Search This Blog

Saturday, February 26, 2022

ZAWADI YA ADHABU - 3

   

Simulizi : Zawadi Ya Adhabu

Sehemu Ya Tatu (3)


“Potelea mbali.. Najua ataniadhibu.. Au atanitukana. Au ataniambia “Nilikuonya”, lakini sijali.. Hayo si zaidi ya adhabu wanazonipa hawa nyamaume!” Alijisemea huku akilisogelea geti la nyumbani kwao, nyumba ambayo hakuwa amefika toka alipotoka siku alipolumbana na baba yake juu ya yeye kupata mchumba.

Haikuwa rahisi hata kidogo kuuelezea upuuzi ule kwa Mzee Chiziza. Ilimtumia Clifford zaidi ya masaa matatu kujieleza kwa kina huku mara kwa mara akikabiliana na maswali yasiyo na majibu kutoka kwa baba yake. Hapa na pale, ilibaki kidogo mzee yule amtandike ngumi hasa pale alipokuwa akimweleza kuwa alimpenda Nunu kwa dhati..

“Kupenda?? Kupenda?? Unajua nini kuhusu kupenda Malaya mvivu wewe usiyejifunza hata kwa Malaya wenzako? Unampenda mtu anakupangia Kiswahili kuhusu hata nduguze halafu unaniambia ulimpenda kwa dhati? Mjaa laana wewe..” Aling’aka Mzee Chiziza kabla ya kumruhusu Clifford kuendelea.

Walipojadili kwa kina, mwisho wakawa hawana namna. Tayari suruali ilikuwa magotini na suluhisho pekee lilikuwa ni kuchutama na kuirudisha kiunoni. Hapakuwa na mwafaka, lakini Clifford akaruhusiwa kwenda kupumzika.

Utu uzima dawa, na umwamba wa Chiziza ukaonekana!!

Haikupita hata wiki moja, ile hofu ikamtoka Clifford. Hakuna polisi ambaye alihusika, wala mwanajeshi. Jeshi la Chiziza peke yake lilituliza tufani. Ile mibazazi ikapotea katika uso wake asiione tena. Ni kama vile ilikuwa imefutika kwenye uso wa dunia!!! Nunu yeye hakupotea, lakini kila alipokutana na Clifford, alionesha hofu ya waziwazi, huku mwendo wake ukionekana kama vile una shida fulani. Ilisemekana tu kuwa kuna wachache waliwahi kuziona picha zile chafu za Clifford, lakini hakukuwa na madhara makubwa.

“Sasa bwana mdogo…We ujitie una moyo wa kupenda tena. Nije nisikie tena umejiingiza kwenye misukosuko ya kipumbavu. Hakyamungu utanishuhudia nikisimama kutoa ushahidi kuwa ulifumaniwa na kukuweka ndani mwenyewe kwa gharama zangu. Sitaki litoto la kuvunja heshima niliyoijenga kwa miaka mingi nchi hii… Clifford Chiziza, nakwambia tena, OLE WAKO!” Alijisema Mzee Chiziza huku akiwa hampi kabisa umakini Clifford.

Naam.. Maisha ya Clifford yakaanza upya. Hakutaka tena kukaa jijini Dar es Salaam. Alihisi kuwa, ipo siku ile mibazazi itarudi tena. Lakini pia, alihisi ipo siku angeweza tena kumsamehe Nunu na kurudiana naye, jambo ambalo hakutaka kabisa litokee… Akaamua kufanya maamuzi magumu. Kampuni akamwachia rafiki yake ili aendelee kuiendesha, huku akiwa na wazo la kufungua tawi popote atakapokuwepo ili kuiendeleza. Akaomba kazi upya. Alitaka kuwa mbali na nchi, lakini akahisi kuwa alihitaji kwanza kuwa karibu na Mzee Chiziza ili aendelee kusafisha sifa zake na jina lake. Mungu akamsaidia, akapata kazi ya mkataba kufundisha Tanzania Institute of Accounancy, tawi la Singida…

Hayo yote yalitokea miezi kumi na nne iliyopita.. Na sasa alikuwa ameufikia mlango wa chumba namba 116 alipokuwa akihitajika kwa kipindi cha ‘Cost and Management Accounting’ mchana ule…

Kama alidhani yale ya Dar es Salaam yalitosha kumfunza adabu, hakuwa ametambua kuwa ya Singida yangemfanya kuwa mwanafunzi mdogo tu asiyeijua ‘aa’ wala ‘bee’..

Clifford Chiziza alikuwa katikati ya bahari yenye mkondo mmoja tu..

Bahari imsafirishayo kuelekea katika kisiwa cha majuto na Ardhi ya Majanga, kushiriki mashindano ambayo, iwe isiwe, ni lazima angeshinda. Alipaswa kushinda kwa kuwa hakuwa na wakushindana naye. Na kweli alishinda na kupewa zawadi..

Zawadi ya adhabu…!!



