Search This Blog

Saturday, February 26, 2022

MASHARIKI YA MBALI - 1

  

IMEANDIKWA NA : GEORGE IRON MOSENYA

********************************************************************************

Simulizi : Mashariki Ya Mbali

Sehemu Ya Kwanza (1)



Hekaheka zilizoanza takribani majuma mawili na nusu nyuma, zilikuwa zimechochea moto katika siku hii. Ikiwa ni siku moja tu kabla ya tukio lililoleta hekaheka hizo.

Katika jiji la Mainstream kilichokuwa kinazungumzwa zaidi ni kuhusiana na maandamano ya amani kupinga uteuzi wa waziri mkuu ambaye alikuwa akijihusisha na vitendo vya kishoga waziwazi. Licha ya kwamba sheria ya nchi yao iliruhusu uhalali wa vitendo vya ushoga bado wananchi hawakuridhia kabisa kuwa na waziri mkuu shoga. Walikuwa radhi kuishi na mashoga mtaani lakini sio kuwaona katika magari ya serikali wakitimiza wajibu wao.

Walishindwa kutimiza wajibu wao wa kuwa wanaume wataweza kutimiza wajibu wao kama viongozi? Hili lilikuwa swali kuu.


Baada ya kuhamasishana kwa takribani majuma mawili kwa kutumia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii. Maandamano haya yalikuwa habari kubwa sana nchini Semedari.

Mitaa ilingoja kwa hamu sana kuishuhudia siku hiyo ambayo waziri mkuu angepaswa kung’atuka kwa namna yoyote ile. Huku Mashoga na wanaoongoza taasisi zao wakifanya dua zao maandamano yale yasifanikiwe wabaki kuwa na waziri mkuu aliye upande wao.

Siku zikahesabika na hatimaye ikabaki siku moja tu.

Na sasa yalikuwa ni masaa.

_____


Daniel katunzi alikuwa amejifungia chumbani kwake tumbo likiwa linamuuma kwa juhudina kichwa kikigonga kwa fujo sana.

Hakuwa Daniel yule mchangamfu, huyu wa siku hii alikuwa amepooza sana. Wanafamilia kwa ujumla walitambua hali hii na kuhisi huenda anaumwa.

Lakini Daniel ni wa kushindwa kusema angali anaumwa? Hili lilikuwa swali la kila mmoja kujiuliza……

Haikuwa kawaida yake hata kidogo.


Akiwa chumbani Daniel alishindwa kulala kama alivyokuwa ameaga baada ya kushindwa kumaliza chakula, usingizi ulipaa mbali naye.

Alijigeuza huku na kule na kisha akaamua kuufungua mlango na kurejea tena sebuleni.

Chumbani palikuwa hapakaliki!!

Aliikuta familia nzima ikiwa imepooza…. Chakula kikiwa kama alivyokiacha.

“Dany.. unaumwa kijana wangu.” Mama wa familia ile aitwaye Diana alimuuliza kwa upole.

Ni kama swali hilo aliuliza kwa niaba ya familia nzima kwani kila mmoja alitikisa kichwa kuunga mkono.

“Kichwa kinaniuma sana. Na tumbo pia… lakini si kwamba ninaumwa.” Alijibu Daniel Katunzi kwa unyonge.

Jibu lile likawa moja kati ya mastaajabisho ya usiku ule.

Ati! Anaumwa lakini haumwi.

“Unamaanisha nini?”

“Ni kichwa kinauma na tumbo pia lakini mimi najua siumwi.” Alijibu huku akijibweteka katika kochi kubwa la kustarehe lililokuwa jirani naye. Likanesanesa kisha likatulia naye akatulia tuli.

“Kesho nd’o ile siku nadhani.” Alizungumza bila kujulikana kama anauliza ama anaanza kujenga hoja.

“Ndio Dany, kesho tunaingia barabarani… kila mmoja ameandaa bango lake nawe tumekuandalia moja utajichagulia lolote la kuandika. Ikiwa afya itaruhusu basi tutaenda wote. Tena kuandamana ni mazoezi… maana utatembea kidogo walau nawe uuone mji wetu ukijaa watu unavyokuwa. Uone wanavyotabasamu…” Maria, Binti mdogo katika familia ile ya watoto watatu alijibu kwa uchangamfu mkubwa.

“Tabasamu?” Dany alishtuka.

“Mazoezi?” akaujazia uzito mshtuko wake. Na hapo akaketi vyema akiwa anawashangaa wanaomshangaa yeye.

Wakashangaana!

“Napenda kuwashauri tubaki ndani tusiende katika maandamano hayo…” alizungumza akiwa katika mchanganyiko wa huzuni na fadhaa.

“Whaaat! Huo ni usaliti…. Familia yangu haiwezi kufanya dhambi hiyo…” Diana. Mama wa familia aling’aka akiwa wima.

“Daniel…”… Maria alimuita kwa unyonge lakini asiweze kusema lolote hata Daniel alipomtazama.

“Si chini ya miaka mitano ama sita imepita. Lakini kamwe sijaisahau Mashariki ya mbali. Mashariki inayokaliwa na raia kama mimi ambao akili zetu zimeruka na kukaa mashariki, ubongo umelalia mashariki bila kujua magharibi ni wapi sahau kuhusu kusini……” akaweka kituo akameza funda la mate na kuketi vyema akiwa anatazama chini.

“Hali ilikuwa kama hii niionayo kwenu, lakini sababu zetu zilikuwa tofauti. Naona yenu ni sababu dhaifu sana……”

“Sababu dhaifu! Una maana gani, yaani tunaongozwa na waziri aliyeolewa na mwanaume mwenzake halafu unasema ni sababu dhaifu. Semedari ni nchi kubwa sana kiuchumi duniani, haipaswi kuongozwa na mtu dhaifu….” Danstani alizungumza kwa mara ya kwanza katika hali ya kufoka. Huyu akiwa ni kijana mkubwa wa Diana.


DANIEL ANASIMULIA

Tembo walivamia kijiji cha Mafisa, huko Mashariki ya mbali ninapotoka. Uvamizi wao wa kwanza ulianza kwa kuharibu mazao. Wananchi walioharibiwa mashamba wakatoa taarifa katika serikali ya mtaa juu ya hili. Afisa wa serikali ya mitaa yeye hana shamba hivyo hakuguswa na habari hii, akaipokea taarifa na kuiweka katika meza yake kama taarifa isiyokuwa ya msingi. Mashamba yaliendelea kuharibiwa…. Tembo ni mnyama na hana akili…. Alipomalizana na mashamba akaanza kudhuru watu. Watoto wawili walikanyagwa na tembo na kupoteza maisha. Kwa sababu wale watoto hawakuwa wa afisa wa kata aliipokea taarifa na kuiweka katika meza yake kama taarifa ya ziada. Lakini usoni akihuzunika na kutoa pole za dhati kwa wafiwa.

Huzuni ya kinafiki!!

Mtoa taarifa akarejea baada ya siku nne kuulizia maendeleo yoyote kuhusu kuchukua hatua za kiusalama. Afisa akadai kuwa kwa takribani juma zima simu yake haina pesa za kupiga wala kutuma meseji (SMS). Na hapo akaanza kulalamika kuwa mtoa taarifa si mzalendo kabisa, ametoa taarifa lakini hakulipia hata senti tano ya kuchangia wino wa kujaza katika muhuri. Afisa akaenda mbali na kusema kuwa wananchi wanajitazama wao pekee wakipatwa na matatizo lakini hawatazami upande mwingine wa shilingi. Na hapo akatoa hitimisho kuwa wapambane na hao tembo kama watawaweza.

Mtoa taarifa akaondoka akiwa mwenye huzuni sana akawafikishia wakulima wenzake na wananchi waliokuwa katika kijiwe hicho.

Wananchi wakashangazwa sana na majibu yale, kwa jinsi walivyovimba kwa jazba hawakutaka kungoja. Wakaondoka kuelekea nyumbani kwa afisa huyo.

Hawakumkuta ofisini wakamfuata nyumbani kwake. Wakamfokea kwa maneno makali hasahasa ya kulewa madaraka yale madogo na kuwasahau wananchi.

