Search This Blog

Saturday, February 26, 2022

GENGE - 5

    *

Simulizi : Genge 

Sehemu Ya Tano (5)


Kamanda Amata akachukua kadi mmweko na kumpatia msichana huyo, “fungua hiyo nikuoneshe kitu,” akamwambia.

“Mtu kazini?” Lulu akauliza.

“Yap!”

Lulu akaipachika ile kadi kwenye kompyuta yake, sekunde kadhaa ikaonesha picha za watu kama sita hivi.

“Enhe…”

“Huyo mwanaume, huyo mtu mzima…”

“Huyu?” akasogeza panya kwenye picha hiyo.

“Yes!”

“Enhe,”

“Nataka nijue kwenye kumbukumbu zenu za ofisi, mtu huyu yupo hapa nchini?” Amata akauliza. Lulu akafanya mambo yake kwenye mtandao huo takriban dakika tano hivi. Akamgeukia Amata.

“Anaitwa Christopher…” Lulu akasema.

“Christopher?”

“Christopher McTee…” akamalizia. Kamanda Amata akatikisa kichwa juu chini.

Christopher McTee! Amata akawaza. “Maelezo Zaidi…”

“Mzaliwa wa Australia…”

“Sihitaji hayo, nataka kujua yupo hapa nchini?”

“Oooh ok…” Lulu akajibu na kuendelea kuchakata kompyuta yake akizidi kuingia ndani kabisa ya mtandao wa uhamiaji, ambao ni wachache wanaweza kuuingia.

“Alikuja nchini mwaka 1999 mwezi September kupitia uwanja wa ndege wa Kilimanjaro…” Lulu akaeleza. Amata akafungua masikio kusikia zaidi kuhusu mtu huyo. “Sikiliza Lulu, nataka kujua Zaidi kuhusu huyu mtu,” akamwambia.

“Christopher McTee kama nilivyokwambia, alikuja nchini mwaka ’99 kwa nia ya kuwekeza kadiri ya taarifa zilizopo hapa, japo zipo kwa uchache. Viza yake ilikuwa ya kibiashara…” Lulu akaeleza.

“Sawa! Asante sana Lulu… sina zaidi,” Amata akasema na tayari alikuwa keshainuka kutoka kwenye kiti chake.

“Ndo unaenda?”

“Ndiyo… nilichotaka nimepata. Kuna zaidi?” akamuuliza.

“Hakuna…” Lulu akajibu.

“Ok!”

Kamanda Amata akaagana na Lulu na kutoka katika ile ofisi, akateremka ngazi za mlango mkubwa na kulifikia gari lake. Akaingia na kuketi. Akachukua kitabu chake cha kumbukumbu na kuandika mambo kadhaa.

Nitamjua tu, nan itajua yuko wapi! Akajiwazia na kuwasha gari. Akatoka eneo hilo na kuchukua barabara ya Ohio kuitafuta ile ya Ali Hassan Mwinyi mpaka daraja la Salenda. Akautafuta ufukwe wa Coco na kunyoosha na barabara hiyo mpaka Msasani.

Australian Honorary Consulate! Kibao chenye hayo maandishi kikamkaribisha. Amata akaweka vizuri koti lake. Akaitazama ile closed-circuit television camera iliyokuwa mbele yake, juu ya kiambaza cha jengo hilo. Akajiweka tai vizuri, na kuvuta hatua kuelekea katika lango la ofisi hizo. Mbele ya walinzi, akajitambulisha kama afisa uhamiaji na kuruhusiwa kuingia.

Ndani ya ofisi hiyo, Amata akakutana na afisa anayehusika na uhifadhi wa taarifa zote za raia wa nchi hiyo wanaoingia nchini.

“Karibu sana,” akakaribishwa. Amata akaketi kwa utulivu kabisa huku macho yake nay a yule bwana yakiwa yanasomana, yakaelewana.

“Naitwa Mr. Spark,” akajitambualisha na kuonesha kitambulisha chake.

“Karibu sana Mr. Spark. Naitwa Mr. Peterson…naweza kukusaidia …” akamwambia. Amata akaingiaza mkono ndani ya koti, mara hii akatoa picha na si kadi mmweko kama kule kwa Lulu.

“Mwaka 1999, mwezi wa tisa, bwana Christopher McTee aliwasili nchini akitokea Australia. Pasipoti yake na viza vimemtambulisha kama raia wa nchi hiyo. Katika kufanya tafiti juu ya watu wanaoishi nchini kinyume na taratibu, huyu amekuwa mmoja wao. Nimekuja kwenu kujua kama mna taarifa zozote za mtu huyu…” Amata akaeleza.

Peterson, akaichukua ile picha na kuitazama kwa makini, akakusanya yale maelezo na kuingiza kwenye kompyuta yake. Akaitisha taarifa ili kujua chochote juu ya mtu huyo. Dakika sita hivi baadae, akashusha pumzi ndefu na kugeuza kiti chake kumtazama mgeni wake.

“Spark!” akaita. Kamanda Amata akamtazama kwa macho makali yaliyokuwa yakimwambia

‘sema nakusikiliza’.

“Christopher McTee, mwenye surah ii, alikwishakufa. Na hata hapa kwenye mtandao wetu wa utambuzi, imejiandika ‘Deceased’”. Peterson akaeleza.

Kamanda Amata akashusha pumzi ndefu na kujiegemeza kitini.

“Amekufa!” akasema.

“Yeah!”

Peterson akamwonesha na tarehe na mwezi na hospitali gani mtu huyo alipofia. Kamanda Amata akasukuti kwa jozi la sekunde, akili yake ikafanya kazi kwa haraka kidogo. Akamtazama tena yule bwana.

“Sasa … huyu aliyeingia Tanzania mwaka huo ni nani? Hebu tazama pasipoti namba hiyo imekatwa lini?” Amata akauliza.

“Swali lako lipo sawa… tarahe ya kuja kwake, na tarehe za pasipoti zote zimefanyika baada ya kifo chake,” akaeleza. Sasa wote wawili vichwa vikawagonga.

“Huyu bwana kaingia nchini, na hakuna maelezo yoyote kuwa amekwishaondoka… ina maana yupo hapa hapa,” Amata akasema. “Nashukuru sana Mr…”

“Mr. Peterson!”

Kamanda Amata akainuka, kabla hajavuta hatua kutoka akazuiwana kauli.

“Mr Spark, maada nina hii taarifa, nitakujulisha kama nitapata lolote,” akamwambia. Amata akachomoa kadikazi yake na kumpatia. Akaondoka.

Ndani ya gari lake, aliketi kimya kabisa akifikiri nini cha kufanya. Akajikuta akipiga ngumi usukani wa gari hiyo na kutoa tusi la nguoni. Akatia injini moto na kuondoka eneo lile.

* * *

Dakika kama thelathini zilizofuata, Amata akaegesha gari katika makutano ya barabara ya Ohio na Garden. Akateremka na kuliendea jengo mojawapo lililobeba ofisi za ubalozi wa Mauritius. Hapa hapakuwa na maswali mengi kama alikotoka. Akapandisha mpaka ghorofa ya sita na kuzipata ofisi azitakazo. Makaribisho yaliyojawa kila aina ya ukarimu yalimlaki kijana huyo mtanashati pindi tu alipolifikia dawati la mapokezi. Mara baada ya kueleza shida yake, akaongozwa moja kwa moja kwenye ofisi inayohusika na kazi iyo ya kuratibu raia wan chi hiyo wanaoishi nchini.

Hapa alikutana na kijana mwingine mrefu, mwembamba mwenye kichwa kisicho na nywele.

“Karibu bwana…” akamkaribisha kwa Kiswahili.

“Asante sana, nimekaribia,” Amata akajibu na kisha wote wakaketi baada ya kusalimiana.

“Naitwa Mr. Spark,” akajitambulisha na kumpa mkono yule bwana.

“Karibu sana Mr. Spark… naitwa Hamadou Hassan,” naye akajitambulisha kisha wote wakaketi chini.

“Yes Mr…”

“Mr. Spark,” Amata akamalizia.

“…naweza kukusaidia?”

“Ndiyo Mr Hamadou… nimekuja kutoka Wizara ya mambo ya nje, mimi ni afisa uhusiano wa Wizara,” akaeleza. Akatoa kitambulisho kingine na kumwonesha. Yule bwana akakitazama na kutikisa kichwa. Akamrudishia. Kamanda Amata akatoa picha nyingine na kumuwekea mezani yile bwana.

“Utanisamehe, wizara inahitaji kumtambua huyu mtu raia wa Mauritius ambaye ameomba ajira katika ofisi zetu pale. Kabla ya kumpa jibu lake, tunapenda kujiridhisha kuhusu yeye,” Amata akamwambia. Uongo mtupu. Hamadou akaichukua ile picha na kuitazama, kisha akamtazama Amata.

“Jina lake…”

“Aimer Jonathan,”

Yule bwana akaingiza yale majina kwenye kompyuta yake na kusubiri kidogo. Kama dakika tatu hizi akaanza kuandika tena vitu kadhaa kwenye kompyuta hiyo. Dakika chache zilizofuata, akainua simu na kupiga moja kwa moja Mauritius kuuliza taarifa za mtu huyo. Baada ya kuongea na mtu wa upande wa pili, takribani dakika tano hivi, akakata simu na kumgeukia Amata.

“Mr. Spark… kuna utata wa mtu unayehitaji taarifa zake. Kwanza tumepata watu wengi sana wenye jina kama hilo katika Mouritius. Wamefikia watu sitini na tisa. Lakini katika hao wote hakuna anayeoana na picha hii,” akaeleza. Amata akaonesha mshituko bandia.

“Inawezekanaje?”

“Hapa kuna mambo mengi sasa, inawezekana ameghushi taarifa na si mtu wa Mauritius,”

“Na ndiyo maana nikaja hapa kuhakikisha kwa kuwa haya mambo ya kidiplomasia, tusije kuingia kwenye matatizo ya kimahusiano baina ya nchi na nchi kwa kuajiri jasusi la nchi nyingine,”

“Haswaaa hapo sasa panatufanya na sisi kumtafuta huyu mtu…” Hamadou akamwambia Amata. Wakiwa bado katika mazungumzo hayo ile simu ikaita.

“Samahani…” Hamadou akamtaka radhi Amata na kuinyakuwa ile simu. Dakika mbili zilizofuata akaitua na kumrudia tena Amata.

“Unaona bwana,” akatulia kidogo, baadae nukushi ikaingia, akachomoa lile karatasi na kumpatia Amata.

Alipoipokea, akaisoma. Karatasi ile ilimweleza mtu mwenye picha hiyo kuwa ni Farouk AlFakry, raia wa Djibout na isitoshe tayari amekwishakufa miaka mitano ilopita.

“Asante kwa taarifa hii. Naomba niifikishe panapohusika halafu sisi na ninyi tutaona la kufanya,” Amata akamwambia Hamadou, wakaagana na kuachiana kadi kazi zao.

Mara baada ya mazungumzo yale, Kamanda Amata akashika njia mpaka kwenye gari lake. Akaingia na kuketi nyuma ya usukani. Akaitazama ile picha na ile ya kwake. Zinashahabiana kwa asilimia tisini na tisa.

Washenzi wamejificha nyuma ya sura za marehemu! Akawaza. Kisha akaziweka kwenye kiti cha kando yake. Akawasha gari na kuondoka.

* * *



Washenzi wamejificha nyuma ya sura za marehemu! Akawaza. Kisha akaziweka kwenye kiti cha kando yake. Akawasha gari na kuondoka.

* * *

Ndani ya jiji la Port Luis, Big J alikuwa kimya ndani ya ofisi yake akitafakari hili na lile na kupanga lile na lile kule. Kazi aliyotakiwa kuifanya sasa ilikuwa ni kupanga safu ambayo itaweza kutekeleza lile waliloadhimia.

Hii ni turufu ya mwisho! Akajiwazia wakati mkononi mwake akiwa na picha ya Dana.

Mwanamke huyu atakuwa mzuri sana katika serikali yetu ijayo hasa upande wa usalama! Akazidi kuzama mawazoni. Juu ya meza yake palikuwa na picha kadhaa za watu mbalimbali.

Itakuwa serikali ndogo, yenye ufanisi wa hali ya juu. Na tukifanikiwa, nitapigania Muungano uvunjike na hili litakuwa pigo kubwa kwa waasisi wa taifa hili hukohuko waliko. Tanganyika lazima irudi!

Akatabasamu.mipango yote hii ambayo ilikuwa mezani kwake, iliratibiwa na genge hilo miaka kadhaa nyuma na sasa ilikuwa ikifikia hitimisho. Big J aliweka kabrasha lake vizuri na kulitia ndani ya mkoba wake wa safari. Yalikuwa ni maandalizi ya safari ambayo kwayo ingeweza kufanikisha mkakati huo. Huko aendako kuliandaliwa mkutano wa kazi. Mkutano ambao ungewakutanisha wadau wa mkakati huo ambao ulishindikana enzi na enzi. Lakini mara hii ulidhamiriwa kufikishwa tamati.

Nilikuwa namwogopa Chameleon tu, Mungu amlaze pema peponi! Akasema huku akiendelea kuweka hiki pale na hiki kule.

Ilikuwa imepita mwezi mmoja tangu wakutane mahali hapo na mfadhili wao Colonel Ivan katika jiji hilo. Na tangu hapo walikuwa wakiwasiliana naye kwa njia ya mtandao tu, hawakujua ni wapi alipo jamaa huyo. Mpanga mipango asiyeshindwa. James Msambamagoya akasimama na kuiacha meza yake, akajitazama kwenye kioo kikubwa na kuiweka tai yake vizuri. Naam, ilimkaa.

