilikuwa ni lazima amtese na kumfanya ajute katika maisha yake,pembeni alikuwa na walinzi wake waliojazia misuli hawa nao walikuwa wanajeshi, mita chache mbele yake alikuwa amesimama Daphine amevaa ‘jeans’, shati chini raba.Bado hakutaka kuamini kwamba msichana huyo mdogo ameweza kufanya jambo hatari kiasi hicho.

“Daphine”

Brigedia Karanje akaita.

“Abee”

“Vipi wakuongeze kinywaji?”

“Hapana,huu mzinga unatosha nikiongeza hapa nitashindwa ku drive”

“Usijali ni siku yako ya kufurahi,kunywa kunywa utarudishwa kwako salama kabisa”

“Ahsante sana”

Mziki ulikuwa ukiendelea taratibu huku watu wakinywa mvinyo wakijiburudisha,katika chumba hicho Daphine ndiye aliyetia fora sababu alikuwa ni mwanamke peke yake,hiyo haikumuumiza sana kichwa.

Aliwachukulia wanajeshi hao ni kama ndugu zake tu na wote walikuwa katika harakati moja ya kumsulubu Raisi wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh.Leslie Benjamin alimchukia raisi wake kuliko kifo,alitamani siku hiyo hiyo amvamie ikulu amfanyie kitu kibaya lakini alisubiri amri kutoka kwa mkuu wake Brigedia Karanje,hakuelewa kuwa alipandikizwa mbegu mbaya ya chuki, kifupi Daphine alikuwa nyuma ya kila kitu kinachoendelea.


Pombe ziliendelea kunyweka na Daphine alikuwa akiongeza tu mpaka zinafika glass saba alikuwa bwii,siku hiyo alikunywa kiasi kingi cha pombe ndiyo maana akaanza kurembua na kukaa juu ya sofa.Kizunguzungu kikali kilimshika,kichwa chake kikawa kizito.

“Kamongooooo nipeleke nyumbaniiiii tafadhaliiii”

Daphine aliongea kwa sauti ya ulevi na kumvuta mkono Mwanajeshi aliyekuwa pembeni yake.

“Subiri kidogo”

“Mpeleke akapumzike hakikisha anafika salama”

Brigedia Karanje akatoa amri,hiyo ilimaanisha jambo hilo lifanyike mara moja.M.P Kamongo akamshika Daphine na kumuinua akaichukuwa mikono yake na kuizungusha begani mwake.

“Mkuuuu,mimi tayariii see you tomorrow.Lazima tufanye kazi yetu,tumalizeeee kile tulichokianza tupo pamoja,kwa leo inatoshaaaaa”

Daphine alikuwa anaongea maneno mengi mfululizo akimuaga Brigedia, wakatoka mpaka nje huku akikokotwa,ambapo aliingizwa ndani ya gari.

“Usisahau kushusha netiiiiiii kuna mbu leeeo”

“Bado hujafika kwako”

“Kumbe hapaaaa wapiiiii?”

“Upo kwenye gari”

“Weeee mimi sio mpuuzi,nipo kwaaangu hapaaaa.Shusha neti”

M.P Kamongo hakutaka kuangaika na Daphine sababu alijuwa haongei na yeyote bali ni pombe zilizokuwa kichwani mwake.Ulikuwa ni usiku mzito sana,M.P Kamongo aliendesha gari kwa mwendo wa kawaida siku hiyo na baada ya dakika arobaini na tano walikuwa magomeni, akamfikisha Daphine mpaka anapoishi.

****

Ngesa alikuwa akikimbiza Difenda kama mtu aliyechanganyikiwa akili, ilikuwa katika gia namba tano pembeni alikuwa amekaa Mh.Frank Man’sai licha ya kufunga mkanda lakini alijishika vizuri.

Jinsi gari lilivyokuwa linakimbia ilimfanya aogope mno,roho yake ilikuwa mkononi.

“Tunaenda wapi?”

Mh.Frank Man’sai akamuuliza Ngesa na kuvunja ukimnya.

“Bagamoyo”

“Kwanini tusiende kwangu?”

“Hapana,sasa hivi utakuwa unatafutwa sana,Una simu?”

“Ndiyo”

“Nipatie”

Mh.Frank Man’sai alivyotoa simu Ngesa aliichukua na kuitupa nje kupitia dirishani,akazidi kusonga mbele.

“Kwanini umefanya hivyo?”

“Kupitia hii simu wanaweza kuku track kupitia namba zako za simu”

Ngesa alikuwa ni mpelelezi na alijuwa njia zote za polisi kuwashika wahalifu hivyo alikuwa ana uhakika anadhibiti njia zote wanazotumia.Ulikuwa usiku mnene na ilivyofika saa tisa ndipo walipoingia Bagamoyo,taratibu akapunguza mwendo na kupaki gari nje ya nyumba ndogo kiasi yenye miti ya michongoma kwa nje.

“Shuka Muheshimiwa”

Wote wakateremka,Ngesa akatembea mpaka nje ya nyumba na kugonga mlango.Ndani ya sekunde moja akaona taa imewashwa na mlango ukaanza kufunguliwa.

“Ngesaaaaa!”

“Gabriel”

“Naota au?Ulikuwa wapi?tulijuwa umekufa”

“Ni stori ndefu sana naomba nikaribishe ndani”

“Huyu si Muheshimi…”

“Ndiye yeye”

“Okay karibuni”

Mwanaume mrefu mweusi aliyetambulika kwa jina la Bwana Gabriel alishtuka mno sababu alijuwa kuwa Ngesa alishafariki miaka mingi iliyopita akiwa mkoani Morogoro, hakuelewa kuwa alitupwa msitu wa Mabira nchini Uganda na hivyo ndivyo ndugu zake wote walijuwa,Msiba wa Ngesa uliliza watu wengi sana hakuna mtu yoyote aliyejuwa kwamba alifungiwa ndani ya kambi ya jeshi akila mateso makali, walimtafuta bila mafanikio kwa mwaka mzima na mwishowe kudhani wenda alikufa,ndiyo maana Gabriel akashtuka na kudhani wenda anaongea na mzimu ama yupo ndotoni,alimuangalia Ngesa mara mbilimbili akiwa na hofu.

“Ngesa niwewe kweli isije ikawa ninaongea na jini”

“Ndiyo mimi,funga mlango”

Hakukuwa na stori nyingine baada ya mlango kufungwa, Ngesa alimgeukia Mh.Frank Man’sai akamtizama kwa kama sekunde tano.

“Ninachohitaji hapa ni ushirikiano wako la sivyo utaendelea kutafutwa mpaka kihama na utafungwa kifungo cha maisha ukikamatwa”

“Nipo tayari kutoa ushirikiano”

“Kuna barua ilikutwa nyumbani kwa Marehemu Tonny na inasemekana wewe ndiye umeandika a…”

“Hapana sio m…”

“Subiri nimalize kuongea,naelewa wewe hauwezi kufanya kitu kama hicho.Uhusiano wako na Tonny ninaufahamu”

“Ni kweli”

“Hiyo barua wewe uliiona?”

“Ndio walinionesha nilivyokuwa kituoni na kinachoniogopesha ni mwandiko wangu kabisa”

“Una uhakika?”

“Ndio,mwandiko ni wangu ninaujuwa lakini sijawahi kuandika kitu kama hicho”

“Ina maana kuwa kuna mtu kagushi mwandiko wako?”

“Nadhani”

“Nina amini kuwa ofisini kwako ndiyo rahisi mtu kufanya kitu kama hicho”

“Sina uhakika”

“Tutaenda kesho mimi nawewe”

“Nitakamatwa sasa”

“Unaniamini?”

Swali la Ngesa lilimfanya Mh.Frank Man’sai amtizame, hakuelewa amjibu nini sababu hiyo ndiyo ilikuwa mara yake ya kwanza kumuona katika maisha yake lakini hakuwa na chaguo lingine,mbali na hapo hakuwa na mtu mwingine wa kumuamini,Ngesa ndiye aliyemkomboa kutoka kituo cha polisi.

“Ndio”

****

Hakuna mtu aliyelala mpaka kunapambazuka,Ngesa akiwa na sare za kipolisi alichomekea vizuri na kuweka kofia kichwani akaivuta usoni kabisa ili isiwe rahisi kugundulika.

“Gabriel,ahsante sana tutarudi”

Ngesa aliaga,wakaanza kuongozana na Mh.Frank Man’sai mpaka ndani ya Difenda ambapo aliwasha na kuanza safari ya kuelekea Posta,ofisi ya waziri wa nishati na madini Mh.Frank Man’sai.

Walifika maeneo ya Kigogo na kuzidi kunyoosha, wakafupisha njia na kupitia jangwani ili wakwepe msongamano wa magari.

“Ukiwapata hao wahalifu utawafanya nini?”

Lilikuwa ni swali kutoka kwa Mh.Frank Man’sai.

“Nitamuuwa mmoja baada ya mmoja kwa mikono yangu”

Ngesa alimjibu na ni kweli alimaanisha,alikuwa ana hasira kupita maelezo yaliyojitosheleza ndiyo maana aliendesha gari kama mwehu,akaingia kariakoo na kuibuka mtaa wa Agrey hapo aliingia mtaa wa kongo na kutokeza barabara kubwa.

“Shit!”

Alikema baada ya kukuta msongamano wa magari,foleni ilisogea kwa mwendo wa kinyonga.Alivyosogea mbele zaidi ndipo alipogundua kuwa sio msongamano wa kawaida bali ni ukaguzi.Maasakri walikuwa wametanda Mnazi mmoja,wakifanya msako kwa staili ya kukagua gari moja baada ya jingine wakati mwingine walishusha watu ndani ya magari.

“Kuna tatizo hapa”

Ngesa akasema huku akichungulia mbele.

“Kuna nini?”

“Wanakaguwa”

“Watakuwa wanataka nini?”

“Sijui”

“Au wameshtuka”

“Sina uhakika”

Ngesa akapiga jicho nyuma na kuona kuna nafasi kidogo.

“Unaweza ukaruka nyuma hapo nikufunike na hilo boxi”

“Ndio”

“Ruka haraka..kachakacha”

Mh.Frank Man’sai alivyoruka viti vya nyuma Ngesa akakoki bastola na kuiweka vizuri juu ya mapaja yake alikuwa tayari kuanzisha ‘ambush’ endapo polisi wangemletea gozigozi,japokuwa aliamini hatoweza kuwashinda sababu walikuwa wengi na wenye silaha za moto,lilibaki gari moja tu ili ifike zamu yake akaguliwe,gari la mbele yake likapita akapiga gia akasogeza gari.

“Jambo afande”

Ngesa akaanza kutoa salamu,akiwa katika sura ya kazi hakuweka tabasamu lolote lile.

“Jambo,tunataka kukagua kidogo”

“Kuna nini kwani?”

“Ni agizo tu,katoa Raisi”

“Hata wenyewe kwa wenyewe afande?embu niache kidogo nikapate chai tangu jana nimekesha zamu usiku.Mkuu wako yuko wapi niongee naye?”

Ngesa alikuwa akitingisha kiberiti na kupima maji,alishaelewa kuwa hakuna mtu anayemfahamu sababu ndani ya jiji la Dar es salaam kulikuwa na zaidi ya askari milioni mbili hivyo ilikuwa ni vigumu kufahamiana.

“Mkuu wako yuko wapi?Nimekuuliza swali”

“Yuko kule”

“Mwambie namuita nataka nimwambie unachotaka kukifanya hapa nadhani hajui mimi ni nani,unanichelewesha hapa natakiwa ikulu sasa hivi”

Jinsi askari huyo alivyoanza kubabaika ilimfanya Ngesa awe mkali kidogo,mkwara wake ulianza kuzaa matunda.

“Yuko wapi?”

Ngesa akajifanya anataka kushuka ndani ya gari.