Nimefundishwa kuwa…

Hakuna kisichowezekana kabisa duniani.. Kule kukifikiria kit utu hata kisichokuwepo ni dalili kuwa kuna nafasi ya kukifanya kiwepo. Lakini, kuna gharama katika kile unachotaka kiwezekane. Ni pale tu tunapoogopa gharama za kuvifanya vitu viwezekane, au tunapozikwepa gharama hizi tunaanza kuzuia yale yanayowezekana kufanyika. Mfano, hata wewe unaweza kuwa mtu bora wa kuwaonyesha wengine njia ya kupita. Lakini ni wengi wamekusa njia kwa kuwa, mar azote umekuwa ukifikiria gharama utakazohitaji kufikia lengo lako.

Una hiyari ya kukubali au kukataa….

******

*** NINAWAANDIKIA HAYA KATIKA SEHEMU YA SITA ***

“Good afternoon” Alisalimia darasa lenye wanafunzi 38 wa mwaka wa tatu na wa mwisho wa masomo yao yatakayowawezesha kupata shahada ya kwanza ya uhasibu. Wachache waliitikia kwa kusimama kwa kusitasita na kabla hata hawajafikia nusu ya kusimama, Clifford aliupunga mkono kuwaashiria wakae.

“Well well… CR I asked you to collect your papers from my office earlier. Hope that you did..” Aliongea huku akimsogelea kiongozi wa darasa ambaye mara moja aliitikia

“Yes sir”. Mwanafunzi mmoja ambaue tayari alikuwa akijishughulisha kuunganisha computer ya Clifford na projector ili kuanza kipindi alijibu.

“Hamjafanya vizuri sana kwenye test ya mwisho. Sijui ni wapi hapakueleweka vizuri. Nitajaribu kuwa na nafasi jumamosi hii ili kama kuna yeyote ambaye anahisi hakuelewa nionane naye. Next week tutaandaa Markup test kwa watakaohitaji. Otherwise leo tutaenda hatua moja mbele.. We’ll be talking on ‘Cost accumulation for inventory valuation and profit measurements’.

“Well then.. At the end of today’s session, you will be able to…..”

Ufundi ukaanza. Kurasa ziliendelea kupepea katika ubao maalumu ulionururishwa na mwanga wa kifaa kile maalumu kilichokuwa kikichukua maandishi kutoka katika computer huku hapa na pale Clifford akiendelea kuusulubu ubao mwingine wenye rangi nyeupe kwa kalamu maalumu ili kuelezea vema zaidi yale aliyokuwa anayaelezea kwa ufasaha mkubwa.

Mwanafunzi mmoja aliyekuwa amekaa katikati ya wengine alikuwa ametumbua macho kwa umakini, hapa na pale akiukunja na kukuna kichwa chake. Ni wazi kuwa alikuwa akijitahidi kusikiliza na kuelewa kile kilichokuwa kinafundishwa bila mafanikio. Clifford ni kama aliliona hilo na hapa na pale akawa anapunguza mwendo wa kufundisha na kurudia rudia baadhi ya vipengele. Darasa zima likawa limechangamka na ni wazi kuwa walikuwa wanaanza kuelewa kwa ufasaha kile kilichokuwa kinafundishwa.

“Now please… Can someone here differentiate a payroll and a labour cost accounting?” Aliuliza kwa utulivu Clifford huku akitabasamu kirafiki na kalamu yake akiiweka juu ya meza. Nusu ya darasa mikono ikawa juu.. Hakujali sana, akasimama akimtazama mwanafunzi yule aliyeonekana kujawa na hofu wakati wote.

“Neema… Can you?”

“Eeeh.. Sorry sir.. Can you repeat the question?”

“Neema.., Can you please, and kindly, tell the difference between payroll and labour cost accounting?” Aliuliza Clifford huku kwa mara nyingine tena akitabasamu, akijipindapinda mbele na nyuma kwa mbwembwe, wakati huu macho yake akiwa ameyakaza kwa Neema.

“N…. No.. Sir… I can’t”. Alijibu Neema kwa huzuni huku nusu ya macho ya wanafunzi wenzake yakiwa yamemwelekea.

Aibu iliyochanganyika na hofu vilimjaa.

“Well well… Lets try something different then… Can you briefly remind us all Material Recording Procedures in a well defined store?”

“Material recording what in a well defined what?” Alihoji Neema huku akianza kuonekana kutokwa na jasho kwa mbali. Zaidi ya nusu ya darasa wakacheka kwa nguvu. Hata Clifford naye alijikuta akicheka huku akitikisa kichwa. Hakuonekana kusikitika hata kidogo. Akarudisha kurasa nyuma na kukifikia kile alichokuwa amemuuliza Neema. Akarudia kukifundisha taratibu huku macho yake yote mawili yakiwa yamemuelekea Neema. Alitumia dakika ishirini akirudia rudia huku akitoa mifano mingi zaidi. Wengine wakaonekana kuchoka kwa kuelewa zaidi na hapa na pale wakawa wanajibu haraka hata kabla Clifford hajauliza.

Mpaka kipindi kinaisha, Neema aliweza kuyajibu maswali yale kwa ufasaha mkubwa huku akionekana kuchangamka zaidi ya alivyokuwa Mwanzo.

