Search This Blog

Saturday, February 26, 2022

ZAWADI YA ADHABU - 4

   

Simulizi : Zawadi Ya Adhabu

Sehemu Ya Nne (4)


Wakauchuna!

Neema akaingia na kutoka kwenye mtihani wa kwanza, na wa pili na mingine yote mpaka masomo yote nane aliyokuwa nayo kwa muhula ule yakakamilika. Alifanya vizuri sana kwenye muhula wa kwanza, kwa mara ya kwanza katika miaka mitatu akiwa na GPA ya 4.2. Hii ilimpa amani sana wakati akifanya mitihani yake ya muhula wa pili, ambayo alikuwa amejiandaa vizuri sana.

Akamaliza salama! Alikuwa muhitimu mwenye furaha zaidi kuliko wote. Kwanza anamaliza chuo akiwa na maarifa kichwani, pete kidoleni, mume moyoni na mtoto tumboni!Nini kingine alikihitaji mwanamke wa umri wake? Hakika alikuwa na furaha!

Ujauzito wake ulikuwa na miezi mitano sasa. Sasa hakuwa na uwezo wa kuuficha tena. Ulichomoza mbele kwa fujo na kumlazimisha kubadili mavazi yote na kuanza kuvaa mavazi mapana mapana.

Lakini Amani yake ikakatizwa mara kwa mara na maswali kutoka kwa Masagida Kaswalala Masalu ambaye alijua wazi kuwa, binti yake alishamaliza masomo yake na alimuhitaji mara moja nyumbani. Ulitafutwa uongo, ukasakwa kwa kila namna, na lengo lilikuwa jema tu. Walitaka sasa walau kwanza Neema ajifungue. Ndio. Hii ingewasaidia kwanza kupokelewa bila maswali, na wakati mchakato ukiendelea, ingejulikana tu kuwa kilichotokea kimetokea, na wakati huo, mahari ingeshakuwa imelipwa, na ndugu wa pande zote mbili kuonana.

Kizuri zaidi, ndugu wenyewe walikuwa mbalimbali. Mzee Chiziza alikuwa Dar, na mzee Masagida Kaswalala Masalu alikuwa Mwanza, huku wao wakiwa Singida. Vikao vingefanyikia Dar au mwanza. Nani angeyajua kwa undani ya Singida bila wao kusema? Na si tayari walishaamua kutokusema? Ilikuwa rahisi sana. Lilikuwa swali la muda tu!

“Nimepata kazi ya muda mfupi baba. Hapa nilipokuwa nasoma wamenibakisha ili nisaidie kwenye idara ya fedha kule kama mhasibu msaidizi. Wananilipa kidogo lakini walau hutahangaika kunitumia tena….” Hakumaliza.

“Nini wewe? Wamekuajiri namna gani wakati hata matokeo bado? Umeshaanza uhuni wako?” Alifoka Mzee Masagida bila kusubiri maelezo ya ziada.

“Baba.. Najiheshimu sana mwanao.. Na kweli nilishakataa kwa kuwa hata mimi nimepakumbuka sana nyumbani. Ila walisisitiza kuwa ni vema nikabaki kwa kuwa hata ajira siku hizi zinasumbua. Hapa naweza kuunganishiwa nikapata kazi serikalini au kwenye taasisi binafsi upesi kuliko kurudi tu nyumbani” Alijitetea Neema.

“Lakini kwanini usingenipigia simu kuomba ruhusa unaamua kujiamulia tu mwenyewe? Kakwambia nani una nguvu kiasi hicho cha kuamua mwenyewe, eeh? Nasemaje, nimekataa.. Staki.. Staki!! Rudisha kiuno hapa!!” Alifoka Mzee Masagida

“Baba.. Nathamini sana juhudi zako za kunilea. Sitaki kukuvunjia heshima. Nikirudi na kukaa tu nyumbani naweza kukutana na vishawishi baba. Wewe mwenyewe umenifundisha kuwa akili isiyo na majukumu ni kiwanda cha shetani. Nataka nijibidiishe ili kuilinda heshima yako na heshima ya marehemu mama yangu aliyepambana ili niwe hai leo”. Neema alijua pa kumshika baba yake.. Alijua anapomtajia marehemu mkewe anakuwa ameshamaliza kazi..

“Aaah.. Ni sawa.. Ni sawa lakini… Kwanini wasingekupa hata wiki moja ukaja mama angu? Unajua wewe ndio jicho langu kwasasa. Wewe ndio mke, ndio mama, ndio binti, ndio dada, ndio kila kitu kwangu sasa. Muhula wa kwanza ulisema unafanya field, nikakubali. Sasaaaa tena…. Ah., sawa. We fanya kazi mama, ndio heshima ya mwanamke hiyo. Ila ukipata muda hebu uje walau mwisho wa wiki utusalimie. Na Machimu si unajua atakuwa na mahafali ya kidato cha nne mwezi wa kumi? Uje mwanangu” Alimaliza mzee Masagida kwa sauti yake yenye utajiri mkubwa wa lugha ya kisukuma.

Miezi ikakatika na furaha ikazidi kutawala nyumbani kwa Clifford. Pamoja na kutokuwa na kipaji cha kuimba, Clifford alikuwa mpenzi mkubwa wa kwaya. Katika kanisa la Moyo Mtakatifu wa Yesu alipokuwa akisali, alikuwa ni rafiki na mfadhili wa kwaya ya Watakatifu Mashahidi wa Uganda, na akawa pia rafiki wa karibu wa wanakwaya mbalimbali. Mara kwa mara walikuwa wakimtembelea nyumbani kwake na Neema ndiye akawa mama mwenye nyumba aliyewakaribisha na kuwahudumia kwa mapenzi makubwa.

Hawa ndio wakawa marafiki zao wa karibu, na mara kwa mara wangesikika wakijadili namna watakavyohakikisha kuwa harusi ya mfadhili wao yule itakavyofana. Walimu walishaanza kufikirifikiri juu ya hata nyimbo za kutumbuiza siku ya harusi.

Kila mmoja alitamani kufika siku hiyo.

Halafu..