“Haina sababu ya kufika huko,ni mambo madogo tu hayo pita pita”

Ngesa akakanyaga ‘clutch’ na kupandisha gia namba moja,akaondoa gari.Akashusha pumzi ndefu na kuzidi kusonga mbele,alivyohakikisha kapotea machoni mwa polisi alimwambia Mh.Frank Man’sai akae.

“Ofisi yako ipo wapi?”

Walivyofika Posta,Ngesa akauliza.

“Hapo kwenye hilo gorofa mbele kidogo”

“Pale karibu na benki ya NMB?”

“Ndiyo”

“Gorofa namba ngapi?”

“Kumi na mbili”

“Okay”

Taratibu Ngesa akaweka gari kando kwenye moja ya maegesho na wote kushuka, wakanyoosha mpaka ndani ya gorofa na kuingia ndani ya lifti.Akabonyeza namba 12 lifti ikaanza kupanda juu,ilivyofika ikatoa mlio kisha mlango kufunguka.Mh.Frank Man’sai na Ngesa wakatoka,kila aliyemuona Mh.Frank Man’sai alishtuka hususani wafanyakazi wake,hiyo ilionesha kuwa habari za tukio lililotokea walilijuwa na walivyomuona Ngesa iliwashtua zaidi sababu alikuwa na nguo za kipolisi walidhani kuwa yupo chini ya ulinzi.

Wakatembea mpaka kwenye ofisi yake na kuingia.Kisha kufunga mlango.

“Ofisi yako ina CCTV camera?”

“Ndio”

“Naomba unipe rekodi ya tangu mwezi uliopita”

“Kwanini?”

“Fanya hivyo”

Mh.Frank Man’sai akaingia kwenye kompyuta na kuanza kupekua akitafuta rekodi zote kama alivyoambiwa,ghafla akapigwa na butwaa la waziwazi mpaka Ngesa aliyekuwa mlangoni anaangalia usalama kugeuka.

“Vipi?”

“Embu njoo Mara moja”

Ngesa akasogea na kutupa macho yake juu ya kioo cha kompyuta.

Alionekana mwanamke anatembea mpaka kwenye mafaili na kupekuwa pekuwa kisha kupiga picha karatasi zenye mwandiko wa Mh.Frank Man’sai kisha baada ya hapo alichukuwa simu na kuonekana akiongena na simu,wote walitizama video hiyo.

“Unamfahamu huyu Mwanamke?”

“Ndiyo,anaitwa Martha Msoso ni sekretari wangu”

“Unajuwa anapoishi?”

“Ndio”

“Huyu ndiye kachukuwa mwandiko wako,nipeleke kwake”Aliongea kwa hasira na kuyabana meno yake.

Hapohapo Ngesa na Mh.Frank Man’sai walianza kutoka nje,walivyofungua mlango walikumbana na lundo la maaskari wakiwa na mitutu mikononi.

“Mpo chini ya ulinzi,weka silaha yako chini pigeni magoti mikono wekeni juu sasa hivi”

Hakukuwa na ujanja mwingine wa kutoka,askari walikuwa wengi tena wameshika mitutu kumaanisha kuwa wangeenda kinyume wangemiminiwa risasi.

Ngesa taratibu alitoa bastola yake kiunoni na kuiweka sakafuni akapiga magoti na Mh.Frank Man’sai akafanya hivyohivyo walikuwa chini ya ulinzi mkali,askari wakasogea na kuwapiga pingu kwa nyuma.

“Mpo chini ya ulinzi”




Ngesa na Mh.Frank Man’sai walilazwa kifudifudi wakapigwa pingu kwa nyuma,wakainuliwa huku mitutu ikiwa kila upande,nyuma, mbele, kushoto na kulia.Askari waliwazunguka wakawaweka katikati, jinsi walivyopewa taarifa kuwa Ngesa ametoroka kituo cha polisi akitumia Difenda ya polisi iliwafanya wadhani kuwa mtu huyo ni hatari ndiyo maana wakawa makini na kumuweka chini ya ulinzi mkali wakiwa na silaha za moto,kesi ya mauwaji ya Tonny Benjamin ndiyo ikatia uzito wa swala hilo.

Ngesa alimuangalia kila askari alijuwa kivyovyote vile akienda kinyume angemiminiwa risasi na uhai wake ungeishia hapo duniani hata kabla hajamaliza kazi yake,hakutaka kufa bila kumaliza alichokianza ndiyo maana akasalimu amri.Wakatolewa nje,haikujulikana waandishi wa habari wametokea wapi.Kitendo cha kutoka ndani ya gorofa waandishi wa habari waliwavaa wakitaka habari,Ngesa akainamisha kichwa chake chini kwani hakutaka sura yake ianikwe popote pale.

“Tunaomba njia,hatutojibu swali lolote lile”

Mkuu aliyekuwa anaendesha operesheni hiyo aliyefahamika kwa jina la Afande Colman Constatine alisema na kuwapanguwa waandishi ingawa waliendelea kupiga picha za mnato.

“Tunaomba tueleze nini kimetokea”

“Nimesema sitojibu swali lolote”

Ngesa na Mh.Frank Man’sai waliingizwa ndani ya gofu la polisi viti vya nyuma wakiwa wamefungwa pingu kwa nyuma,askari wakaingia kwa mbwembwe na kuruka juu ya difenda na kuondoka kwa mkwara mzito tena na ving’ora juu.

“Huyo mwanamke anaishi wapi?”

Ilikuwa ni sauti ya Ngesa akimnong’oneza Mh.Frank Man’sai karibu na sikio lake, gari lilikuwa linaendeshwa hakuna hata askari mmoja aliyesikia.Ngesa akageuza shingo yake nyuma akaona Diffenda nyingine tatu nyuma yao,kumaanisha ulinzi ulikuwa mkali kupita kiasi.

“Anaishi Kinondoni B,block 41 nyumba namba 16k nadhani,geti jeusi”

“Sawa”

“Unataka kufanya nini?”

“Bado nahitaji kujuwa ukweli”

Ngesa hakutaka kukubali swala hilo kirahisi alielewa nini maana ya kufikishwa kituo cha polisi, huko asingeweza kutoroka kizembezembe kwake nafasi rahisi ilikuwa ni hiyo,akapiga hesabu za harakaharaka akachungulia mbele akaona msafara mwingine wa Diffenda.

“Vipi? umekalia kipisi cha karoti au?”

Lilikuwa ni swali kutoka kwa Askari aliyekuwa mbele kushoto,jinsi Ngesa alivyohangaika mara aangalie huku na kule ilimfanya askari huyo aulize swali la kejeli.

“Afande nisikilize mnafanya makosa makubwa sana,Muheshimwa hana kosa lolote.Tulikuwa tushampata muhusika nyie mmeingilia”

“Nani kakuruhusu uongee,subiri ufike ukakalie chupa ya bia.Utaeleza leo kilichomtoa kanga manyoya”

“Naomba niongee na Raisi Leslie”

“Kaa kimnya kuku wewe”

Ngesa alijaribu kuzungumza nao kiuungwana lakini askari walikuwa wakaidi kuelewa,akaangalia dirishani vizuri akaona wanakaribia kufika daraja la salenda.


Gari zilikukwa katika mwendo wa kasi kuliko kawaida kumaanisha kuwa Difenda za mbele kazi yao ilikuwa ni kusafisha barabara.

Akaangalia kiunoni mwa askari akaona funguo za pingu pamoja na bastola.Alikuwa amefungwa pingu kwa nyuma asingeweza kufanya chochote,hapo ndipo taratibu akaanza kupitisha mikono kwa chini,kadri alivyokuwa anaipeleka mikono yake chini pingu zilizidi kukaza,akaanza kuhisi maumivu makali,zikaanza kumkata damu zikaanza kumtoka lakini hiyo haikumfanya asitishe zoezi hilo,akainuka kidogo na kupitisha mikono yake chini ya miguu,mikono ikawa kwa mbele.

Zilikuwa zimebaki mita kama kumi hivi kulifikia daraja la salenda hakutaka gofu la polisi livuke daraja hilo,akaanza kuhesabu kimoyomoyo ilivyofika tatu gofu likagusa daraja la salenda, hapohapo kama umeme akamvaa polisi aliyekaa kiti cha mbele kushoto, akachomoa bastola yake kabla ya dereva kufanya lolote akatulizwa na kiwiko cha pua,akapoteza uelekeo wa usukani gari likaanza kuyumba huku na kule,Ngesa mahesabu yake yalikuwa funguo akazichomoa.Ndani ya gari Ngesa alikuwa akitembeza ngumi,alimvuta askari huyu akamtwanga kichwa cha pua,akamvaa dereva na kumkaba shingoni,akashika usukani yeye, tena kwa mkono mmoja ili kuliweka gari sawa.Alivyoona haikuwa rahisi akafungua mlango na kumtupa dereva nje,ambapo alibiringika na kukanyangwa na Difenda zilizokuwa nyuma zinaenda kwa kasi.

Ngesa akakamata usukani bado alikuwa na pingu mikononi.

“Muheshimiwa jishike vizuri”

Hapohapo akaweka mguu kati na kuvuta ‘handbreak’akazungusha usukani gari ikazunguka na kuelekea Magharibi yaani Bahari ya Hindi,ilivyokuwa asingeweza kuendelea mbele wala kurudi nyuma,akili yake ilimwambia alitose gari darajani.Hicho ndicho alichokifanya hapohapo akaweka gia,akakanyaga mafuta mengi gari likachomoka kama mshale.

“Griii grii paa paa paaaa”

Polisi wakaanza kulirushia risasi lakini tayari gari liligonga daraja la salenda na kutumbukia ndani ya bahari ya Hindi,askari hawakutaka kushindwa walisogea mpaka darajani na mitutu yao,wakaanza kumimina risasi juu ya maji.

“Shiiit,Wekeni ulinzi.Toeni taarifa kwa IGP Ditopile mwambie kuwa wahalifu wamekimbia…Imekuwaje?”

Polisi walichanganyikiwa tukio lilitokea lilikuwa kama sinema ya kijajusi lakini huo ndiyo ulikuwa ukweli halisi wa mambo,Ngesa na Mh.Frank Man’sai waliwatoka.

Kazi ya jeshi la polisi lilikuwa ni kutoa taarifa kwa mkuu wao,maaskari wakazidi kujaa juu ya daraja la Salenda wakiwa wameshika mitutu yao.Wengine walishuka mpaka chini lakini wapi,hakukuwa na dalili yoyote ile ya mtu kuibuka.

****

Ilikuwa ni vigumu kupita kiasi kwa Ngesa na Mh.Frank Man’sai kuogelea sababu walikuwa na pingu mikononi mwao na kuibuka juu ya maji lilikuwa ni jambo la hatari mno sababu walisikia milio ya risasi,Ngesa alikuwa hodari wa kucheza na maji mbali na hapo alikuwa ni mpelelezi wa kujitegemea ndiyo maana akili yake ilikuwa ikifanya kazi kwa kasi ya mwewe,kitu cha kwanza kukiwaza ni funguo.

Alikuwa amebana pumzi na ilikuwa ni lazima baada ya dakika tatu atoe kichwa chake juu ili avute pumzi.Akapapasa mifukoni mwake sababu alivyokuwa ndani ya gari ndipo alipoziweka,akazitoa kwa umakini maana alijuwa zingemtoka mikononi mwake kibarua kingekuwa kizito,bahati nzuri ilikuwa kwake akajifungua pingu zikaachia mikono yake ikawa huru,akayachapa maji na kumsogelea Mh.Frank Man’sai ambaye alikuwa anaelea ilionekana tayari alikuwa amepoteza fahamu,akamfungua pingu.Akapitisha mikono yake kiunoni wakaanza kusonga mbele,wakasogea kwa umbali wa kama mita kumi wakaibuka,walikuwa wameliacha daraja la salenda mbali kidogo hapo ndipo Ngesa akayachapa maji mpaka nchi kavu ambapo kulikuwa na miti mingi akamuweka Mh.Frank Man’sai.Akachukuwa gogo la Mti na kuliweka kwa chini akamuweka juu yake akaanza kumkamua maji ili kumpa huduma ya kwanza.