Narudi tena Ikulu, sasa si kama mwanausalama bali waziri kamili mwenye dhamana ya ulinzi wa nchi! Akajisemea na kutabasamu. Akachukua mkoba wake na kuiacha ofisi hiyo. Chini ya ghorofa lile, akaingia kwenye taksi na kupotelea anakokujua yeye.

* * *

Chiba wa Chiba akashusha kamera yake kubwa kutoka katika jicho lake. Canon ilikuwa imeshafanya kazi yake. Picha ya Big J ilikuwa tayari ndani ya kifaa hicho. Chiba na Gina walikuwa ndani ya jiji la Port Luis nchini Mauritius kwa siri. Yote haya, Madam S aliyapanga ili kufanikisha zoezi zima la kuuzima mpango wa mapinduzi ya damu uliyopangwa na genge hilo hatari.

Wakaingia garini, Gina nyuma ya usukani, Chiba pembeni yake. Akatoka katika maegesho na kuifuata ile taksi ili kujua ni wapi hasa inakoelekea. Safari ile iliwachukua mpaka nje ya jiji hilo na kujikuta katika bandari ndogo ya Mauri-Port.

“Egesha gari hapo,” Chiba akamwambia Gina. Naye akafanya hivyo. Kutoka pale, wakamwona mtu wao. James au Big J aliteremka kwenye ile taksi cha kushangaza, hakushuka peke yake. Big J alifuatana na mwanamke kando yake. Chiba aliinua kamera yake na kuitega. Alijaribu kuipata sura ya yule mwanamke lakini likuwa ngumu sana.

“Shiit!” akang’aka. Picha zote alizozipata zilikuwa za upande wa nyuma. Big J na yule mwanamke wakaingia katika moja ya jingo lililoonekana kama supermarket katika eneo hilo.

“Bingo!” Chiba akasema. Akafungua droo ya gari hilo na kutoa miwani yake maalum iliyotengenezwa na kamera ya kificho ndani yake. Akachukua na kamera yake kubwa na kijidaftari kidogo.

“Mwanahabari wa sirika gani?” Gina akauliza.

“BBC” Chiba akajibu na kufunga mlango wa gari. Akaelekea kwenye lile lile jengo.

Akapotelea ndani. Ndani ya jengo hilo Chiba alimwona vizuri sana Big J na yule mwanamke. Akapata picha kadhaa za sura ya mwanamke huyo lakini hakumjua ni nani. Alikuwa mweusi, mwafrika haswa, kwa kuitafsiri sura yake, alionekana kuwa na huzuni muda wote, mawazo au tuseme msongo wa mawazo. Hakuwa anaongea. Muda wote huo wakati Big J akicheza na kipakatilishi chake, yeye alikuwa akinywa sharubati ya nazi.

“Huyu ni nani?” Chiba akajiuliza kwa sauti ndogo. Kisha akainuka na kutoka eneo lile. Wakti akifanya yote hayo Big J alikuwa akiendelea kuperuzi kipakatilishi chake lakini kwa jicho pembe alikwishamuaona Chiba na yote anayoyafanya.

“Shenzi kabisa… anafanya ujanja wa kitoto!” akasema Big J na kunyanyuka.

Chiba alikuwa maliwato akijiweka sawa mbele ya kioo kikubwa kilichobandikwa ukutani. Katika kioo hicho akaiona taswira ya Big J akimjia nyuma yake. Sura yake na tambo lake kubwa vikamfanya apate mshituko. Akatahayari. Kabla hajajua cha kufanya akajikuta akipokea kofi la nguvu lililotua kisogoni pake. Akatikisa kichwa na kugeuka. Konde lingine likauparaza uso wake na hii tu ni kwa sababu aliwahi kuliepa.

“Mzee mbona unapiga watu?” sauti ya mtu mwingine ikauliza. Big J hakujali, alikamata Chiba na kumkunja shati.

“Nani kakutuma?” akamuuliza Chiba aliyekuwa akivuja damu puani. Chiba hakujibu. Big J akampekua mifukoni na kutoa kitambulisho.

Douglas Remmy, BBC News reporter

Port Luis.

Big J akachukua camera ya Chiba na kuigeuzageuza, akabonya mahala Fulani na kuchomoa kadi sakima iliyowekwa ndani yake.

“Na hii kadi, hutoipata!” akamwambia na kumwacha. Chiba akaokota vitu vyake pale sakafuni na kuvirudisha mifukoni, akaivaa kamera yake na kujitazama kwenye kioo. Akajisafisha na kujiweka sawa. Akaliendea kabati dogo lililowekwa alama ya msalaba mwekundu, akafungua na kuchukua pamba na dawa, akajiganga. Kisha taratibu akatoka katika jengo lile huku watu wachache walioshuhudia tukio lile kule chooni wakimpa pole. Alipofika ndani ya ile supermarket akatupa jicho pale walipoketi Big J na yule mwanamke, hawakuwepo. Akavuta hatua na kutoka nje. Moja kwa moja akalifikia gari walilokuja nalo, akaingia na kuketi.

“Vipi?” Gina akamuuliza baada ya kumuona kaibana pua yake.

“Jamaa kanistukia, kanipa kipigo mpaka basi…”

“Umeshindwa kusimama naye?”

“Hapana, sikutakiwa kufanya lolote maana ningelikuza tatizo. Amenikagua na kitabulisho cha BBC kimenilinda,”

“Camera…”

“Ipo salama, ila amechukua kadi ya kumbukumbu,” Chiba akajibu.

“Ooh Shit, kwa hiyo kazi yote bure?”

“Mi siyo mjinga namna hiyo…”

“Kivipi?”

“Kila picha niliyokuwa napiga, ilikuwa inajituma moja kwa moja kwenye ubamba wangu. Hivyo basi, picha zote ninazo hapa,” akainua ubamba wake wa Apple na kuupunga hewani.

“Safi sana!” Gina akasema.

“Ila sasa nitampa tabu sana…”

“Kwanini?”

“Ninaiprogram hapa ile kadi, akiiweka tu kwenye kompyuta, atakapoifungua, itaungua pamoja na mfumo mzima wa kompyuta yake. Kama hajafanya backup ya taarifa ya mipango yao basi kila kitu kitakuwa kimekufa,” Chiba akeleza.

“Woyoooo! This is Chiba…” Gina akashangalia na kuwasha gari.

“Umewaona wa kitoka?” Chiba akamuuliza Gina.

“Ndiyo, wamepanda boti na kutokomea katikati ya bahari,” akamjibu.

* * *

Siku tatu baadae

Jioni ya siku hiyo, Kamanda Amata aliegesha gari lake nje ya baa kubwa maeneo ya Chang’ombe. Akateremka na kuliacha hapo gari lake. Mwendo wa miguu ukamfikisha mbali kidogo na baa ile. Eneo lenye utulivu. Majumba makubwa ya kizamani yalikuwa kimya kabisa. Kila jumba likiwa ndani ya uzio wa michongoma mirefu na mageti ya kisasa. Nyumba iliyojengwa kwenye kitalu namba sitini na tatu ndiyo haswa aliyokuwa akiitafuta. Akasimama mbele ya geti lake kubwa na kubonyeza kengele. Baada ya mibonyezo mitatu hivi, kijimlango kidogo cha geti lile kikafunguliwa. Mwanaume mmoja akajitokeza, mwenye kifua kipana na mikono iliyojaa misuli yenye nguvu.

“Habari ya jioni, nikusaidie nini?” yule bwana alisalimia na kuuliza. Amata akatafakari kwa sekunde chache hivi kisha akasema shida yake.

“Dana nimemkuta?” akamuuliza. Yule jamaa akamkazia macho Amata.

“Hayupo!” akajibu huku akiurudishia mlango kutaka kuondoka. Kabla hajafanya hilo mguu wa Amata ulikuwa tayari umeuzuia mlango ule.

“Si nimeshakwambia hayupo, mbona unataka shari?” yule bwana akauliza.

“Shari unaitaka wewe,” akamwambia. “Nimekuuliza Dana, unajibu tu na kuondoka, unajua namuulizia kwa lipi?” Amata akamwambia.

“Nyi si ndo wezi wa wake za watu,” yule bwana akajibu. Lakini mara tu alipomaliza kusema hayo akajikuta akitazamana na domo la Beretta Pico, bastola ya Kiitaliano. Amata akampa ishara ya kuingia ndani. Yule bwana hakubisha, mikono yake ikiwa juu, akaongoza mpaka sebuleni. Katika sebule hiyo kulikuwa na watoto wawili wadogo wakicheza huiku luninga kubwa ikionesha kipindi cha michezo. Amata akaingiza mkono wenye bastola katika mfuko wa koti. Alipoketi yule bwana, yeye akaketi upande wa pili.

“Dana yuko wapi?” akamtupia swali.

“Hayupo!”

“Kenda wapi?”

“Ameniaga anakwenda Mafia kuna kuna kazi wanaenda kuikamilisha,” yule bwana akajibu.

Amata akatafakari kwa sekunde kadhaa.

Mafia! Akawaza.

“Mafia?” akamuuliza tena.

“Ndiyo Mafia,”

“Kaenda na nani?”

“Kuna mwenzake wa ofisini kwao, amekuja hapa ndo wametoka pamoja mchana wa leo,” yule bwana akajibu kwa ufasaha. Amata akajikuta kimya, akitafakari. Mafia! Akawaza.

“Wewe ni nani?” Amata akamuuliza yule jamaa.

“Mimi ni mzazi mwenziye, na hawa watoto ni watoto wetu,” akajibu. Amata akawatazama wale watoto.

“Ok, asante. Naenda!” akainuka na kuaga. Yule bwana hakuwa hata na haja ya kuuliza swali. Wakaagana.

Ndani ya gari lake, Amata akatulia kimya akatoa hili kichwani na kuweka lile. Akawasha gari na kuliacha eneo lile.

Baada ya kutoka Chang’ombe, kamanda Amata akaegesha gari katika baa ya Rose Garden, pembezoni mwa barabara ya Bagamoyo. Akateremka na kutafuta sehemu nzuri ya kuketi. Tayari giza lilikwishataradadi, anga lilikuwa jeusi kuashiria mvua itakayonyehsa muda mfupi ujao. Kamanda Amata akaketi na kuagiza kinywaji akipendacho, Safari Lager.

Nusu saa baadae, Madam S akaungana naye mezani hapo.

“Karibu mwenye nyumba…” Amata akamkaribisha.

“Asante,” Madam S akamjibu na kujivuta mezani akamwinamia Amata naye akafanya hivyohivyo, “umempata?” akamuuliza.

“Hayupo, ameenda Mafia na rafiki yake,” Amata akajibu na kutulia. Kisha kila mmoja akaegemea kiti chake.

“Mafia?” akauliza.

“Ndiyo, Mafia…” Amata akajibu.

“Unajua Dana naye ni mmoja wao na nahisi bado yupo kwenye mkakati,” Madam akasema. “Haupo mbali na ninalofikiria,” Amata akajibu. “Vipi na habari za upande wa pili, zina matunda?” akaongeza swali.

“Chiba amekutana uso kwa uso na Big J jioni ya juzi,”

“We!”

“Kaonja kibano cha mtu mzima,”

“Loh! Ikawaje?”

“Ah si unamjua Chiba, akatulia tu. Ila ameleta tafutishi zisizo mawaa,” Madam S akachukua bahasha aliyokuja nayo na kumpatia Amata. Akaicha na kutoa ndani yake picha kama kumi na moja hivi. Akazitazama kwa makini sana akisaidiwa na miwani yake yenye nguvu ya kuona vizuri kwenye mwanga hafifu.

“James Msambamagoya, Big J” akasema.

“Yes! Amejificha nyuma ya jina hilo na uso wa marehemu,” Madam S akachombeza. Amata akaendelea kutazama zile picha kwa makini Zaidi. Akajikuta anavutiwa na mwanamke yule.

“Huyu mwanamke ni nani?” akauliza.

“Swali letu wote hilo… na anaonekana kama mtu anyekokotwa tu… tazama hii picha hapa,” Madam akachagua picha moja na kumwonesha. Amata akaitazama tena na tena. Aliporidhika akazikusanya zile picha na kuziweka kwenye ile bahasha.

Madam S akachukua bahasha nyingine na kumpatia, “na hii chukua kama kawaida,” akamwambia. Amata akaipokea na kuichana. Ndani yake akatoa karatasi kama zile za wakati ule alizopewa alipotakiwa kwenda kumuua Mwanachia na Mwakibinga.

“Na sasa hukumu ya Msambamagoya itimizwe!” Madam akamwambia. Kamanda Amata akashusha pumzi.

“Port Louis, Mauritius…” akamwambia tena. Amata akabaki kimya kabisa akimtazama mwanamke huyo.

“Wakati haya yote yanafanyika, ulikuwa wapi miaka hiyo?” Amata akauliza.

“Nilikuwa msichana mdogo sana nikihudumu katika Ikulu. Nilikuwa msichana mzuri sana, mrembo wa kuvutia. Bosi wangu alikuwa Chameleon na huyu Msambamagoya mshenzi,” Madam S akaeleza huku akitabasamu.

“Bahati yako sikuwapo wakati huo… nisingekuacha!”

“Shenzi we huna adabu…! Madam akamwambia huku akisimama wima tayari kuondoka. Amata naye akasimama na kutia zile bahasha ndani ya koti lake.

“Madam S, nasikitika kukwambia kwamba sintokwenda Mauritius kwa sasa. Kuna misheni inayohusiana nah ii nataka niikamilishe kwanza,”

“Ipi?”

“Nataka nijue Dana kaenda Mafia kuna nini! Mafia ni kisiwa, na hawa jamaa wanafanya mambo yao katika kisiwa kimoja ndani ya bahari ya Hindi… je si Mafia?”