Kwa Clifford hii ilimpa moyo na akajikuta akiondoka darasani akiwa na hali nzuri zaidi. Alitamani sana anaowafundisha wamwelewe kwa kina, na hili alilitimiza kwa gharama yoyote ile.

Narudia hapa.. “Gharama yoyote ile”

***

Ilikuwa jumamosi ambayo walimu wengi waliitumia kupumzika na kufanya mambo yao nje ya chuoni, lakini haikuwa hivyo kwa Clifford Chiziza. Saa mbili kamili ilimkuta ofisini kwake akiwa anakabiliana na vitabu akijiandaa kuanza kuonana na wanafunzi wake wenye mahitaji muhimu na maalumu. Hakutaka amwache yeyote nyuma, hasa wale wa mwaka wa mwisho aliokuwa akiwafundishwa kwa namna ya kuwaandaa zaidi kuingia katika soko gumu la ajira.

Hamu hii iliongezeka kwa kuwa, ndio kwanza walikuwa wameingia mwaka wa tatu, na aliamini kuwa kama angewajenga vema Mwanzo kabisa mwa mwaka ule, huenda wangefanya vizuri na kusahihisha makosa yao yote ya nyuma.

Aliamua maisha yake apigane kufa na kupona kuandaa wasomi wa darasani na sio wahuni wanaosoma mtaani na kuwa waovu kama Nunu!!

Siku hii alikuwa na miadi na wanafunzi tisa ambao walijiandikisha siku moja iliyotangulia, huku wengine akiwatengea siku nyingine. Kama ilivyokubaliwa, saa tatu kamili walianza kuingia. Wapo walioingia wawili wawili na wengine mmoja mmoja. Mpaka kufikia majira ya saa saba, tayari alikuwa ameshaonana na wanafunzi nane ambao wote walitoka wakiwa na tabasamu huku wakiwa wamepewa kazi maalumu ya kufanya ambayo wangetakiwa kuikabidhi wiki iliyofuatia.

Kisha.. Saa saba na dakika kumi na nne, akaingia Neema.

Aliingia akiwa mnyonge na alionekana wazi kuwa na wasiwasi kama alivyokuwa wakati hajaelewa kule darasani.

“Good afternoon sir” Alisalimu huku akiangalia chini.

“’Afternoon Neema.. ‘Course you can sit down” Aliitikia Clifford. “Well.. Tell me Neema.. Muda mwingi unaonekana ukiwa na hofu sana.. Whats wrong with you?”

“Si…Sir… Sielewi. Yani najitahidi sana kuelewa lakini mara nyingi najikuta sikuelewi vizuri. Masomo ni magumu sana na baba hatanielewa nikifeli. Dady ni mkali sana, yani zile supplementary za last semester zilisababisha anipunguzie hadi kiasi cha matumizi. Anataka nifanye vizuri ili nisipoteze hela yake. Sijui nikifeli kama atanisamehe. Anaweza kunifukuza hata nyumbani kwake. Sidhani kama umewahi kukutana na mtu mkorofi kama baba yangu”. Neema aliongea huku akionekana wazi kulengwalengwa na machozi.

“Ungemjua Mzee Chiziza ungenyamaza we binti.. Ila kwa kuwa humjui endelea kufikiri baba yako ni mkorofi” Clifford alijisemea kichwani kwake huku uso wake ukiumba lile tabasamu lake tamu. Kidogo Neema akaonekana kuanza kuzoea kuwepo pale.

“Sikiliza Neema… Unafeli kila mara unapokubali kuwa kuna kufeli. Forget about your father.. This is between your books, your lecturers and you. Huu ni muda wako wa kujithibitishia mwenyewe kwanza kuwa, You will make it. Yani una maanisha kuwa baba yako akikubali kukupokea hata ukiwa failure ndio utakuwa na furaha?” Aliuliza Clifford akiwa amemtazama Neema.

“Hapana.. Sipendi kufeli” Alijibu Neema kwa sauti ya chini.

“There you are.. That is what will take you through.. Jiambie ‘sitaki kufeli’, tena jikumbushe kila mara. Baba awepo au asiwepo, kataa kufeli.. Akulipie ada au asikulipie, kataa kufeli.. Anza kukataa sasa hivi kabla hatujafanya chochote.. Mkatae ‘kufeli’ na mambo yake yote, na fahari zake zote” Clifford alisema huku akiachia tena lile tabasamu lake.

E bwana ee.. Neema alisimama wima, akakunja ngumi moja na kuipigapiga kwenye kiganja chake cha mkono..

“Nakataa kufeli.. Nasema sitaki kufeli, na sitafeli.. Nitafaulu. SITAKI KUFELI”

Shabash!!

Tabasamu likachanua kwenye nyuso zao. Kipindi kikaanza. Walianza tangu somo la kwanza alilofundisha Clifford siku ya kwanza ya muhula ule. Akampitisha taratibu kwenye barabara pana ya taaluma, huku akimpa na mifano kedekede ya hiki na kile, hapa na pale akamruhusu kuuliza maswali ya uelewa, akayajibu kwa majibu rahisi lakini yenye maana kubwa. Hapa wakaenda mbele, pale wakarudi nyuma. Sehemu fulani wakasimama kwa zaidi ya dakika ishirini, wakarudia tena na tena, hesabu ndogondogo za mara kwa mara zikawekwa sawa na maelezo magumu magumu yakatafutiwa lugha nyepesi..