“Muheshimiwa…”

Ngesa akamuita na kuanza kumpiga piga kwenye mashavu, Mh.Frank Man’sai akaanza kukohoa na kucheua maji,taratibu akaanza kufumbua macho.

“Ne..nda kamsake huyo mwanamke la..sivyo nitaendelea kusakwa ta..fadhali fany..a hivyo”

“Siwezi kukuacha hapa,twende”

“Hapana,wewe nenda”

“No”

“Taf.a.dhali nenda kija..na”

Ngesa alimuangalia Mh.Frank akimuonea huruma,upande wa pili wa shilingi aliona kuwa yupo sahihi sababu kupatikana kwa mwanamke huyo ndipo ukweli ungejulikana na wote wangekuwa huru.

“Wacha mimi niende”

“Oka..y”

Hapohapo Ngesa aliingia katikati ya miti na kupotea.Akaruka mitaro lakini alivyochungulia ufukweni mwa bahari akaona watu wanaogelea akasogea karibu na kuchukuwa nguo zao.

“Inabidi nibadili hizi nguo”

Ngesa akaiba nguo akaingia kichakani na kuzivaa,akatokeza barabarani alichoona ni Difenda za polisi bado zinapita alijuwa bado wanasakwa.

“Psiii psiii,Boda”

Pikipiki iliyokuwa inapita aliisimamisha,ikasimama Ngesa akatembea mpaka karibu yake.

“Nipeleke mlalakuwa,bei gani?”

“Kule elfu kumi na mbili”

“Poa twende”

“Kwanini tusipite huku Kariakoo kuna mtu naenda kumuangalia mara moja”

Dereva akatii amri ya abiria wake,alifurahi kupata pesa nyingi siku hiyo ndiyo maana akatabasamu.

Hakuelewa Ngesa ana mahesabu gani kichwani mwake laiti kama angejuwa asingempakia kwenye pikipiki yake.

Pikipiki ikazidi kuingia mitaani,dereva akajichanganya kupita kichochoroni walivyofika maeneo ya Upanga nia yake ilikuwa ni kufupisha njia bila kuelewa anamrahisishia Ngesa hesabu zake.

“Embu simama kidogo hapo,mkojo umenibana”

“Poa bro fanya fasta basi”

“Poa”

Pikipiki ikasimama Ngesa akashuka,hapohapo akamvaa dereva akamshusha na kumtwanga kichwa kikali na ngumi moja nzito ya pua na mtama juu,dereva akawa anaona nyota pua yake ilikuwa ikivuta sio mchezo,kitendo cha kufumbua macho yake hakuona pikipiki yake,tayari Ngesa alikuwa ameondoka nayo.

***

Ngesa alitamani pikipiki ipae jinsi alivyokuwa akikimbiza ilitisha,alikunja kona na kuingia maeneo ya jangwani akiwa katika kasi ileile.Ilikuwa ni lazima afike Kinondoni B block 41 akaonane na mwanamke anayeitwa Martha Msoso,ilikuwa ni lazima ajuwe ukweli,kifo cha Tonny Benjamin kilimuuma ajabu.

Dakika kumi na sita baadaye alikuwa Kinondoni Block 41, akapunguza mwendo akasimama na kuangaza huku na kule,akakumbuka maelekezo ya Mh.Frank Man’sai.Akaona geti la rangi nyeusi nyumba namba 16k upande wake wa kushoto,akaweka pikipiki kando.Akateremka na kuanza kuizunguka nyumba ili kukagua ni jinsi gani aingie, hakutaka kuingilia getini akihofia maswali,akatembea mpaka nyuma ya nyumba.


Akaangalia huku na kule akaurukia ukuta na kuanza kuchungulia ndani,alivyoona hakuna dalili ya mtu akajivuta na kuingia ndani,akatua kiutalaam kama ninja bila kutoa kishindo,akatembea na kuingia mlango wa uwani.

“Yeah baby nimeshafika nyumbani sasa hivi…Nakumisi tu,week end bwana tutaonana..Hata kama… yes sio hivyo bwana..”

Ngesa alisikia sauti hiyo ikitokea ndani ya chumba kilichokuwa upande wake wa kulia,akatulia aliogopa kuingia sababu mwanamke huyo alikuwa akiongea na simu kumaanisha akiingia kwa pupa atasababisha operesheni yake iwe ngumu.Akatulia mlangoni akasikia Mwanamke huyo anatembea akafungua mlango.

“Tulia hivyo hivyo usipige kelele,ingia ndani”

Sura ndiyo ilikuwa ileile sababu alimuona kwenye Kompyuta ya Mh.Frank Man’sai masaa machache yaliyopita,Ngesa akafunga mlango kwa funguo.

“Una una taka nini wewe ni nani?”

“Nataka kujuwa ukweli na sina muda wa kupoteza nani kamuuwa Tonny Benjamin?”

“Ni Mh.Frank Man’sai,nilisikia jana kwenye taarifa ya ha…”

Martha Msoso alikatishwa na kofi kali la shavu akayumba na kudondoka chali,kanga yake ikamtoka mwilini akabaki na chupi na sidiria peke yake.

Ngesa hakuishia hapo akazikamata nywele zake akamsimamisha na kukikamata kichwa chake vizuri akakipigiza juu ya meza ya kioo iliyokuwa na vipodozi mpaka ikapasuka.

Tayari hasira zilikuwa zimemkaba kohoni alihema kwa fujo akamvuta na kumbamiza ukutani.

“Ongea ukweli nani kamuuwa Tonny Benjamin?nitajie Malaya wewe,NITAKUUWA”

Ngesa alifoka macho yake yalikuwa mekundu tayari,anatetemeka kwa hasira.Martha alikuwa akivuja damu usoni vioo vilikuwa vimemkata vibaya sana,Ngesa akam-buluza mpaka ukutani na kumuwekea mkono shingoni, akalibana koo lake la hewa.

“Nani kakutuma upige picha upate mwandiko wa Mh.Frank Man’sai?Naniiiii?”

“Ni..nii ni….anait..wa Vit…l Kam..e..re”

“Ndio nini? sikusikii,Ongea kwa sauti”

“Vitaaal Kameree”

Martha Msoso alitaja jina hilo kwa tabu sana, koo lake la hewa likiwa limebanwa ukutani na mkono wa Mwanaume huyu wa shoka, DERICK NGESA!




“Vaa nguo zako unipeleke”

“Si tayari nishakuelekeza anapoishi?”

“Nimekwambia vaa nguo unipeleke kwake”

Ngesa alisisitiza tena akiwa amesimama anamuangalia Mwanamke aliyekuwa mbele yake amevaa chupi na Sidiria,anavuja damu usoni.

Alikuwa ana hasira kupita kiasi,tayari alishajuwa jina la mtu aliyefanya ukatili huo na ilikuwa ni lazima ale naye sahani moja.Martha Msoso akachukuwa nguo zake na kuingia bafuni ambapo alivyotoka alikuwa tayari keshajiandaa na kujipangusa damu usoni,wakatoka chumbani na kufika seblen.

“Una gari?”

Ngesa akageuka na kumuuliza.

“Nd..io hapana”

Martha akajibu huku akibabaika kidogo,Ngesa akatembea mpaka dirishani na kufungua pazia,akaona gari aina ya Vitz lipo nje.

“Usinijaribu,nipe funguo za gari.Fanya haraka”

Martha akatembea mpaka kabatini akachukuwa funguo za gari na kumkabidhi Ngesa, ambapo walitoka nje,akatembea mpaka nje ya geti akatizama huku na kule kuangalia usalama akarudi ndani na kufungua geti baada ya hapo akazama ndani ya gari akashikilia usukani akalitoa gari nje.

“Anaishi wapi?”

Lilikuwa ni swali kutoka kwa Ngesa akiwa nyuma ya usukani,hakuonesha sura ya kucheka hiyo ikamfanya Martha atandwe na hofu.

Alihofia maisha yake sababu aliambiwa akitoboa siri atauwawa kwa njia moja ama nyingine ndiyo maana alitetemeka akihofia uhai wake,alimuelewa vizuri mfanyabiashara huyo aliyeitwa Vital Kamere jinsi alivyokuwa na mtandao mkubwa jijini Dar es salaam kwa maana hiyo asingeweza kumkimbia.

“Oysterbay”

“Oysterbay ni kubwa”

“Oysterbay polisi pale tukifika nitakuelekeza”

Ndani ya gari hakukuwa na mazungumzo yoyote yale kichwa cha Ngesa kilijawa msongo wa mawazo alielewa kwa wakati huo angekuwa anatafutwa na alitakiwa akimalize mapema kitu alichokianza,alikuwa ana usongo wa kumuweka Vital Kamere mikononi mwake hakuelewa angemfanya nini,tayari walikuwa wamefika Msasani wakapita kituo kilichoitwa macho wakaingia kulia ili kufupisha njia.

Walivyofika Oysterbay polisi, Martha ndiyo akawa ana kazi ya kutoa ramani ya kufika nyumbani kwa Mzee Vital Kamere.

“Pale kwenye geti jeusi”

Martha akasema huku akisonta kidole mbele.

“Kwenye lile gorofa jeupe?”

Ngesa akauliza huku akijaribu kuvuta kumbukumbu zake nyuma sababu alishawahi kuingia ndani ya nyumba hiyo akiwa na tajiri yake,Mr.Magembe.Alikusanya vitu vingi nyuma kompyuta ya kichwani kwake ikazidi kupekua mafaili ya kumbukumbu,ni kweli alikuwa sahihi nyumba hiyo haikuweza kumtoka.Akaweka gari kando.

“Una uhakika ndiyo hapa?”

“Sina sababu ya kukudanganya”

“Okay nisubiri”

Ngesa akazima gari akachomoa funguo na kushuka,akatembea mpaka getini.

“KAMA UPO NDANI USIFUNGUE MLANGO,KUNA KITU KIMETOKEA KAMA UNA MUDA NIPIGIE TAFADHALI”

Martha Msoso alituma ujumbe haraka kwa Mr. Vital Kamere,hazikupita hata dakika tano simu yake ikaita akamuangalia Ngesa aliyekuwa getini akapokea simu kwa tahadhari.

“Halloo,upo wapi?usifungue geti kuna mtu ameniteka nyara amenitishia kuniua amejua kila kitu kuhusu kifo cha Tonny Benjamin”

Martha Msoso aliongea haraka kama cherehani iliyotiwa mafuta ya grisi.

“Sikusikii vizuri subiri nitoke kwenye kelele…”

Baada ya kama sekunde tisa Vital Kamere akarudi kwenye laini.

“Ulikuwa unasemaje?sijakuelewa”

Harakaharaka akaanza kujielezea kila kilichotokea kwa kifupi.

“Nipo kwenye msiba hapa,usijali ahsante kwa taarifa”

Hapohapo simu ikakatwa,akamuona Ngesa anatembea anarudi, alivyolifikia gari akaingia.

“Nimeambiwa yupo kwenye msiba,mpigie simu mwambie unahitaji kuonana naye hapa nyumbani kwake”

“Laki..”

“Fanya hivyo”

Huo ulikuwa mtihani mwingine kwa Martha.

***

Rais Leslie Benjamin alizungukwa na viongozi wa nchi na wengine kutoka nchi jirani wakimpa pole,siku hiyo alikuwa akilia kama mtoto mdogo kwa kuondokewa na mdogo wake wa pekee,alikuwa nyumbani kwa Mdogo wake marehemu Tonny Benjamin hapo ndipo ndugu jamaa na marafiki walipokusanyika.Bado hakuamini kwamba hatomuona tena katika maisha yake.Muda wote alikuwa ameinama ameweka kitambaa usoni,anakoroma kwa kulia.Hata walivyom-bembeleza ilikuwa kazi bure,alilia kama mwanamke, hakuweza kujikaza kisabuni hata kidogo.