“Amata!” Madam S akajikuta akiita huku akipigwa na butwaa, “na mmoja wao yuko hapa nchini… umenifungua akili. Nipe hiyo bahasha!” akamwambia. Amata akamrudishia ile bahasha.

“Nakupa siku nne unipe jibu la hiyo misheni,” akamwambia.

“Sawa!” wakaagana.






















MAFIA


Usiku wa siku hiyo, boti ya kisasa kabisa iliwasili katika kisiwa hicho kiolichopo nchini Tanzania. Baada ya kupata maegesho yake, watu wawili wakateremka; mwanamme mwenye tambo kubwa na mwanamke. Wakapokelewa na mwenyeji wao, Mc Tee.

“Ha haaaa Comrade!” Mc Tee akamkumbatia Big J, “naona sasa umerudisha mrembo wetu katika himaya yake.

“Aaaaa kabisa, ameshakula upepo wa Port Luis vya kutosha…” Big J akasema huku akivuta hatua kuingia katika jumba hilo la kifahari. Katika kisiwa hiki kulikuwa na hoteli kubwa ya kisasa iliyojulikana kama Kilindoni Camp Site. Ndani ya hoteli hii kulitolewa huduma mbalimbali kama kumbi za mikutano, sherehe, malazi, utalii wa bahari na mambo mengine mengi. Kilikuwa kituo kikubwa sana cha watalii kutoka katika pepo zote nne za dunia.

Kibwana Mtokambali mara tu baada ya kubadilishwa sura yak e na kupewa uraia wa inchi ya Australia, alirudi tena Tanzania mwaka 1999 kupitia uwanja wa ndege wa Kilimanjaro. Mara hii akijifanya muwekezaji na kufanikiwa kununua eneo hilo la Mafia na kujenga hoteli hiyo kubwa nay a kisasa. Alihodhi mikutano mingi ya serikali na makampuni binafsi huku akiwa katega vinasa sauti kwenye kumbi za mikutano na kila chumba cha kulala. Hakuna kilichoongelewa ambacho hakukisikia wala kukiona. Aliweza kufuatilia mikutano yotre na kujua nani kaja na kasema nini. Alikuwa na uwezo wa kutazama vyumba vyote na kuona kila anachotaka seuze kusikia. Hii yote aliiweka kutokana na mpango wao uliokuwa ukiendelea kuratibiwa mahali hapo.

“Hassna!” akaita. Mwanamke huyo mrembo akaitika na kufika mara moja, “mpeleke Egra chumbani mwake,” akaagiza. Hassna akamchukua Egra na kumpeleka mpaka kwenye chumba ambacho kwacho aliishi miaka kadhaa nyuma.

Egra aliingia ndani na kufungiwa kwa nje. Hakuwa na uhuru kabisa wa kufanya lolote. Ndani ya chumba hicho kulikuwa na kila kitu, hakupaswa kutoka nje. Alibaki kasimama kwa muda na macho yake yakauona tena msalaba wa mumewe ambao alikabidhiwa pindi tu alipouawa. Akatikisa kichwa kushoto kulia, machozi yakamtiririka. Akakumbuka kifo kibaya kabisa kilichomfika mumewe usiku tu wa siku ya harusi.

Mungu atanilipia! Aliamini. Akajitupa kitandani na kulia kwa vikwifukwifu. Chumba cha Egra kilikuwa upande wa pili wa kisiwa kile. Hivyo kupitia dirishani aliweza kuiona ile hoteli kwa vizuri kabisa ikiwa imetengwa kwa ghuba.

* * *



Mungu atanilipia! Aliamini. Akajitupa kitandani na kulia kwa vikwifukwifu. Chumba cha Egra kilikuwa upande wa pili wa kisiwa kile. Hivyo kupitia dirishani aliweza kuiona ile hoteli kwa vizuri kabisa ikiwa imetengwa kwa ghuba.

* * *

McTee na Big J walikutana katika sebule kubwa ya gharama kubadiishana mawili matatu.

Wakipeana taarifa hii na ile. Big J akampa habari ya mpiga picha aliyekutana naye huko Mauritius.

“Umemuua?” McTee akauliza.

“No! nimemtia disprin tu, ila nimechukua memory card ya camera yake… hivyo hana kumbukumbu yoyote,” akamwambia McTee.

“Unafikiri ana madhara kwetu?”

“Ni ripota wa BBC, angekuwa hana kitambulisho, angepata tabu sana,” akamwambia. Big J akatoa ile kadi kutoka alipoihifadhi na kumpatia McTee. Akaipokea na kuiendea kompyuta yake ya kisasa kabisa ili kuweza kuona nini kilichomo.

“Ngoja tuone picha alizopiga, huenda zikatuambia kitu,” akasema huku akiipachika kwnye ile kompyuta yake ambayo daima ilikuwa on. Mara tu alipoipachika, ile kompyuta ik. ampa ishara kuwa ile kadi ipo tayari kufunguka. Big J akasogea pale alipo McTee. Akatembeza kipanya na kufungua upande wa document, alipoiamuru kufunguka ikamletea ujumbe kuwa; kwa kufungua kadi hiyo kungeiharibu kompyuta yake. Akapuuzia, akaiamuru tena, ikampa ujumbe uleule, hakutii akaiamuru ifungue tu. Kyoo cha kompyuta kikawa cha buluu kabisa, halafu cheusi, mwisho ikazimika.

“What?” McTee akauliza kwa sauti. Akabofya huku na huku, wapi. Akaiinua na kuitikisa, hakuna kitu. Akamtazama Big J huku macho yake yakiwa yametona machozi.

“Vipi?” Big J akauliza.

“Sielewi kilichotokea… sijui ndiyo imekufa au vipi,” akatia shaka. Big J naye akajaribu, wapi. Kompyuta ile ilikuwa kimya kabisa.

“Shiiiit!” McTee akang’aka na kujishika kichwa, “data zote zimepotea, nooooooo,” akajikuta akipiga kelele kama aliyechanganyikiwa.

Kazi ya Chiba ilitimia.

* * *

Kamanda Amata alisimama mbele ya nyumba moja ya kizamani huko Manzese kwa mfuga mbwa. Haikuchukua muda kufunguliwa mlango wa nyumba hiyo na kukaribishwa ndani. Akaingia na kuketi kitini. Mbele yake kulikuwa na mwanamama wa makamo na vijana wawili wa kiume.

“Karibu baba,” yule mama akamkaribisha. Amata bado alikuwa kimya pasi kusema neon lolote. Alimtazama yule mama na kuusoma msiba usiokwisha ndani ya macho yake.

“Shikamoo mama,” akamwamkia naye akaitikia. “Samahani kwa kukusumbua usiku huu, mimi naitwa Inspekta Jaffari kutoka kituo cha polisi cha kati…”

“Ndiyo karibu baba!” yule mama akaitikia na kukaribisha kwa shauku ya kutaka kujua nini kimemleta mgeni huyo nyumbani kwake usiku huo. Amata hakupoteza muda, akachomoa picha ile iliyopigwa na Chiba kule Mauritius, sasa akiwa ameikata na kubaki kipande cha yule mwanamke tu. Akamkabidhi yule mama.

“Unaweza kumatambua huyo mwanamke kwenye hiyo picha?” akamuuliza. Yule mama akajikuta kama kapigwa shoku ya umeme. Machozi yakaanza kumtiririka, akawapatia vijana wake ile picha. Nao wakaitazama na kubaki vinywa wazi.

“Huyu mwanamke anafanana kabisa na dada yetu Egra ambaye hatuwezi kusema kama amekufa ila alipotea mwaka 1990 mara tu baada ya sherehe yake ya harusi. Ukweli haujifichi mwaka ule na sasa lazima abadilike…” mmoja akasema huku bado akiwa kaishikilia ile picha.

“Sawa, nashukuru kwa maelezo… samahani sana kwa kuwakumbusha machungu, mnaweza mkailaumu serikali kuwa haifanyi chochote kwa swala la mpendwa wenu. Sivyo! Tunalifuatilia mpaka unavyoona nimekuja hapa…”

“Unataka kutuambia kuwa dada Egra ni mzima?” yule mwingine akadakia.

“Siwezi kusema ndiyo wala hapana… ila uchunguzi unaendelea na naweza sema tupo mahala pazuri kutoa jibu la tukio lile. Serikali huwa hailali katika kuhakikisha usalama wa raia na mali zao,” akawaambia huku akiwa wima tayari kuondoka. Wakaagana.

Ziara ya Amata usiku huo ilikuwa ndefu, alitaka kuhakikisha cheni aliyoifanyia kazi anaipitia tena ili tu kuhakikisha watu wake wako wapi. Alitumia mbinu hii kujua nani na nani wangeweza kuwa funguo katika mtanange huu. Alihisi hatari inalikaribia taifa, hakupenda iwe hivyo. Kila alipotaka kukata tamaa kiapo cha kazi yake alichoapa mbele ya Rais kilimsuta, ‘FOR MY PEOPLE, FOR MY NATION’.

Giza lilitawala mara baada ya umeme kukatika upande wa Kigogo mpaka Mburahati kwa hiyilafu iliyotokea kwenye transfoma linalogawa maeneo hayo. Amata aliendesha gari lake kwa umakini ili asije kuginga walevi usiku huo. Akiwa katawaliwa na mawazo ya kutosha, ilikuwa bado inamlazimu kuufukuza usingizi na kuhakikisha anakipata kile anachokitafuta.

Taa za gari lake zikapungua mwanga pindi alipoikaribia nyumba aliyoitaka. Nyumba ambayo ilikuwa kwenye safu ya NHC katika kitongoji cha Mburahati. Akaegesha gari mita kama ishirini hivi kabla ya ile nyumba na kuzima injini. Dakika moja ilitosha kuyasoma mazingira. Akateremka na kufunga mlango nyuma yake, hatua zake zikamfikisha mbele ya nyumba ile. Hakuhitaji kugonga hodi, amgongee nani? Funguo Malaya zake zikafanya kazi, akaingia. Akavipita vyuma kadhaa na kukifikia kile akitakacho, upande wa uwani. Kutoka mfukoni mwake akachukua kamera yake ndogo iliunganishwa na waya mgumu, akaipenyeza kwenye tundu la ufunguo, ikapenya. Akachukua simu yake na kuipachika upande wan je kwenye muisho wa waya ule. Naam, kamera ile ilimpa picha aitakayo. Ndani ya chumba hicho kuikuwa na mtu mmoja tu. Mwanamke aliyekuwa kalala fofofo kitandani. Akaigeuza huku na huko, hakuona mtu mwingine. Akaiondoa na kuirusidha kwenye mfuko wa koti lake. Akapachika funguo na kuingia ndani.

Uzembe wa hali ya juu kuiondoa funguo mahala pake, unatakiwa uigeuze tu na kuiacha hapohapo ili mtu akija kwa nje ashindwe kutumbukiza yake! Akamsema kimoyomoyo. Akajipenyaza ndani na kuurudishi ule mlango, hakuwasha taa aliacha ileile ya pembeni mwa kitanda iendelee kuangaza kwa mwanga unaotia matamanio. Akaketi kitandani. Dakika mbili za ukimya, simu yake ikichunguza kama kuna kamera au kinasa sauti. Hakuna. Akashika shuka taratibu na kuufunua uso wa huyo aliyelala, naam ndiye yeye, Mariam. Akamwamsha kwa upole kama afanyavyo mume kwa mkewe au mpenzi kwa mpenziwe pindi anapohitaji. Mariamu akaamka kivivuvivu, macho yake akagongana na mtu hasiyemjua. Akashtuka na kutaka kupiga kelele. Haraka, kono la Amata likamdaka na kumziba mdomo. Akatikisa kichwa kushoto kulia kama ishara ya kumtaka asifanye hivyo.

“Unanikumbuka?” Amata akamuuliza Mariam pindi tu alipomuachia huru. Binti huyo alikuwa akitetemeka akikusanya shuka na kuyaficha matiti yake.

“Si-si-ku-kumbuki,” akajibu kwa woga.

“Usiogope… ndimi niliyeyaokoa maisha yako kutoka nyumba namba 73A Mtaa wa Galu Kinondoni…” akamkumbusha. Mariam asingeweza kukumbuka kwani alikuwa katika mzimio. Akatikisa kichwa kuwa hakumbuki.

“Unata-ka ni-ni Kwang usiku huu?” Mariamu akatupa swali.

“Namtafuta Andrew…” alipotaja jina hilo, sura ya Mariamu ilibadilika. Amata akalisoma hilo.

“Sijui alipo… we ni nani?” akauliza. Sasa hakuwa na woga tena.

“Mimi ni askari mpelelezi. Unajua Andrew ni jambazi?” Amata akamwambia.

“Najua, na ndiyo kisa cha kuachana naye,”

“Sasa yuko wapi?”

“Mara ya mwisho alikuja hapa mwezi umepita kunitaka turudiane kimapenzi,”

“Enhe…”

“Nikamkatalia,”

“Sasa unajua yuko wapi?”

“Hapana ila tu mara yeye Zaidi anapatikana hapa Dar na Mafia,”

“Umeshawahi kwenda naye Mafia?”

“Ndiyo, kipindi kirefu nyuma,”

“Sehemu gani na mlienda kufanya nini?”

“Tulienda mapumziko ya Idd pili… pale kuna hoteli kubwa inaitwa Camp Site sijui,

hukohuko…”

“Sawa. Namtafuta sana, nikajua kwako nitapata taarifa zake,”

“Tulishaachana kaka yangu. Sitaki hata kumsikia aichonifanyia si cha kibinaadamu,”

“Alikufanyia nini?”

“Tuyaache hayo..”