Miezi tisa ikatimia. Kelele za Mzee Masagida kumtaka bintiye zikiwa katika kilele huku akitishia kumfwata mwenyewe huko Singida, Neema polepole akaanza kupatwa na uchungu wa kuzaa. Maandalizi yote yalishakuwa tayari na walipanga akajifungulie Hospitali ya Makiungu iliyokuwa kilometa kadhaa kutoka Mjini. Kwa kuwa tayari wakati huo Clifford alishapata tena usafiri, haraka akamuwahisha mkewe hospitali akisindikizwa na marafiki zake wawili ambao wote walikuwa wanakwaya. Njia nzima alikuwa akiendesha gari huku mara kwa mara akimsemesha mkewe ambaye uchungu haukuwa umemfika hatua ya kushindwa kuongea.

Alimtania na kumchekesha, na safari ikawa fupi kuliko walivyotarajia.

Wakafika Makiungu hospitali.

Neema akapokelewa na kuingizwa chumba cha kujifungulia.

Clifford Chiziza na wenzake wakangoja..

Walingoja…

Wakangoja tena…

Wakangoja sana...

Halafu…. Ah!




******

Nimefundishwa kuwa…

Sio wote utakaokutana nao na kuwatendea mema watayakumbuka mema hayo maisha yao yote. Na tena, sio wote wote ambao utawaonesha ukarimu wako siku moja watakulipa kwa kukuonesha ukaribu utakapohitaji. Kukumbuka fadhila nacho pia ni kipaji, na sio wote wanacho. Lakini hii iwe tu ni sehemu ya wewe kujifunza kuwa, wajibu wako kwa wengine ni kuwatendea mema. Ukielewa vema hili na ukaanza kulitenda, dunia nzima itakuwa na binadamu wanaotendeana wema tu!! Kila jema linaanza na wewe!!!

Una hiyari ya kukubali au kukataa….

******

*** NINAWAANDIKIA HAYA KATIKA SEHEMU TISA ***

Masaa matatu yalipita.

Sasa mishale ya saa ilikuwa ikiwaaminisha kuwa, ilikuwa saa mbili na dakika kumi na moja za usiku. Clifford alishatembelea maeneo yote muhimu katika hospitali ile kuanzia vyooni, kwenye wodi za wagonjwa, sehemu za kuuzia vyakula, maegesho ya magari nahata nje kabisa ya geti. Sasa alishamaliza kote na ni sehemu moja tu ilikuwa imebaki ambapo alitamani sana kuingia.

Chumba kile alipoingizwa Neema wake.

Rafiki zake Laurent na Thobias walikuwa naye bega kwa bega, wakajadili kuhusu hili, likaisha, wakahamia kwenye lile, nalo likaisha, zikaja na mada zisizo na mvuto wowote, wakazimaliza. Sasa wote macho walikuwa wameyatumbulia kwenye korido ndefu ambapo ndipo alikokuwa amepelekwa Neema. Ni Mungu pekee aliyejua ni nini kila mmoja alikuwa akikiwaza kichwani mwake.

Naam..

Mlango ukafunguliwa.

Kijana mrefu mwenye sharubu nyingi na mawani kubwa akatoka akionekana kuchoka kwelikweli. Akavuta hatua haraka haraka kuelekea upande mwingine wa korido ile mbali na walipokuwa wamekaa Clifford na wenzake. Lakini hakumaliza hata hatua kumi, Clifford tayari alikuwa naye bega kwa bega.

“Yes Dr. Mark, poleni sana” Alimsalimu daktari yule ambaye alikuwa ameshakutana naye zaidi ya mara tatu alipomleta Neema kuhudhuria kliniki.

“Njema.. Oooh, bwana Cliff.. Twende ofisini mara moja” Alisema Dr. Mark bila ya kupunguza mwendo wala kumtazama Clifford usoni. Clifford alisimama ghafla na kumtazama Daktari yule ambaye hakugeuka nyuma. Alitazama ingawa hakumwona! Kisha akanyanyua tena hatua na kuanza kumfuata nyuma nyuma kama kondoo aliyekwenda machinjoni.

Tayari alishaanza kuwa na majibu mengi kwa swali moja, na yote yalionekana kuwa sahihi.

Walifika katika chumba kidogo ambacho Clifford alishaingia zaidi ya mara mbili wakati wa matembeleo ya kliniki, lakini chumba kilionekana kuwa kigeni kabisa kwake. Alihisi kukichukia na wala hakutaka kuwa pale muda ule. Alimtaka Neema wake na mtoto wake awe amempakata mikononi akijaribu kucheza naye. Alikuwa akiyaona mashavu ya Neema katika uso wa mtoto wake. Alikuwa akiutazama uso wa kuvutia katika mtoto wake. Alitaka muda ule ule awe amemshika mtoto wake. Ni vipi sasa Dr. Mark anamleta katika hiki anachokiita ofisi huku hakina dalili yoyote ya kuwa na kitanda kitakachompokea Neema na mtoto wake watakapotoka huko walipo?

“Enough Dr. Mark!! This isn’t a joke anyhow. Please speak out, how is my good wife and a baby? Are they fine? Is everything alright?” Aliuliza Clifford huku akionekana wazi kughadhibika hasa kwa kuwa, Dr. Mark aliendelea kujishughulisha na kifaa hiki au kile akimwacha Clifford akiwa amesimama dede!!

“Yes yes Clifford.. Just have a sit brother.. We need to talk” Alijibu Mark huku akijipangusa uso na kuiweka sawa mawani yake. “We need to talk? Talk on what you swine?” Alijisemea Clifford ndani ya kichwa chake. Akamtemea kohozi zito kimawazo na akajiapiza kuwa, hatazungumza tena na daktari yule akishatoka hospitalini na Neema wake na mtoto wao.

Akaridhika kiasi. Hasira zikampungua.

Akaketi kishingo upande huku akimtazama Dr. yule usoni. Alikuwa mbaya!!Alimchukia na kushangaa ikiwa ni yuleyule kijana mwenye sura nzuri ambaye alikuwa akimuhudumia mkewe! Akamtukana tena tusi la nguoni kimoyomoyo, akaridhika zaidi, akatulia na kumkazia macho.

“Kuna vitu inabidi tuviweke sawa…” Alianza Dr. Mark.