“Pole sana Muheshimiwa Raisi,ni kazi ya mwenyezi Mungu”

Ilikuwa ni sauti ya Waziri mkuu wa Tanzania Mh. Emmanuel Kauwedi Mrosso huku akimpiga piga begani hata yeye aliguswa,msiba ulijaza umati wa watu na wengi wao pia walikuwa wafanyabiashara wakubwa kama Johnson Masangula,Mohamed Utaly na Vital Kamere hao walikuwa pia pembeni ya Raisi Leslie Benjamin wanampa pole ya kufiwa,ulikuwa ni msiba mzito uliotingisha nchi ya Tanzania kwa ujumla.

Msiba ulitangazwa na kuwafikia nchi jirani kama Kenya na Uganda ndiyo maana hata baadhi ya viongozi wa nchi jirani walisafiri na kwenda kumpa pole.

Katika watu wote zaidi ya mia walioudhuria kuna mmoja wao alikuwa akisikitika kinafki sababu alikuwa anajuwa kila kitu,hakuwa mwingine bali ni Vital Kamere alijifanya kuguswa sana.

“Mara ya mwisho kuonana na Marehemu Tonny ilikuwa kwenye mkutano wa UWARIDI tulivyokuwa na Ibrahim Gama na akina Suleiman Kijogoo,aliongea vitu vingi sana.Hapa ninavyoongea siamini kabisa”

Huwezi kujuwa kilichokuwa ndani ya mtu kwa macho sababu maneno aliyokuwa anaongea Vital Kamere yalikuwa ni tofauti kabisa,yeye ndiye aliyehusika kumuua akajifanya ana masikitiko makubwa sana.Kilichomshtua ni ujumbe wa simu kutoka kwa Martha akausoma juu na kufanya mapigo yake ya moyo yashtuke.

“Samahani kidogo naomba nikapige simu nje”

Vital Kamere alizungumza na kutoka nje ambapo aliwapangua wakina Mama na kutoka nje kabisa,hata huko kulikuwa na watu wengi,msongamano wa Magari ndiyo usiseme.Akatembea na kujificha nyuma ya gari moja wapo kisha kumpigia simu Martha ili kujuwa kila kitu kilivyokwenda.

Mambo aliyoambiwa na Martha yalimshtua na baada ya kukata simu alimpandia Brigedia Karanje hewani dakika hiyohiyo,akamueleza kila kilichotokea.

“Huo ni uzembe,nilikwambia baada ya kumtumia huyo mwanamke umuuwe”

“Mimi nilimwamini”

Vital Kamere alikuwa akiongea kwa sauti ya chini sana kama ananong’ona huku akitizama pande zote,mambo aliyokuwa anaongea kama angesikiwa kitanzi kingemuhusu sababu raisi Leslie alikuwa ana hasira na watu waliomuuwa mdogo wake.

“Utafanya hata operesheni nyingine zikwame,huyo mwanamke yuko wapi?”

“Nimeongea naye nimepanga kuonana naye nyumbani lakini siwezi kwenda ni hatari”

“Acha nilishughulikie hili swala,nitakupigia simu”

“Okay”

Vital Kamere alikata simu na kumuacha Brigedia Karanje akiwa katika mawazo mengi sana,alikasirika kupita kiasi. Hapohapo akachukuwa simu nyingine na kumtafuta Daphine hewani.

“Uko wapi?”

“Nipo nyumbani”

“Kuna kazi nataka ukafanye”

“Sawa,wapi?”

Hilo ndilo jambo lililomfurahisha Brigedia Karanje,Daphine siku zote alikuwa tayari kufanya matukio hata kama angekurupushwa usiku wa saa saba,angetii amri bila kuuliza ni kazi gani.

“Nyumbani kwa Kamere kuna nzi fulani wanataka kuleta shida”

“Nyumbani kwa Dad?”

“Ndio,wanataka kumuuwa.Bastola yako bado ina risasi?”

“Za kutosha,mara nyingi sipendi kutumia silaha lakini nitaenda nayo.Just incase”

“Ukifika nyumbani kwa Vital Kamere nipigie simu,kitu kingine…”

“Yes”

“Usisahau kuvaa mask”

“Okay”

Simu ilivyokatwa,Daphine akainuka kutoka kitandani akafungua kabati na kutoa bastola yake,akachomoa ‘magazine’ kukagua kama risasi zipo za kutosha.Risasi zilikuwa zimepungua akafungua ‘draw’ lingine na kuchukuwa magazine nyingine ambayo ilikuwa amejaa risasi,akabeba kiwambo cha kuzuiwa kelele akakichomeka mbele.

“Kacha kacha”Mlio wa bastola kukikowa ulisikika,akaweka bastola kitandani akaingia bafuni kujimwagia maji,alivyotoka akaingia kabatini na kuvaa nguo zake nyeusi na chini kiatu aina ya ‘All star’ iliyopanda juu,hiyo pia ilikuwa ya rangi nyeusi,akavaa na ‘gloves’ mikononi,akashusha pumzi ndefu akachukuwa bastola na kuiweka nyuma ya kiuno chake akavaa koti na kuifunika,akachukuwa begi lake dogo lenye baadhi ya vitu vyake vya kazi na kulivaa,akatoka mpaka nje na kuingia ndani ya gari lake ambapo alianza safari ya kwenda nyumba kwa Vital Kamere,mzee aliyemuheshimu na aliyemsomesha na kumuonesha njia zote, kwa maana hiyo kuambiwa kwamba kuna watu wanataka kumuuwa alikuwa ana mori ya kuwawahi ili awavamie,aliendesha gari akitamani kufika mapema,Msongamano wa magari ulikuwepo Magomeni Mikumi ndiyo ulifanya aone muda unakwenda ingawa alivuta subira,taa za kijani zilivyowaka akaweka gia akazidi kusonga mbele.


Dakika thelathini baadaye akawa amefika Oysterbay akakunja kona na kuiacha barabara kubwa,ambapo kwa mbali aliliona gari aina ya vitz.Hapohapo akatoa simu na kumpigia Brigedia Karanje kumwambia kwamba keshafika.

“Nipo hapa jirani tayari kama mita hamsini hivi”

“Sawa usikate simu,Ngoja nikuunganishe na Kamere”

“Okay”

Walikuwa hewani kwa kama sekunde hamsini ndipo Vital kamere akawa kwenye laini,wakawa watatu kwenye mazungumzo yaani Brigedia Karanje,Daphine pamoja na Vital Kamere.

“Halloo”

“Yes Shikamoo Dad”

“Oh Marahaba Mwanangu hujambo?”

“Sijambo,Anco Karanje amenielekeza kila kitu.Ni kweli Dad?”

“Ndio Mwanangu”

“Nishafika hapa kwako,nasubiri maelekezo”

“Mr. Kamere”

Brigedia Karanje akaingilia mazungumzo.

“Yes”

“Hao watu bado wapo?”

“Ndio huyu binti kaniambia yupo kwenye gari yake,anatumia vitz rangi ya silver”

“Nimeiona hapa Dad,bado ipo”

Daphine akadakia,hapohapo akazungusha usukani na kuweka gari kando.

Vitz aliitizama mbele yake ikiwa umbali wa mita kama ishirini.

“Unajuwa cha kufanya nadhani”

“Ndio”

“Goodluck and take care”

Brigedia Karanje alisema akimsisitiza Daphine awe makini na kitu anachotaka kukifanya.

***

Muda ulizidi kwenda mbele akiwa ndani ya gari yupo na Martha wanamsubiri Vital Kamere atokee ili amuweke chini ya ulinzi lakini hakutokea,hivyo ndivyo Martha alivyoongea naye kupitia simu kwamba amsubiri.Ngesa hakuelewa kwamba alikuwa kwenye mtego mkali,ilivyofika saa kumi na moja ya jioni bado hakukuwa na dalili za Vital Kamere kutokea,magari yalikuwa yakipita lakini kilichomshtua Ngesa ni gari aina ya ALTEZA nyeusi sana,vioo vyake vilikuwa hivyohivyo pia yaani tinted,ilikuwa imesimama nyuma yao mbali kidogo na hakuna mtu yoyote aliyeshuka ndani ya gari.

Kuna kitu alianza kukihisi lakini hakutaka kuyapa mawazo yake kipaumbele ingawa macho yake mara kadhaa aliyatupa kwenye ‘site mirror’muda wote alikaa kimachale,macho yake hayakutulia.

Giza likazidi kuingia.Kama Mungu vile,kitu kikamwambia aangalie tena kwenye ‘site mirror’ akamuona mtu analisogelea gari alilokuwepo ndani ingawa hakuweza kumuona sura sababu ya giza,akayalazimisha macho yake,kivuli kikazidi kusogea karibu zaidi.Moyo wake ukapiga paa!Alivyoona kivuli cha bastola.

“Marthaaaa…Pyuuu pyuuuuuu pyuuuuu”

Ngesa alipiga kelele kumshtua Martha pembeni yake lakini alikuwa amechelewa tayari kwani alipigwa risasi za kichwa na damu zikaruka na kutapakaa kwenye vioo,ubongo wa Martha ukawa umechenguliwa na risasi tatu,kilichomsaidia yeye ni kufungua mlango na kuruka nje kwa kasi ya mwewe,risasi zilimkosakosa zikampitia juu ya kisogo vioo vikamrukia kichwani.

“Pyuu pyuuuu”

Daphine aliendelea kulipiga risasi gari,akimtafuta mwanaume aliyeshuka.

Ilikuwa ni lazima awauwe wote.Ngesa alikuwa upande wa pili amelala kifudifudi juu ya mchanga,moyo wake ulikuwa ukidunda kwa nguvu mno.Daphine nayeye alikuwa akitembea taratibu kuzunguka upande wa pili bastola kaishika kwa mikono miwili,kifupi walikuwa wakiwindana.

Ngesa ndiyo alikuwa ana hofu mno sababu hakuwa na silaha yoyote ya kujitetea.

“Pyuu pyuuuuu pyuuuu”

Daphine alizidi kurusha risasi,Ngesa akazidi kuogopa,wazo likamjia akajibuluza mpaka chini ya uvungu wa gari akawa anaona viatu vya jambazi huyu anayetaka kuutowa uhai wake,akajivuta taratibu.

Alivyohakikisha amekaa vizuri,akaikamata miguu ya Daphine na kuivuta kwa nguvu,Daphine akadondoka chini chali bastola yake ikaenda kando,Ngesa akasimama kwa kasi ya umeme,alivyotaka kumvaa Daphine akamkosa sababu Daphine alijibiringisha nayeye akasimama.

Akakunja ngumi akatisha kama anarusha ngumi ya kushoto ili kumzuga,Ngesa akababaika ikarushwa ngumi ya mkono wa kulia ikamfikia kwenye taya,kabla ya kukaa sawa alirukiwa ‘round kick’ ambapo teke lilimfikia kichwani akajibamiza kwenye kioo cha gari.

Daphine hakuishia hapo alirusha teke lingine lakini hilo halikuzaa matunda kwani Ngesa aliliona na kuinama chini,likapita hewani.Nayeye akakaa sawa, alishaelewa tayari mtu anayepambana naye ana mafunzo ya kutosha hivyo ilibidi awe makini mno,Ngesa alizidi kumuangalia mpinzani wake huku akikunja ngumi taratibu akiwa mwenye hasira!



Kila mtu alikuwa makini kupita kiasi,akimtizama mwenzake kuanzia juu mpaka chini,Ngesa alishindwa kuona sura ya mtu anayepambana naye kutokana na uso wake kuzibwa,macho ndiyo yalikuwa yanaonekana,lakini alivyomuangalia kifuani vizuri akagundua kwamba anayepambana naye ni mwanamke,kabla ya kuendelea kutafakari zaidi aliona ngumi inakuja upande wa kulia,akahepa kushoto.