Wakaondoka na jazba zao na kuhamasishana kuwa hawana mtetezi basi watalazimika kujiunda vikundi vikundi na kuyalinda mashamba yao pamoja na familia kwa ujumla.

La mgambo likalia na jambo lenyewe likatangazwa.

Baada ya siku mbili tembo wawili waliuwawa.

Na punde baada ya tembo wawili kuuwawa serikali ikahamia katika kijiji cha Mafisa. Walipouwawa watoto wawili serikali haikutokea hata msibani lakini tembo walipouwawa ikajaa pale kijijini na msako ukaanza wa nani aliwaua tembo.

Afisa wa kijiji kile alipofuatwa akawataja wahusika kuwa ni wale waliomfuata nyumbani na kumfokea, akawapatia majina ya wale waliomwandikia barua mbili ofisi kumpatia taarifa kuwa wamevamiwa na tembo.

Haraka sana wakakamatwa na kudhalilishwa mbele ya familia zao. Ilikuwa ni usiku wengine wakiwa uchi wa mnyama na wengine wakiwa na nguo fupi za kulalia.

Walipigwa sana huku wakishutumiwa kuwa wao ni wawindaji haramu.

Uharamu huo nd’o hatukuwahi kuufahamu, tembo hakung’olewa jino wala pembe yake….. aliuwawa tu.

Mmoja kati ya wale watuhumiwa alipoteza maisha akiwa rumande, polisi wakamtupa mitaroni na kudai kuwa alifanya jaribio la kutoroka wakapambana naye….. nchi ikasikia juu ya wengine sita kuwa wapo ndani na wana majeraha makubwa sana.

Kilio cha Mafisa kikadondosha chozi lake katika ardhi nzima ya Mashariki ya mbali.

Wananchi wakaanza kuhamasishana kuhusu maandamano ya amani kuhakikisha wakazi wale wa Mafisa wanaipata haki yao.

Kilichotokea nd’o kinachoniumiza kichwa hadi leo.

Hatukuwa na silaha, tulijitahidi hata tusitembee na kalamu mifukoni wasije wakasema ni visu vya kisasa. Hata waliokuwa na nywele ndefu tuliwaambia wazinyoe maana hawakawii kusema kuwa lile lundo la nywele limeficha bangi ndani yake.

Tulihakikisha maandamo yetu yanakuwa swafi kuliko namna tujiwekavyo kila tuendapo katika ibada.

Ule usafi tuliojitahidi uwe ukatuachia doa. Ilikuwa ni bahati sana ukivunjwa na kuachwa hai, kuna waliotolewa macho na hadi sasa wanamshukuru Mungu kwa kuwatetea…..

Kama mtu anamshukuru Mungu kwa kung’olewa jicho pekee. Jiulize wasioshukuru ni kipi ,kiliwasibu?

Nilikuwa naziona vita katika runinga lakini kule mashariki ya mbali nilijiona nipo katika vita, niliuona mlipuko wa mabomu na niliona kwa macho na sikio langu lilisikia mtu akiwa anataka kukata roho lugha mpya anayoiongea inavyoumiza kusikiliza hata kama hauelewi asemacho.

Mashariki ya mbali tuliuwawa kwa kujaribu tu kuwatetea wale waliokuwa wanafia rumande bila hatia. Na sio kwamba sisi tulitaka waachiwe huru la! Sisi tulitaka watibiwe wasije kufia rumande kama wenzao. Hilo tu!!!

Nikisema sababu yenu ni dhaifu msinihesabu kama muoga.

Nilishiriki maandamano yale ya amani ambayo yaligeuka vita kati ya wenye silaha na wasiokuwa nazo.

Kwa kifupi huko mashariki ya mbali tulipigana vita ya uonevu.

Shangazi yangu mpole kabisa alikamatwa akiwa katika mgahawa wake na mtoto wake mdogo mgongoni alipigwa na kupoteza maisha mbele ya mtoto wake. Kisa ni cha kuchekesha…..

Alikuwa anamwaga maji barabarani, bahati mbaya iliyoje yale maji yaliyokuwa na masalia kidogo ya ukoko wa ubwabwa yakalifikia gari la polisi lililokuwa likikatiza.

Wakasimamisha gari ghafla na kumvamia wakimlazimisha alioshe gari lile kwa sababu ana dharau.

Shangazi akalifuta gari pale palipoguswa na ukoko, wakamlazimisha aoshe gari lote.

Shangazi akahoji kwanini wanamfanyia vile angali amesema ni bahati mbaya.

Na hata kabla hawajamjibu mtoto wake akaanza kulia, shangazi akamjali mwanaye na hiyo kwao wakaitafsiri kama dharau kwao.

Shangazi aliuwawa!

Naomba muamini kuwa sababu yenu ya kesho ni dhaifu sana.

___________


Ilikuwa ni simulizi ya dakika ishirini na tano, simulizi iliyojenga ukimya wa hali ya juu. Na hata Daniel alipokinyanyua kichwa chake alikutana na uso wa Diana ukiwa umelowana kwa machozi, Maria alikuwa ameuficha uso wake, Danstan alikuwa anajikaza kiume kwa kung’atang’ata meno yake.

“Serikali ilitoa tamko gani kwa ukatili huo” Danstani aliuliza huku akionyesha jazba za waziwazi.

“What’s the fuck!! Ingetoa tamko gani Danstani, labda ingetangaza kuwa IMESHINDA VITA kwa kishindo..” Diana alizungumza huku akishindwa kudhibiti hamaniko lake.

“Daniel mwanangu. Huku kwetu hakuna kitu kama hicho. Tuna uhuru asilimia 100 wa kufanya maandamano kwa lolote ambalo tunaona kwamba halipo sawa. Ni wajibu wetu kuikumbusha serikali kuwa wananchi ni moja ya nguzo kuu katika serikali na tunapaswa kuiwajibisha serikali yetu kila inapokwenda njia isiyokuwa sahihi na bunge likiwa kimya.” Diana alimgeukia Daniel na kutoa ufafanuzi.

Akatoa ufafanuzi zaidi kwa kutoa mifano yakinifu ya matukio kadha wa kadha yaliyowahi kutokea nchini humo.

“Daniel na bado kila siku unasisitiza kuwa unahitaji kurudi Mashariki ya mbali.” Maria alimuuliza kwa unyonge sana.

“Hakika natamani sana kurudi Mashariki ya mbali. Ni huko nilipozaliwa na nitarejea. Si kwa sababu za kuibadilisha nchi bali kula kwa pamoja raha na karaha za ardhi ile.”

“Raha? Kuna raha gani katika nchi inayoua raia wake sasa…” Diana aling’aka

“Juma lililopita nakumbuka niliwasikia mkizungumzia juu ya waziri wa nishati aliyejiuzuru baada ya umeme kukatika bungeni kwa muda wa dakika tano.

Kule kwetu kuna raha ya aina yake, na raha nyingi tunazozipata husababishwa na karaha tunazopitia. Kule kwetu tukisikia waziri kama huyo aliyejiuzuru eti kisa dakika tano kwetu ni kichekesho kikubwa sana, na kwanza ni uzembe mno wa kimaamuzi. Umeme unakatwa kwa siku tatu mfululizo na waziri anapita tunapungia mkono kwa shangwe… sio raha hizo?

Katika hizo siku tatu umeme unapokatika tunatoa kila aina mpya ya matusi kwa taasisi husika, lakini hayo matusi tunaambizana sisi kwa sisi sio kwamba tunawatukana wao. Bado tu huioni raha?

Baada ya hizo siku tatu za umeme kukatika pindi utakaporejea tunaungana kwa pamoja nchi nzima, akina baba kina mama na watoto tunasema kwa pamoja ‘HUOO’. Hujapata tu sababu ya kufurahi?

Na kisha kila mmoja anaendelea na maisha yake, matusi yanaishia hewani na hatutukani tena. Ukijifanya unaendelea kutukana angali umeme umerejea watu wanabaki kukushangaa.

Lazima nitarejea Mashariki ya mbali.” Daniel aliweka kituo katika simulizi yake.

Nyuso za tabasamu zikatawala nyumba ile, Daniel alikuwa amewapa sababu mbili kwa pamoja. Kwanza aliwatupa katika msiba na vilio kisha akazisafisha nyuso zao na tabasamu japo lilikuwa tabasamu la karaha.