“Vitu gani? How much? Sema, pesa ngapi nikupe mwanaume? Sema upesi, au nikupe……” Kihoro kilikuwa kimempanda Clifford.

“Clifford you must learn to listern and listern good!” Mark alijibu kwa mkato kwa sauti ya upole lakini kwa mbali, ilionekana kuwa na msisitizo fulani unaolazimisha jambo fulani. Clifford akatulia tuli.

“Imekuwa ni ajabu kidogo. Mkeo alihudhuria kliniki zote na kila kitu kilikuwa sawa kabisa.. Hata wakati wa tembeleo la mwisho nilimpima mwenyewe na hali yake ilikuwa sawa na ingempasa ajifungue kawaida. Lakini tuligundua kitu tunakitita “abnormal Presentation”. Mkao wa mtoto haukuwa sahihi na wakati tunajiandaa kufanya upasuaji, kulitokea hali nyingine ambayo tunaiita “Amniotic Fluid Embolism”, ambapo katika namna isiyo ya kawaida, kuna fluid tunaiita Amniotic Fluid ilianza kupenya kwenye mfumo wa damu, na fluid hii hupelekwa hadi kwenye mapafu na kusababisha hali tunayoiita kitaalamu “Arteries contractions” ambapo…

“Dr Mark get to the business buda, get to the damn thing!!.. Ningependa zaidi utumie lugha nyepesi tu, MKE WANGU NA MWANANGU WANAENDELEAJE? Achana na habari za amphibia, flomborism, autopia na mamalia, nitakuita wiki ijayo uje unifundishe nikiwa na kalamu na daftari. Nataka kujua hali ya Neema bana.. Amniotic arteries na Manini nini sijui huko utaniambia siku nyingine”. Alikuja juu Clifford.

“Clifford.. Wewe ni mwanaume, na unapaswa kujikaza. Mtoto ametoka salama na tayari wauguzi wanamuandaa. Lakini mke wako…. Neema ame…. Ametutoka Clifford. Haikuwa rahis….” Alisema Mark huku akijaribu kuiweka sauti yake kuwa ya kubembeleza.

Lile kofi la kisogo alilowahi kubamizwa na Martin Bazu likarejea tena kwa fujo kwenye mawazo yake, likambabatiza kwa nguvu. Lakini hili halikuambatana na maumivu, lakini madhara yalikuwa yaleyale. Na tena, Aliwaona akina Dr. Mark wanne wanaofana wakimtazama.

“Whaaaat?? Nini wewe? Unasemaje Mark? Neema ame.. Amefanya nini?” Clifford alishajikabidhi mwenyewe chini kwa kishindo! Hakuwa tena anajua kinachoendelea.

Vijana wa Kiswahili wangesema amekata moto!

***

Ulikuwa usiku wa hekaheka kwa Laurent na Thobias. Taarifa za kifo cha Neema ziliwatia ganzi na kule kupoteza fahamu kwa Clifford kukawaingiza katika tanuru ambalo halikuonekana. Walifuta jasho, wakapanda na kushuka. Haraka, mwili wa Neema ikaburuzwa kwa machela na kuingizwa katika chumba cha maiti. Shemeji ambaye walikuwa wakitaniana naye masaa kadhaa yaliyopita alikuwa kimya..

Kimya cha daima!!

Kitoto kichanga cha kike kilikuwa kikitumia mikono yake midogo kupangua hewa na kulia kwa bidii. Watawa wa kanisa katoliki ambao walikuwa wakiihudumia hospitali ile wakakanyakua juu juu na kukapeleka katika chumba maalumu na kuanza kukahudumia.

Ulikuwa ni uchungu usiovumilika kwa Clifford baada ya kupata fahamu. Alidumu katika hali ya kutokujitambua kwa saa moja na nusu ndipo alipofungua tena mboni zake na kuanza kuweweseka. Clifford alilia, akasimama, akakaa, akagaragara chini, akajipaka na vumbi, lakini sauti pekee aliyoisikia haikuwa ya Neema wala mwanae yule.. Sauti pekee ilitoka kwa Thobias aliyekuwa akitoa maneno yote kutoka katika biblia, tenzi za rohoni, katekisimu za kanisa na hata sala alizozifahamu yeye.

Zote hazikuwa na msaada wowote kwa Clifford.

Taarifa zikafika Singida mjini. Majirani, marafiki pamoja na jamaa wa karibu na Clifford wakayasikia yaliyomtokea. Usiku uleule, wakarudi mjini huku wakimwacha Neema akipigwa na ubaridi usiomithilika na kichanga kile kikiwa chini ya uangalizi wa wataalamu.

Usiku ule ule, tayari kikundi cha wanakwaya pamoja na majirani wengine wa Clifford walishafika nyumbani kwake. Nyumba ikaendelea kujaa kila baada ya dakika chache na mpaka kufikia siku iliyofuata asubuhi, tayari na turubai lilitundikwa juu ili kuwasitiri watu kwa jua. Clifford hakuwa na nguvu ya kuongea chochote. Alikuwa amejiinamia huku akiliona jinamizi kubwa la kifo likimjia na kumzomea. Ni wazee wachache na marafiki zake hasa wale wanakwaya waliokuwa wakishughulika kila kitu.

Hakika aliuona upendo wa watu!

Lakini wote wale walikuwa wakihangaika bure tu. Hakuna hata mmoja kati yao aliyeonekana yuko tayari kumpa msaada wa kupata majibu magumu ambayo yalikuwa yakitembea kichwani mwake..

Angemweleza nini Mzee Chiziza?

Angemweleza nini Mzee Masagida Kaswalala Masalu?

Angempeleka wapi Neema?

Angempeleka wapi yule mtoto asiye na jina ambaye hata alikuwa hajamtia machoni?

Kamasi zilimchuruzika na wala hakuona umuhimu wa kuhangaika nazo. Alikuwa na mambo ya msingi ya kuwaza kuliko kuwaza zile kamasi na machozi yaliyokuwa yanamtoka bila kibali maalumu. Tayari alishaonekana kuchoka kuliko kawaida. Hakuwa mtu wa kuzungumza, na wote waliokuja kumpa pole aliwaona wanafki na wazandiki wakubwa.