“Ok, asante… usimwambie mtu kama nilikuja,” Amata akamuaga Mariamu. Mwanamke huyu akabaki kinywa wazi asijue kama kaongea na binadamu au mzimu. Maana alijikuta woga unamwishia jambo ambalo si kawaida kwa mtu kuibuka chumbani kwako usiku. Ila elimu ya Amata ya kumfanya mtu aondokewe na woga hata wa kifo ilifanya kazi.

Kamanda Amata alijikuta katikati ya jiji saa saba usiku akiwa hana la kufanya.

Ingekuwa Mafia kunafikika kwa gari ningeondoka sasa hivi! Akawaza akiwa anaegesha gari lake katika casino kubwa la Las Vegas maeneo ya Upanga. Akateremka na kupotelea ndani ya jengo hilo kuumaliza usiku.

* * *

“Kila kitu kipo sawa kwa upande wetu,” Dana alilieleza jopo. Kilikuwa kikao cha watu wachache wenye dhamana ya juu katika genge linalotaka kufanya mapinduzi. Dana akiwa kama mwanachama mchanga aliyelishwa sumu tangu akiwa Lisbon, alipewa kitengo cha kuhakikisha anawahadaa baadhi ya wanajeshi watakaokuwa tayari kushika silaha. Kwa ubembe wake wa kike alifanikiwa. Na siku hii tayari walitakiwa kufika kisiwani hapo ili kuweka mikakati ya mwisho.

“Tutafanikiwa kwa asilimia kubwa sana, maana watu niliowaandaa ni wav yeo vya chini ambao daima tunasema nndiyo kundi linaloteseka jeshini, wamekubali kwa sauti moja ilhali wao wenyewe hawajuani. Kwa ujumla nimepata vijana mia moja wakakamavu wasiopenda kurudi nyuma. Na tayari leo asbuhi tumewaingizia pesa za safari na maandalizi,” akafafanua.

“Hah hah haaaaaaa… msichana unajua kazi, Mwanachia hakukosea kukuchagua. Enhe na vipi ndani ya TNS hakuna chochote kinachozungumzwa?” sauti ya kiongozi wa mkutano ikasikika.

Katika kikao hiki kilichofanyika ndani ya ukumbi mdogo wa wastani, wajumbe hawakuweza kutambuana kutokana na mwanga hafifu uliofanya giza la wastani.

“Ndani ya TNS kupo kimya kabisa, lakini kuna kitengo kingine ambacho ni hatari zaidi kuliko TNS… hiki ndicho yabidi kukitazama. Kina watu wenye weledi mkubwa sana. Mkuu nimefanya kila mbinu kujua japo makao yao yapo wapi nimeshindwa. Ila mtu mmoja wa kitengo hiki ninamfahamu na ndiye aliyemuua Mwakibinga kule Brussels na Mwanachia kule Lisbon, anaitwa Amata Ric au Kamanda Amata TSA 1,” akaeleza.

“Huyo habari zake tunae. Ndugu wajumbe, anayetajwa hapa ni kiumbe hatari ambaye inabidi adhibitiwe haraka. Na kitengo hicho ni kitengo hatari ambacho yapaswa kifutwe kwanza…”

“Huyu jamaa kapewa hati ya kutuua sisi wane; wawili keshafanikiwa ila kwa sisi tuliobaki maji yamekuwa marefu kwake. Wamegonga ukuta… na mapinduzi yatafanikiwa,” Big J akaunga mkono, “kama alivyosema mjumbe mjumbe Epsilon, ni kitengo chenye watu wenye weredi mkubwa. Na ninahisi, sina uhakika ila ninahisi, kiongozi wa kitengo hiki ni mwanamke anaitwa Selina, alikuwa mwanausalama wa Ikulu pindi nikiwa pale kama mwanausalama namba mbili wa Rais. Mwanamke huyu amejifunza mengi kutoka kwa Chameleon, mtu hatari sana aliyetibua mipango yetu mwaka ule…” akasisitiza.

“Sasa tunajadili wanausalama au kazi inayotukabili?” sauti ya kiongozi ikaingilia kati.

“Alfa!” Big J akaita.

“Beta!” yule kiongozi akaitika.

“Hawa tunaowataja hapa watatusumbua, si ajabu wanasikiliza kila tunachokiongea hapa, lazima washughulikiwe ndani ya saa ishirini na nne. Tukiwamaliza kazi yetu itakuwa nyeupe sana…” Big J au Beta katika mkutano huo akazungumza.

“Beta, Umesomeka,” akajibiwa.

Kikao kile kiliendelea kwa takribani saa mbili Zaidi, mikakati ikiwekwa na mpango ikasukwa. Usiku huohuo wapo waliorudi kwa boti kwa kutumia njia za siri na wapo waliosubiri kupambazuke ndipo waondoke.

* * *


Kikao kile kiliendelea kwa takribani saa mbili Zaidi, mikakati ikiwekwa na mpango ikasukwa. Usiku huohuo wapo waliorudi kwa boti kwa kutumia njia za siri na wapo waliosubiri kupambazuke ndipo waondoke.

* * *

Asubuhi ya siku iliyofuata, Amata alikuwa na akili moja tu. Kufika Mafia. Akaegesha gari lake karibu kabisa na ofisi za Azam Marine. Akateremka na kuhakikisha amefunga milango vizuri. Akiwa na mkoba wake mdogo mgongoni, aliipachika miwani yake sawia kujikinga na miale mikali ya jua asubuhi hiyo. Akavuta hatua mpaka kwenye dirisha la mkata tiketi.

“Karibu baba!” akakaribishwa na mwanadada mwenye lafudhi ya kipemba. Amata akatoa tabasamu lile ambalo daima uliweka akiba ili kulitumia kwa warembo kama hawa.

“Asante, kuna usafiri kuelekea Mafia leo?” akauliza.

“Umepata baba angu, tena boti inaondoka nusu saa ijayo. Boti maalumu kwa watalii nitakutia humohumo,” yule mwanadada akajibu huku akimaliza kumhudumia mteja mwingine. Dakika tano tu Amata alikuwa tayari keshakamata tiketi yake mkononi.

“Usiwe na wasiwasi baba, hiyo inaenda kasi sana, masaa matatu tu utakuwa Mafia, enjoy likizo yako…”

Eh! Mwanamke anaongea kama chiriku! Amata akawaza na kuondoka dirishani hapo. Sehemu ya juu kabisa ya boti hiyo ndipo alipochagua kukaa, kamera yake kubwa ikining’inia kifuani, mkoba wake mgongoni, alichagua siti ya kukaa. Pembeni yay eye aliketi mwanadada wa kizungu aliyevalia kofia kubwa ya mkeka. Kama alivyoambiwa, nusu saa ileile, safari ikaanza. Katika boti ile watu weusi ungeweza kuwahesabu kwa uchache wao. Hilo kwa Amata lilikuwa changamoto kubwa kwani ilimbidi kumchunguza kila mmoja ili agundue kama kuna yoyote mwenye sura ovu. Safari haikuwa mbaya, bahari ilitulia muda wote. Ni boti moja tu waliyopishana nayo kwa mbali ikirejea kutoka Mafia.

Saa tatu zilezile, ile boti ikaegeshwa katika bandari ndogo ya Kilindoni. Mara baada ya kuwekwa gatini, abiria walianza kuteremka kwa shauku ya kukinyaga tu kisiwa hicho. Wakati watu hao wakiwa na furaha ya kufika hapo, ni mtu mmoja tu kwenye boti ile alikuwa na mawazo mengi sana. Amata. Yeye alikuwa wa mwisho kabisa kushuka. Kwa hatua za taratibu alifuata msafara wa watalii waliokuwa wakipita kwenye ujia mrefu kukifikia kisiwa hicho. Huku akipiga picha ya hapa na pale aliendelea kutembea mpaka kufika katika pwani ya kijiji cha Nyamisati. Taksi zilizokuwa hapo zikawapokea, watalii wakachukuliwa na magari ya makampuni ya utalii. Kamanda Amata akavuta hatua mpaka upande wa pili wa barabara. Pale palikuwa na taksi moja kuukuu, dereva wake naye alikuwa mzee vilevile.

“Ee kijana gari hii kijana, usiione mzee, injini ipo oda kabisa,” yule mzee alipigia debe gari lake. Amata hakuuliza, aliingia na kuketi katika kiti cha mbele. Kamera yake iliendelea kupiga picha mbalimbali.

Mara baada ya kuketi, yule mzee naye akaingia upande wake na safari ikaanza. Barabara yaenye lami mbovu ndiyo aliyoitumia mzee huyo.

“Safari ni ya muda gani?” Amata akauliza.

“Dakika kumi tu! Mbona siyo mbali? Kwa huyo bwanyenye! Sasa hivi tunafika,” akamjibu huku akibadili gia na kuongeza mwendo kuyapita yale mashimo bila hata kuangalia.

“Kwanini mnamwita bwanyeye?”

“Aaaa ana ukwasi sana yule bwana, mtu anaishi hata kumuona nje ni kwa nadra!”

“Hata watoto wake hawatoki nje?”

“Watoto apate wapi? Sijui mgumba alipo pale au na ye amechukua uchawi wa kikwetu…”

Amata akajikuta anashindwa kujizuia kucheka hasa kwa lafudhi ya huyo mzee, “aisee!” akasindikiza cheko lake.

“Unajua mi nilijuwa we mmerekani mweusi bwana kuwa hujui kingreza,” akamwambia Amata.

“Hapana! Mi mzaramo wa Monerumango hapo. Ila ni mwandishi wa habari,” Amata akajibu, wakati huo yule mzee Alikuwa akiegesha gari lake karibu na sehemu ya kushukia abiria.

“Shilingi ngapi?”

“Elfu mbili tu mwanangu,”

Amata akatoa noti ya shilingi elfu tano na kumpatia, “keep change,” akamwambia.

“Asante mwanangu, asante sana, ubarikiwe na Allah!” akiwa anashukuru hivyo tayari Amata alikwishafika katika dawati la mapokezi la hoteli hiyo.

“Karibu Chole Camp Site Hotel,” mwanadada mwenye asili ya kiarabu akatoa karibisho lililojaa huba. Amata akamtazama kwa jicho la wizi wakati akipokea leja ya kusajiri wageni. Akajaza taarifa zake na namba za vitambulisho na kila kitu. Akasukuma leja ile na kumrudishia yule mwanadada.

“Utakuwa kwa siku ngapi?”

“Tatu tu,” akajibu.

“Oh! Mbona chache sana? Utakuwa umemaliza kutembelea Mafia?”

“Kisiwa chenyewe kwa miguu tu natembea siku moja… lakini siwezi kukaa Zaidi labda kama utakuwa mwenyeji wangu,” akaanza ubembe.

“Mmmmmh!”

“Unaguna nini?”

“Hapo kwenye uenyeji… haya ni shilingi laki nne na nusu kwa chumba ulichochagua,” yule mwanadada akaeleza. Amata akachomoa kadi yake ya malipo na kumpatia. Pamoja na kadi hiyo chini yake kulikuwa na kadi ya kibiashara yenye namba za simu. Baada ya kufanya malipo yote, akachukuliwa mpaka ghorofa ya nne na kuoneshwa chumba chake.

Alipohakikisha yule mhudumu ameondoka, akatazama vizuri kitasa kile, kisha akatumbukiza funguo na kufungua ule mlango. Akaingia taratibu na kuweka begi lake juu ya meza. Akakikagua kwa macho kabla ya kugusa chochote. Alipojiridhisha katika awamu hiyo ya kwanza, akafungua begi lake na kuchukua SpyFinder, kifaa maalumu ambacho huweza kutambua endapo kuna kamera au vinasa sauti vya siri. Akakiwasha na kukiweka mezani sekunde tano zilikuwa nyingi kikaanza kutoa mwanga mwenkundu. Amata akatikisa kichwa juu chini.

Camera za nini kwenye vyumba vya hoteli? Akajiuliza. Akachukua mkoba wake na kuuweka kitandani, kamera yake kubwa nayo akaitupia hapohapo, kidaftari chake cha kuzugia kama mwanahabari nacho akakitupia hapo.

Sawa nitazamaeni mpaka nitakapowaonesha mi nani! Akajisemea na kujiandaa kwenda kuoga.

* * *

Vijana wa chumba cha usalama katika hoteli hiyo walikuwa na kazi ngumu ya kufuatilia chumba kimoja kimoja, kuona kila mgeni anafanya nini chumbani mwake. Hakukuwa na usiri.

Wakiwa bize katika kamera zao ni mmoja tu aliyevutiwa na mgeni aliyeingia nusu saa iliyopita.

Kwanza kilimvuta gari alilofika nalo, nay eye muonekano wake. Alikuwa kijana jamali kwa hali. Akamfuata kwa kamera hizo mpaka mapokezi na kuvutiwa Zaidi na uchangamvu wake akiwa mbele ya mwanadada yule. Alijitahidi kunasa mazungumzo yao laini hakufanikiwa. Hakuishia hapo, akatazama korido zote ni wapi anaelekea. Chumba namba 406, akakikariri. Akazungusha kiti chake na kuifuata luninga inayoonesha vyumba vyote vya ghorofa ya nne. Akawasha za chumba namba 406 na kuendelea kumwangalia mgeni yule. Kitu kingine kilichomfanya amkazie macho ni kuwa alimwona mwerevu sana, hili lilimvuta pia. Wageni wengi aliyowazoea, wangefika tu na kujitupa kitandani au kwenda bafuni. Lakini huyu haikuwa hivyo. Aligundua kua kila kitu anakifanya kwa hesabu na mpangilio. Akamkubali.