Ngesa akazunguka kiutaalam na kurusha teke ambalo lilimfikia Daphine shingoni akayumba kidogo,hapohapo akapokea teke lingine la tumbo,akaserereka upande wa pili,ambapo alidondoka chini chali,alivyopiga jicho pembeni aliona bastola yake ipo karibu,akaiwahi lakini kabla ya kufanya chochote mkono wake ulioshika bastola ulipigwa teke na Ngesa bastola ikaruka mbali.Akamshika vizuri na kumburuza na kukibamiza kichwa chake juu ya boneti la gari.Tayari Daphine alikuwa amezidiwa ingawa hakutaka kukubali swala hilo, lilikuwa ni jambo la aibu sana kwake,hakuelewa angemjibu nini mkuu wake wa kazi endapo hatomuuwa mtu huyu anayepambana naye,anayeonekana ni mkali wa ngumi.Kichwa chake kilikuwa kinabamizwa juu ya boneti la gari,kilivyotakwa kubamizwa mara ya nne akaweka mikono juu kuzuia jambo hilo lisiendelee tena, hapohapo akamzungusha Ngesa na kumtwangwa kichwa cha pua kikali sana,akapanda juu ya gari na kuruka teke ambalo lilitua juu ya kifua cha Ngesa,akadondoka puu! kama gunia,Ngesa akashikwa vizuri akaanza kupigwa ngumi zisizokuwa na idadi kamili za usoni,mpaka zinapita sekunde tatu alikuwa tayari amechanika mdomo damu zinamvuja,Daphine alimvuta na kumkaba shingoni nia yake ilikuwa ni kum-maliza kabisa,amvunje shingo amuuwe.

Daphine alikuwa nyuma,Ngesa kapiga magoti,shingo yake inakabwa,alijaribu kuutoa mkono wa Daphine lakini alishindwa, alihisi nguvu zinamuishia taratibu.Macho yakazidi kumtoka,alihisi kinyesi kinam-bana alielewa fika kwamba hiyo ni dalili ya umauti kumfika.

“Agrrr aagrrr”

Ngesaalikuwa akikoroma kama kondoo anayechinjwa,hiyo ilimaanisha kuwa pumzi zake zimeanza kukata huku akizidi kurusha rusha mikono yake.Ilikuwa ni kama Mungu alikuwa upande wake,mwanga wa taa za gari kuanza kumulika,kuna gari lilikuwa linakatiza kwa mbali.Daphine alifanya kosa kubwa sana kushtuka na kulegeza roba,hapo ndipo Ngesa aliinuka kwa nguvu,kichwa chake kikamgonga Daphine chini ya kidevu akayumba, ili kujiokoa,hapohapo Ngesa akarukia bastola.

“Pyuu pyuuu”

Daphine alipanda juu ya gari na kuruka beki yaani sambasoti kama Ninja,akatokea upande wa pili kuelekea kwenye gari lake.

“Pyuu pyuu pyuuu”

Ngesa alizidi kurusha risasi,Jinsi Daphine alivyoingia ndani ya gari ilitisha.Alipiga gia ya kurudi kinyumenyume,akakanyaga mafuta mpaka mwisho matairi yakazunguka.

“Pyu pyuuu”

Ngesa alikuwa mbele ya gari anamkimbiza huku akirusha risasi kwenye gari ambapo risasi zilikuwa zinapasua kioo cha mbele,Daphine alikuwa ameweka kichwa chake chini vioo vinamrukia huku akizidi kurudisha gari nyuma.

“Piiii piiiiiiiii”

Aliingia barabara kubwa bila kuangalia ambapo gari aina ya Mark II grande ilipiga honi,na kuligonga gari la Daphine kwa nyuma.Daphine hakujali akazungusha usukani gari likazunguka,akaweka gia namba moja na kuserereka kwa kasi ya ajabu.

***

Mbele alikuwa amesimama mkuu wake Brigedia Karanje,amekunja sura ajabu habari za Daphine kufanya uzembe zilimkera kwa kiasi cha kutosha,katika maisha yake kitu uzembe kilikuwa adui yake.Ndio maana Daphine alipiga magoti mbele yake akiomba msamaha kwa kosa alilofanya.

“Kitu gani kilikufanya ushindwe kumuuwa huyo kijana?”

Brigedia Karanje alimuuliza Daphine macho yake yalikuwa mekundu kama mtu aliyevuta ganja!

“Mkuu na..”

Daphine alijaribu kujitetea lakini alitulizwa na teke la kifua lililomfanya adondoke chali,Brigedia Karanje alimsogelea na kumvuta kwa juu akampiga kofi kali,Daphine aliyumba na kudondoka tena hakuishia hapo, Brigedia Karanje alimpiga Daphine vibaya sana,wenzake walivyojaribu kumshika walisukumizwa mbali,Daphine alihisi maumivu makali sana akiwa chini licha ya yote aliamini kuwa anastahili adhabu kwa uzembe alioufanya.

“Simama Juuu”

Brigedia akatoa amri,Daphine akasimama huku akiwa anavuja damu puani na mdomoni, jicho limemvimba na lingine limevulia damu,alitia huruma.

“Mimi nikimtuma mtu kazi nahitaji ifanywe kwa umakini,umenielewa?”

“Ndio m..kuu”

****

Maiti iliyokutwa ndani ya gari aina ya Vitz imepigwa risasi ilizuwa hali ya sintofahamu kwa wakazi wa eneo la Oysterbay baada ya kupambazuka,ilibidi simu ipigwe moja kwa moja kituo cha polisi Oysterbay ambapo Difenda tatu zilifika na maaskari wakashuka hata wao walipigwa na butwaa, hawakuelewa ni saa ngapi risasi zilifyatuliwa.

“Jamani tunaomba mkae mbali na eneo la tukio”

Askari mmoja aliyefahamika kwa jina la Kamanda Wilson Kibaigwa alitoa kauli hiyo na kupita moja kwa moja mpaka ndani ya gari,alivyoangalia chini aliona makasha ya risasi,akazidi kuchunguza alivyopiga jicho kwa mbali aliona vioo vipo chini vimepasuka.

“Inaelekea hawa majambazi walikuja na gari,hivi ni vioo vilivyopasuka”

Askari wengine wakasogea na kuzidi kuona makasha ya risasi,wakazidi kudadisi na kupiga picha za maiti ya mwanamke aliyekuwa ndani ya gari kichwa chake kimechenguliwa na risasi.

“Unalitambua hili gari?”

Kijana mmoja aliulizwa,akalitizama gari aina ya Vitz kwa kitambo kidogo.

“Hapana kwa kweli”

“Mimi nalifahamu”

Msichana mmoja akadaika,askari akamsogelea.

“Kivipi?”

“Mara ya mwisho nililiona linaingia kwenye ile nyumba pale ya Mr.Kamere”

“Unataka kuniambia huu mtaa hakuna mwenye gari kama hili?”

“Hapana,nina uhakika”

“Sawa,ahsante”

Ingawa Jeshi la polisi walipata jibu lakini hawakuridhika,waliendelea kuwahoji wakazi wa oysterbay maswali kisha baada ya lisaa limoja wakaipakia maiti ndani ya gari kwa ajili ya uchunguzi wa kina.

****

“Pangalaaaaa”

Mlio wa kioo cha gari kikiwa kimepasuliwa ndio uliosikika,baada ya kupigwa na jiwe.Alikuwa ni Ngesa baada ya kutoka kupambana usiku huo, alitembea umbali wa kama mita kumi, aliona magari yameegeshwa akachukuwa jiwe na kuvunja kwa nia ya kujaribu kuiba.Alivyopasua kioo akapenyeza mkono wake ndani ya dirisha na kufungua kitasa,akazama ndani.Akitumia kitako cha bastola akaanza kupiga piga sehemu ya kuchomokea funguo za gari.Sehemu hiyo ilivyopasuka akavuta nyaya mbili hasi na chanya,akang’ata na kuzichubua kisha akazigusisha.

Gari ikawaka hapohapo,akapiga gia na kuondoka zake,bado alihisi shingo yake inamuuma kupita kiasi,hakutaka kuelekea sehemu nyingine usiku huo,alitaka kuingia Bagamoyo.

Hivyo alikimbiza gari usiku huo mpaka alivyofika Bagamoyo kwa Bwana Gabriel.

Akagonga mlango na kufunguliwa.

“Ngesa,vipi?Nini kimetokea?”

Gabriel aliuliza maswali mfululizo baada ya kumuona Ngesa amelowa damu.

“Naomba maji ya kuoga kwanza na chakula”

“Sawa”

Hicho ndicho kitu kilichotokea,Ngesa aliingia bafuni na kujimwagia maji.Na baadaye kuanza kula chakula,akashushia na maji.

“Ahsante sana”

“Niambie nini kimetokea?”

Ngesa alianza kusimulia kila kitu kilivyokwenda kinagaubaga,mpaka akaachana na Mh.Frank Man’sai daraja la salenda,Gabriel alikuwa makini akisikiliza kila nukta ya sentensi,masikio yake alikuwa ameyatega kama anasikiliza habari za vifo redioni.

“Ndio hivyo”

Ngesa akahitimisha na kuingia chumbani ambapo alirudi na simu.

“Hii simu ya huyo Martha,humu nitapata kitu”

Alivyoingia kwenye uwanja wa meseji alishtuka.

“KAMA UPO NDANI USIFUNGUE MLANGO,KUNA KITU KIMETOKEA KAMA UNA MUDA NIPIGIE TAFADHALI”

Ujumbe huo ulimshtua alivyoangalia ulitumwa kwenda wapi,aligundua kwa Vital Kamere.Akazidi kuchokonoa kila namba na ujumbe.

“KAZI YENU TAYARI MZIGO WANGU INGIZENI HUMU 300311122063 EQUITY BANK,MARTHA MSOSO”

Kilichomzindua kutoka kwenye simu ni habari iliyoanzwa kutangazwa kwenye luninga,sura ya Mh.Frank Man’sai ilitokea huku akiwa amepigwa pingu.

“Mh Frank Man’sai ameshikiliwa tena na jeshi la polisi baada ya kujaribu kutoroka kituo cha polisi,Saidi Karim ana habari kamili”

Macho ya Ngesa yalikuwa kodo juu ya kioo cha televisheni akamuona Mh.Frank Man’sai anaingizwa ndani ya gari,kutokea daraja la salenda alipomuacha.

“Hii habari ya lini?”

Ngesa akamuuliza Gabriel.

“Jana,haya ni marudio”

“Shit”

Ngesa akakema kwa hasira,kukamatwa kwa Muheshimiwa huyo aliamini kwamba ni kosa kubwa sana sababu hakuwa na hatia yoyote ile,ilikuwa ni lazima afanye mambo haraka ili amuweke Mh.Frank Man’sai huru.Baada ya hapo sura ya Ngesa ilionekana juu ya kioo cha luninga akiwa anatafutwa hakuelewa ni kivipi waliipata sura yake.

“Wananitafuta,inabidi nifanye jambo hili haraka sana”

“Ni kweli”

Ngesa alitembea mpaka chumbani akijaribu kupanga mikakati ya kumsaka Mr.Vital Kamere,hapohapo sura ya tajiri yake Magembe ikamjia,sababu huyo ndiye aliyeenda naye mpaka nyumbani kwa mfanyabiashara huyo hakuelewa kama nayeye alikuwa miongoni mwao ama la!


“Ndio ndio afande nipo naye hapa Bagamoyo hapa vijibweni nyumba namba 10,ndiyo yupo ndani kwangu njoeni haraka”

Alikuwa ni Gabriel akiongea na mmoja wa askari aliyekuwa kituo kikubwa cha polisi Bagamoyo,akitoa unoko, pesa alizoziona kwenye televisheni zilimtoa udenda,kwake zilikuwa kama za bure sababu Ngesa alikuwa ndani kwake,kumchoma kwa maaskari ilikuwa ni sawa na kulala maskini na kuamka tajiri.