Wakaagana kwa mara nyingine wakikiacha kile chakula mezani na kila mmoja kwenda katika chumba chake kuuchapa usingizi.

Akiwa chumbani kaka mkubwa katika familia ile, Danstan alianza kuingiwa na ushawishi wa kuitembelea Mashariki ya mbali.

Hakujua nini maana ya tamanio lake hilo.


NAAAM! RIWAYA hii ya Mashariki ya bali itakuwa ikikujia muda na wakati kama huu kila siku mpaka itakapotimu tamati yake…….




KATIKA SEHEMU YA KWANZA:

Daniel katunzi katika hofu kuu ya kushiriki maandamano katika nchi ya kigeni, anahisi yaliyowahi kutokea Mashariki ya mbali yanaweza kujiri tena huku. Wenyeji wanastaajabu… lakini anapowasimulia juu ya mashariki ya mbali… hali inabadilika….


ENDELEA

MAJIRA ya saa nne na nusu usiku, Danstani alitoka chumbani kwake na kwenda katika chumba cha Daniel Katunzi.

Alikuwa amejaribu sana kupambana na tafakuri nzito juu ya nchi iitwayo Mashariki ya mbali…..

Akiwa ni mwanafunzi wa chuo kikuu katika masomo ya utabibu na afya ya mwanadamu, simulizi ya Mashariki ya mbali ilianza kukichanganya kichwa chake.

Kwa muda ule mfupi tangu waachane na Daniel kisha kila mmoja kuingia kulala ili kuikaribisha ile siku ya maandamano tayari Danstani alikuwa ameingia mtandaoni na kujaribu kuitafuta historia ya nchi hiyo ya Mashariki ya mbali. Alichoambulia kukutana nacho ni habari njema kuhusu nchi hiyo kubwa.

Akajiuliza. “Yale aliyotusimulia Daniel, ameyatoa wapi?”

Swali hili likamwacha katika njia panda. Akapigia mstari kuwa yawezekana Daniel hayupo sawa kiakili, na ilikuwa ni jambo la hatari sana kuishi katika nyumba moja na mtu ambaye akili yake ina walakini, husussani katika familia ile ambayo kuna watoto wadogo pia.

Danstan akamkuta Daniel akiwa yungali macho bado.

“Haujalala Daniel.” Alizungumza huku akiliendea kochi na kuketi.

“Ooh! Nimelala tayari, ni usingizi tu haujaamua kunitembelea bro.” alimjibu kiutani huku akiketi kitandani ili kumkaribu mgeni wake vyema.

Danstan hakutaka kuzunguka sana, akamuuliza Daniel kwa utulivu sana juu ya nchi aliyoisimulia.

“Unakumbuka umetoka nchi hiyo lini?”

“Hapana sikumbuki.”

“Unamkumbuka raisi wa nchi yako wakati unaondoka?”

“Namkumbuka kwa jina mpaka sura yake….” Alijibu kwa kujiamini.

“Kwanini imekuwa rahisi kumkumba raisi kuliko mwaka ulioondoka huko?”

“Mashariki ya mbali pia kuna chaguzi kama nionavyo katika nchi yenu hii. Lakini uchaguzi wa kule ni wa aina yake, una vibweka vya kila aina. Lakini namkumbuka vyema kwa sura na majina kwa sababu ya mama yangu.” Akavuta pumzi na kumeza mate kisha akaendelea kusimulia.


DANIEL ANASIMULIA


Iwe katika kuuza bagia zake na visheti, iwe katika kuuza pombe zake za kienyeji, iwe katika kutupikia chakula na iwe katika kulala. Mama yangu alikuwa anafanya kampeni kubwa sana juu ya raisi na mbunge wa chama ambacho baadaye ndicho kilikuja kuchukua ushindi.

Aliwaimbgia walevi nyimbo za kukisifu chama, tulipolalamika kuwa hatuna viatu vya shule alicheka na uso wake ukionyesha nuru. Akatumia dakika kumi kukisifu chama na kutueleza kuwa raisi atakayeingia madarakani atatununulia viatu na pia ameahidi kutoa magari ya kutupeleka shuleni. Neno lake lilikuwa moja tu “VUMILIENI WANANGU MTASOMA KAMA MALAIKA”.

Tuliendelea kusubiri naye aliendelea kupiga kampeni kwa juhudi. Naikumbuka kanga jozi moja aliyopewa na mgombea udiwani huku wakikumbatiana.

Mama yangu hakuishia hizo kampeni za chinichini, hata kwenye majukwaa mama yangu aliitwa kwa heshima zote na kwenda kucheza ngoma za kijadi huku akiimba nyimbo za kukisifu chama.

Hatimaye jua la uchaguzi likachomoza na kisha wakati ile rangi ya udhurungi ya kumaanisha linazama matokeo ya uchaguzi yalianza kuonyesha ishara ya nani mshindi.

Na baada ya siku tatu matokeo yalikuwa tayari. Ikawa ni wakati wa mama kupumzika na kuingoja neema ya sisi kuishi na kusoma kama malaika.

Uhalisia ulioonekana mwanzo ukageuka mazingaombwe, diwani akabaki kuwa mwanakijiji aliyetingwa kupita wote sio yule aliyekuwa anakuja nyumbani hadi tunasonga ugali na kula pamoja. Mbunge yeye mara ya mwisho nilimwona katika luninga, sahau kuhusu raisi.

Lakini kutoweka kwao sio tatizo, ila kilichotushtua ni kwamba waliishi na sisi wakati mama anauza pombe zakienyeji na kuwachezea ngoma majukwaani.

Walipoyashika madaraka ghafla ile pombe ikawa haramu.

Mama yangu akakamatwa kwa amri ya diwani kuwa anauza pombe za kienyeji zinazosababisha watu wawe legelege na kushindwa kwenda kazini.

Nakumbuka sura ya mama yangu siku anatolewa mahabusu, ikiwa ni baada ya msoto wa siku tatu mfululizo bila dhamana.

Alitoka akiwa amekonda sana.

Na alipotoka alikuwa amevaa kanga yake ileile ambayo mbele ina picha ua raisi na nyuma picha ya diwani.

Alinitazama kwa muda kabla chozi la uchungu halijaanza kumwagika, nilimkimbilia na kumkumbatia.

Akaninong’oneza.

“Laiti kama ingekuwa ndani ya uwezo wangu ningezivua hizi kanga muda huu na kuzichoma moto. Nimeonewa mwanangu!” alizungumza kwa hisia kali.

Tulirejea hadi nyumbani.

Kwa sababu mama ndiye pekee wa kuitazama familia alilazimika kutafuta kitega uchumi kingine.

Akaanza kukata miti na kuikausha kisha kuiuza kama kuni. Ilikuwa shughuli pevu lakini ililazimika tuifanye.

Hatukutulia sana kabla hayajatokea mauzauza mengine, barua ya kuitwa katika uongozi wa kitongoji.

Mama akaelezwa kuwa anapewa onyo la kuacha kukata miti hovyo kwani anaharibu uoto wa asili.

Uoto wa asili? Tulistaajabu, yaani kijiji chetu tumeishi hivyo kwa miaka nenda rudi tukitegemea miti ile kwa ajili ya kuni leo hii imekuwa uharibifu wa uoto wa asili?

Mama akatii! Lakini ajabu alikuja kukamatwa tena siku nne baadaye japokuwa safari hii hakulazwa mahabusu.

Mama akakosa pa kuegemea na magonjwa nayo yakaitumia fursa ile kumtembelea. Alipozidiwa sana akaniagiza kwa diwani nikamweleze kuwa ‘yule mama mcheza ngoma wakati wa kampeni anaumwa’. Mama alinisisitiza nitumie kauli ile huenda diwani amelisahau jina lake lakini sio kusahau alichotenda.

Nilifanikiwa kuonana na diwani yule mjivuni wa tabia. Akanisikiliza huku anachezea simu yake. Kisha akanieleza kuwa yapaswa tumpeleke mama hospitali maana akisema aanze kutumia ofisi yake kusikiliza ripoti za wagonjwa basi hospitali haitakuwa na kazi.