Yakaeleweka!!

Ni kule kuzama kwa jua ndio kuliwakumbusha kuwa muda ulikuwa umekwenda sana. Clifford akatazama saa yake. Saa kumi na mbili kasoro dakika chache, hakuhangaika kuzihesabu. Si Neema wala yeye aliyeonekana kuchoka. Neema alifurahia somo na Clifford alifurahia kazi yake inayomlisha na kumvalisha.

Jembe jipya lilikuwa limepata mpini imara.

Mpaka wanaachana majira ya saa kumi na mbili na nusu, Neema alikuwa na tabasamu pana lililoashiria kiasi alivyoelewa somo. Wakaagana na Neema akaelekea hosteli alizokuwa akiishi mitaa ya Sabasaba na Clifford akipanda bajaji na kuelekea mitaa ya Mwenge, Karakana alipokuwa akiishi katika nyumba kubwa aliyopanga zaidi ya mwaka uliopita alipohamia tu Singida.

Alikuwa na Amani kwa kazi aliyoifanya siku ile.

***

Hali ya kimasomo ya Neema iliimarika. Alikuwa akishiriki kikamilifu kujibu maswali popote yalipoulizwa kwa ufasaha mkubwa. Alijitahidi kuwa karibu na Clifford kama wanafunzi wengine, na mara kwa mara, hakusita kumfuata ofisini na kumwomba amwelekeze kile ambacho kilikuwa kikimshinda. Kuna wakati akawa anafundishwa hata yale ambayo darasani Clifford angeweza kuyasahau. Hii ikajenga urafiki hata wa nje ya masomo baina yao.

Kwa Clifford hili halikuwa na tatizo. Alipokuwa chuo kikuu cha Dar es Salaam, mara kwa mara alikuwa na utaratibu wa hata kualikwa kwenye sherehe za kuzaliwa za wanafunzi wake, au kualikwa kupata chakula cha mchana au usiku. Hii haikumpunguzia umakini wake wa kazi na badala yake, akajijengea heshima zaidi kwa kuwa, wanafunzi wale hawakumwomba upendeleo wowote katika masomo yao, bali walizidi kumtumia vema kuelewa kile walichokuwa wakifundishwa.

Neema naye akawa miongoni mwa wanafunzi wa Clifford walioondokea kuwa marafiki zake wa karibu.

Waliposhindwa kuonana chuoni kwaajili ya kueleweshana jambo fulani, wakakutana hata katika mikahawa nje ya chuo, barabarani au pahala pengine popote ambapo wangeweza kutimiza kiu yao ya kitaaluma. Kiu ya mwanafunzi kusoma na mwalimu kufundisha.

Hamadi! Neema akafika hata nyumbani kwa Clifford.

Kitabu kikasomwa kuanzia ukurasa wa kwanza hadi wa mwisho.. Mwalimu akafundisha na mwanafunzi akafundishika.

Lakini sasa, vitabu karibu vyote walishavimaliza. Mtaala wa muhula ule uliisha ndani ya muda mfupi tu. Wakasoma na magazeti, yakaisha. Hekaya za Zee la Kale na za abunuwasi, zikamalizika. Wasome nini sasa?

Wakakosa cha kufundishana.

Wakaanza kufundishana yasiyo kwenye mtaala.

Kizaazaa kikazaliwa, na kikaanza kukua…

Kikakaa, kikatambaa na kisha kikasimama kwa miguu yake…

Ama kweli!!




Nimefundishwa kuwa…

Kama vile nywele ziotavyo pasipo sisi wenyewe kujua mwenendo wake, au kama vile tunavyoendelea kukua pasipo kuweza kuamua ni kasi gani tuitumie, ndivyo hivyo mawazo yetu yanavyokua. Ujinga mdogo unaoupalilia leo unaendelea kukua taratibu, bila wewe kujua ni kwa kiasi gani unaongezeka. Tabia mbovu halikadhalika, hata kama ni kwa kiasi kidogo, inaendelea kukua taratibu taratibu tu. Ipo siku, kama unavyoshangaa nywele zako kuwa ndefu, utagundua kuwa, ujinga au tabia mbovu ulivyokuwa unavipalilia vinakudai uvifanyie sherehe ya kutimiza miaka hamsini!!!

Una hiyari ya kukubali au kukataa….

******

*** NINAWAANDIKIA HAYA KATIKA SEHEMU YA SABA ***

Walikutana.. Wakapendana!!

Wala haikuchukua muda mrefu baina ya Clifford na Neema kujenga ngome imara ya mapenzi baina yao. Walipendana kwa dhati na Clifford aliazimia kuwa, yule angekuwa mke wake wa ndoa. Lile doa ambalo liliingia katika maisha yake kwa mkono wa Nunu likaanza kufutika taratibu. Lakini sasa akaapa kuwa atakuwa makini. Alitaka kufuata taratibu zote za kitamaduni kumuoa Neema. Hakutaka tena kupumbazwa na jinamizi liitwalo ‘kupenda kwa dhati’.