Hakuelewa kwamba Ngesa alikuwa kwenye korido amejibanza kama paka shume na kila alichokuwa anazungumza alisikia.Hakutaka kuamini kama Gabriel anafanya kitu kama hicho!

“Ulikuwa unaongea nani?”

Ngesa akauliza baada ya kutokeza.

“Ah,rafiki yangu mmoja hivi anaitwa Kennedy yupo Shinyanga.Tuachane na mambo ya simu,inabidi uwasake wahalifu Ngesa,bila kufanya hivyo Mh.Mansai atakuwa matatani namimi nakuunga mkono nipo nawewe bega kwa bega”

Gabriel alianza kuongea vitu vingi hakuelewa kwamba Ngesa alimsikiliza kila kitu na alikuwa akimchora.Ngesa akamkata jicho kali la hasira hakuelewa amfanye nini mwanaume huyu mnafki!



Picha ya Ngesa ilibandikwa kila kona ya jiji la Dar es salaam na baadhi ya mikoa kama Iringa,Arusha,Morogoro,Mbeya na kwingineko, alikuwa akitafutwa na jeshi la Polisi kwa wudi na Uvumba.Jiji la Dar es salaam lilichambuliwa kama Karanga watu walitolewa vyumbani mwao,polisi walidiriki kuingia mpaka uvunguni mwa vitanda kumsaka Ngesa,ndani ya daladala watu walipekuana.Ngesa alitafutwa kama Almas sababu kupatikana kwake ilikuwa ni sawa na kuokota kipande cha dhahabu jangwani,picha yake chini iliambatana na kiasi cha shilingi milioni mia moja na hamsini endapo mtu yoyote akimpata jambazi huyo sugu basi kiasi hicho cha pesa kingekuwa halali yake.

Ndiyo maana hata ndani ya madaladala kila mtu alimuangalia abiria mwenzake vizuri kama hakuwa Ngesa.

Raisi Leslie Benjamin alikasirika vibaya sana,swala hilo akawakabidhi mpaka wanajeshi alivyoona polisi wameshindwa kufanikisha operesheni hiyo.

****

“Hii sura mbona sio ngeni?”

Lilikuwa ni swali kutoka kwa Brigedia Karanje akiwa na Picha ya Ngesa mkononi mwake,kumbukumbuku zake zikasafiri nyuma kwa kasi ya umeme,akakumbuka tukio zima lililotokea mkoani Morogoro.Ngesa alitakiwa auwawe baada ya kumtetea mtoto mchanga.Nayeye ndiye aliyehusika kumtesa na aliamini kwamba kijana huyo alikufa miaka mingi iliyopita,haikuwezekana hata kidogo awe hai.

“Nitafutie Luteni Kayahira haraka sana anipe maelezo”

Ndani ya kambi ya Jeshi la Lugalo siku hiyo hapakutosha,Brigredia Karanje alikasirika kwa kiasi cha kutosha uhai wa Ngesa ulimaanisha mambo yake yangeyumba siku moja sababu yeye ndiye alikuwa ana jua baadhi ya siri zilizotokea miaka mingi ya nyuma iliyopita.Mwanajeshi mfupi mwingine akaingia ofisini kwake akiwa mwenye wasiwasi mkubwa sana,akachapa mguu chini na kupiga saluti kama kutoa heshima kwa mkubwa wake wa kazi.

“Unaweza ukanieleza juu ya hili?”

Brigedia Karanje akaweka picha ya Ngesa juu ya meza,Luteni Kayahira akaitizama kwa umakini.

“Huyu kijana tulimtupa Uganda msitu wa Mabira ni lazima atakuwa ameliwa na Simba”

“Ameliwa na Simba yupi?”

“Simba mkuu. Wa porini”

“Huyu kijana yupo hapa Dar es salaam atafutwe kabla polisi hawajamtia mikononi mwao,jambo hilo lifanyike ndani ya masaa ishirini na manne.Nadhani unajuwa nini maana yake endapo hautompata”

“Ndiyo mkuu”

Yalikuwa ni maneno ya kutisha kutoka kwa Barigedia Karanje,na kauli hiyo Luteni Kayahila aliifahamu fika sababu alishawahi kuwashuhudia wenzake wakipigwa risasi na kufa mbele yake ambao waliokuja na kusema kwamba wameshindwa kutekeleza jambo.

Luteni Kayahira akashusha pumzi ndefu ya uwoga na alivyokaribia kuufikia mlango wa ofisi,akaitwa.

“Hey”

Akageuka.

“Nimesikia kwamba jambo hili pia jeshi limeshirikishwa,nani anaongoza hiyo operesheni?”

“Major General Mkuu”

“Unamsemea Nomba?”

“Ndiyo”

“Hakikisha nawewe unaingia kwenye hiyo operesheni”

“Sawa mkuu”

Luteni Kayahira akasukuma mlango na kutoka nje.

*****

“Agrriii agriiiiiii agriii”

Ni sauti inayokoroma mithili ya mbuzi anayenjiwa ndiyo ilikuwa inasikika ndani ya gari,alikuwa ni Gabriel akitoa sauti hiyo.Mikono ya Ngesa ilikuwa shingoni mwake inamkaba wapo ndani ya gari baada ya kumtoa usiku huohuo.

Hakutaka kubaki tena Bagamoyo akiamini kwamba polisi wangemkuta na angekamatwa.Ndiyo maana alikuwa amelikaba koo la hewa la Gabriel ili baada ya dakika nne apoteze fahamu amtupe,hakutaka kumuuwa sababu alikuwa ni mtu wake wa karibu.Gabriel alitupatupa miguu akijaribu kuutoa mkono wa Ngesa shingoni mwake lakini alishindwa.

“Tulia Gabriel,tulia”

Ngesa alisema huku akizidi kuukaza mkono wake,Mpaka Gabriel alipotulia.Akashuka ndani ya gari na kuzunguka upande wa pili,akamuweka begani na kuingia katikati ya mashamba ya mihogo akamlaza.

“Pumzika hapo ule mihogo na Viazi”

Ngesa akaangalia huku na kule na kuingia ndani ya gari,kulikuwa kumeshapambazuka saa kumi na moja ya asubuhi,akazidi kuendesha gari mpaka alivyofika Tegeta Mwisho,akashuka na kuweka uso wake chini ambapo alitembea mpaka kwenye soko linalouza nguo za mitumba.

“Hili sweta kiasi gani?”

“Buku sita hili”

“Poa,nipe na hiyo miwani nyeusi”

Muda wote Ngesa sura yake ilikuwa chini,hakutaka kuinua shingo yake kuhofia kujulikana kutokana na mwanga wa asubuhi kuchomoza.

Kuinua shingo yake kulimaanisha yeye kujiingiza kwenye matatizo.Kijana aliyekuwa anauza nguo za mitumba alimtizama Ngesa kwa kitambo kidogo.

“Kaka vitu vyako hivi hapa,buku tisa tu”

Muuza mitumba akazidi kumdadisi Ngesa,akainama kwa chini akizuga anachambua nguo.Sura aliyoiona mbele yake ilimshtua kupita kiasi,ndiyo hiyo ambayo ilikuwa inatangazwa katika vyombo vya habari mbalimbali.Tayari muuza mitumba aliona ametajirika,akapata kiwewe cha ghafla.

“Vipi?”

Ngesa akauliza baada ya kumuona Muuza mitumba mara ashike ichi mara aache kile.

“Hakuna kitu kaka”

“Nipe hilo sweta”

Muuza mitumba akatoa sweta na miwani akafunga na kumkabidhi Ngesa kisha hapohapo akatoa simu mfukoni ili kutafuta namba za polisi.

“Shika”

Ngesa akatoa noti ya shilingi elfu kumi na kuondoka zake,akaingia ndani ya gari na kuvaa sweta pamoja na Miwani ya rangi nyeusi,safari ya kuelekea Oysterbay nyumbani kwa Mr.Vital Kamere ndilo jambo alilokuwa anataka kulifanya kwa wakati huo,alijitizama kwenye kioo cha katikati akagundua kwamba ana mabadiliko ya kutosha na isingekuwa rahisi kwa mtu yoyote yule kumgundua.


Kitu kilichomfanya aingiwe na mashaka ni baada ya kufika ‘interchick’ kulikuwa na msongamano wa magari ajabu,jambo hilo lilimshangaza kwa sababu barabara hiyo haikuwa na historia ya kuweka msongamano kama huo.Magari yakaanza kusogea,alivyopiga jicho mbele akaona askari, tena wameshika picha mikononi mwao,akaangalia nyuma yake akaona kuna magari mengine.Magari yakazidi kusogea mpaka ikafika zamu yake.

“Habari za kazi?”

Afande mmoja akatoa salamu kwa Ngesa, kichwa chake kilikuwa chini.

“Nzuri”Akajibu.

Askari akapiga macho yake juu ya picha aliyoishika iliyokuwa na sura ya Ngesa.

“Vua miwani”Askari akaamuru huku akitingisha miguu yake akiangalia huku na kule.

“Vua miwani”

Akasema tena baada ya kuona dereva wa gari hilo ametulia.Ngesa alikuwa mbali kimawazo kuivua miwani yake kulimaanisha kukamatwa na hata asingevua angewekwa chini ya ulinzi pia,ilikuwa ni lazima afanye maamuzi magumu ya kijasusi tena kwa haraka.

“Wewe embu vu…”

Kabla ya askari kumalizia sentensi yake,kichwa chake kikavutwa ndani.Miguu yake ikiwa nje Ngesa akapiga gia na kurudisha gari nyuma,akaligonga gari aina ya Corola lililokuwa nyuma yake,akaweka gia namba moja na kuzungusha usukani ambapo alitanua na kuingia barabara ya vumbi.

Kichwa cha askari bado kilikuwa ndani,miguu yake ipo nje,alivyohakikisha kaingia barabara nyingine ya vumbi akamtupa askari nje akakamata usukani kwa mikono miwili.

Akazidi kutokomea mitaani.

Askari wote waliacha kazi ya msako wao,wakaingia kwenye difenda zao na kuanza kumfukuzia,kukimbia kwa gari hilo kulifanya wajuwe moja kwa moja huyo ndiye Ngesa wanayemtafuta.Hivyo walikuwa wana usongo mno.Jinsi Difenda za polisi zilivyokuwa zinakimbia ilitisha.Walivyoingia barabara isiyokuwa na lami vumbi lilitimka na kufanya watu wasionane!


Gari la Ngesa lilikuwa mbele yao mita kama ishirini na waliliona jinsi linavyokunja kona,wakalala nalo.

“Afande ukipata saiti nzuri piga risasi matairi”

Ilikuwa ni kauli kutoka kwa dereva wa difenda akimwambia mwenzake aliyekuwa upande wa kushoto,hata yeye alikuwa askari vilevile.

“Kacha kacha”

Askari wa kushoto akakoki bastola,hiyo ndiyo ilikuwa difenda inayoongoza msafara nyingine tano zipo nyuma zinatimua vumbi sio mchezo.

Ngesa alikuwa anaendesha gari kama mtu aliyevurugwa akili,alikanyaga mafuta mpaka mwisho na kupandisha gia mpaka nambari tano akizidi kupandisha milima na kushusha,kila alipopiga jicho nyuma yake aliona vumbi linatimka.Difenda za polisi zilikuwepo nyuma yake.

“Paaaaaa”

Risasi ya kwanza ilifyatuliwa na askari,ikapiga gari yake, vioo vya nyuma vikapasuka.Kwa mshtuko Ngesa akapoteza uelekeo lakini akajitahidi na kuweka usukani sawa.Akalala na kona moja ya kulia,gari ikazunguka na kupiga msele alimanusura agonge ukuta,akaweka gari sawa.Difenda iliyokuwa nyuma yake ilipojaribu kuiga,ikagonga ukuta.