“Halafu mimi nilisomea mambo ya uongozi na utawala sio madawa na tiba asilia.” Alimalizia kwa kauli ile njema kwake, mwiba katika moyo wangu.

Nikiwa kama mwendawazimu nilienda hadi kwa mama na kumweleza kilichojiri.

Nadhani nilifanya makosa makubwa, lakini yalikuwa mazito sana yale, nisingeweza kuhimili.

Baada ya siku mbili mama alitoweka.

Tulianza kumtafuta huku na kule.

Mwisho tulimkuta akiwa katika poro lile tulilokatazwa kukata vijimiti tu kwa ajili ya kuni.

Hakuwa katika shughuli ya kukata kuni, safari hii alipanda hadi juu ya mti kabisa na kisha kwa kutumia kanga zile zilizochapishwa picha ya raisi na diwani wake na maneno ya sifa kwa chama.

Mama alitumia kanga zile kujinyonga mpaka kupoteza maisha.

Niliziona zile kanga, niliziona katika mwili wa marehemu mama.

Nilipotoka ni mbali sana, Mashariki ya mbali. Lakini nitasahau mengi mno, sio sura ya raisi yule mwenye tabasamu la mauti na diwani wake yule wakala wa kifo na mateso. Diwani mnafiki ambaye jamii ikamruhusu naye kusema neno katika siku ya maziko ya mama yangu.

Akaongea kwa uchungu mkuu huku akitumia kitambaa chake kujifuta machozi, akasema kuwa mama yangu alikuwa ‘mfia chama’ na atakumbukwa sana kwa wema wake.

Hata leo nikiiona kanga inayofanania na ile nitaitambua bila kutumia sekunde kumi kufikiri.

Mama yangu alidhulumiwa uhai wake na watu aliowathamini kwa dhati angali wao wakimthamini kwa unafiki.

Ile dhuluma ilikuwa moja ya sababu zangu za kuikimbia Mashariki ya mbali.


_________


Daniel alimaliza kusimulia mkasa ule akiwa ameketi palepale kitandani.

Danstan akasimama na kumfuata pale kitandani, akampigapiga bega kumpa pole huku akimwomba radhi kwa kumkumbusha yote yaliyojiri huko Mashariki ya mbali.

“Natamani sana kwenda kuitembelea nchi hiyo…” Danstani aliongezea.

“Kwa maisha yenu haya ya milo sita kwa siku utapaweza kweli kule?” Daniel alimuuliza kwa upole.

“Mimi ni imara sana Dany, usinione hivyo. Mimi naweza kukaa hata siku nzima bila kula au nakula mara moja tu. Sitashindwa kitu….” Alijitapa Danstani.

Daniel akacheka sana kabla hajajilaza kitandani.

“Hauamini nisemacho ama… mbona unacheka.” Alihamaki.

“Nenda ukalale kwanza. Tukimaliza maandamano ya kesho unieleze tena kama unayo nia ya dhati. Ukimaanisha nitakusindikiza Mashariki ya mbali.” Daniel Katunzi alimaliza na kumuaga Danstan McDonald kijana mkubwa wa familia ile ya nchini Semedari katika jiji la Mainstream.

Danstan alipondoka, Daniel akajisemea kwa sauti ya chini.

“Kutokula siku moja ama kula mlo mmoja huyu bwana cheupe ndo anauita ujasiri. Ama kweli tembea uyaone. Karibu sana Mashariki ya Mbali Danstan McDonald”



Goodmorning Semedari!

Ndivyo anga lingeweza kusema tena kwa uchangamfu, Semedari ilipokea mawio katika namna ya kutia tumaini, katika jiji la Mainstream ilipokuwa inaishi familia ya bibi Diana pamoja na mgeni wao Daniel, ambaye sasa hakuwa mgeni tena bali mwanafamilia kutoka Mashariki ya mbali huku napo kila mmoja alikuwa amebeba bango lake tayari kwa kuingia katika maandamano ya kitaifa kumpinga waziri mkuu anayejihusisha na masuala ya kishoga.

Ile hali ya Semedari kiujumla ilimshangaza Daniel, hapo awali alipokuwa anawaona askari alikuwa anaiandaa miguu yake kwa ajili ya kukimbia.

Ajabu na kweli! Askari waliwapungia mkono waandamanaji.

Uhuru wa aina gani huu! Alistaajabia huku akiendelea kufuata mkumbo.

“Daniel!” Danstan, kijana mkubwa wa familia hii alimwita huku akimshika mkono kumaanisha apunguze mwendo.

Daniel akatii, Danstani akamwinamia kidogo na kumweleza kwa kunong’ona.

“Unawaona hao wanaume watatu mbele yetu”

“Nawaona, si hao waliovaa masweta…”

“Ehee!! Huyo wa kushoto na huyo wa katikati nikikwambia dhamana zao hapa jijini huwezi amini na wao wameshirikiana na sisi. Nd’o maana nilikwambia hili jambo ni kubwa sana Dany…..kubwa sana” Danstan alizungumza kwa bashasha ya aina yake huku akionyesha dhahiri kuwa kila anachokizungumza anakifurahia kutoka moyoni.

“Ni akina nani?” Daniel katunzi mmoja kati ya waandamanaji wachache weusi aliuliza ili ajibiwe maana Danstan alionyesha kulingoja hilo.

“Ni waalimu!!” alisema kwa kushtukiza ili auone mshtuko wa Daniel.

Kweli Daniel akashtuka!

Danstani akabaki kuishi katika tabasamu zito la ushindi wakati anautazama mshtuko ule.

“Jiulize, waalimu na wao wameguswa wamekuja kuandamana na wananchi. Halafu useme kuwa hili jambo ni dogo, huyu mpuuzi lazima ang’oke!” sasa aliongea kwa hisia kali zaidi zilizokaribia kuwa hasira.

“Ni waalimu wa chuo kikuu bila shaka.” Alijazia maongezi Daniel katika namna ya kuuliza swali lenye jibu tayari.

“Hapana, mmoja anafundisha shule anayosoma Maria ni shule ya msingi na huyu mwingine ni wa hatua ya awali. Anapendwa sana hapa mainstream na anaheshimika… unajua mwalimu ni mzazi namba mbili kwa mwanao.” Akaweka kituo kama mtu asiyetarajia upinzani wowote.

Daniel akatikisa kichwa akiwa anasikitika.

“Tunaweza kupata nafasi ya kuzungumza tukiwa katika treni?” Daniel alimtupia swali.

“Haswaa! Bila shaka.”

“Basi tutazungumza.”

_____


Baada ya dakika kadhaa tayari walikuwa ndani ya treni ya umeme kuelekea katika eneo la makutano kwa ajili ya maandamano ya amani.


DANIEL ANASIMULIA.

Unavyozungumzia waalimu, ama kuwa mwalimu…. Huko Mashariki ya mbali baada ya miaka kadhaa neno ‘mwalimu’ linaweza kuwa mojawapo kati ya tusi la kutosha kumtia mtu hasira akarusha konde. Ukiachana na matusi yaliyozoeleka ya kutukaniwa tupu ya mama yako katika namna ya mzaha na haukasiriki.

Tupu ya mama ni jambo la kawaida sana Mashariki ya mbali.

Sitaki kuamini katika simulizi za zamani nilizowahi kuzisikia eti kuwa kuna kipindi waalimu waliwahi kuwa watu muhimu katika nchi ile.

Kwa sababu sihitaji ulaghai uliojaa katika historia zisizo’maana basi ni heri nikuelezee niliyoyashuhudia tu katika kizazi nilichokiacha huko Mashariki ya mbali.

Maelfu ya watu ambao ni waalimu wanajificha katika kujitambulisha kwa sababu ukiwa mwalimu unaweza ukakosa mke unayemuhitaji na badala yake ukapata mke atakayekusaidia kutimiza maandiko ya nendeni mkazaane muujaze ulimwengu.

Ukiwa mwalimu kuna baadhi ya wadogo zako hawatakanyaga nyumbani kwako kwa lengo la kuja kuimalizia likizo yao huko. Ukiona amekuja ni aidha amekosa pahali pa kwenda, ama la anatimiza usemi usemao kuwa damu ni nzito kuliko maji.