Katika kisiwa cha Jibondo, pembeni tu wa kile cha Mafia, kulikuwa na jumba moja la kifahari lililokuwa mkabala na hoteli ile kwa umbali wa kama kilomita moja vikitengwa na mlango bahari. Hilo ndilo lilikuwa jumba la Mc Tee na mambo yake yote. Akiwa katulia kwenye luninga na mgeni wake wakibadilishana mawazo, hakujua kabisa kama kiumbe hatari kilichoshika kifo chao mkononi mwake kilikuwa tayari ndani ya kilomita mbili za eneo kutoka pale walipo. Simu ya mezani kwake ikaita, akainuka na kuinyakuwa. Akaiweka sikioni.

“Chumba namba 406 kuna mgeni ameingia mchana huu, anaonekana ni mwerevu sana…” yule kijana akaufikisha ujumbe kwa bosi wake.

“Hakikisha jicho lako halitoki kwake, kisha unipe taarifa kama kuna jambo la hatari tumtembelee…” akamjibu na kukata simu. Akarudi kitini na kuketi huku mazungumzo yake na Big J yakiendelea. Hawakukaa sana simu ileile ikaita tena, mara hii ikatoa taarifa ya kupokea nukushi, akakubali. Dakika moja iliyofuata tayari alikuwa na karatasi mkononi lililokuwa na ujumbe aliotumiwa.

Mzigo umeondoka leo Chechinya,

Saa sabini na mbili upokee kwenye bandari bubu.


Nukushi ile ikaishia hapo. Mc Tee akashusha pumzi ndefu. Mapigo ya moyo wake yakabadilika na kuongeza kasi. Akamapa taarifa mgeni wake ambaye naye alikuja hapo kwa ajili hiyo.

Kumekucha! Mc Tee akawaza na kujitupa kwenye kochi.

“Tunaanzia wapi?” Big J akauliza.

“Yatupasa kufika kambini kuwaweka vijana sawa kwa ajili ya tukio, ili wajue wanachokisubiri kimewadia,” Mc Tee akasema.

“Safi sasa naiona Tanganyika yetu iko mikononi…” Big J akatamka huku akisimama na kumpa mkono Mc Tee.

“Likitimia, tutafufuka kutoka kaburini… tutavuwa haya masura na kurudi kwenye uhalisia wetu,”

“Kabisa,” Big J akaunga mkono. Mc tee akavuta hatua na kuliendea jokofu, akatoka na chupa kubwa ya Captain Morgan na kuiweka mezani, bilauri mbili zikasogezwa hapo, wakaanza kupiga kinywaji.

“Barbier ataingia saa ngapi?” Big J akauliza.

“Yeye ataingia hapa jioni ya leo, na moja kwa moja tutampeleka site ambako atakutana na wapiganaji. Ataweka mikakati sawa tayari kwa kazi,” Mc Tee akaeleza.

“Umeshaandaa suti ya uapisho?”

“Tayari niliagiza kutoka Uingereza,”

Wote wawili wakaanga kicheko na kugonga cheers.

* * *

Ndani ya chumba namba 406, Kamanda Amata alikuwa amelala kimya kitandani. Akii yake ikifanya kazi jinsi ya kuanza uchunguzi wake katika eneo hilo. Alijuwa wazi uwa kila anachokifanya ndani ya chumba kile anaonekana, hivyo aliamua kuwa mpole na kufikiri jinsi gani ataikomesha hali hiyo. Usingizi wake haukuwa tua kama usingizi bali ulibeba mambo mkuu mawili; mosi mapumziko, pili kupanga mikakati. Mkakati mmoja wapo ilikuwa ni kumnasa yule mrembo wa mapokezi kimapenzi, si tu afurahiye kile akitakacho bali amtumie kwenye kazi yake ya kuchunguza eneo hilo na mmiliki wa hoteli hiyo. Pili jinsi gani ataweza kumfikia mmiliki ili amjue kwa sura na haiba kujiridhisha kama ndiye amtafutae.

Hivyo kulala kwake kimya kulikuwa na maana kubwa, pamoja na kmhadaa yule anayemtazama katika hizo kamera. Mtikisiko hafifu wa saa yake ukamfanya ageukie upande wa pili. Akabofya kitufe Fulani na saa ile ikaanza kuingiza ujumbe. Akiwa bado kalala ubavuubavu, aliweza kusoma kile kikaratasi kilichokuwa kimefika. Alipomaliza akakivuta na kukikata, akakitia kinywani na kutafuna. Bila kujiuliza alikimeza. Dakika kumi na tano hivi zilizofuata akaamka na kuvaa kaptula yake, shati jepesi, kofia na miwani nyeusi. Akachukua kamera yake kubwa na kutoka nje ya hoteli huku miguuni akiwa na makubazi. Vitu vingine vyote aliviacha kitandani tena shaghala baghala ikiwamo kitambulisho chake bandia.

Alifika mapokezi na kuacha funguo za chumba. Kwa mara nyingine akagongana nan a yule mrembo.

“Umeshakuwa mwenyeji?” yule mwanadada akamuuliza.

“Hapana, ila nataka kufanya utalii wa majini kidogo has wakati wa sunset,” akamjibu. “Vipi ndo’ watoka?”

“Ee nimemaliza kazi mpaka kesho asubuhi,”

“Hongera, ila utaniacha mgeni wako mpweke mpaka hiyo kesho,”

“Hah hah hah watu wa bara nyi’ mna maneno! Karibu kwetu basi,”

“Kwenu au kwako?”

“Haya basi kwangu…”

“Utapika nini nije kula?” Amata akaona hii nafasi si ya kuiacha. Lazima kuzichanga karata.

“Wali nazi na samaki,”

“Oh asante nitakuja hakika…” wakamaliza mazungumzo tayari wakiwa nje kabisa ya hoteli ile. Mara alipoachana na huyi mwanamke akaingia katika ofisi ndogo za Scuba Diving zilizo katika eneo hilo. Pale akakodi boti ya kuendeshwa akiomba kuzungushwa kisiwa kizima ilia one mandhali yake. Lakini moyoni mwake alikuwa anatazama kitu kingine kabisa. Safari ikaanza. Wakaanzi upande wa kusini kuzunguka. Amata alikuwa ametingwa na kamera yake kupiga picha mbalimbali. Kamera ile ilikuwa imeunganishwa kwa njia ya mtandao kiasi kwamba kila picha anayopiga kuna batani akibonyeza picha ile inasafiri mpaka kwenye kompyuta yao kubwa iliyofungwa huko Shamba.

“Unapenda sana kupiga picha,” nahodha wa chombo hicho akamuuliza wakiwa tayari umbali wa takribani kilomita kumi upande wa Kilindoni.

“Yaani ndiyo hobi yangu na pia ni kazi yangu,” akamjibu.

“Safi sana, basi hapa utapata picha nyingi, nzuri na zenye kuvutia,”

“Nitashukuru sana ikiwa hivyo,” akamjibu. Ile boti ikazidi kuongeza kasi, na Amata aliendelea kupiga picha.

“Wewe ni mwenyeji hapa kisiwani?” Amata akamuuliza.

“Nimezaliwa na kukulia hapahapa, kwa hiyo haitoshi tu kuniita mwenyeji bali mzawa,” akajibu na kisha wote wakacheka.

“Hii Chole Camp Site Hotel inamilikiwa na nani?” akauliza huku akeindelea kujiweka bize.

“Hii ni ya mwekezaji mmoja raia wa Australia huko, anaitwa Mc Tee Christopher, ukiwa na bahati utamwona huwa anapenda kujakuja hotelini pale,” akajibu.

Wakati yeye akiwa kwenye utalii huo, kule chumbani kwake kijana mmoja alijitosa ndani kama alivyoagizwa. Alichotakiwa ni kuchukua kitambulisho tu na si kitu kingine. Akaingia kwa tahadhali kubwa sana, akakinyakua kitambulisho pale juu ya kitanda na kukipeleka kwa yule kijana wa kule chumba cha usalama. Yule kijana akakitumbukiza kwenye mashine yake maalumu ya kudurufu kitambulisho. Akatoa nakala yake ikiwa imefanana kwa asilimia zote.

Alipomaliza akampatia na kumtaka arudishe kulekule alikokitoa. Yule bwana wa chumba cha usalama alifanya hila na kurudisha kitambulisho feki wakati kile orijino akibaki nacho. Akakitia kwenye bahasha na kupiga simu upande wa pili.

Hazikupita dakika tano, boti moja ya kifahari iliegeshwa upande wa nyuma wa hoteli hiyo. Hassna akateremka akiwa na bikini na kikoti chepesi mwilini mwake. Akapita mlango wa nyuma na kutokea moja kwa moja kwenye ile ofisi. Akakabidhiwa bahasha na kuondoka pasi na kuongea na mtu yoyote.




Hazikupita dakika tano, boti moja ya kifahari iliegeshwa upande wa nyuma wa hoteli hiyo. Hassna akateremka akiwa na bikini na kikoti chepesi mwilini mwake. Akapita mlango wa nyuma na kutokea moja kwa moja kwenye ile ofisi. Akakabidhiwa bahasha na kuondoka pasi na kuongea na mtu yoyote.

* * *

Hassna aliikabidhi bahasha ile kwa Big J ikiwa salama kabisa. Mabwana hao wakaingia katika ofisi yao ndogo na kuskani.

“Una wasiwasi n huyo bwana?” Mc Tee akauliza.

“Watu wa usalama kule hotelini ndo wamemhofia wanasema anaonekana mjanja sana,”

“Ok ngoja tumuone ni nani…”

“Unajua mwandishi wa habari ziku zote ni mchunguzi. Hata huyu si unaona ni mwandishi lazima awe na tabia za mtindo huo,” Mc Tee akasema.

“Mheshimiwa, ujanja ni mwingi mjini,” Big J akamwambia huku akijaribu kuichunguza ile picha kwenye mashine yake kama kuna maelezo mengine yoyote kuhusu mtu huyo.

“Vipi?”

“Clean?” Big J akajibu, “Lakini hata hivyo huyu mtu lazima nimfuatilie, sasa hivi hatutakiwi kupuuzia vitu vidogovidogo kama hivi,” akamwambia.

“Sasa hiki kitambulisho kitabaki hapa, hatukirudishi, lazima tujue lolote alilonalo moyoni,” Mc Tee akasisitiza na kukitia kile kitambulisho katika mfuko wake wa shati.

* * *

“Kwa hiyo huyu jamaa ana pesa chafu!” Amata akamwambia yule nahodha.

“Aaa bwana we, wenzetu walitangulia kuiona dunia, pesa zinatengenezwa kwao, watashindwaje kumiliki vitu kama hivi? Sisi tunafurahi kwa sababu katuletea fursa ya biashara kama hivi,” yule nahodha alieleza. Wakaendelea kukizunguka kile kisiwa akiangalia kwa makini maeneo anayoyahitaji kwa kazi yake.

“Punguza mwendo…” Amata akamwambia yule kijana.

“Kaka hapo haturuhusiwi kupita polepole,”

“Kwa nini?”

“Hilo ndo jumba la tajiri wetu kaka, linalindwa kwa nguvu zote,” akajibu.

“Ok, pita mpaka kule upande wa pili,” akamwamuru. Yule kijana akaongoza kile chombo karibu kabisa na soko dogo la samaki.

“Ok, mi nashuka hapa,” Amata akamuaga yule kijana na kuteremka.

Mara kile chombo kilipopotea, akavuta hatua mpaka kwa mama ntilie na kuagiza ugali kwa samaki.

“Bila kusahau maharage!” akamwambia yule mwanadada anayehudumia. Akaendelea kula taratibu huku akisikiliza mazungumzo ya watu walio karibu yake labda ataambulia mawili matatu lakini hayakumhusu.

Usiku wa leo lazima nilivamie lile jumba! Akajisemea. Mipango ilipangwa kichwani wakati ugali ukiishia tumboni. Akiwa kazama katika mawazo, saa yake iktikisika tena. Akainua mkono kuitazama, taa ndogo ya buluu ilikuwa ikiwakawaka. Akatabasamu na kutikisa kichwa juu-chini. Akabofya kinobu cha pembeni na kuruhusu ujumbe huo ufanyiwe kazi. TSA 1 alijua tayari, anaowahisi wameshaingia kwenye mtego wake. Sasa akaweka hesabu yake; moja jumlisha moja mbili na si kumi na moja tena. Kwa kuwaka taa ile kwenye saa yake, alijua wazi kuwa chumba chake kimepekuliwa na kitambulisho chake kimeibwa. Sasa kwa kuruhusu ujumbe ule maana yake ni kwamba ameruhusu vifaa vya TSA viweze kunasa mawasiliano ya moja kwa moja kutoka katika kitambulisho hiko.

Lazima wamwage mtama wote! Akawaza na kusimama tayari kwa kuondoka. Akamaliza kula na kulipa, akaweka kamera yake vizuri na kutoka kwenye mgahawa huo. Akiwa kasimama kando ya barabara, kabla hajavuka, yule mhudumu akaja mbio kumrudishia chenji yake. Akamtazama kwa sekunde kadhaa.

“Asante kwa ukarimu wako, hiyo ya kwako utaendea saluni kutengeneza nywele,” akamwambia. Yule mwanadada akatabasamu na mibonyo yake ikaonekana wazi pasi na kujificha. Hakuwa mzuri wa sura, ila aliumbwa na umbo zuri, tepetevu, akitembea lazima macho yako yatue upande wake wa nyuma, mitikisiko itakusisimua mwili.

“Unaitwa nani?”

“Sikudhani Hamisi,”

“Sawa sikudhani, asante kwa chakula,” akamshukuru na kumuaga.