Taalumua yake ya ualimu ikatumika kwa makini kabisa.

Kwanza, hakuwa kiherehere wa kumuhudumia Neema kwa kila kitu kama alivyodanganyika kwa Nunu. Alijibakiza kwa sehemu yake! Alikuwa mwalimu na msaada mkubwa aliopaswa kuutoa haukuwa fedha wala zawadi nyingine yoyote zaidi ya elimu. Wakaweka vikao, wakayaandika mapenzi yao katika karatasi na namna watakavyoyaficha ili yasije yakawaharibia machoni pa watu. Kila mmoja akapewa jukumu lake la kutimiza ili kulinda mapenzi yao.

Wakakaa macho…

Kila mmoja akiwa makini kabisa na mwenzake!!

Haikuwa ngumu kwa kuwa, pamoja na ule woga wake na aibu zake; aibu ambazo Clifford alizifananisha na zile za Nunu ingawa za Neema zilikuwa za dhati; Neema alikuwa msichana mwenye misimamo chanya na isiyotikisika. Mara kwa mara aliendelea kumzungumzia baba yake kuwa ni mtu mkorofi, na hii ikawa kete yake ya kujitunza vema. Alienda nyumbani kwa Clifford kwa machale sana, na popote alipokwenda, kwanza alitanguliza masomo na kisha mengine ndipo yakafuata.

“Utakapomaliza chuo.. Tutafanya mpango twende kwenu kwanza. Niwajue baadhi ya ndugu ingawa kwa kificho. Halafu sasa hapo nitakupeleka kwa Mzee mmoja anaitwa Chiziza. Unajisifia sana kuwa baba yako ni Mkali, ila kuna kiumbe kinaitwa Chiziza sina haja ya kuzisema sifa zake hapa. Utakapomuona ndipo wewe mwenyewe utathibitisha kuwa baba yako anaweza kuwa Malaika Mwema kabisa mbele ya Malaika mtoa roho aitwaye Chiziza” Clifford aliongea kwa utani akizichezea kucha za Neema baada ya kumaliza kumfundisha.

“Mh.. Karibu sana Kanda ya ziwa.. N’tafurahi ikiwa hilo litatimia. Mh! Sema watu watashangaa! Yani mwalimu kumuoa mwanafunzi wake???” Neema alisema kwa aibu..

“Kwani ubaya uko wapi? Tena ndio vizuri, tukizaa watoto nakuwa nawasimulia kuwa mama yenu alikuwa kilaza mimi ndio nikawa namfundisha” Alisema Clifford huku akianza kucheka..

“Cliff.. Cliff umeanza uchokozi.. Bwana mi staaaki.. Staki nakwambia, staaki.. Mi sio kilaza bwana, nilikuwa tu na hofu.. Na ukiwaambia mi nanuna” Alisema Neema huku akiigiza kununa. Uzuri wa binti yule wa kisukuma ukatutumka usoni pake! Akajidai kununa zaidi, lakini mikono iliyokuwa ikimfundisha muda mfupi uliopita ikawa ikimtambaa kila kona ya mwili wake.

Kule kununa kukabadilika, kukawa kuguna na kujipinduapindua kama joka lililoogeshwa mafuta ya taa. Kukuru kakara za hapa na pale zikaendelea. Vitabu vilivyowafanya wakajuana wakavisaliti, wakavisukuma kwa miguu mbali na upeo wa macho yao, navyo vikatii, hiki kikaangukia kule na kingine kikajificha chini ya uvungu kwa aibu. Hakukuwa na joto lolote lililowalazimu kupunguza nguo katika miili yao, lakini wakajikuta wakiwa uchi wa mnyama.

Mwalimu akawa mwalimu kweli, na mwanafunzi akabaki kukubali kila somo alilokuwa akifundishwa. Wakajikuta katika sakafu yenye marumaru zilizopoa kwa ubaridi mkali, lakini jasho likiwa limewaenea mwili mzima. Kwa dakika thelathini nzima hawakuwa kwenye dunia ya masomo ya kihasibu, bali pembezoni kabisa mwa dunia yenye raha na Amani isiyoeleweka.

Huyu alikaa vile na mwenzake akaiga na kukaa vilevile bila yeyote kuwafundisha chochote. Baada ya “kuzozana” kule, aibu ikawarudia. Walikuwa uchi huku wakitwetwa. Kama vile waliopeana ishara, wakaamka kwa haraka na kukimbilia chumbani huku maungo yao nyeti yakipata shida ya kuogelea katikati ya hewa iliyokuwa ikiwazomea.

Wakajikuta bafuni wakiwa wamekumbatiana huku maji yakiisalimu miili yao. Waliporidhika na usafi ule, wakarudi chumbani. Hakuna aliyemuangalia mwenzake machoni ingawa Clifford alijikaza na kujaribu kumtazama Neema. Naye alipotaka kufanya hivyo, wote wakaangalia pembeni kwa pamoja.

Penzi likatunga tenzi!, Neema akalala kwa Clifford kwa mara ya kwanza!