Jua likawaka na kupunguza makali. Jioni ikafika. Wenye busara wakaona kimya, na kwa kuwa utu uzima wao ulishawakutanisha na mambo makubwa kuliko lile, wakaamua kuweka kikao kwa nguvu.

“Sasa Bwana Clifford.. Yaliyotokea yameshatokea. Neema ametutoka, Innallilah Wainai Lillah rajiun. Waislamu sisi tunasema Kul nafsin zakatul Maut, nadhani hana nanyi ndugu zetu katika Imani mnalikiri hilo, tumetoka kwake na kwake tutarejea”. Alianza kuzungumzwa Mzee Ibrahim Upodo, moja kati ya wazee ambao Clifford aliheshimiana nao mno pale Singida.

“Acha uongo wewe.. Neema hajafariki” Clifford alisikia kitu kikimuwaka ndani yake, na kwa mara ya kwanza akamchukia Mzee Upodo. Bahati tu ilikuwa upande wake kwa kuwa maneno haya yaliishia katika kichwa chake tu. Mzee Upodo akaendelea.

“Alhamdullilah Mwenyezi Mungu ameweka mkono mtoto amemnusuru. Kuna Ibra katika hili ndugu zangu.. Kuna mazingatio hapa na ni vema tukayashika na kuendelea kumcha M’nyaaazi Mungu mwingi wa reh’ma. Ni vema tukamshukuru M’nyaaz Mungu Subhannahu Wataalah wandugu. Lakini sasa, kule kwetu Tabora huwa tunasema Msiba haukosi pa kuingia. Na sasa kwetu umeingia. Nadhani labda kama umeshaongea na wazee ungetupa mrejesho ili walau tujue tunafanyaje bwana Clifford” Alimaliza Mzee Upodo na zaidi ya watu nane waliokuwepo pale sebuleni wakaafiki.

“Kwa kweli… Kweli sijui nianzie wapi.. Nashindwa… Nashindwa kujua ni balaa gani ili limenigongea hodi asubuhi na mapema.. Mi sijui kwakweli, sijui” Kilio cha kwikwi kikaanza kumtoka Clifford. Mzee Upodo akahisi kuwa lipo jambo, na upesi akawabagua waliopo pale ndani. Wakabaki wanaume wanne pekee, na haraka, Mzee Upodo kama vile ajuaye yanayomsibu Clifford, wala hakuhangaika kumbembeleza.

Akatoka nje na kuagiza vijana kadhaa kwenda huku na kule, wakati huo huo simu yake ikifanya kazi. Dakika arubaini baadae, sebule ile ikawa kama kikao cha ukoo. Wazee kadhaa wenye heshima pamoja na marafiki wa karibu zaidi wa Clifford wakawa wamekaa kwa kuelekeana, idadi yao ikiwa watu kumi na sita. Mzee Upodo ni kama vile alishajipachika cheo cha mwenyekiti na kila mara alikuwa akikagua kagua ili kujirishisha kuwa akidi imetimia, kisha sasa akafungua mjadala.

“Naam wazee wenzangu na vijana wangu wachache. Nimeona tuitane mara moja kuwekana sawa kwa yale yaliyompata kijana wetu. Nadhani wote hapa tunakiri kuwa huyu kijana amekuwa ni kijana wetu sasa. Heshima yake na utii kwetu vimempa jina jema miongoni mwetu. Huu ndio ujana wenye manufaa, pamoja na elimu kubwa aliyonayo lakini bado anatuheshimu sisi wazazi wake kwa kituo.

Sasa yamemfika mambo. Ana msiba. Ukimya wake tangu msiba ulipomfika umenishitua kama mtu mzima na nikaona muwepo watu wenye vifua ninaowafahamu. Tafadhali kama kuna anayejua hana msaada hapa, na labda nimemuita kimakosa, ajiondokee mara moja” Alianza Upodo na kimya kilipozidi kuzizima akaendelea.

“Haya bwana mkubwa.. Clifford, ulipojaliwa hayo maumbile hapo katikati ya miguu ulipewa na zawadi nyingine kubwa. Zawadi ya uanaume. Mwanaume si mtu legevulegevu, hata yamfike makubwa yepi, huangalia kwanza namna ya kuyakabili halafu ndipo aanze kulia. Sasa tumekutana hapa kusaidiana nawe kuyakabili hayo. Hebu funga fundo gumu kooni, kisha liteme hapa lililo moyoni mwako. Nakuapia hata liwe na uzito wa dunia, tutalibeba mabegani na kutembea nalo kwa madaha kabisa” Upodo alisema huku akiweka kifua mbele.

Ujasiri ukamuingia Clifford.

Kwa mara ya kwanza akatamani Upodo angekuwa ndiye baba yake mzazi!

“Acha ujinga wewe, baba yako ni Chiziza…, Chizi Chiziza ambaye akisikia uliyoyafanya atakuachia laana ya kudumu” Ile sauti ikamjia tena lakini akaipuuza. Alifungua kinywa chake na kwa zaidi ya saa zima aliendelea kuwasimulia waliokuwa wakimsikiliza habari za Mzee Chiziza, kisha Neema na jinsi walivyokuwa wamepanga, na namna ujauzito ule ulivyowalazimisha kungoja, na juu ya uwepo wa Mwalimu korofi aliyeitwa Masagida Kaswalala Masalu ambaye wakati huo labda alikuwa akihangaika kumtafuta binti yake bila mafanikio kwa kuwa alikuwa na kawaida ya kuongea nae kila siku mara mbili au mara tatu.

Mpaka anafika mwisho wa simulizi yake, sebule nzima ilikuwa imezizima kwa ukmya usiomithilika. Hakuna hata mmoja aliyenyanyua kinywa kuhoji wala kushauri.

Wote walikuwa wamesawajika!

“Mmmmh… Ama kweli ‘pachonge pangali panene’. Babu yangu aliwahi kunifundisha msemo huo miaka mingi iliyopita. Hiki kweli kizaazaa. Lakini bado sijaona dalili za kushindwa. Kwanza, nadhani wa kwanza kumuarifu habari hizi ni baba mzazi wa kijana. Mpigie simu Mzee Chiziza nami nitaongea nae taratibu na kwa kituo. Yeye akshatuelewa, nadhani tutakuwa na karata ya kwanza ya kututoa katika mtego huu” Alisema Mzee Upodo kwa kauli iliyokosa ule ujasiri wa awali.