Amata akavuka barabara na kuzunguka kuifuata hoteli aliyofikia. Alipofika moja kwa moja akalifuata dawati la mapokeazi na kuchukua fungo zake. Akakwea ngazi mpaka chumbani mwake na kujitupa kitini. Akatulia kwa ukimya kama dakika tatu hivi, kisha akachukua kalamu na kile kijidaftari chake na kuanza kuandika.

Kutoka kule chumba cha usalama walikuwa wakimwangalia kila anachofanya. Mtu maalum aliwekwa kumfuatilia kila nyendo yake, kuanzia ndani mpaka nje. Tayari alikwishaweka orodha ya watu aliokutana nao ama kwa mazungumzo au kwa lolote lile. Kazi ilifanyika kikamilifu.

Akiwa bado pale kitini anaandika anavyovijua yeye, simu yake ikapata uhai. Akaiangalia namba ile hakuijua. Akainyakuwa na kuiweka sikioni.

“Hello!” akaita.

“Weweeee jamani chakula kinapoa…” Amata kwa haraka akaitambua sauti ile.

“Hukunielekeza hata nije wapi!” Amata akamwambia huyo aliyekuwa akiongea simuni.

“Mmmmmh uje Marimbani, ukifika uliza kwa bibi Ashura na ukifika kwa huyo bibi mwambie wewe ni mgeni wa Shakila,” akatoa maelekezo.

Amata akatafakari afanye nini katika hilo, alikwishapanga ratiba ya usiku huo, na pia alitamanai sana kwenda kwa mwanadada huyo, Shakila.

Kazi kwanza, mapenzi baadae! Akajisemea. Akaiweka simu mezani na kuinuka, akakusanya vitu vyote na kuvitia kwenye begi lake kiahs akajitupa kitandani na kulala kiuongouongo. Simu yake ikaita, akausogeza mkono mpaka kinywani na kuanza kuzungumza taratibu.

“Nimewekewa kamera mpaka chooni,” akamwambia mtu wa pili.

“Ina maana wanajua kama upo hapo?”

“Hapana, bali kila chumba kina kamera,”

“Kamera mpaka chooni?”

“Ndiyo!” Amata

Ukimya wa sekunde kadhaa ukafuata katia ya Amata na mtu wa upande wa pili.

“kinachoendelea…”

“Usiku huu nina mpango kabambe wa kuhakikisha kama tunayemtafuta ndiye huyu au la,”

“Black Bag?”

“Yes!”

“Ok nitakulinda kuanzi saa saba usiku…”

“Sawa!”

* * *

Chiba akaitua simu mezani, akamtazama Madam S pale alipoketi.

“Vipi?” Madam akauliza.

“Hiyo hoteli ina kamera mpaka chooni…” Chiba akasema.

“Ina maana usiri wa wageni upon je kabisa?”

“Kabisa!”

Chiba na Madam S walikuwa Shamba katika chumba maalumu cha mawasiliano ambacho kwacho waliweza kuyanasa mazungumzo ya Mc Tee na Big J walipokuwa wakijadiliana kuhusu mkakati wao. Yote haya yalisafirishwa kupitia kile kitambulisho cha Amata kilichochukuliwa chumbani mwake. Wakati mazungumzo hayo yakiendelea, Chiba alikuwa kaunganisha kompyuta yake kubwa na kifaa kinachoweza kuoanisha mawimbi ya sauti. Hapa alikuwa akioanisha sauti tatu tofauti. Aliiunganisha sauti hiyo aliyokuwa akiisikia kwenye mitambo yake, pamoja na ile aliyoichukua miezi kadhaa nyuma pale RTD na zile simu zilizokuwa zikipigwa kule Kinondoni nyumba namba 73A.

“Ndiyo yeye!” Chiba akasema. Madam S akatabasamu, akauona ushindi waziwazi.

“Sasa kazi imebaki kwa Amata, anatakiwa amalize mchezo huu haraka …” Madam akasema.

“No, hiyo ni kazi ya mwisho, kwanza tunatakiwa kuzuia mpango mzima wa mapinduzi ambao umepangwa kisha ndo tuwamalize hao watu wawili. Tumwache Amata afanye kazi yake usiku wa leo, kisha kesho tutaona pamoja tunafanya nini,” Chiba akamwambia Madam naye akakubali.

“Inabidi tuwe tayari, tuandae kila kinachowezekana kwa ajili ya kuzuia hayo mapinduzi. Unajua hiyo ni vita ee? Umesikia hapo wanazungumzia mzigo unawasili, mzigo gani? Kuanzia sasa inabidi doria zianze kwenye bahari ya Hindi ili kuona kama kuna chochote kinapitishwa kwa siri,” Madam kakasema.

“Haswa!”

* * *

Kamanda Amata aiwa palepale kitandani, bado alikuwa akipanga mipango yake kwa siri kubwa hukku akihakikisha kuwa wajnaomtazama hawajui lolote. Alipanga mipango yake na Chiba na Madam S kwa muda huo, akiwahakikishia kuwa windo lao lipo eneo hilo kwa uhakika wa asilimia sitini. Huko Shamba, Chiba na Madam S nao waliikuwa wakijipanga kuona cha kufanya.

“Amata anahitaji msaada ili kuamilisha uchunguzi,” Chiba akamwambia Madam S.

“Chochote anachohitaji apatiwe hata kama kipo nje ya uwezo wetu, atapata,”

“Sawa!”

“Msikilize… na katika hili naomba kila mmoja awe tayari, nimesomeka?”

“Umesomeka,” Chiba akajibu na kuendelea kuzungumza na Amata katika mtindo uleule.

Katika chumba cha mawasiliano, simu iliita. Yule kijana aliyekuwa akikifuatilia chumba cha Amata, akanyakua ile simu na kuiweka sikioni.

“Unaendelea kumfuatilia?” akaulizwa.

“Ndiyo,”

“Unamuonaje?”

“Naona hana madhara, limelala tu kama toto taahira,”

“Achana naye!” sauti ya upande wa pili ikamwambia. Akaiacha simu na kuendelea na kazi nyingine. Hakutilia tena maanani kile chumba maadam tu kaambiwa ‘achana naye’.

Katika chumba kile, Kamanda Amata alikuwa kalala kimya, lakini ulalaji wake haukuwa wa bure, alikuwa akiendelea kuwasiliana na Chiba ambaye kwa wakati huo alikuwa Shamba kwenye chumba cha mawasiliano. Kwa msaada wa kile kitambulisho cha Amata ambacho kilikuwa nyumbani kwa McTee, Chiba aliweza kunasa mazungumzo yote ya watu hao wawili. Mipango, mikakati na kila kitu. Huku akioanisha zile sauti katika mashine maalumu aling’amua kuwa anayezungumza ni Kibwana Mtokambali ambaye sasa amejivika u-McTee.

“Kwa upande wa sauti, asilimia themanini na tano, huyo ni Kibwana,” Chiba akamwambia Amata.

“Sawa! Vipi unaweza kukata mawasiliano ya simu na CCTV? Nataka kufanya blackbag usiku huu, kuanzia saa saba mpaka saa tisa,” Amata akamuuliza Chiba.

“Upande wa simu inawezekana, sijajua kama CCTV zao zinatumia mfumo gani…”

“Unamaanisha nini?”

“Yaani zinatumia waya kusafirisha mawimbi ya sauti au WiFi!”

“Ni za kisasa sana zinatumia WiFi kote,”

“Basi wameumia… saa saba kamili nitakata mawasiliano yote. Wao watahangaika kurudisha hawatafanikiwa, nitarejesha saa tisa kasoro dakika tano. Hakikisha uwe umerudi!”

“Sawa,”

Amata akakata simu aliyokuwa akitumia kuwasiliana na Chiba, akaendelea kupiga usingizi wa uongo. Alijua wazi kuwa hapaswi kuamka mapema, lazima asubiri mpaka ahadi yake na Chiba itimie.

“Amata una dakika sitini tu za kuifanya kazi! Unaenda kutafuta nini?” akajiambia na kujiuliza mwenyewe.

“Naenda kutembea!!” akajijibu.

Saa 7:05 Usiku

Katika chumba cha usalama cha hoteli ile, luninga zote zilikuwa giza ghafla. Yule bwana alihangaika hapa na pale hakupata suluhisho.\

Nini imetokea? Akajiuliza. Akachukua simu yake kuwasiliana na mafundi wa hoteli hiyo. Simu haipatikani. Mkanganyiko.

Kilomita moja kutoka kwenye ile hoteli na lile jumba la kifahali ambalo kwalo waliamini kuwa Mc Tee au Mtokambali alikuwa akiishi, Chiba alikuwa amewasili kwa boti iendayo kasi. Boti ya jeshi la wananchi iliyokuwa ikiongozwa na Scoba. Nmdani ya boti hiyo, alikuwami, Chiba mwenyewe, Scoba kama nahodha, Gina kuimarisha ulinzi. Kifuani mwake, mwanamke huyo alining’iniza bunduki kubwa kifuani mwake.

Chiba alirusha hewani kifaa kama drone. Lakini ndani yake alikuwa ameunganisha mfumo maalumu unaojulikana kama IoT ambao aliuchezea kidogo na kuingiliana mawasiliano ya camera hizo, akafungua nywila zake na kuweka mpya kisha akazima kabisa huku akiwa ameandika pembeni nywila za mwanzo. Alipohakikisha ilo lipo sawa, akaingilia pia mfumo wa simu za hewani, akazuia mtandao eneo hilo kwa kilomita tano za mraba.

Yeye, mara tu alipotakiwa na Amata kufanya hivyo, akamwita Scoba na Gina akawaeleza kazi ya kufanya usiku huo. Hawakusita. Scoba TSA 4 alijua anachopaswa kutenda, alikwenda kuchukua boti kule wanakoziweka. Boti ya mwendo kasi ambayo inaweza kukifikia kisiwa cha Mafia kutoka Dar’ kwa saa moja au moja na nusu. Wakapakia kila kitu na safari ikaanza. Walisafiri usiku kwa usiku na hatimaye walikifikia kisiwa hicho. Ile boti, ilikuwa maalumu sana, walipoona sasa umbali unatosha kufanya kazi yao, Scoba akaizima injini. Kutoka kwenye batani nyingine, ikajifunika juu na wao wakawa ndani kisha ikaenda chini ya maji kwa mita mbili na kutuli hapo bila kutikiswa.

“Tutakaa hapa chini ya maji kwa saa zote mbili?” Gina aliuliza.

“Unaogopa?” Scoba akajibu wakati Chiba akiwa bize, ametingwa na kompyuta yake ndogo.

“Mh!” akaguna na kutulia kitini. Dakika chache baadae, Chiba akafanikiwa kukirusha angani kile kidubwasha chake ambacho kilikwenda juu mita mia tano na kukata mawasiliano eneo lile.

* * *




Mh!” akaguna na kutulia kitini. Dakika chache baadae, Chiba akafanikiwa kukirusha angani kile kidubwasha chake ambacho kilikwenda juu mita mia tano na kukata mawasiliano eneo lile.

* * *

Kamanda Amata aliitazama saa yake, ilikuwa imetimu saa saba nadakika kumi usiku, akaitazama simu yake, ‘Network Searching’. Akajua kumekucha. Akakiacha kitanda na kuchukua mavazi yake meusi ya mpira, akavaa. Akafunika kuanzia kichwa mpaka miguu. Kisha akavaa viatu vilivyomuwezesha kutembea pasi na kusikika. Miwani yake ya kumuwezesha kuona kwenye giza akaining’iniza shingoni ili muda wowote ikitakiwa basi angeivaa. Nguo ile haikuhitaji gloves kwani ilitengenezwa tayari. Alipohakikisha yuko sawa, akachagua zana chache ambazo zingemfaa. Bastola moja yenye risasi za moto, nyingine ilikuwa na vijishale vyenye dawa mbaya kabisa ya usingizi, ambayo ingekulaza kwa saa tatu. Kifaa chake cha gesi ya hewa safi, akakibana kiunoni, viwili kwa idadi yake. Kurunzi ndogo, kisu, funguo, kifaa cha kielektroniki ambacho kinaweza kusoma nywila yoyote ya mlango wenye kitasa kama hicho. Vitu vyote akavipachika kwenye hiyo nguo yake ambayo mifuko yake ilibana vizuri. Hata kama angeingia kwenye maji basi hakuna ambacho kingelowa.

Kamanda Amata hakutokea mlangoni kwani upande huo usingekuwa salama kwake. Akafungua kioo cha dirisha taratibu na kutoka kupitia njia hiyo. Akashukia kwenye bakoni ya ghorofa ya chini yake. Akafanya vivyo hivyo mpaka alipofika chini. Akaambaaambaa na ukuta wa hoteli hiyo mpaka karibu upande wa mbele. Akaacha kuelekea huko na kufuata barabara inayoelekea kule Scuba Diving. Akafika eneo hilo, akaangaza macho hakuona mlinzi.

Ina maana eneo hili halilindwi? Akajiuliza. Badala ya kujibiwa akasikia michakacho ya kiumbe cha miguu minne. Akajua kumekucha. Mkono wake ukaiendea bastola ile yenye vijishale vya sumu. Alipogeuka hakukosea. Jibwa moja kubwa lenye mashavu yanayoning’inia. Akaliwahi kwa kishale kimoja tu kabla halijamuharibia usiku wake. Haikulichukua hata dakika moja likajilaza taratibu. Bila kufanya kelele ya maji akajitoma baharini na kuanza kuogelea. Katika swala zima la kuogelea, Amaa halikumpa shida. Alishajua wapi pa kupita ili alifikie jumba lile. Ndo faida ya utalii wake. Alioegelea mpaka akafika katika kisiwa kingine kidogo ambacho jumba lile la kifahari lilijengwa juu yake.