***

Ikawa usiku, ikawa alfajiri.

Wiki zikageuka Mwezi… Wa kwanza na wa pili, kisha wa tatu.

Neema akamaliza muhula wa kwanza wa mwaka wa tatu, na ilimpasa kwenda kwao kwa mapumziko mafupi ya mwezi mmoja. Lakini angeendaje amuache Clifford wake mwenyewe? Haikuwa rahisi. Walishaamua kupendana na kuwa pamoja muda wote, ingawa kwa usiri ambao si Clifford wala Neema aliyeusaliti. Uongo ukatungwa, Neema yuko field Singida.. Hakwenda kwao!!

Zulfa, mkufunzi mwenza wa Clifford waliyekuwa wakitumia ofisi moja alihisi jambo, lakini haraka upepo ukageuzwa kisomi. Yeye mwenyewe alikuwa ni miongoni kati ya wanawake waliotamani kuwa karibu na Clifford, tena ukaribu wa kimapenzi. Hapa na pale alimualika Clifford nyumbani kwake na yeye kumtembelea, mara nyingine nyakati za usiku na kujibaraguza baraguza kuwa alikuwa na mambo ya kitaaluma ya kujadili.

Taaluma gani ijadiliwe baina ya Mhadhiri wa masomo ya Rasilimali watu na gwiji wa Uhasibu na usimamizi wa fedha? Alikuwa na lake jambo, na Clifford alishalijua, na hivyo haikuwa kazi ngumu kumkwepa.

Neema alishamtosha!

Likizo ambayo ilishamirishwa na harakati za kimapenzi pamoja na masomo hapa na pale ikaisha. Neema akarejea darasani na Clifford akarejea ubaoni. Vipindi vikaendelea bila matatizo. Kule kuonana kwao mara kwa mara hakukuathiriwa sana na ratiba ngumu zaidi ya masomo aliyokuwa nayo Neema, lakini ule uwepo wa Clifford ukamsaidia kwa kuwa alikuwa akipata pia muda wa ziada kusoma masomo ya ziada.

Masomo ya ziada chuo kikuu!!

Halafu sasa likazuka jambo!!!

Tena ghafla tu!!

***

Hakuwa na elimu kubwa. Kidato cha nne na kisha chuo cha ualimu, na kisha kurudi uraiani akiwa mwalimu aliyeipenda kazi yake kuliko chochote katika maisha yake. Alifundisha kwa makini masomo ya hesabu na lugha, na akawa kipenzi kwa wanafunzi wake kutokana na umahiri wake wa kufundisha masomo yale, hasa kwa darasa la nne na darasa la saba yaliyokuwa madarasa ya mitihani ya taifa. Shule ya Msingi Nyakato ndiyo iliyompokea na hapo ndipo makali yake yakaonekana.

Mwalimu Masagida KaswalalaMasalu alikuwa mwalimu aliyeelewa maana ya ualimu! Alikuwa ni msaada mkubwa kwa wanafunzi wengi waliopitia Shule ya msingi Nyakato. Mitihani yake ilijizolea umaarufu mkubwa Mkoani Mwanza na kanda nzima ya ziwa kwa kubeba maswali ambayo yangetoka pia katika mitihani ya taifa.

Mwanafunzi wa darasa la saba ambaye hajapata mitihani ya kutosha yenye herufi “MKM” hakujiona kuwa aliye tayari kufanya mtihani. Waliobahatika kufaulu na kujiunga kidato cha kwanza walikiri kuwa, nusu au robo tatu ya maswali waliyokutana nayo kwenye mtihani wa taifa, yalikuwa yamechukuliwa neno kwa neno, namba kwa namba kutoka kwa fundi yule ambaye hata shuleni walishazoea kumuita “MKM”.

Lakini pamoja na sifa isiyoisha ya umahiri wa kufundisha hisabati na lugha, Masagida Kaswalala Masalu alikuwa ni mwalimu aliyeogofya!! Kisingekuwa kile kipaji chake kisichoelezeka cha kufundisha, hakuna mwanafunzi ambaye angetaka hata kuwa naye karibu! Alikuwa ni mkali wa kupindukia na hakutaka kabisa urafiki usio na tija na yeyote katika maisha yake. Muda wote aliokuwa peke yake, alijitenga na dunia nzima na kuhangaika na madaftari ya wanafunzi wake tu!

Lakini hakuna mkate mgumu mbele ya chai. Hatimaye akafunga pingu za maisha ya binti aliyekuwa muuguzi katika hospitali ya Bugando. Maisha yake yakaendelea huku ile sifa yake ya ukali ikifichwa chini ya ule mwavuli wa umahiri wake wa kufundisha pamoja na ule upole wa mkewe Beatrice Budodi. Mwaka wa kwanza na wa pili ukakatika, wakajaliwa mtoto wa kike waliyemuita Neema.

Neema akayamulika maisha yao! Ili kumlea vema, Masagida akazidisha juhudi mara dufu. Akafanya kazi kwa bidii zaidi na jina lake likazidi kujengeka. Hatimaye akapandishwa cheo na kuwa Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Nyakato.