Ngesa akazidi kunyoosha mguu gari ikazidi kuchomoka kwa kasi ya risasi.

“Paaaa paaaaa”

Jeshi la Polisi la Tanzania halikuwa na mchezo hata kidogo na askari wake walikuwa makini siku zote,baada ya kujuwa ni wapi Ngesa angetokea Difenda nyingine mbili zikapita njia nyingine kumlia denge,hapo ndipo walipoachia risasi mbili zikapasua tairi la gari analoendesha Ngesa,Mbaya zaidi lilikuwa tairi la mbele.

Moyo wa Ngesa ukapiga paa,kutokana na kasi ya ajabu aliyokuwa anatumia kuendesha gari, usukani ukamvuta gari likamshinda,likapiga mueleka na kubiringika kama mpira,mbaya zaidi kulikuwa kuna mlima.

Ngesa alikuwa ndani ya gari vioo vikapasuka na kuanza kumkata vibaya sana.Gari likazidi kubiringika,likagota kwenye jiwe puuu!Hakuna alichohisi zaidi ya maumivu makali kwenye mguu wa kulia,alivyotaka kutoka alishindwa,mkono wake ulikuwa umekandamizwa na kiti unavuja damu nyingi,hapo ndipo alipojuwa kwamba ulikuwa mwisho wake,kila alipojaribu kutaka kujinasua alishindwa kabisa!Kwa mbali akaona Diffenda zinakuja kwa kasi ya ajabu!



Hakuwa ana ujanja mwingine wowote, alitamani kujitoa ndani ya gari lakini alishindwa kabisa sababu alikuwa amebanwa,hiyo ilimfanya atulie asitishe zoezi la kutaka kujinasua ili akimbie, Difenda zikapiga breki polisi wakatua ardhini na kulizunguka gari lililokuwa chini limepinduka na ndani alikuwa Ngesa,anawatizama huku damu zinamvuja usoni.

Askari hawakutaka kupoteza muda, mmoja akaingia ndani ya gari na kumtoa nje,ambapo alimpiga na kitako cha mtutu kichwani.

“Hivi unadhani unaweza ukakimbia mkono wa Serikali wewe?”

Lilikuwa ni swali kutoka kwa Afande Kondoa,akimuangalia Ngesa aliyekuwa chini anavuja damu.Jambo la kujinasua ndani kutoka ndani ya gari lililomkandamiza ndilo alikuwa anawaza baada ya kupata ajali na kwa wakati huo alikuwa tayari yupo nje lakini amewekwa chini ya ulinzi.Ngesa siku zote akili yake ilikuwa inachaji kama kompyuta,akageuza shingo nyuma ya gari lililopata ajali akalitizama kwa umakini akamgeukia askari huyu aliyekuwa anampiga, hakuelewa kwa kufanya hivyo alikuwa ni kama anampa muda afikirie zaidi.Ngesa bado hakupata njia ya kujinasua,askari walizidi kufika eneo la tukio lakini baadhi yao walisimama mbali wakifanya mawasiliano yao kwa njia ya redio upepo,Kazi ya Ngesa ilikuwa ni kuwaangalia askari wote kwa zamu bado aliisumbua akili yake akitafuta njia ya kuwatoka kwasababu aliamini kitendo cha kurudishwa tena kituo cha polisi kingemaanisha kunyongwa ama kutorudi tena uraiani jambo hilo hakutaka litokee hata kidogo.

Upande wa pili kulikuwa na kichaka chenye mitimiti,akapiga hesabu zake za harakaharaka lakini bado zilikuwa ngumu.

“Simama juu”

Afande Kondoa akiwa ameshika mtutu alimuwekea Ngesa kichwani akimpiga mkwara,Ngesa taratibu akajizoa na kusimama wima,alivyolitizama gari,akapata akili mpya baada ya kuona gari linavuja mafuta ya petrol yaani tenki lilikuwa limepasuka,akaliangalia kwa kitambo na kulitafakari zaidi jambo analotaka kulifanya baada ya dakika moja mbele.

“Embu simama wewe”

Ngesa alijiangusha makusudi ardhini baada ya kutaka kusimama na kushika mbavu zake,akajikunja.

“Afande alafaliak…”Ngesa akasema kwa sauti ya chini kwa maneno yasiyoeleweka.

“Afande Kondoa mchukuwe yupo chini ya ulinzi huyo jambazi”Askari mmoja akaropoka.

Kwa Ngesa kufanya kitendo hicho kwao walikichukulia kama upotevu wa muda hivyo walikuwa wenye hasira na kilichowapandisha mori zaidi ni kutokana na kumtafuta Ngesa usiku na mchana hiyo ndiyo iliyowafanya wachoke zaidi.Kufumba na kufumbua Ngesa akasimama akampiga ngumi takatifu ya tumbo Afande Kondoa na kurukia mtutu aliokuwa nao akamchukua na kumgeuza akawa mbele yake.Afande Kondoa mbele mtutu upo mgongoni mwake.

“Wekeni silaha zenu chini”Ngesa akatoa kauli hiyo huku akiwa nyuma ya Afande Kondoa na isingewezekana hata kidogo kwa askari kuachia risasi sababu hawakumuona Ngesa vizuri, kuachia risasi kungemaanisha kumpiga askari mwenzao,hawakuelewa ni kitu gani wakifanye.Ngesa akamkwida shati kwa nyuma na kuanza kurudi naye kinyumenyume.

“Tulia hivyohivyo,nadhani unanijua mimi ni nani.Ukifanya kitu chochote cha kipumbavu sitoshindwa kukumiminia risasi”

“Usiniue ndugu yangu”

“Kelele”

Ngesa alikuwa anaongea kwa sauti ya chini iliyojaa hasira huku akiyabana meno yake.Aliwatizama maaskari walipokuwa wameshika mitutu wanamuangalia kwa usongo wa hali ya juu,walitamani kurusha risasi lakini hawakupata saiti nzuri ya Ngesa aliyekuwa nyuma ya askari mwenzao kamuweka mateka,Ngesa alivyohakikisha amefika karibu na msitu wenye mitimiti mingi.Akalitizama gari lililopinduka umbali wa kama mita ishirini kushoto kwake,akamsukumiza afande Kondoa kando.

“Griiiii griii griiii griiiii”

Ngesa aliachia risasi, zote zikawa zinalifikia gari,hazikupita hata sekunde mbili.Mlipuko wa ajabu ukatokea askari waliokuwa karibu na gari hilo walitupwa,hakuwa ana muda mwingine wa kupoteza akaingia mitini huku akiacha askari wengine wakirusha risasi lakini walimkosa tayari aliingia katikati ya miti mingi.

***

“Wanasoma shule gani?”

“Dr.Didas Masaburi,lakini mmoja amehamishwa yupo Las Vegas Marekani”

“Ile shule iliyokuwa Chanika?”

“Ndio”

“Vizuri sana,aliyebaki anaitwa nani?”

“Ritha Leslie Benjamin”

“Shukrani”

“Alafu mkuu…”

“Vipi?”

“Yale mabomu ya Nucler vipi?”

“Ipo siku yake,punguza papara”

Yalikuwa ni maongezi mazito usiku wa saa tatu kasoro saba,Brigedia Karanje alikuwa juu ya kochi akiwa na watu wake wa kazi Seblen na shughuli ya kutafuta shule wanazosoma watoto wa Raisi Leslie Benjamin tayari walikuwa wamezipata,kifo cha Tonny Benjamin aliamini kwamba kilimuumiza raisi wa jamhuri ya Muungao wa Tanzania lakini hakutaka kuishia hapo,ilikuwa ni lazima ampe tena pigo lingine kubwa zaidi.Hapohapo akasimama wima akaingia chumbani na baada ya dakika moja akarudi na simu mkononi mwake.

“Yule binti keshafika?”

Brigedia aliwauliza walinzi wake.

“Ndio mkuu sasa hivi wapo njiani wanampeleka kambini”

“Hapana,waambie wamlete hapa kwangu”

“Sawa mkuu”

Kauli anayotoa Brigedia Karanje siku zote ilikuwa ni amri na ilitakiwa itekelezwe dakika hiyohiyo bila kupingwa,hapohapo mmoja wa walinzi akachomoka na simu na kufanya alichoambiwa,alivyomaliza mazungumzo akamrejea mkuu wake wa kazi.

“Wanakuja”

“Walikuwa wamefika wapi?”

“Tabata Mwananchi”

“Sawa”

Siku zote Brigedia Karanje aliwaza visasi tu,alikuwa ni mwanajeshi mwenye roho ya kinyama.Hata baadhi ya wanajeshi wenzake walimuhofia na jambo alilokuwa amelipanga kulifanya kwa watoto wa Raisi Leslie Benjamin aliamini kwamba atalia na kusaga meno.


Jumba kubwa lililokuwa linalindwa na wanajeshi takribani ishirini wakiwa na mitutu walikuwa wakizunguka huku na kule.Nyumba ya Brigedia Karanje ililindwa kuliko Ikulu, ilikuwa ni raisi kuingia ndani ya Kasri ya mfalme lakini sio nyumbani kwa Brigedia huyu anayelindwa kama almas.Nje zilikuwa zimeegeshwa gari za jeshi tuu na moja ya kawaida, endapo Brigedia Karanje angehitaji kwenda kucheza disco basi alitumia gari hiyo ndogo.Hammer mbili za jeshi zilikuwa nje ya geti zinamulika taa,bila kupoteza wakati geti likafunguliwa Hammer zikaingia zikasimama eneo maalum yalipokuwa magari mengine.Wanajeshi wakashuka,Hammer ya pili walishuka pia wanajeshi isipokuwa mmoja wapo aliyekuwa amevaa nguo za kiraia, Msichana mwenye umri kati ya miaka 24-28 alikuwa ana umri mdogo mrembo kiasi lakini alionekana mkakamavu.

Wote wakaongozana na kuingia ndani ya nyumba, seblen.Wanajeshi waliofika wakachapa miguu chini wakapiga saluti kwa mkuu wao.

“Mkuu,binti huyu hapa.Anaitwa Zaitun”

Mmoja wa wanajeshi akasema.

“Karibu kiti binti”

“Ahsante”

Sio kwamba Zaitun hakumfahamu Brigedia huyu Karanje,alishawahi kumuona sio chini ya mara tatu akiwa nchini Urusi kwenye mazoezi kambini, ndiyo maana hakushtuka sana.Akaketi na kushukuru sana, akashusha pumzi ndefu.

“Karibu nyumbani Tanzania,usiogope kabisa”

“Ahsante mkuu”

“Sitaki kupoteza wakati,kuna kazi unatakiwa kuifanya keshokutwa.Kesho utapumzika jioni tutapiga picha kwa ajili ya hiyo kazi”

“Sawa Mkuu”

“Bosco”

Brigedia Karanje akamuita mmoja wa walinzi wake.

“Naam Mkuu”

“Mpeleke huyu binti chumba cha juu akapumzike”

“Sawa mkuu”

“Na baada hapo apewe chakula”

“Sawa mkuu”

Zaitun akasimama ambapo mgongoni alikuwa ana begi dogo na kupanda ngazi kuelekea juu gorofani,akaoneshwa chumba cha kulala ambacho kilikuwa na kila kitu mpaka bafu.

****

Ndani ya jumba la Brigedia Karanje kulikuwa na kila kitu ikiwemo Studio ndogo ambapo huko walikuwa wakigushi vitu mbalimbali kama vitambulisho vya serikalini.Hapo ndipo Zaituni alipopelekwa siku iliyofuata saa kumi jioni, picha yake ya passpot ikachukuliwa na kijana mmoja machachali aliyeitwa Paul Mahagi,huyu ndiye alikuwa mtaalam wao katika maswala ya kucheza na kompyuta aliijuwa kompyuta utafikiri aliitengeneza yeye.Picha ilivyopigwa tu,pembeni alikuwa ana kitambulisho kingine cha mfanyakazi wa ikulu kazi yake ilikuwa ni ku ‘copy’ na ku ‘paste’ndani ya dakika thelathini kitambulisho kikawa tayari jina la Zaitun Haji lilikuwa juu ya kitambulisho wamegushi kama mmoja wa wafanyakazi kutoka ikulu ya Raisi.