Akapita juu ya mchanga laini mpaka kwenye ngazi ndefu ya kupanda juu kidogo ambako angepambana na milango kadhaa kuingia ndani. Akasimama kimya kusikiliza chochote ambacho kingemfurahisha. Hakikuwapo Zaidi ya mawimbi ya maji. Akakwea ile ngazi na kulifikia lile jumba.

Naam! Lilikuwa jumba kubwa au tuliite ngome. Washenzi walinunua kisiwa? Akajiuliza.

Kwanza akalizunguka jumba lote na kuhakikisha anaua upinzani wote uliowekwa nje yake. Akashangaa hakukutana na mlinzi hata mmoja.

Haiwezekani! Akashangaa, lakini ndivyo ilivyokuwa. Akarudi mpaka kwenye mlango wa kuingia ndani ya wigo wa jumba hilo. Haukumpa shida kufungua, akajitoma ndani. Akasimama kimya kusikiliza chochote. Masikio yake yalikuwa na nguvu ya kusikia kitu kidogo ambacho wewe usingeweza kusikia. Au kusikia kitu tofauti na cha hatari katikati ya kelele nyingi. Alifundishwa kuchambua kelele na kusikiliza. Watu kama hawa ili upate kazi kama hii ilibidi uwe na sense ya ajabu, mlango wa fahamu wa sita. Inatakiwa uwe mwepesi kujua, kuelewa, kujifunza, kung’amua mambo mbalimbali yanayokuzunguka kila siku. Ujue uongea na moyo, na akili na kuwasiliana na viungo vyako vyote vya mwili. Dakika moja ilimtosha, akavuta hatua ndefundefu mpaka alipoufikia mlango wa kuingia ndani. Hapo akasikia kile hasichotarajia, miguu ya mtua anayekuja upande wake. Akajibana vyema kwenye kiambaza cha jumba hilo. Kweli, mtu mmoja akatokea upande wa nyuma, alipofika hapo akasimama. Mtu yule alivaa mavazi ya kiaskari, meusi. Na yeye alikuwa mweusi ti. Akasogea taratibu mpaka pale asimwone Amata.

TSA 1 alikuwa kajificha kwa mtindo wa ajabu sana aliyowahi kujifunza huko Japan. Aina na mitindo ya kujificha gizani ukiwa chini ya miti, kwenye mawe nk. Kwa kumshtukiza, akamrukia na kutu mgongoni mwake. Akajiangusha na kuviringika naye kiasi kwamba mtu wa mita kumi na tano hasingesikia kishindo kile. Alipotua katika mwili wa yule jamaa, kiganja chake cha kulia kikawahi kumziba mdomo, magoti yake yakampiga yule jamaa kwa nyuma ya miguu yake, wakaenda chini pamoja.

Akamwonesha ishara ya kunyamaza kwa kuweka kidole kimoja kati a midomo yake. Yule jamaa akiwa chali na bunduki kando, alibaki katoa macho, hana la kufanya. Amata akachomoa bastola yake kwa mkono uleule na kumuelekezea jamaa huyo.

“Mlango wa kungia ndani upo wapi?” akamuuliza kwa sauti ndogo. Yule jamaa akamwonesha kwa kugeuza kichwa. Amata hakuangalia kwani aliijua vyema mbinu hiyo. Ukigeuza kichwa kuangalia, umewahiwa.

“Mko wangapi?” akamuuliza.

“Wanne!” akajibiwa. Akafyatu ile bastola na kijishale kikachoma kwenye nyama ya mkono. Dakika tu, usingizi. Akamnyanyua kwa ufundi kabisa na kumuweka mahala.

Wapo wanne? Nne mara mbili ni nane. Au nne toa nne, sifuri! Akajiwazia na kupiga hesabu zake vizuri. Akatazama saa yake, saa saba na dakika thelathini na saba. Muda unayoyoma. Akazunguka lile jumba taratibu akitarajia mawili, ama kukutana na walinzi nane au hasikute kabisa. Akajikuta anafika palepale alipotokea. Hakukutana na mtu.

Haiwezekani! Akawaza. Hakuamini kutokana na unyeti na usiri wa watu waliokuwa humo ndani kukaa bila wainzi wa kutosha. Lakini pia alifikiri kwamba inawezekana kuwa kuwapo na walinzi wengi ni sehemu ya kuvujisha mipango ya kile mnachokusudia. Akatikisa kichwa juu chini kukubaliana na alichofikiri mara ya pili. Akauendea mlango ambao kwao yule jamaa aligeuzia kichwa. Akaupapasa anavyojua yeye, kitasa cha mwingereza kikafyatuka. Hakuingia mzima mzima, ila nusunusu.

Don’t put your best foot forward! Sauti ikamjia kichwani akaitii. Akatulia kama dakika nyingine akisikiliza ndani humo nini kitatukia. Kimya!

Kama kuna mlinzi basi anajua anachopaswa kufanya. Acha papara, subiri umuone adui kikamilifu ili ujue wapi pa kumdhoofisha! Akakumbuka mafunzo, akatabasamu, akajiandaa kuingia ndani na kwa mapambano ya aina yoyote ile. Akaingia nusu, na kumalizikia sekunde tatu baadae. Amata akajikuta kwenye korido ndefu iliyokuwa na milango upande mmoja. Akanyata kuufuata mlango wa kwanza, akautomasatomasa ukafunguka. Ndani yake kulikuwa na madumu mengi ya mafuta, harufu yake hafifu ambayo wewe na mimi tusingeing’amua, ilimjuza kuwa ni Petroli.

Mafuta ya boti! Akawaza. Akaurudishia mlango huo na kuufuata wa pili, ulikuwa wazi. Maboksi kadhaa yalipangwa. Akaingia na kuchukua boksi moja, akalifungua. Vitabu vya baiolojia, histori na vingine vingi.

Tunasaidia wanafunzi mashuleni! Sauti ikamjia kwa ndani ya moyo wake akajikuta anashtuka. Akatoka kwa utaratibu uleule, akauendea mlango wa tatu, akanyonga kitasa, kikafunguka. Chumba kitupu lakini kilichomshangaza kilikuwa kimejaa maji. Chumba kikubwa cha kutosha Land Cruiser V9. Ukiachana na kingo zake ambazo ungeweza kutembea juu yake na kuzungukwa na bomba safi za alluminium, kulikuwa na ngazi kama zile za kupandia kutoka kwenye bwawa la kuogelea. Zaidi ya hilo hakukuwa na kitu kingine.

Swimming pool? Akajiuliza. Akiwa hapo anashangaa akasikia sauti za watu wakiongea na kuja uapnde wake. Kumekucha.

“Tazameni chumba cha mawasiliano nini kimetokea mtatue mara moja,” sauti yenye mamlaka ikasema.

“Sawa!” nyingine zikaitikia. Amata akarudisha mlango na kubakisha uwazi kidogo. Akawaona wale jamaa wakipita kuelekea nje. Akatulia palepale. Mara sauti ya mtu anayepiga mlunzi ikamfikia masikioni. Mtu huyo alikuwa akija katika uelekeo uleule. Amata haraka, akaingia kwenye yale maji bila kufanya kelele. Akatulia kimya akiwa kajiweka katka staili ambayo huwezi kumtambua haraka ila yeye anakuona vyema. Yule mtu hakuingia, alishika mlango na kuufunga vizuri.

Shiit! Amata akang’aka na kujitoa taratibu kwenye kile kidimbwi. Siyo swimming pool, hapa nafikiri wanaegesha boti zao kutoka na kuingia kwa siri kwenye hili jumba! Akawaza. Akauendea ule mlango na kujaribu kucheza nao, ukafunguka baada ya takribani dakika tano hivi. Akatoka taratibu na kuendelea na ziara yake. Mlango uliofuata, alipoufungua, akakaribishwa na stoo kubwa sana yenye makorokoro mengi. Akafikicha macho kutazama vizuri anachokiona kama ndicho au la. Ilikuwa stoo yenye vitu vingi, muundo wake na vilivyomo vilifanana kabisa na ile ya kule msitu wa Kumisnaya ambako alifungwa.

Walewale! Akatikisa kichwa. Akaendelea kuhakikisha kile anachokidhania. Akatazama saa yake, saa nane kasoro kumi. Akaingia kwenye kile chumba na kuufunga mlango.

Kama ramani ni ileile, basi pale kwenye kona panapeleka ninapotaka! Akawaza. Na kweli, alipoifikia ile kona akakutana na mlango. Huu ulikuwa na kitasa cha kielektroniki. Akachukua kile kifaa chake, akakiwasha. Kilikuwa kama simu. Kamera ya kifaa hicho ikawaka, akaskani ile padi iliyokuwa na dijiti tisa na herufi chache. Kifaa kile kiliweza kuona batani zinazoguswa mara nyingi, hivyo kikamwonesha batani hizo kwa mpangilio wake. Akabonya haraka na kile kitasa kikakubali. Akaingia na kufunga ule mlango. Hapo akakutana an ngazi inayokwenda juu, akaikwea kwa tahadhari, hku bastola yake ya vile vishale ikiwa mkononi. Alipofika juu akajikuta kwenye sebule kubwa, nzuri ya kisasa sana. Iliyosheheni samani za thamani na fahari. Akaipekuwa kwa macho kwanza. Kisha akaliendea kabati kubwa lililojaa vitabu. Akatazama na kupekua hapa na pale, hakuna cha maana.

Akaliacha na kufuata ngazi nyingine inayopanda juu. Huko akajikuta kwenye uwanda mwingine. Kulikuwa na milango saba ya kisasa sana. Kitu pekee kilichomshangaza ni kutokukutana na upinzani ambao aliutegemea. Na hilo hakulitegemea. Lakini hisia yake ya pili ilimpa jibu la kwanini hiyo.

Amata, kwa mtindo uleule, akafungua wa kielektroniki akafungua mlango wa kwanza. Chumba kidogo, chenye sofa za mtu mmoja mmoja, nne. Kompyuta kubwa ‘apple’ ilikuwa mezani, printa, mashine ya nukushi na kabrasha kadhaa zilikuwa hapo. Akaanza kupekua moja baada ya jingine. Miuhtasari ya vikao kadhaa vilivyofanywa na wale mabwana, akasoma haraka haraka. Akachukua simu yake na kuanza kuskani moja baada ya jingine, vile tu alivyoona vina umuhimu. Pembeni kulikuwa na kadi mmweko ndani ya kibeta kidogo, akaichukua na kuipachika kwenye simu yake, bila kuangalia kuna nini, akanakili vyote na kuirudisha. Katika chumba hiki alitumia muda kidogo. Alipojiridhisha, akatazama saa yake. Saa nane na dakika ishirini.

Taratibu sana akatoka kwenye kile chumba na kukiendea kingine, kiko wazi. Akasukuma mlango. Chumba cha kulala. Kitanda kikubwa kilikuwa kimeparanganyika, aliyelala hayupo.

Kaenda wapi? Akajiuliza. Kengele ya hatari ikalia kichwani mwake. Nimezungukwa! Akawaza. Amata alitazama kile chumba kwa makini sana. Akagutushwa na sauti ya kukohoa mtu kutoka maliwato. Yupo! Akawaza na kushusha pumzi. Akatulia. Dakika tu, ule mtu akatoka akiwa kama alivyozaliwa kurudi kitandani. Mwanaume, mnene kiasi, sura na mwili wake kwa kiasi Fulani zilikuwa na tofauti ya rangi. Akamtambua mara moja, Mc Tee au Kibwana Mtokambali.

Nilikuwa namsikia kwenye redio tu nilipokuwa shuleni! Akawaza na kumsubiri apande kitandani. Ikawa hivyo. Kwa kutumia bastola yake, akafyatua kile kijishale, kikampata shingoni. Akajikuna kidogo na usingizi ulipokuwa ukimpata Amata aliingia ndani ya kile chumba.

“Kifo chako kimekaribia,” akamwambia. Mtokambali alimwona Amata katika taswira iliyovurugia, hakuelewa kama ni shetani au mzimu.

“Kkkkiiifffooo ccchhhakkkooo kkkiiiimmmeeekkkaaarrriiibbbiiiaaaa!” Mtokambali akajaribu kurudia yale mananeno kwa shida, akabebwa na usingizi. Amata akamtazama mheshimiwa rais mtarajiwa, akasikitika.

Rais hana mlinzi! Akajisemea. Akakizunguka kile chumba na kuustaajabia umaridadi wake. Kitanda kikubwa chenye shepu ya mtumbwi kilikuwa humo. Luninga kubwa ilikuwa juu ya meza safi ya kioo. Akaliendea kabati na kulifungua, suti za bei mbaya zilikuwa zimening’inizwa. Akapekua hapa na pale, vitu vya kawaida. Akaiendea droo ya kitanda na kuivuta, loh, maburungutu ya pesa yalikuwa yamelala kwa utulivu. Akatazama saa yake, muda unakimbia, saa nane na dakika ishirini na tano. Akatoka haraka, akatazama vyumba vingine na kujiuliza kama aende au la. Akagombana na nafsi yake.

Kimoja tu kisha naondoka! Akawaza na kuanza kuvuta hatua, akapita chumba cha kwanza bila kukigusa, akaifuata cha pili, alipotaka kukifngua, akasita. Akakiacha. Mwisho kulikuwa na mlango mwingine, akaufungua, ukafunguka. Akakutana na ngazi fupi inayopanda juu kidogo. Akaifuata na kukutana na mlango mwingine. Akacheza nao kwa sekunde chache ukafunguka. Akaingia. Amata alijikuta kwenye chumba chenye viti vichache, huku na huko kulikuwa na milango miwili. Akaufuata wa kwanza, akausukuma, upo wazi. Akaingia, jikoni. Akatoka na kuufuata mwingine, akausukuma, chumba cha kulala. Juu ya kitanda kidogo kulilala mwanadamu ambaye shuka lilikuwa limesukwasukwa kando. Alipotaka kuvuta hatua, yule mtu akashtuka.