Neema alipokuwa na miaka minne, mama yake akapata ujauzito mwingine. Furaha ikayafunika kabisa maisha ya Masagida. Alikuwa ni mwalimu mwenye furaha zaidi duniani. Miezi tisa ikatimia na mkewe akaingia kwenye chumba cha kujifungulia.

Haikuwa kama walivyopanga.

Haikuwa kama walivyotegemea.

Beatrice hakutoka chumbani mule akiwa hai. Mtoto alikuwa amekalia nyonga na hivyo jitihada za kujifungua kawaida zikagonga mwamba. Mama alikuwa ameshachoka sana wakati wataalamu walipoamua kumfanyia upasuaji! Walifanikiwa kumtoa mtoto mkubwa na mzuri wa kiume aliyekuwa na afya tele. Wakati wakilishona tumbo la Beatrice, walikuwa wakilishona tumbo la Maiti yake tu.

Beatrice mwenyewe alikuwa anayajongea malango ya muumba wake!

Alifariki dunia!!

Kifo chake kiliacha uwazi usiozibika katika maisha ya Mwalimu Masagida Kaswalala Masalu. Kifo kilichomwacha na jukumu la malezi ya Neema aliyekuwa na miaka minne tu na mdogo wake wa kiume aliyemwita Machimu, akimaanisha Mikuki. Ni kweli kabisa mtoto yule alikuja kama mkuki ulioutoboa moyo wake na kuyachukua maisha ya mama yake.

Hakutaka kuoa tena..

Akaamua kuwalea watoto wake kwa mapenzi makubwa huku mdogo wake wa kike na ndugu wengine kadhaa wakimsaidia pale nyumbani.

Neema na Machimu wakakua katika upweke wa kumkosa mama yao. Kuna wakati sura ya aliyeitwa mama yao ilikuwa ikimjia Neema kwa mbali sana, lakini hakuweza kukumbuka chochote. Kwake yeye, baba yao mwalimu Masagida Kaswalala Masalu ndiye alikuwa mama na baba. Ukali wake ukamjenga na kumuandaa vema kuwa binti aliyemfurahisha baba yake.

Kisha sasa, hili linatokea akiwa mbali na baba yake…



******

Nimefundishwa kuwa…

Kesho ni siku nzuri sana.. Huenda ikawa ni kweli au isiwe kweli, na hilo si la muhimu sana. Lililo la muhimu ni kuwa, kesho; ingawa inaweza ikawa ni nzuri au vinginevyo, lakini itafika. Ikiwa itafika ikiwa nzuri, tutaifurahia na ikiwa itakuja ikiwa mbaya, tutaipokea. Ukweli utabaki kuwa, hata kesho; ikiwa tutakuwepo, ni lazima tutaendelea kuishi. Sasa tukiwa na Imani kuwa hata kesho maisha yataendelea, ina faida gani kuishi leo huku tukiiharibu kesho yetu au kesho ya wengine kwa makusudi?? Yafaa nini kuishi leo kwa furaha inayoiharibu kesho yetu? Kwangu, huu ni uzembe wa fikra!!

Una hiyari ya kukubali au kukataa….

******

*** NINAWAANDIKIA HAYA KATIKA SEHEMU NANE ***

Hili hawakulipanga, wala kulitamani…

Ingawa Mwanzo ilikuwa ni hofu tu ya kawaida, Mwanamke yule mrefu aliyekuwa amevalia koti refu kiasi jeupe huku macho yake makubwa na mazuri akiwa ameyaficha nyuma ya mawani makubwa ya macho aliithibitisha hofu ile kuwa ulikuwa ndio ukweli sahihi kabisa. Bila kupepesa macho, aliwaangalia wote wawili usoni na kutabasamu.

“Hongereni sana.. Muda sio mrefu mnaenda kuwa wazazi vijana kabisa” Aliwaambia huku akitabasamu kwa mbali na kuacha uwazi mdomoni mwake ulioonesha ule mwanya mpana aliokuwa nao. Alivutia pamoja na kuwa mtu mzima sana.

“Asante sana dada” Alitikia Clifford huku mwili ukimsisimka kwa ukweli ule. “Muda sio mrefu naenda kuwa baba. Nami nakuwa baba jamani, dah!!” Haya aliyasema mwenyewe tu kwenye mawazo yake bila kuyaacha yatoke kupitia mdomo wake. Lakini cha kushangaza, mama yule akacheka.

“Ndio unaenda kuwa baba. Hukuwa umetegemea au hujiamini?” Aliuliza huku akimtazama kwa chati. Aibu ikamfunika usoni Clifford kwa kuropoka kule ambako wala hakuwa ametarajia. Akamgeukia Neema haraka. Hakuwa ametabasamu wala kununa. Ni kama vile alikuwa amening’inia baina ya vyote viwili, hofu na furaha.

Alikuwa amepigwa na bumbuwazi!

Mengine yote yaliyopangwa kufanyika yakafanyika pale. Wakapima vipimo vyote vya muhimu, wakapata majibu na kupewa ushauri wa hapa na pale, kisha wakapangiwa tarehe ya kuanza kliniki, na wakaondoka wakiwa kimya kabisa. Muda wote huo hawakuwa wamepata nafasi ya kujadiliana juu ya jambo lile.