“Daphine Keshafika?”

Lilikuwa ni swali kutoka kwa Brigerdia Karanje akiwa anashusha ngazi anaingia Seblen,anawauliza walinzi wake.

“Bado lakini nadhani ndiyo huyo anaingia mkuu”

Mlinzi aliyekuwa dirishani ndiye aliyetoa jibu hilo sababu alivuta pazia na kuona gari aina ya Mark x linaingia.Ni kweli alikuwa Daphine amefika akashuka na kuwasalimia walinzi akagonga mlango,akafunguliwa.

“Daphine”

“Naam Mkuu”

“Njoo haraka kuna kazi huku”

Daphine na Brigedia Karanje wakapanda ngazi mpaka ndani ya chumba cha kupigia picha.

Macho ya Daphine yakaganda juu ya msichana mdogo aliyekuwa amekaa pembeni,akawa kama mtu anayefananisha kitu.

“Zaitun”Akaita.

“Daphine”

Wote wakarukiana kwa furaha ya ajabu sababu hakuna hata mmoja wao aliyeamini kwamba wangekutana tena.Walikuwa wana mengi ya kuongea lakini Brigedia Karanje aliwakatisha,ili zoezi liendelee.

Daphine alikaa kwenye kiti kitambaa cha rangi ya kijani kikawekwa nyuma yake akapigwa picha.Na baada ya dakika kadhaa kitambulisho chake kikawa tayari.

“Kesho saa tano mnatakiwa kuwa Dr.Didas Masaburi.Ninachohitaji ni mtoto wa Raisi Leslie Benjamin.Anaitwa Ritha Leslie,mtasema mmetoka ikulu mtawapa vitambulisho ili kuwatoa wasiwasi”

“Baada ya hapo?”

Daphine akadakia kwa swali.

“Mumlete hapa,mkishampata.Mtaenda na dereva”

“Sawa”

Daphine akaitikia na kumtizama Zaitun machoni alionekana alikuwa mwenye mengi ya kuongea na rafiki yake ambaye waliachana miaka mingi sana nchini Urusi.

*****

Gari aina ya Landcruiser V8 ilikuwa nje ya geti kubwa ambalo juu liliandikwa kwa maandishi mekundu Dr.Didas Secondary school asubuhi ya saa nne.Usukani ulikuwa umeshikwa na dereva aliyevaa suti na nyuma walikuwa warembo wawili Zaitun na Daphine.

Siku hiyo walivaa kiheshima yaani mashati meupe na makoti meusi pamoja na sketi za rangi nyeusi.Usingebisha ungeambiwa kwamba walikuwa wafanyakazi wa ikulu, nywele zao walikuwa wamezibana vizuri,zinawaka.

“Piii piiii”Dereva akapiga honi.

Mlinzi wa Kimasai akafungua geti gari likaingia ndani,taratibu likaenda mpaka kwenye majengo meupe ya utawala,gari likasimama.Ili kuwazuga walimu dereva akashuka akafungua mlango wa nyuma, Daphine na Zaitun wakashuka.

Walimu waliokuwa wanapitapita waliwashangaa.

“Samahani kidogo”

Daphine akamsimamisha mwalimu mmoja aliyekuwa ameshika fimbo na vitabu mkononi.

“Bila samahani”

“Naulizia ofisi ya mwalimu mkuu”

“Ni hilo hapo dirisha,zunguka kwa huko”

“Ahsante”

Kauli hiyo iliwafanya Daphine na Zaituni watembee na kugonga mlango wa ofisi ya mwalimu Mkuu,wakaruhusiwa kuingia ndani.

“Karibuni mketi”

Mwalimu Mkuu akawakaribisha huku akiwaonesha viti viwili vya wageni.

“Ahsante sana” Zaitun na Daphine wakakaa juu ya viti.Bila kupoteza muda wakasema shida yao,wakatoa vitambulisho.

“Ritha Leslie Benjami?”

“Ndio,kama tulivyosema tumetoka ikulu.Tumekuja kumuombea Ritha gatepass”

“Hakuna shaka,kuna tatizo lakini?”

“Hakuna tatizo,baba yake anahitaji kumuona”

“Sawa nisubirini”

Mwalimu mkuu aliyefahamika kwa jina la Abdallah Henku alisimama kutoka kwenye kiti cha kuzunguka,akanyoosha mpaka nje.

Ambapo baada ya dakika tano alirudi na msichana mdogo aliyevalia sare za shule akiwa pembeni yake.

“Ritha.Nakuandikia passout,unahitajika. Wamekuja kukufata hao unaowaona hapo baba yako anataka kukuona”

Mwalimu mkuu akasema.

Ritha akawaangalia wanawake hao wawili waliokuwa ofisini kwa kitambo kidogo.

“Mbona Dad nimeongea naye jana,hakuniambia chochote.Naomba niongee na Dad kwanza.Nina shida naye kabla sijaenda kumuona”

Zaitun na Daphine wakamgeukia Ritha na kumuangalia usoni baada ya kusikia kauli hiyo.



Daphine alikuwa wa kwanza kusimama baada ya kusikia kauli hiyo kutoka kwa mtoto huyu Ritha,kutaka apigiwe simu baba yake kulimaanisha kitumbua kuingia mchanga kisingewezekana kulika.Kwa maana kuwa kazi yao ingekwama kwa njia moja ama nyingine,ndiyo maana akamvuta pembeni.

“Ritha njoo tuongee kidogo”

Daphine akamshika mkono Ritha akatoka naye nje ya ofisi.

“Ritha mwanangu,mimi naitwa Anti Daphine baba yako amenituma,kuna kitu hataki ukijuwe lakini mimi nitakwambia”

“Kitu gani anti?”

“Nitakwambia kachukuwe gatepass kwanza”

Ingawa Ritha alikuwa anahoji maswali lakini Daphine alimshinda akili na kichwa chake siku zote kilikuwa kinachaji kwa kasi ya umeme.

“Sawa anti”

Hatimaye akakubali.

Alivyoingia ofisini baada ya dakika tano alitoka akiwa na karatasi kama kibali cha kutoka nje ya shule,walimu hawakuwa na kipingamizi sababu alikuwa ni mtoto wa Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ndiyo maana hawakutaka kuhoji kama wanavyofanya kwa wazazi ama walezi wengine endapo wakija kuwaombea ruksa watoto wao.Zaitun na Daphine waliaga na kuingia ndani ya gari,ambapo liliwashwa na kuanza kurudi kinyumenyume safari ya kuondoka ikaanza mara moja,ambapo geti lilifunguliwa na mlinzi wa kimasai.


Ritha alikuwa viti vya nyuma kulia kwake yupo Daphine kushoto Zaitun ambaye chini kwa chini alitoa kitambaa cheupe na kumimina dawa juu yake,zoezi lilivyokamilika akamvuta Ritha na kumuwekea kitambaa puani ambacho kilikuwa na dawa kali za usingizi za calfom,Ritha alitaka kujitoa akijitahidi kuutoa mkono wa Zaitun Puani kwake lakini ndani ya sekunde kumi akapoteza fahamu.

Hapo hapo Daphine akachukuwa simu na kumtafuta Brigedia Karanje hewani ili ampe taarifa hizo nzuri.

“Tayari tupo na mtoto wa Raisi”

“Okay vizuri sana,mleteni hapa kwangu”

“Sawa”

Simu ilivyokatwa Daphine akatabasamu na kumgeukia Zaitun.Ritha alikuwa amelala haelewi kitu chochote kinachoendelea,zoezi la kumteka nyara mtoto wa raisi likawa limefanikiwa kiurahisi zaidi.

***

Ngesa alihisi maumivu makali sana mkononi mwake kutokana na gari lililopinduka na kumbana mkono,alikuwa akivuja damu nyingi na ingeendelea kutoka kwa wingi aliamini kwamba angehisi kizunguzungu na mwisho wa siku angepoteza fahamu zake,ndiyo maana akachana nguo yake kidogo akajifunga juu ya jeraha akiwa chini ya mti,akaugulia maumivu makali. Hakika alihitaji msaada wa huduma ya kwanza,alivyosikia vishindo vya watu akasimama na kuzidi kusonga mbele aliamini kwamba bado jeshi la polisi linamsaka kwa wudi na uvumba.

Alikuwa sahihi kabisa,askari bado walikuwa wana usongo naye na walipiga simu jeshi likaongezeka wakazidi kupiga doria, waliamini kwamba Ngesa hatoweza kwenda mbali zaidi.

“Afande”

Askari mmoja alishikwa bega na mwenzake wakiwa katika msako huo ndani ya kichaka wakimtafuta Ngesa.

“Vipi?”

Mwenzake akaangalia chini wakaona michilizi ya damu,hapohapo wakapeana ishara ili waifatilie damu, waliamini kwamba Ngesa alijeruhiwa vibaya sana na asingeweza kwenda popote pale kwa maana hiyo asingefika mbali.Wakazidi kuifuatilia damu mpaka wakatokea barabara kubwa ya vumbi hapo ndipo damu ilipoishia,hawakuweza kuiona tena.

Hisia zao ziliwatuma kwamba ni lazima atakuwa amepanda gari na kutokomea,bado walikuwa kwenye kitendawili kikubwa wasijuwe ni wapi muhalifu Ngesa alipo.

****

Baada ya kujifunga kipande cha shati alichokichana na kutaka kuondoka alisita baada ya kuangalia nyuma na kuona michirizi yake ya damu,kivyovyote aliamini kwamba wangetumia damu hizo kumfuatilia, hivyo alichofanya ni kukifungua kitambaa na kuacha damu zivuje huku akitembea kuelekea barabara kubwa,alivyofika alifunga jeraha lake vizuri na kurudi ndani ya kichaka. Aliogopa kujitokeza uraiani sababu aliamini kwamba picha zake zimetapakaa jiji zima kwa kitendo alichokifanya iliwezekana kabisa wakazi wa eneo hilo wakawa na taarifa zake,ndiyo maana alirudi kichakani na kupanda juu ya mti wa mwembe,ambapo huko alikalia tawi kubwa.

Akiwa juu aliwaona polisi kwa chini wanapita huku na kule,akajivuta vizuri kwenye tawi ambalo aliamini lipo salama kabisa,akazidi kuwaona askari wanaranda huku na kule.Alitulia juu ya tawi la mti mpaka alivyoona hali imetulia jioni yaa saa kumi na mbili,akateremka taratibu huku akiwa mwenye maumivu mengi sana mkononi na kilichomuumiza zaidi jinsi alivyotua ardhini, alidondokea mkono akajitonesha damu ikaanza kutoka tena,akatembea kwa kupepesuka huku akihisi kizunguzungu kikali sana,hiyo ilitokana na kupoteza damu nyingi sana mwilini mwake alikuwa akiyumba kama mlevi,mbele alianza kuona ukungu hiyo ilimaanisha muda wowote atadondoka chini hakutaka hilo litokee ndiyo maana akajikaza kisabuni.


Alipata nguvu kimtindo baada ya kuona kuna taa za nyumba zinamulika.Hakuwa ana uhakika kwa jambo analotaka kulifanya lakini alitaka kujaribu sababu hakuwa na tegemeo lingine,akazidi kusonga mbele alivyoifikia nyumba, aligonga geti.

“Ngwe ngwee ngweeee”

Aligonga kwa fujo na lilitoa mlio mkubwa sababu lilikuwa ni geti la mabati,akahisi kuna mtu anakuja lakini kabla ya geti kufunguliwa akaona giza nene mbele yake,akaishiwa nguvu na kudondoka chini puu kama mzigo.

****

  ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

BLOG