“Halafu imekuwa ajabu kweli. Mwalimu Masagida Kaswalala Masalu anayeongelewa mimi namfahamu vema sana. Mzee wangu aliwahi kufundisha naye pale Nyakato lakini yeye baadae akahamishiwa Geita. Nadhani naweza pia kumwomba baba yangu atusaidie upesi kuwasiliana na Mzee mwenzake ili walau tuone msimamo wake”. Joshua Tegu ambaye alikuwa rafiki wa Clifford akachangia.

“Unaona sasa Clifford? Haya mambo bwana ukikaa na watu wanayamaliza. Haya bwanaaa…. Nani vile?” Alihoji Upodo

“Tegu.. Tegu.. Mr. Joshua Tegu” Alijibu Tegu ambaye alikuwa mhandisi wa maji.

“Naam Tegu.. Hebu wewe na Mzeeee…. Makambaaaa, Nyonzo naaaa… Mmole.. Wewe, Makamba na Mmole chukueni jukumu la kuwasiliana na Mzee wako pamoja na kuhakikisha kuwa mpaka saa mbili kamili tunapata mrejesho juu ya huko nyumbani kwao marehemu kwa huyo Mzeeeee” Alisema na hakungoja mtu amkumbushe.. Alikuwa akipitia karatasi ambalo muda wote wa masimulizi alikuwa akiandikaandika mambo ya muhimu.

“kwa mzee Masalu”. Alimaliza.

“Mimi, Clifford, Mzee Babudiii.. naaaa…, nani mwingine jamani? Tujitokeze..”

“Mimi hapa” Aliitikia mtu wa makamo aliyekuwa ameegamia ukuta.

“Hewalaaa.. Mimi, Clifford, Babudi na Lasway tunajishughulisha na mawasiliano na Mzee Chiziza na upande mzima wa Clifford. Kama kawaida, mbili kamili tunakutana hapa kuweka vichwa pamoja tuone tumefikia wapi. Wengine wote tuliobaki, chini yaaaa… Oh, ndio.. Ningepitiwa hapa.. Chini ya Bwana Kimati.. Ambaye mimi napendekeza awe mwenyekiti wa kamati ya mazishi. Ninyi anzeni mipango mara moja. Wekeni sawa bajeti zote, angalieni kama tuna fedha ya kutosha na kila kitu kiwe sawa. Sisi tukija na majibu tu tunaendelea kutoka mlipoishia” Alimaliza Upodo na kuangalia kama kuna aliyekuwa na nyongeza.

“Sawa.. Mi nakubali. Na napokea jukumu hilo mara moja. Ila kwa kuwa shughuli hii itahitaji pesa, nashauri hapa kuwa mwenye nacho aanze kukiahidi au kukiweka kabisa mezani ili tujua tunaanzia wapi. Mimi nitachangia taslimu Milioni nne, na magari matatu” Alisema Kimati.

Hoja ikapita mara moja. Huyu akaahidi hiki na huyu kile. Ndani ya dakika tano tu, Milioni sita na nusu zikapatikana pale pale ingawa nyingine zikiwa ni ahadi. Kikao kikakamilika na watu wakasambaa wakikubaliana kukutana tena saa mbili na nusu.

Walikuwa na masaa mawili tu ya kufanya kazi ngumu kwelikweli!

Kazi ambayo hata hivyo…

Mh!!





Nimefundishwa kuwa…

Sio lazima ujichanganye na watu wote muda wote. Kila binadamu ameumbwa na namna fulani ya hali inayomfanya wakati fulani atake kuwa peke yake tu. Hii ni kawaida kabisa hata kwa sisi wengine, sio kwako tu!! Unapoona kuwa inakulazimu kujitenga na wengine, fanya hivyo. Lakini daima jijengee hali ya “kufikika”. Wafanye wengine wakuone kuwa mtu wanayeweza kumfikia katika hali walizonazo. Unapojenga aina ya kisiwa cha kukaa mwenyewe, kuna wakati unajitenga na fursa ambazo huenda hata wewe unazihitaji sana!!

Una hiyari ya kukubali au kukataa….

******

*** NINAWAANDIKIA HAYA KATIKA SEHEMU KUMI ***

Hali sasa ilikuwa tete!!

Kama Clifford alidhani alikuwa anaufahamu vema ukali wa baba yake, alikuwa amejidanganya vibaya sana! Mzee Chiziza alimsikiliza huyo wa kuitwa Upodo kwa umakini mkubwa tangu Mwanzo wa simulizi yake mpaka mwisho. Hapa na pale, Mzee Upodo alikuwa akitumia muda mwingi kuelezea busara za Clifford na namna alivyokuwa na heshima kwa watu anaoishi nao, na Mzee Chiziza alikuwa kimya tu akimsikiliza kwa umakini. Kwa mbali, timu ile ya watu wanne wakaanza kuhisi kuwa walikuwa wanaelekea kufanikisha jukumu lile kirahisi kabisa.

Mzee Upodo akamaliza.

“Umemaliza mzazi mwenzangu?” Sauti kavu ilisikika kwenye simu.

“Naam Mzee mwenzangu. Na nikaona hili nililete mimi kama…”

“Huwa napenda jibu moja kwa swali moja, huenda Clifford hakukueleza hilo. Msamehe tu, huenda hajakueleza mengi bado.. Nipe jibu la swali langu tafadhali” Sauti ile kavu na yenye wingi wa mamlaka ikamkatiza Upodo.

Wajumbe wale wanne wakatazamana, lakini haraka Clifford akatazama chini. Alishajua balaa linalokuja.

“Naam.. Nimemaliza Mzee mwenzangu” Upodo alijibu kinyonge.

“Sawa. Kwahiyo huyo bwana mdogo alikuwa akiishi na mwanamke, akampachika mimba na kuendelea kuficha akiamini kuwa baada ya kujifungua ndipo napaswa kupigiwa simu ili tu kutoa jina la mtoto, sio?” Aliuliza Chiziza.

“Eeeh.. Nadhani ndiyo ilikuwa maana yake, na huenda kulikuwa na….”