Haraka wakaagiza bajaji huku sasa Clifford akiazimia kuwa, muda wa kutafuta gari lingine baada ya lile la kwanza kuporwa na ile mibazazi iliyomtengenezea kisa wakishirikiana na Nunu. Bajaji ikaamrishwa kuwapeleka mpaka nyumani kwake, Mwenge, Karakana. Walipofika na kuhakikisha wameshajifungia ndani, ndipo sasa Neema akapata nafasi ya kufanya kile ambacho hakuwa amekifanya muda mrefu sasa.

Alianza kulia kwa uchungu mkubwa.

“Nitamwambia nini yule mwalimu, Clifford? Nitamweleza nini Masagida Kaswalala Masalu? Yani kweli Napata mimba kabla ya ndoa, tenahata kabla ya kumaliza masomo? Ni kipi tutamweleza atuelewe Cliff? Ooh Mungu wangu, Neema mimi nitafanyaje?” Katikati ya kilio kikali Neema alijisemea. Ingawa alikuwa akiongea na Cliff, ni kama yote alikuwa akijiuliza na kujijibu mwenyewe.

“Hebu acha utoto Ney.. Acha kujiliza kwa maswala ya kipuuzi” Alisema Clifford akimsogelea Neema wake.

“Ya kipuuzi? Ya kipuuzi? Cliff we ni wa kuniambia hivyo kweli? Sasa mi ntaenda wapi jamani? Nitaenda wapi mimi?” Neema aliendelea kulia kwa uchungu.

“Come on Ney, uende wapi kufanya nini? Nini ambacho ulitaka nifanye na sikukufanyia? You are my wife, full stop. Hayo ya Masagida Kaswalala Masalu niachie. Nitaenda mwenyewe kwa miguu yangu, nimkabidhi ng’ombe wake hata kama ni mia, nimwombe baraka zake nawe uwe wangu wa maisha. Mbona swala rahisi tu hilo? Si ni ku’credit account ya Masagida na ku’debit account ya Clifford, shida ikwapi?” Clifford aliongea huku akiwa amepiga magoti mbele ya Neema.

“Au hutaki kuolewa na mimi Neema? Neema don’t you love me?” Aliuliza Clifford.

“Ooofcoourse I love you Clifford.. Nakupenda sana Mume wangu.. Its just… Just… just…” Neema alikosa cha kuongeza.

“Hakuna cha just, everything is just so long as we want it to be that way. I will marry you.. Na hii sio ahadi hewa. Inuka sasa hivi twende kwa mkuu wa mkoa, na mkuu wa wilaya, na ustawi wa jamii, na kwa paroko, na kwa kwa wale wafanyabiashara wote pale sokoni, niahidi mbele yao kuwa nitakuoa.. Namaanisha. Inuka twende. Nampigia kabisa na Swai aniandalie lile gari lake la matangazo. Twende” Alisema Clifford akiwa tayari amesimama akimnyooshea mkono Neema ili waondoke.

Neema akacheka katikati ya kilio..

“Staki bwanaaa… Hebu toka hukoooo.. Mkuu wa wilaya na mkoa sijui na wamachinga wanahusikaje sasa?” Alisema huku kukiwa na dalili za kudeka, lakini akasimama. Hawakwenda kwa mkuu wa mkoa, wala kwa kamanda wa polisi, wala kwa mkuu wa kikosi cha mbwa..

Walijikuta tu chumbani wakiwa uchi! Mkuu wa mkoa na wilaya ambaye alishuhudia makubaliano yao walikuwa ni kitanda na yale mashuka ambayo nayo kwa bahati mbaya yalijikuta chini bila huruma.

Mjadala ukawa umefungwa!

******

Mapenzi yao sasa yalishamiri. Neema alibakiza miezi miwili tu amalize masomo yake, na ni tumbo lake lilimpa ushirikiano wa kutokuchomoza upesi. Zulfa sasa hakuhisi tena, bali alitambulishwa rasmi kuwa, Neema ndiye mchumba wa Clifford. Akakubali na kutii huku kwa mbali kiwivu kikimtafuna. Masomo yaliyoendelea kuwa magumu kila siku pamoja na ile hali mpya ya ujauzito vikawa vikimwelemea Neema, lakini uwepo wa Clifford aliyekuwa mwanaume mwenye kujali na kumtunza vema vikampa unafuu.

Hawakuwa na haja ya kujificha kama Mwanzo. Pete ya uchumba ikaveshwa kidoleni mwa Neema kimya kimya na akawa akila na kuamkia nyumbani kwa Clifford. Mpango wao ulikuwa mzuri kabisa. Walitaka kwanza Neema amalize mitihani yake, kisha wangeanza rasmi taratibu za kwenda kwao kwaajili ya kuiweka wazi nia yao. Kwa hatua ile, Clifford hakutaka kabisa kumshirikisha Mzee Chiziza juu ya lile. Alimjua vema baba yake na namna ambavyo angeanza kumkumbusha habari za Mwanzo.


ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

BLOG