Yaani hata watoto wadogo wanafahamu kuwa ualimu ni ugonjwa!!

Ukiwa mwalimu jiandae kuishi maisha ya mashaka ya kutoijua kesho yako. Huku serikali haijakupa ongezeko la mshahara angali unazidi kuukaribia uzee na hakuna ulichofanya, na huku wanafunzi wanakusubiri mtaani wakuponde mawe kwa sababu uliwacharaza bakora walipofanya makosa shuleni, na hapa unapaswa kuvumilia kuhusu majina ya kishenzi watakayokuwa wamekubandika bila sababu za msingi.

Danstan! Hebu fikiria, mwanafunzi ambaye wewe mwalimu ni sawa na baba yake, anakitazama kichwa chako jinsi ulivyo mweusi na kisha anaweka kikao cha dharula na wanafunzi wenzake wanakubandika jina wanakuita ‘KOBOKO’.

Huyu anayefanya hivi ni mtoto unayeweza kumzaa.

Waalimu wa kike wanaipata shughuli zaidi; huku kwenu naona wanafunzi wana miili mikubwa lakini wana nidhamu.

Huko mashariki ya mbali, mwanafunzi ana mwili mkubwa, akili za kupima kichwani na bado nidhamu hana.

Mwanafunzi kama huyu anaenda kumtaka kimapenzi mwalimu wake wa kike.

Nidhamu ipo wapi!

Sawa, tuseme kuwa haya yanaweza kuvumilika. Vipi kuhusu kuingizwa kinguvunguvu katika siasa, yaani mshahara hauongezwi, lakini wakati wa mambo yao ya siasa wanawatumia waalimu tena ni jambo la lazima sio ombi.

Fulana za chama mtavaa, ukijifanya mpinzani jiandae kufanyiwa fitina na kuipoteza kazi yako….

Nikitumia kaulimbiu kuwa ‘waalimu wa mashariki ya mbali hawana tofauti na mpira wa kiume (kondomu), wanatumika na kukosa maana wanatupwa huko’, je? Nitakuwa nimekosea hapo?

Sijawahi kumsikia Maria akirejea nyumbani huku analalamika kuwa amecharazwa viboko shuleni.

Ama! Ule utabiri wa hayati mama yangu kuwa tutasoma na kuishi kama malaika nadhani alikuwa anazungumzia nchi yenu. Nchi ambayo hakuwahi kuota kuna siku atafika…

Waalimu wa kule kwetu wamechanganyikiwa, akili zao zimeelekea mashariki tayari. Wamegundua kuwa serikali haina mpango nao, wametambua tayari kuwa wao ni ‘mipira ya kiume’.

Na wameamua kuishi hivyo!

Mwanafunzi hapaswi kustaajabu akicharazwa jumla ya viboko arobaini hadi hamsini kisha akaongezewa adhabu ya kuchimba kisiki na shimo la kutupa taka (jaa). Mimi nashindwa kuielewa Mashariki ya mbali, hadi sasa ni ngumu kuzungumza jambo na kujikuta unautetea upande mmoja kwa asilimia mia.

Mfano waalimu na akili zao zilizolalia mashariki badala ya kuangalia wanapambana vipi na serikali yao. Wao wanatumia hasira zao kuzihamishia kwa mabinti wasiojua mbele wala nyuma.

Mwalimu wa kike kutongozwa na mwanafunzi inaonekana kama mwanafunzi amelaaniwa.

Najiuliza ni laana kilo ngapi watakuwa wamebeba waalimu wa kiume katika nguo zao kwa kuwatongoza wanafunzi wa kike na kuwaharibia lau ndoto zao ndogondogo za kumaliza kidato na kisha kuolewa.

Kosa kubwa ni pale ambapo mtoto wa kike atajaribu kukataa.

Mwalimu wa Mashariki ya mbali atageuka malaika mtoa roho na atakuwa akiisaka roho ya huyo binti kwa udi na uvumba.

Na ili usitolewe roho huna budi kukubaliana na ombi ambalo limegeuka kuwa shurti!!!

Inasikitisha, inachekesha lakini zaidi inatia hasira. Hizo jazba kwa nini usiziunganishe ukawashirikisha waalimu wenzako ili muupe likizo ule ujinga wa kuwa ‘ma-kobe’ mbele ya chama tawala, kwanini msikasirike na kukataa katakata kuwa hamtaki kuwa kama ‘mipira ya kiume’.

Kweli ni jambo la kipekee ulilonambia Danstan kuwa waalimu wameungana nanyi katika maandamano. Kule kwetu hawahawa waalimu watatekenywa kidogo na ahadi ya ongezeko wa mshahara, hiyo ikiwa hadi ya kumi mfululizo bila matekelezo.

Watakaririshwa nyimbo za kutisha na kwenda kuziimba mbele ya wanafunzi ili wasithubutu kuandamana na zaidi wakiuunge mkono chama kilichoondoa uhai wa mama yangu mzazi.

Inasikitisha sana lakini sina budi kusema kuwa waalimu wa nchini kwangu sifa kuu waliyonayo ya kipekee. Huenda ni watu wanaopokea salamu nyingi kila siku kuliko waajiriwa wengine.

Shkamoo mwalimu!

Upuuzi!

______


Danstan alikuwa amechachamaa usoni bila kusema neno lolote wakati anamsikiliza Daniel.

Uso wake ulikuwa mwekundu sana kwa hasira.

“Daniel nahitaji kufanya ukombozi katika hiyo nchi ya Mashariki ya mbali. Hao wanaoteseka ni wanadamu kama sisi… kwanini waendelee kuishi maisha hayo ya mashaka. Nahitaji sana kufanya kitu.”

Daniel akamtazama Danstani kwa sekunde kadhaa. Na bila kufungua mdomo wake akabaki kujisemea kichwani huku akiwa bado anamtazama.

“Huo uso umekuwa mwekundu bila kupigwa, wewe ukikutana na askari kijana wa kule kwetu aliyekosa mshahara kwa miezi mitatu. Akucharaze na kirungu chake kabla hajakutishia bastola…. Utakufa bila kuaga ndugu yangu”

Baada ya kujisema hayo akafungua kinywa chake. “Danstan… unataka kwenda kuwakomboa watu ambao wameshindwa kujikomboa wenyewe. Yaani ukombozi Mashariki ya mbali ni mgumu sana, kwa kusimuliwa unaweza kuuona ukombozi unawezekana lakini kiuhalisia ambao unataka kuwakomboa wao hawapo tayari. Tazama Danstan, huko Mashariki ya mbali mwanamke anaolewa iwe kwa sherehe ama iwe kwa kutolewa tu mahari na wengine mahari haitolewi. Mwanamke huyu anajikuta katika utumwa wa ndoa, majirani wanasikia kabisa jinsi anavyopigwa na mume wake mlevi, wanayaona manundu yanayoweka ‘parking’ katika uso wake. Mwanamke anapambana kuvaa vazi la hijabu ili kuyaficha manudu, hii inamaanisha anapambana kuuficha uovu wa mume wake.

Majirani wakihoji anasema hakuna kinachojiri, mpaka siku anadidimiziwa visu ndipo anapiga kelele kuomba msaada. Wewe unayejiita mkombozi unaenda kumkomboa nani Mashariki ya mbali.

Tunaelekea maandamano ya kumpinga huyo Shoga ambaye ana dhamana kubwa serikalini…. Lakini kule kwetu kwa ‘ujinga’ wao wa kuamua kuwa kimya, akinamama wengi tu wanaingiliwa kinyume na maumbile. Hawasemi wanajikaza eti kisa tu kumfurahisha mume. Na baadhi yao nd’o wale ambao kilio chao kila siku kilikuwa “Lini tunamaliza shule nikaolewe??”

Haya Danstan, kama mtu anajikaza ili kumfurahisha shetani wewe unataka kwenda kumkomboa nani?

Au unataka kwenda kuwabadili mashetani wauache ushetani wao.

Ajabu katika mashariki ya mbali, unaweza kumbadili shetani akauacha ushetani wake, halafu yule aliyekuwa anafanyiwa ushetani akaanza kulalamika ‘Shetani unafanyia wapi ushetani wako mbona mimi haunitembelei siku hizi”

Je? Unajiandaa kupasuka kichwa ndugu yangu….” Daniel aliweka pumziko akamtazama tena Danstan.