“Unaonekana nawe unaanza kuwa mzee mpumbavu mwenye kusahau sahau mambo. Nimesema swali langu moja huwa linahitaji jibu moja tu.. Hayo majibu yako yatunze, maswali yake ninayo pia” Hapa hasira zilionekana wazi wazi kwenye sauti ya Chiziza. Lakini tofauti na matarajio ya wengi, Mzee Upodo wala hakukasirika, alizidi kuwa mpole na uso wake kuwa makini zaidi.

“Nahisi hivyo bwana” Alijibu Mzee Upodo.

“Clifford ni mwalimu mzuri sana darasani. Naona amefika Singida amepata na wanafunzi wazee watu wazima ambao nao amewafundishwa somo linaloitwa “kuhisi”.. Kwahiyo utaacha muda gani “kuhisi” ili unipigie tuanze kuongea vitu halisi na sio hisia?” Aliuliza Chiziza huku akiweka msisitizo fulani kwenye baadhi ya maneno.

Clifford tusi zito likamtoka lakini jicho kali la mzee Upodo likamtuliza jazba!

“Mzee mwenzangu.. Lililopo mbele yetu ni tatizo kubwa, na wewe kama baba mzazi…” Upodo alijaribu kujitetea.

“Angalia bwana, nilisema nikiuliza swali lijibiwe kwa jibu moja, hayo maelezo kuna wakati ntakuja kuyahitaji halafu usiwe nayo bure. Jifunze kuwa na akiba ya maneno. Na kwa kukukumbusha tu ili usije ukakosea mara nyingine, Mimi sio “kama baba mzazi wa Clifford”, mimi ni “Baba mzazi wa Clifford”.

Simu ilikatwa!!!

Bumbuwazi ikatawala.

Mzee Babudi na Laswai walitazamana, wakatikisa kichwa kwa pamoja. “Hivi baba yako ni kabila gani?” Aliuliza Mzee Babudi macho yakiwa yamemwelekea Clifford. Kabla hata hajajibu, Mzee Laswai akajibu kwa hasira.. “Huyu lazima atakuwa kabila mbovu tu.. Mali mbovu.. Mswahili sana huyu Mzee, doh”

“Tulizeni jazba, bado tuna nafasi kubwa kwenye hili. Hebu nipatie hiyo namba nimpigie kwa simu yangu, kuna jambo nimejifunza hapa” Upodo akapatiwa namba na dakika mbili baadae, alikuwa tena kwenye mazungumzo.

“Naam.. Nakupongeza kuwa kuacha kuhisi ndani ya muda mfupi tu. Haya sasa, hebu nieleze. Wewe ndiye uliyeyabariki hayo mahusiano ya huyo barazuli kuishi na mtoto wa watu, kumjaza mimba na kuendelea kuficha akiamini kuwa akishajifungua ndio anaweza kuwaambia wazazi wake?” Alikuwa ni Mzee Chiziza aliyeanzisha mazungumzo.

“Kwakweli hakuna mzee au mtu mzima yeyote anayeweza kubariki jambo kama hili. Kilichofanyika ni kosa na kilikuwa kosa tangu awali. Tatizo ni kuwa, vijana wetu kuna wakati wanafikiri kuwa wana dunia yao peke yao, na ni busara tukawaacha waamini hivyo. Lakini ni dunia hiyo hiyo inapowafunza, yatupasa tuwarudi na kuwakumbusha kuwa, njia uijuayo panapo mwanga huwezi kuiendea vema palipo na kiza” Hakukuwa na hofu wala mashaka yoyote katika sauti ya Upodo.

Alishaanza kuonesha ujabali wake!!

“Anhaa.. Kwa maana nyingine unamaanisha kuwa, Clifford, aliiona njia mchana wa jua kali. Akaipitia mara mbili mara tatu, na kiza kilipotua akajiaminisha kuwa njia ile anaifahamu vema, akafumba na macho kabisa na akapita tena, na mwishowe alipofungua macho amejikuta amepotea, sio?’ Alihoji Chiziza.

“Naam ndugu yangu.. Nadha…, Hapana, naamini kuwa kijana kwenye hili, sio kwamba tu amepotea. Lakini ametupoteza hata na sisi ambao inatulazimu sasa tumtafute, tumpate na kwa pamoja turudi hadi Mwanzo wa safari. Tumfundeshe tena namna ya kutembea gizani” Upodo alizidisha Kiswahili.

“Sasa mimi neno langu ni moja… Neno langu ni moja tu…” Alianza Chiziza.

“Naam”

“Na huwa nina utaratibu mmoja. Clifford atakueleza vema kama akiamua kufanya hivyo. Nikishafanya uamuzi juu ya jambo moja, natamani ufuatwe kama ulivyo, bila kupakwa rangi wala kupuliziwa uturi…, tuko pamoja?”

“Naam.. Nakusikiliza bwa’mkubwa”

“Na katika hili, neno langu ni moja. Na nikishamaliza tu kulisema, nitakata simu. Kama unatamani heshima yangu, usinipigie simu mpaka utakapolitimiza, tuko pamoja?”

“Eeeh… Nakusikiliza bwana, na naamini…”

“Achana na Imani yako bwana, nisikilize mimi. Kwanza usiamini usichokijua bwanaaa.. Nani vile ulisema?”

“Mzee Upodo”

“Ndio Upodo.. Usiamini usichokijua.. Sasa neno langu ni hili. Clifford, na mkipenda ninyi pia kushirikiana naye, malizeni huo upuuzi mliokuwa mnaulea pamoja. Kama mtazika, au mtaishi na maiti, au mtamrudisha mtoto wa watu kwao, hilo mimi sihusiki nalo. Sijafundishwa kusaidia watu wazima wanaochezea moto namna ya kuuguza majeraha yao, nilifundishwa kuwaelezea madhara ya moto. Huyo bazazi yalishamkuta makubwa, nikadhani amejirekebisha, na badala yake kaenda kuchuma makubwa zaidi. Sasa malizeni huo upuuzi, mkishamaliza tu, nipigie simu, nitakueleza nini kifuatacho. Nimekuheshimu sana kukupa nafasi hii, na sikumbuki mara ya mwisho niliitoa mwaka gani. Msiba Mwema”.

“Aah.. Lakini Chiziza… Unajua bwana hali iliv…..” Upodo alikuwa akiongea mwenyewe. Simu ilikuwa kimya. Tusi la kiarabu likamtoka kwa uchungu!

Kikao hakikuwa na maana tena, kikavunjika na wote wakaendelea kungoja majibu ya upande wapili.

***

Ilikuwa rahisi sana kumpata Mzee Tegu ambaye mara moja aliwasiliana na mzee Masalu. Bila kukawia, Mzee Masalu akaungwa na waliokuwa Singida na mara moja mawasiliano yakawa baina yake na wao.

Kwa zaidi ya dakika ishirini walijaribu kumuelezea kilichotokea lakini maswali mazito mazito yalikuwa yakirushwa mfululizo. Haraka wakaamua kumshirikisha na Clifford aliyekuwa ametoka kwenye kikao cha kuzungumza na baba yake. Akajieleza kwa kirefu kwa Mzee yule ambaye aliishia kuguna kila alipokuwa akisimuliwa.

“Kwahiyo wewe ulikuwa mwalimu wake wa chuo, sio?” Aliuliza Masalu

“Ndiyo baba”

“Na ulimpa mimba akiwa bado mwanafunzi hapo chuoni?”

“Lakini tulishaanza uchumb…”

“Unalikumbuka swali langu?”

“Ndio baba”

“Naomba jibu”

“Ndiyo, Neema alipata mimba akiwa anakaribia kumal..”

“Akiwa mwanafunzi, acha kuremba mwandiko, kumbuka unaandika imla”

“Nakubali baba, akiwa mwanafunzi”

“Maadili ya ualimu yanasema nini kuhusu mahusiano baina ya mwalimu na mwanafunzi?”

Jasho lilikuwa likimtoka Clifford. Aliona dalili za kupoteza kila kitu maishani mwake.

“Ni kweli si sahihi kuwa na mahusiano ya kimapenzi. Lakini mimi na mwenzangu tulishakubaliana kufunga ndoa, nahata…”

“Wewe ndiye uliyemtafutia kazi chuoni?”

“Hapana baba, hakuwa anafanya kazi.”

“Jibu zuri kabisa. Wewe ndiye uliyemwambia anidanganye kuwa anafanya kazi ili uendelee kumlaza akiwa uchi kufuani pako, sio?”

Clifford angejibu nini sasa hapo? Alinyamaza kimya.

“Halafu.. Ni sheria ipi inamruhusu mwanaume kuishi na mtoto wa mtu kwa karibu mwaka mzima bila kutoa taarifa kwao? Au ndio ujana huo?”

“Tumekosea baba.. Tumekos..”

“Sema umekosea kijana, sema nimekosea”

“Nimekosea baba”

“Sawa.. Sasa mimi ninachojua, binti yangu Neema sio mjamzito wala hajafa. Yuko chuo cha uhasibu Singida akiwa anafanya kazi. Kama utamleta nimwone kuwa ndiye au siye hiyo ni juu yako, lakini binti yangu yuko hai!”

Simu ilikatwa!!

******

Saa mbili kasoro dakika nane wajumbe walikuwa tena pahala pamoja. Yaliyojadiliwa yakawekwa wazi. Kulikuwa na ugumu pande zote mbili, lakini unafuu ukaonekana upande wa Mzee Masalu. Ile kauli yake kuwa apelekewe mwaneye akamwone ilitafsiriwa na wazee kuwa ni kauli ya kiungwana na kishujaa. Huenda Mzee Masalu angeamini kuwa bintiye amefariki baada ya kumuona. Mipango ya kusafirisha ikaanza mara moja.

Kamati zikawekana sawa na marafiki wote wa Clifford wakawa tayari kwa safari. Mwili wa Neema ukaandaliwa na kurudishwa hospitali ya mkoa na mchana wa siku iliyofuata, kila kitu kilikuwa tayari. Pamoja na mchango wake katika kanisa, haikuwezekana kuwepo kwa ibada maalumu ya mazishi. Clifford alihesabiwa kuwa, kwa muda wote alishi suria, na kwa sheria na kanuni za kanisa katoliki, isingewezekana kuwepo kwa ibada ya misa takatifu. Zikasaliwa sala za hapa na pale, wanakwaya wakaimba na kuomboleza, na saa kumi kamili, safari ya mwanza ikawadia.

Gari sita zenye waombolezaji zikaanza safari, huku mkuu wa msafara akiwa Mzee Upodo huku akiwa bega kwa bega na wazee wenzake zaidi ya nane ambao wote waliamua kushiriki kukamilisha shughuli ile ambayo wangeendelea kuiwekea masihara, ingeweza kumwendea vibaya kijana wao Clifford. Tayari mawasiliano yote ya kumwomba Mzee Tegu awe Mwanza mapema ili kushirikiana na wazee wenzake kuupeleka msiba kwa Mwalimu Masagida Kaswalala Masalu yalikwishafanyika, na tayari Mzee Tegu alikuwa njiani kuelekea Mwanza.

Shughuli ilikuwa imepamba moto kwelikweli..

Ziliimbwa nyimbo, machozi yakatiririka, mafuta yakaungua, Mwanza wakatua. Saa sita na robo usiku, msafara wa magari ukawasili jijini Mwanza. Lakini tofauti na ilivyo ada ya misiba, usiku huo isingewezekana kuufikisha mwili wa Marehemu nyumbani kwao.

Nani angewaelewa ikiwa hakukuwa na maandalizi yoyote?

Wazee wakaitana, majadiliano yakafanyika na ikakubaliwa kuwa, alfajiri ya siku iliyofuata, Tegu na wazee wengine kadhaa waende kwanza nyumbani kwa Mwalimu Masagida Kaswalala Masalu na baada ya kuwekana sawa na kupima kile ambacho angewajibu ndipo sasa mwili upelekwe na msiba upate pa kufikia.

Walipitia tena mipango yao, wakachambua chambua na mila za kisukuma, wakauliza na kujibiana juu ya faini ambazo wangeweza kukabiliwa nazo ili mwili ule kupokelewa. Wakapigiwa simu wenyeji kadhaa na kuulizwa hili na lile. Baada ya masaa mawili ya kupanga na kupangua, mpango kamili ukawa umekamilika na ukakabidhiwa kwa wazee watano..