“Unamaanisha kuwa mwanamke anaingiliwa kinyume na maumbile, mume akiacha kufanya hivyo atamuuliza anafanya wapi siku hizi?” alihoji akiwa amehamaki.

“Tena kwa hasira na wivu mkali…” Daniel alijibu kwa kumalizia ile kauli ya Danstan.

Danstan alishusha pumzi zake kwa nguvu sana….. hakuamini alichokuwa anakisikia. Ni kama alikuwa anatazama filamu ya kutisha sana.

“Bado unatamani kwenda kufanya ukombozi… hayo niliyokueleza ni machache tu…..”

“Aaah! Nitaenda kutembea na kusalimia ndugu, jamaa na marafiki” Alijibu bila kujua hata anachojibu.

Daniel akatokwa na cheko kubwa sana. “Una ndugu na jamaa Mashariki ya mbali tangu lini?…” akamalizia na cheko tena.

Danstan naye akajikuta anacheka sana. Hakika hakujua alichokuwa amejibu.

Cheko lile likakoma pale treni ya umeme iliposimama mahali husika ambapo maandamamo yalipangwa kuanzia.

Daniel akamwomba Mungu lisije kutokea lolote la kusababisha vurugu, hakutaka kuyapitia tena maumivu makali aliyowahi kuyapitia hadi kujikuta akiimbia nchi yake ya Mashariki ya mbali.


NAAM! Mambo ndo yanazidi kuwa mambo…. Je? Danstan atatimiza azma yake???

Nini hatma ya maisha ya Daniel katika nchi isiyokuwa yake…..





DANSTAN hakuwa na shamrashamra ya maandamano tena, alikuwa pale kutimiza wajibu lakini kiuhalisia alikuwa na matamanio zaidi kusikia juu ya nchi hiyo; ambayo kwake yeye ilikuwa nchi ya maajabu makuu.

Mashariki ya mbali!

Daniel alishiriki maandamano yale kikamilifu, maandamano ambayo baadaye yalisababisha waziri yule mkuu kung’atuka kutoka katika nafasi yake na kukiacha kiti wazi kwa ajili ya kulinda amani ya nchi ya Semedari.

Kitendo chake chake cha kuachia ngazi kilihesabiwa kama ushujaa kwa nchi yake.

Kila familia ikarejea katika makazi yake huku wakifurahia juhudi zao.

Daniel alikuwa katika kustaajabu yaliyokuwa yanajiri katika nchi hii ya ugenini. Mambo yalikuwa yanaendeshwa kwa kutumia weledi mkubwa huku utu ukiwekwa mbele. Na demokrasia ikiheshimiwa sana.

Wakati wanarejea nyumbani ikawa ni nafasi ya Daniel Katunzi kuuliza mambo kadhaa juu ya tukio hilo.

“Inavyoonyesha huyu sio mtu wa kwanza kuachia madaraka. Maana waandishi wa habari sijaona hata kama wameshtushwa sana….”

“Haswaa! Sio tukio la kwanza, uzuri katika nchi yetu hii katiba inasisitiza juu ya kiongozi kuwajibika ama la angoje kuwajibishwa na wananchi. Huku kwetu katiba inaeleza kuwa kiongozi na mtawala ni vitu viwili tofauti. Na hatuhitaji kuwa na mtawala kwani tunaweza kujitawala wenyewe. Tunahitaji kuwa na kiongozi ambaye tunamwingiza katika ajira kwa kumpigia kura ambazo anaziomba kwetu kwa unyenyekevu mkubwa. Jijini kwetu pale kuna meya aliwahi kutoa amri ya kukamatwa mtu ambaye hakuwa ametenda kosa, mtu huyo akabaki mahabusu akiteseka kwa kuukosa uhuru wake. Baadaye ikaja kubainika kuwa hakuwa ameteenda kosa. Ilikuwa ndani ya masaa ishirini na nne tu baada ya jambo hilo kugundulika, akaomba radhi na kujiuzuru nafasi yake ya umeya. Licha ya hayo yote jamii haikuwahi kumsamehe. Alihamia jiji jingine yeye na familia yake. Huku katiba inatulinda sana..” alimaliza kujieleza Danstani.

Tabasamu hafifu liliuchukua uso wa Daniel kabla halijatoweka na kuacha hamaki iliyomweka katika unyonge na uchovu wa kufikiri.

Akajikuta katika mwayo mrefu kabla hajaanza kuzungumza.

“Uwe umeiba, haujaiba, uwe unamjua mwizi ama haumjui. Ni haki yako kuwekwa mahabusu nchini kwangu.

Uwe una umri mdogo, uwe hauna akili timamu, uwe mwendawazimu, uwe na timamu. Mahabusu ni haki yako.

Useme ukweli,useme uongo. Uwe mwanamke asiyezaa ama anayenyonyesha. Mahabusu utaingia na virungu utapigwa.

Msamiati wa kujitathmini na kuwajibika upo katika kamusi yetu lakini hautumiki tena. Kurasa zake zimeandikwa kwa lugha za kigeni ili wazawa wasiweze kuzisoma.

Umenifurahisha sana kwamba meya alijiuzuru wadhifa wake kisa kamweka rumande mtu asiyekuwa sahihi!!?.... halafu licha ya kujiuzuru na kuomba radhi wananchi hawakumpa msamaha!!

Kule kwetu, virungu unapigwa, anatukanwa mama yako aliyekuzaa jumlisha na ukoo wake wote, rumande unaingia, kosa haujafanya na baadaye ukitoka hakuna mjinga atakayekuomba msamaha. Wewe ni nani katika Mashariki ya mbali mvaa suti mmoja akuombe msamaha?? Eeh! Wewe ni nani Danstan? Si uende basi ukajionee!!” Daniel alijikuta akizidiwa na jazba.

“Basi Dany… imetosha… imetosha ndugu yangu. Nilikuwa najaribu tu kukuelezea namna gani huku kwetu katiba inatulinda sana…. Maana huku kwetu ni heri wabaki wakosaji mia moja uraiani kuliko mwenye haki mmoja kutiwa gerezani kimakosa.” Alimalizia kwa upole sana Danstan ambaye sasa alikuwa ameifuta ile dhana ya kwamba huenda Daniel ni mgonjwa wa akili. Sasa alikuwa anaamini kuwa ipo nchi iitwayo Mashariki ya mbali.

Wakati Daniel akishusha pumzi zake kwa juhudi, treni ya umeme ilisimama katika kituo kwa jili ya abiria wengine kujumuika katika safari.

Akaingia mama mjamzito, hakudumu kwa dakika moja kabla hajawa na chaguo la wapi aketi kwani kila mmoja alijaribu kumpisha katika nafasi, kwa sababu tayari nafasi zilizokuwa zimejazwa na waliotanguliwa.

Daniel akajikuta akitokwa na cheko la ghafla peke yake kati ya abiria wote.

Danstan akashtushwa na cheko lile ambalo hakujua lilipotokea.

“Kulikoni mzee!” alihoji.

“Nimekumbuka tena Mashariki ya mbali. Na sasa natamani kweli twende mimi na wewe ukajionee haya ninayokusimulia kuwa sio ya kubuni bali wakazi mamilioni wanayaishi maisha haya na wanayaita maisha ya amani na furaha.

Tazama huyo mama alivyopishwa aketi, vitendo kama hivyo huenda nd’o vinasababisha huku kwenu wanazaliwa watoto wana sura nzuri sana za kuvutia. Mashariki ya mbali basi tu tunalindwa na imani mlizotuletea ninyi wakati mnatutawala kwa manyanyaso makubwa, mkatueleza kuwa ‘Mungu ametuumba kwa mfano wake’. Basi usemi huu ndo unatulinda, hata ukizaliwa na sura inayofanania na msukule mzoefu. Unarejea ule usemi na kujitetea.

Ila kwa dhati tunaharibika tangu tumboni.

Kule kwetu mtoto anaanza kukasirika tangu akiwa tumboni, fikiria mtoto anajionea waziwazi jinsi alivyokuwa mzigo kwa mama yake halafu anafika eneo kama hili kila mtu anamuangalia tu bila kujali. Kama hiyo haitoshi mama anarushiwa tusi, mtoto analipokea akiwa tumboni. Kwanini sura isikunjamane!