Upodo akiwa mwenyekiti, Tegu kama rafiki wa Masagida, Mzee Babudi, Makamba na Laswai kutoka Singida, na Mzee Urubani Ng’wanzalima aliyekuwa rafiki mkubwa wa Tegu na Masagida.

Wakakaa wakipiga soga na kunywa gahawa kuingoja alfajiri.

Mipango ikiwa barabara kabisa..

Hawakujua kuwa yooote waliyopanga yalikuwa ni kuteka maji kwenye kapu, waliyachota kisimani na kuyaweka kichwani, lakini walipofika nyumbani walikuwa wamelowa..

Walikuwa wakipanga na kupangua ujinga mtupu!!!




BONUS: Ili usibaki katika taharuki wewe fanya hivi, LIKE, weka COMMENT... kisha SHARE simulizi hii kwa rafiki zako… kisha mimi nitakutumia inbox muendelezo wa simulizi hii…..

MWISHO ni saa kumi na mbili jioni….


Nimefundishwa kuwa…

Mambo mengi yanayotuponza ni yale ambayo tunayafanya kwa kuwa ni ya hiyari. Kama mambo yote yanayotuzunguka yangalikuwa ni sheria, tena zisizotupa hiyari ya kuzitii ama la, huenda, narudia tena, huenda, kila kitu kingekuwa tulivu zaidi ya sasa. Lakini haiku hivyo. Tuna hiyari ya kuchagua katika kila kitu tunachokifanya. Mbaya zaidi, tuna hiyari ya kusema kweli au kuikataa kweli, na pale tunapoisaliti kweli na kuamua kuunda urafiki na uongo, tunajikuta kuwa, jambo dogo tunalolifanya kwa hiyari linajenga misingi ya matatizo makubwa yatakayotukuta kwa lazima!!

Una hiyari ya kukubali au kukataa….

******


NINAWAANDIKIA HAYA KATIKA SEHEMU YA KUMI NA MOJA


***

Alfajiri ilifika..

Ni kama kila mmoja alikuwa akimtegea mwenzake aongoze njia.

Lakini ule utu uzima wao ukawasuta na kuwakemea. Wakainuka kwa pamoja, kisha wakaingia kwenye gari moja dogo wakiwaacha waombolezaji wengine wakiwa wamesambaa huku na kule. Wapo ambao toka walipofika walikuwa wamejikita katika ulevi na kupoteza mawazo, wengine walikuwa wamelala tu garini na wengine huku na kule wakijadiliana. Clifford yeye alikuwa amejikunyata garini akiwa mgonjwa wa ugonjwa ambao haujapatiwa damu ya kuponya wala kinga ya kuuzuia.

Ugonjwa wa hofu!

Wazee walishamwonya kabisa kuwa hata kama wangekubaliwa, asingepaswa kuonekana eneo la karibu na msibani kwa kuwa angezusha tafrani isiyo ya lazima. Kule kushindwa hata kushiriki kumzika Neema wake kulizidi kumpa homa isiyotibika.

Wazee watano wakafika kwa Mzee Masalu. Ile hali waliyoikuta tu kwanza ikaanza kuwatia ubaridi. Nyumba ilikuwa katika utulivu wake na hakukuwa na dalili yoyote ya kupokea msiba. Wakatazamana na kuulizana kwa kutumia macho, lakini hakuna aliyeonekana kuwa na jibu.

Walitoe wapi jibu! Ikiwa maswali yenyewe yalikuwa lukuki.

Wakafika na kugonga hodi!

Naaam! Kidume cha futi tano unusu kikatoka kikiwa kimevalia suruali na shati huku kikiwa na kijitabu kidogo mkononi.

“Ohoooo… Bwana Tegu… Doh, Ng’wanzalima… Nawiwa nini nanyi hata mwanijia mapema yote hii?” Aliwalaki Mwalimu Masagida Kaswalala Masalu huku akiwa na uso wake ule ule ambao hata alipotabasamu, ilikuwa ni vigumu kujua kuwa alitabasamu.

“Mgeni aambiwa karibu bwana, tena mwenyeji amwekee na kifua aangukiepo” Alijibu Tegu huku akitabasamu kwa kijilazimisha.

“Tangu lini Tegu akamwomba Masagida kifua aangukiepo? Tegu si wa kuangukia popote atakapo? Labda kama kuna kingine bwana” Alisema huku akijaribu kuwatazama wengine.

“Yapo mengi dunia ya leo bwana, na tena….” Alianza Ng’wanzalima

“Wala si mengi ya kuwakurupua asubuhi yote tena na wageni watu wazima kwangu. Kama ni posa jamani si mngeniarifu niwaandae na ndugu zangu? Au bado mnataka kuniletea huo utani wa msiba?” Alijibu Mzee Masagida huku sasa akiwa amesimama dede.

Hapo akakaribishwa Mzee Upodo. Akajitambulisha, yakafuatia maneno mawili matatu ya utani wa msukuma na mnyamwezi, kisha akaingia kazini. Itoshe tu kusema kuwa, Upodo alikuwa fundi wa kujieleza. Alipangilia kwa umakini mkubwa kauli zake, akayapekua vizuri maneno kabla ya kuyatoa. Akapanga semi na tamathali zake, penye kuweza kutumia neno la kinyamwezi au kisukuma akafanya hivyo. Jambo ambalo asiye mwerevu angetumia dakika mbili tu kulielezea, yeye akatumia saa moja na dakika kadhaa.

Akaweka kituo huku wale wazee wenzake wanne wakitamani wampigie makofi, lakini wakakumbuka pale hawakuwa kilabuni wala kwenye minakasha ya gahawa. Walikuwa nyumba ya mfiwa, tena mfiwa asiye na uhakika. Wakaungana naye kwa kutikisa vichwa tu.

“Umemaliza maelezo yote mzee Upodo?” Alihoji Mwalimu Masagida Kaswalala Masalu

“Naam. Kwa tuo na kituo. Kama kuna lililobaki basi si la…”


ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

BLOG