Mashariki ya mbali upishwe siti?? Thubutu labda iwe katika kipindi cha ile miezi wanayoiita mitukufu, ule wa Ramadhani kwa waislamu na kwarezma kwa wakristo; maana miezi hii nd’o shahada za unafiki huongezeka huko kwetu. Kinyume na hapo jitahidi kuwa imara tu maana ukijifanya unajua kuongea ukaanza kulalama haujapishwa nafasi utalisikia jibu mubashara kutoka kwa kijana anayeweza kuwa mwanao ama mdogo wako wa mwisho. Atakuuliza swali jepesi ambalo kinywa kitaona aibu kutoa jibu.

‘wakati mnabinuka katika starehe zenu tulikuwa wote?’.

Si unalisikia hilo swali, jibu ni jepesi tu lakini hakuna awezaye kujibu. Hivyo mama mjamzito kule hana thamani ya kuwatikisa watu waguswe kumpisha nafasi kama hivi.

Na tatizo hili sio la upande mmoja, ni pande zote akinamama wa Mashariki ya mbali ni mabingwa wa kujishushia heshima wenyewe. Wanafahamu kuwa wao ni akinamama tayari lakini hawauishi umama wao. Hawa nd’o mabingwa wa kutukanana mitaani, ama unakuta hilo tumbo alo’beba ni mzigo kutoka kwa kijana umri sawa na mwanaye wa pili.

Nani akuheshimu sasa ikiwa we mwenyewe umeshindwa kuziheshimu sehemu zako za siri??

Ujue Danstan unaweza kusema mapenzi hayaangalii umri. Lakini hivi kweli mtoto mdogo ni wa kumpa siri nawe ukasema ataitunza??

Ukiweka imani kuwa mtoto mdogo atakutunzia siri, ugonjwa wa akili ulio katika kichwa chako. Tiba pekee ya kuuponya ni kukikata kichwa chako, kisha kukisaga saga, maana tukisema tukitupe. Atatokea mtu atakiokota atakivaa na kuishia kulekule.

Akinamama haohao wakishajifungua hawapitii mabadiliko yoyote, unakuta mama mtu mzima anamtukana mtoto wake matusi mazitomazito tangu masikio yanapofunguka. Mtoto kama huyu ambaye matusi sio kitu kipya kwake atashindwa vipi kumtusi mama mjamzito ndani ya gari ama treni kama hii.

Danstan! Siyahubiri haya kwa ubaya kwa sababu tu sipo Mashariki ya mbali, nayahubiri kwa wema kabisa. Kwa sababu kinywa changu kinanena ukweli mtupu. Ukweli ambao wanamashariki ya mbali wanautambua lakini midomo yao imetiwa ganzi hawawezi kusema na hata wakisema wale wasikilizaji wametia pamba masikioni hawawezi kusikia.

Na ushukuru sana wasiposikia maana wakisikia, wataacha shughuli zao zote chache za maana na nyingi za kipuuzi kisha watakushukia kama tai wa jangwani, wataing’oa shingo yako.

Baada ya hapo watajitangazia ushindi dhidi ya adui mkubwa. Wataandaa hadhira yao ambayo muda wote itapiga mbinja na vigelegele.

Danstan, ukipata likizo ya mwezi mmoja nitaomba sana twende Mashariki ya mbali.

Kabla ya kwenda huko jitahidi kuupa mwili wako wote zoezi la kukabiliana na hasira ndogondogo. Maana Mashariki ya mbali kila upande utakaogeuka unaweza kukusababishia hasira.”

Danstan alimtazama Daniel wakati anaweka kituo kikubwa.

“Unadhani nitaweza kurudi nikiwa hai. Mbona yaonyesha Mashariki ya mbali ni nchi ya kutisha sana.” Danstan aliuliza huku akiwa na dalili zote za uoga.

Kwa mara nyingine tena Daniel akazungumza bila kufungua kinywa chake.

“Ushaanza kutetemeka wakati upo katika nchi yako na umepanda treni ya umeme, hivi utakuwa katika hali gani ukiwa katika mbanano mkubwa wa garimoshi za mashariki ya mbali, kisha baada ya mbanano ukagundua kuwa katika ule mbanano kuna mtu amechukua pesa zako bila hiari yako mwenyewe. Si utarukwa na akili kaka yangu, ndugu zako waseme umetupiwa majini ya Mashariki ya mbali?”

Na baada ya hapo akafungua kinywa safari hii alizungumza na kusikika.

“Ninatokea Mashariki ya Mbali Danstan. Kuingia katika nchi yangu ni bure kabisa, lakini kuishi ni umauti, kutoka pia ni bure lakini hautatoka kama ulivyoingia…. Utatoka wewe na pumzi utaziacha mashariki ya mbali. Utarejea mzoga wako usioweza kusimulia chochote kilichojiri…… hakuna atakayejali kuhusu wewe pindi utakapotupatupa miguu yako na kuyakaribia mauti.

Sikuzuii kuzijua mila na desturi zangu….. nimekupa onyo tu ikiwa kweli nia yako ni thabiti……

Treni imefika mwisho Danstan… tushuke!”

Hata alipomkumbusha kuwa walikuwa wamefikia ukomo wa safari, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka Danstan!



“Katika maisha tunakumbushwa kuwa watu wa kujaribu ili tuweze kuyafikia malengo yetu. Pia tunasisitizwa kuwa kuanguka ni sehemu tu ya safari ya mafanikio.

Lakini hakuna mahali tumeelekezwa kuijaribu sumu kwa kuilamba, kuyajaribu makali ya wembe katika ngozi zetu, kuujaribu usemi wa mtoto wa nyoka ni nyoka kwa kumpatia kidole…..

Sio kila kitu ni cha kujaribu katika haya maisha….


NA HII NI SEHEMU YA TANO


GIZA lilikuwa limetanda katika namna yake ya kawaida lakini likitiwa chachandu ya aina yake na wingu zito lililokuwa limetanda angani kisha kibwagizo cha umeme kukatika kukalifanya eneo lile kuwa mojawapo kati ya maeneo ya kutisha zaidi ulimwenguni.

Kibatari kilichonyong’onyea kwa utambi wake kuikosa haki yake ya msingi ya mafuta kilisaidizana kwa ukaribu na mshumaa uliozidi kutenda wema wake wa siku zote.

Hata siku hii ulitenda wema wa kummulika mgonjwa aliyechanika vibaya mguu wake, hakuna umeme na ni kibatari na mshumaa katika kuhakikisha mtaalamu wa afya analiona jeraha na kulipatia tiba stahiki.

Tiba stahiki la! Haikuwa tiba stahiki, mtaalamu wa afya alikuwa anajaribu kufanya lolote lililokuwa ndani ya uwezo wake. Na pengine hata nje ya uwezo wake.

“Daktari hautafanya makosa kweli katika giza hili?” aliyemleta mgonjwa alimuuliza mtaalamu yule huku uso wake ukiitangaza hofu kuu.

Giza lilimstiri!

“Mimi si daktari. Nilitamani niwe lakini sikuwahi na sitakuja kuwa. Mimi ni muuguzi tu..” alijibu mtaalamu yule huku akiendelea kuyakaza macho yake kutazamana na jeraha lile linalovuja damu.

“Ati nini! Sasa utaweza vipi kushona jeraha hili angali wewe ni muuguzi tu.” Alihamanika.

“Aah! Hata hivyo nakaribia kushindwa kulishona. Nadhani muda si mrefu jibu utalipata.” Alijibu kwa utulivu mkuu huku akiwa anaendelea kutazamana na jeraha lile kana kwamba kuna mazungumzo ya siri anafanya na jeraha lile kwa kutumia lugha inayotambuliwa na pande mbili tu.

Muuguzi na jeraha!

“Tafadhali sana, hebu fanya kitu hiyo damu ipungue dakt… aah! Muuguzi.” Alikwama alipotakakumuita tena kwa kile cheo cha daktari.

“Unaweza kuendelea kuniita daktari, ndivyo wanavyoniita katika kijiji hiki kila wanapopata matatizo.” Alijibu muuguzi yule pasi na kutikisika. Bado alitazamana na jeraha.

Walifanania na majogoo yaliyotwangana na sasa kila mmoja amechoka lakini hata asiwe tayari kusalimu amri.

“Vyovyote… tafadhali fanya kitu.” Mleta mgonjwa aliendelea kuzungumza kama anayelalamika na nusu akiwa anachanganyikiwa.

“Hapa kuna njia mbili za kuikausha hii damu…” alianza kuzungumza yule muuguzi wa kike. Akaiacha ile kauli hewani kisha akageuka na kumtazama bwana aliyemleta mgonjwa wake.

“Tujaribu kumuwekea chumvi…” alisema kwa utulivu mkubwa sana.

“Aaah! Hapana, hapana…. Hiyo siyo njia sahihi. Chumvi itasaidia nini katika jeraha lote hilo. Chumvi itasaidia nini rafiki…sidhani kama ndivyo taaluma yako inavyoelekeza” aling’aka mleta mgonjwa.

“Nilisema kuna njia mbili. Ya pili ushaijua kwani?” Muuguzi akajibu kwa upole bila kujali kuchanganyikiwa kwa mleta mgonjwa.

“Sawa nieleze yaweza kuwa bora… lakini sio kumuwekea chumvi” alijibu kisharishari.

“Utalazimika kufumba macho ukemee kwa imani zako za kiroho damu hii iweze kukatika na kidonda hiki kijifunge mara moja iwe katika jina la Yesu, Mtume Muhamad, ama majina ya mizimu ya babu yako.” Alijibu kwa upole kabisa.

Mleta mgonjwa alijikuta naye anapatwa na ugonjwa wa ghafla.

Mapigo yake ya moyo yalipiga mara mbili ya kawaida, hakuamini kuwa maneno yale yanatoka kwa mtaalamu ambaye anamtegemea amtibie mgonjwa wake katika kile kiza kinene sana.

“Yaani…. Kweli kabisa unani…aaargh!” alighadhabika. Na hapo yule muuguzi akautua chini mguu wa mgonjwa yule asiyekuwa na fahamu zake. Sasa akamgeukia mleta mgonjwa.

“Njia ya tatu ipo…… ni kuendekeza maswali yako ya msingi sehemu isiyokuwa sahihi, hasira zako za kipuuzi kwa mtu aliyebeba mguu mzito wa mke wako sijui mchumba wako, hadi pale atakapokata roho ukahangaike kutafuta mahali pa kumfukia. Napenda kukukumbusha kuwa, kibatari kinakaribia kuzima, mshumaa unakata viuno kuelekea sakafuni na katika kituo hiki tuliahidiwa huduma za vyumba vya kulaza maiti. Huu ni mwaka wa kumi tangu niisikie ahadi hiyo na utekelezaji haujawahi kufanyika. Akifa huyu utambeba mgongoni….” Muuguzi alizungumza kwa ukali na alikuwa akimtazama moja kwa moja mleta mgonjwa yule ambaye alikuwa amejaribu kuyatawala maongezi hapo awali.

Mleta mgonjwa yule alijisogeza hadi nje baada ya kumwomba radhi yule muuguzi na kumsihi amsaidie mgonjwa wake.

Alipofika nje akiwa analindwa na lile giza totoro alianza kuangua kilio cha uchungu mkali.

Kilio cha mtu mzima.

Kilio kisichoambatana na sauti bali mifereji ya machozi, zikiwa ni salamu kutoka katika moyo unaougulia.

Akayafumba macho yake na kuyakumbuka maneno ya wazazi wa yule binti jinsi walivyomsisitiza.

“Danstani, huyo ni mchumba wako sawa… lakini kwetu sisi ni mboni. Jitahidi umlinde kadri uwezavyo, afike na tabasamu lake, arejee na tabasamu lake hivyohivyo.”

Maneno yale yalijirudia katika masikio yake kana kwamba yanatamkwa kwa mara nyingine tena na wazazi wa binti yule aitwaye Cherry.

Sauti zile kabla hazijatoweka vyema, akakumbuka ni kiasi gani Cherry alimkataza katakata juu ya uthubutu wake wa kufanya ziara katika nchi ya Mashariki ya mbali.

Jambo ambalo lilikaribia kuupoteza uchumba wao katika shimo la hewa.

Kama zisingekuwa busara za Cherry kuchukulia uzito wa mapenzi yao basi wangekuwa wametengana na safari ya Mashariki ya mbali ingemuhusu yeye pekee ama na mtu mwingine.

“Ni nguvu ya mapenzi inanipeleka Mashariki ya mbali pamoja nawe, kinyume na hapo nisingekanyaga huko. Wewe endelea kumwona Daniel kama tahira lakini kumbuka kuwa hata saa mbovu kuna muda wake wa kuwa timamu.”

Yalikuwa maneno ya Cherry siku ambayo anakubaliana na Danstan waweze kufanya safari ya kwenda Mashariki ya mbali.

Wapo Mashariki ya mbali, Cherry hazungumzi tena. Usafiri wa baiskeli katika vijiji unakuwa nuksi kwa Cherry, utelezi unamsomba muongoza chombo anaruka mbali na kumwacha Cherry atoe salamu za ghafla kwa ardhi iliyonuna.

Jiwe linamchana vibaya mguu wake na kulazimika kukimbizwa hospitali.

Hospitali gani kijijini?

Zahanati!!

Sawa tuiite zahanati. Kama tu! hakuna jina jingine zaidi ya hilo.

Huku wanakutana na huduma ya aina yake, umeme hakuna, kiza kimetanda na kunogeshwa na wingu zito.

Cherry Stanley aliyezoea huduma za kisasa nchini Semedari katika jiji la Mainstream sasa yupo mahali ambapo ukiwa hai unaishi na matatizo, ukipoteza uhai wewe unageuka kuwa tatizo zaidi.

Baada ya kukubaliana na hali halisi kuwa ile haikuwa ndoto bali kweli tupu. Danstan McDonald aliingia tena ndani na kumkuta muuguzi akiwa amefanikiwa kushona jeraha lile la Cherry, na alikuwa amemlaza chini akiendelea na shughuli nyingine.

“Nadhani angelazwa kitandani. Samahani kwa kuingilia utendaji wako mtaalamu.” Alizungumza kwa utulivu.

Nidhamu ilikuwa imekaa mahala pake.

"Inasemekana wazungu walimkabidhi mbunge wetu vitanda na magodoro, akavihifadhi nyumbani kwake baadhi, kisha akampatia diwani baadhi avilete katika zahanati yetu, diwani ana zahanati yake mjini, akavipeleka kule na hapa alileta vitanda viwili tu huku akiambatana na wapiga picha watatu kwa ajili ya kumuhoji na kumpiga picha akikabidhi vitanda.

Kuna siku wagonjwa waligombania kitanda almanusra wapigane. Nikamueleza daktari siku aliyopita kutusalimia juu ya tukio hilo. Alikasirika sana kisha akafanya maamuzi ya busara. Akavichukua vitanda vile na kuvipeleka nyumbani kwake. Akasema kuwa ‘wakose wote’.” Alijibu muuguzi huku akiendelea na shughuli zake.

“Yaani! Daktari anatoa maamuzi kama mtoto mdogo….” Kabla hajamaliza muuguzi akaingilia kati.

“Ni vyema unamdhihaki angali hayupo. angekuwepo angeliweza kuongozwa na pombe zake akakuchoma sindano ya sumu ukafa….”

Kauli ile ilimtia hofu ya ghafla Danstan, akajikuta anapayuka akiwa amehamanika.

“Namshtaki siwezi kukubali dhuluma na unyanyasaji wa kiwango hicho mimi. Mimi sio kama hao wengine… ajue hilo.” Alifyatuka maneno kwa jazba.

“Ubaya ni kwamba utakapomshtaki katika hiyo mahakama ya wafu ni wewe pekee utakuwa mfu yeye atakuwa hai. Malalamiko yako huoni kama yatachukua muda mrefu kusikilizwa?” Muuguzi alizungumza huku akiwa anajinyoosha mgongo wake. Hakuwa na haraka wala papara kwa lolote alilokuwa anafanya.


ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

BLOG