“Maaaaammm!!!!” hakumaliza kupiga kelele za woga, kijishale kikamchoma shingoni. Sekunde kadhaa akalala kimya.

“Uhhhhh” Amata akashusha pumzi. Akaibana bastola yake. Akamwendea yule mtu akamgeuza pale kitandani.

Egra! Hakuamini. Amata alimtazama mwanamke huyo ambaye sasa umri nao ulianza kumtwaa. Bibi harusi ambaye hakufaidi fungate la mumewe. Akajikuta machozi yanamtoka. Akatamani kuondoka naye lakini alipotazama muda haukumruhusu. Akaliendea dirisha kutazama, loh, kulikuwa na korongo kubwa lililoishi baharini. Akamtazama, akashindwa afanyeje. Akaamua kutoka. Ziara yake akaihitimisha na kuanza kutoka nje ya jengo lile. Akarudi mpaka kule sebuleni na kutoka kwenye ile ngazi akaibukia stoo. Alipotoka tu katika mlango was too akakumbana na mtu mwenye tambo kubwa, mrefu anayeonekana kuwa na nguvu nyingi. Yule mtu hakuuliza wala kushangaa. Alijirusha na miguu yake ikatua kifuani mwa Amata. Hakujipanga. Akayumba na kurudi nyuma. Akajibamiza kwenye mlango mwingine, ukafunguka. Akaangukia ndani.

“Mshenzi sana wewe, leo utajutia uamuzi wako…” yule bwana akasema. Kwa kukimbia akamfuata Amata pale alipoangukia. Kamanda akawahi kuinuka lakini hakukaa sawa, akatandikwa Makonde matatu ya nguvu akajikuta anakosa uzainia wa kusimama. Maumivu makali yalimbana sehemu za mbavu.

James Msambamagoja ana tambo kubwa nan i mpiganaji mzuri sana! Sauti ta Madam S ilimjia.

Ni huyu, hata sura yake ya bandia ndiyo inamtambulisha kama Big J! akajiwazi wakati akijivuta kuinuka. Big J akamfuata Amata na kumkamata, akamuinua.




Ni huyu, hata sura yake ya bandia ndiyo inamtambulisha kama Big J! akajiwazi wakati akijivuta kuinuka. Big J akamfuata Amata na kumkamata, akamuinua.

“Nani kakutuma?” akamuuliza.

“Mama yako!” Amata akajibu ili kumuuzi. Big J hakumtambua Amata kutokana na vazi lake lilivyomficha uso.

Muda unakwenda! Akawaza. Akajaribu kujitutumua, lakini kono la Big J lilimbana sawasawa. Konde lingine likamtua mbavuni, akalegea. Big J akamwachia na kumsukuma chini. Amata akajigeuza kiufundi, na kumpa ngwala mpja ya nyumanyuma, Big J akaenda chini mzima mzima. Amata akataka kumruka, akadakwa mguu na kuanguka vibaya sakafuni. Big J akajigeuza kisarakasi, akasimama wima. Alikuwa na mwili mkubwa lakini mwepesi kama unyoya. Amata alimwona jamaa huyo akimjia kasi, akachomoa bastola yake, akafyatua. Risasi moja ikapenya kwenye bega la jamaa huyo na kulifumua vibaya. Akajilaumu, hakutaka kutumia risasi ya moto lakini akajikuta keshaichomoa Berreta Pico.

Big J akajibwaga chini kama mzigo. Naye akachomoa bastola na kumlenga Amata ambaye alikuwa katika kasi ya kutoka nje.

Mlio ule wa risasi, ukawashtua vijana wawili waliouwa nje, wakaamua kukimbilia ndani kuona kulikoni. Wa kwanza alipofungua mlango tu, Amata alikuwa amefika. Akaruka hewani na kuashia teke kali. Risasi za Big J zikakichana vibaya kifua cha yule jamaa. Amata akatua nje na kukutana na yule mwingine ambaye tayari alishapiga hatua mbilia tatu nyuma kujiandaa kwa mapigano. Kamanda Amata hakuwa na muda, alienda hewani na kumpelekea mapigo kama sita ya karate jamaa akaanguka chini. Akachomoa bastola yake ya vishale na kufyatua kimoja kikamchoma shingoni.

Kamanda Amata akawahi kutoka nje na kujitupa majini. Akapiga mbizi na kuondoka eneo lile huku risasi kadhaa zikimiminika upande huo.

* * *

Katika chumba cha usalama ambacho mitambo ya kuongoza kamera zote ilikuwa hapo, kazi ilikuwa ikiendelea kutafuta tatizo lililotokea liko wapi. Vijana watatu waliokuwa ndani ya chumba hicho walikuwa wametingwa kucheza na kompyuta zao na kujaribu hili na lile. Jasho likawamwagika. Hawakujua kabisa kama huko nje hali ya hewa haiku shwari.

“Yeeeeessss!” mmoja akashangilia baada yujikuta ameweza kugundua shida ilikuwa ni nini.

“Vipi?” mwenzake akamuuliza.

“Kazi imeisha,” akamjibu huku tayari luninga kubwa ikiwa imeanza kuonesha picha za mazingira ya eneo hilo, kuanzi kwenye lile jumba mpaka hotelini.

“Umegundua nini?”

“Nimecheza na hizi kodi tu hapa zikawaka,” akajibu.

* * *

Kule hotelini, katika chumba cha usalama nako kamera zote zikawaka. Na muda huohuo simu ikaingia, yule bwana aliyekuwa zamu akainyakua na kuisikiliza.

“Angalia chumba namba 406, huyo mgeni yupo?” sauti ya Big J iliyokuwa ikiongea kwa shida kidogo ilisikika. Yule jamaa akawasha kamera hiyo na kutazama chumba cha Amata.

“Yupo, amelala bado kama mtoto taahira,” akajibu. Ile simu ikakatwa.

Kutoka kule kisiwani kwenye lile jumba, Big J alipata maswali mengi yasiyo na majibu, akilini mwake alijua kabisa atakuwa ni yuleyule mgeni ambaye tangu mchana alionekana kuwa mjanja mjanja. Lakini kwa jibu alipewa kuwa huyo bwana yupo chumbani kwake kalala, akajiuliza ni nani sasa aliyewavamia usiku huo na alikuwa anataka nini! Utata. Ilikuwa ngumu kuamini kwake.

* * *

Chiba akakishusha kifaaa chake kutoka angani alipokituma, huku Scoba akiirudisha ile boti juu. Akakipokea na kukiihifadhi. Gina alikuwa kimya kabisa haongei lolote.

“Kazi imekamilika, kama kachelewa kujiokoa, sahauri lake!” Chiba akasema. Gina akamkata jicho la kushangaa.

“Unafurahia?” akauliza.

“Sivyo, ila tunafanya kazi kwa muda,” akajibu wakati Scoba ameshakifunga chombo chake na kukizamisha tena kisha kuondoka taratibu. Meseji kwenye simu ya Chiba ikaingia.

Kazi imefanyika kwa ufanisi. Ila nahisi mbavu yangu imevunjika!

Ulikuwa ujumbe kutoka kwa Amata. Chiba akasikitika na kuendelea na safari kimya. Hakuwaambia wenzake nini kimetokea katika ujumbe huo.

Kamanda Amata aliamka majira ya saa mbili asubuhi, akaingia bafuni kuoga na kurudi kujiandaa kutoka. Maumivu makali sana, yalikuwa katika ubavu wake. Lakini kwa kuwa alikuwa akijua kuwa anatazamwa na amefanikiwa kuwalaghai hakujionesha kama alikuwa na maumivu hayo. Alivaa taratibu nguo zake za kawaida na kujiandaa kutoka nje. Simu yake ikaita kwa fujo, namba tupu, akainyakuwa na kuisikiliza.

“Mbona jana hukuja…” sauti ya kike ikamwambia Amata. Haraka akaitambua.

“Nilijikuta naumwa ghafla, sijui mumeo ana wivu sana,” akamjibu huku akiteremka ngazi. Kamera yake kubwa kifuani na kijidaftari chake mkononi. Alipofika mapokezi akakutana na yule binti.

“Sasa we hujanielekeza, mi ngekujaje?” akamuuliza.

“Jamani! Leo tutaondoka wote basi,” binti akazungumza. Amata hakuwa na kinyongo kwa mabinti, akamkubalia na kutoka zake nje ya hoteli hiyo. Joto kali lilitaradadi, akazishuka ngazi na kuyaacha maegesho. Akavuka barabara na kuchukua taksi.

“Nipeleke uwanja wa ndege,” akamwambia yule dereva. Naye bila hiyana akatia moto gari lake na kuondoka eneo hilo.

Uwanja wa ndege mdogo wa Mafia ulioweza kupokea ndege ndogondogo ulikuwa katika

eneo la Nyamisati. Uwanja ulitumika sana kwa shughuli za kitalii Zaidi au za kiserikali. Abiria wenyeji walikuwa wachache sana wanaoutumia. Zaidi walikuwa wakitumia njia ya maji kusafiri wanakotaka. Kamanda Amata aliwasilia uwanjani hapo dakika tano kabla ya ndege ya shiriki la Auric Air kuwasilia. Mara baada ya kumlipa yule dereva naye kuondoka zake, akaingia katika jengo dogo lenye viti vichache. Akaketi.

Dakika kumi baadae ile ndege ilikuwa tayari uwanjani hapo ikishusha abiria. Amata si kwamba alikuwa akisafiri bali alikuja kumpokea mgeni wake kutoka Dar es salaam. Jasmine akiwa na kavaa kofia pana kichwani mwake, blauzi nyeupe na nusu suari pana aliteremka ndegeni akiwa kafuatana na mtu mwingine mnene, mtu mzima mwenye uhaba wa mvi kichwani mwake. Walikuwa wakiongea na kucheka mpaka walipomfikia Amata aliyekuwa kasimama nje ya jengo lile.

“Jaffari, kutana na Dkt. Mwakipesile, mtaalamu wa mifupa kutoka MOI,” Jasmin akamtambullisha, “huyu ni Jaffari, rafiki yangu, yeye ni mwandishi wa habari. Kanikaribisha kidogo leo kuja kufurahi Mafia,” akamalizia utambulisho wake.

“Nashukuru kumfahamu… sawa mimi niwaache, nimuwahi mwenyeji wangu…” yule daktari akasema.

“Umekuja kikazi tu?” Amata akauliza.

“Ee nina hawa jamaa wa Chole Camp Site huwa nawasaidiasaidia kidogo,” akajibu huku akiondoka. Nje ya uwanja huo kuliwasilia Landrover County na kumchukua mzee huyo.

Amata na Jasmini wakaingia ndani ya lile jengo la uwanja huo, wakaomba chumba cha faragha kwa mazungumzo. Wakapewa. Wakiwa chumbani, Amata alilala juu ya kitu kama meza ndefu iliyowekwa kando. Jasmine alifungua mkoba wake na kuchukua vifaa vyake vya kitabibvu na kumsaidi Amata kupunguza maumivu yake.

“Ulipigwa kwa nini?” jasmine aliuliza. “Ngumi, yule jamaa ana mikono kama chuma,”

“Pole!” akampoza.

“Huyu mzee uliyekuja naye inabidi tumweke kwenye uangalizi,”

“Kwa nini?”

“Huko anakoenda ndiko nilikovamia jana. Na kati ya wale washenzi mmoja wao nimepiga risasi ya bega…”

“Kwa hiyo anaenda kumtibia?”

“Bilas haka… Aaaaaaaassss polepole Jasmini, panauma he!” Amata akalalamika maumivu wakati akifanyiwa huduma hiyo. Alipomaliza Jasmine akmchoma sindano ya kutuliza maumivu na kumpa vidonge vya kumeza.

“Asante!” akashukuru na kuvaa tena shati lake. Wakatoka pamoja mpaka eneo la kuketi wasafiri na kuwakuta wachache. Jasmini akaabiri ndege ileile aliyokuja nayo na kurudi Dar akimwacha Amata akiendelea na likizo yake.

* * *


SHAMBA


Madam S, Chiba na Gina walikutana katika meza ya duara kwa mazungumzo asubuhi ya siku hiyo.

“Vipi kazi imefanyika?” akawauliza.

“Pasi na shaka!” Chiba akajibu. “Tumefanikisha upande wetu, tunasubiri Amata anasemaje, nini na nini amefanikiwa kupata. Lakini kwa ujumla imekuwa ya mafanikio,” akaeleza.

“Good! Kazi imefika ukingoni, ngoja tusubiri kaka ‘enu anasemaje. Ila nimesikia amepata kikwazo kidogo ameumia mbavu, nimemtu Jasmini yupo huko na atarudi mchana huu,” akawaambia.

Hata hawakumaliza kuzungumza, jasmine aliwasili katika jengo hilo. Jengo lililojaa siri za serikali, za viongozi, tafutishi za kijasusi na kichunguzi na kipelelezi. Picha za watu anuai waliokufa na kuuawa. Picha na majina ya watu wanaotafutwa ndani na nje ya nchi, yote yalikuwa humo. Isitoshe, ni jengo lililotumiwa na watu sita tu wenye weledi wa hali ya juu katika kuua, kutesa, kuchunguza na kusuka mipango mbalimbali. Hata mkuu wan chi hakujua ni wapi lilipo jumba hilo. Kila aliyetakiwa kufika alifikishwa bila kujua na alitoka bila kuelewa. Hata akisimulia alichokiona asingekwambia ni wapi alipelekwa. Makabrasha laini kwa magumu yalikuwa ndani ya jumba hilo. Nje lilizungukwa na wigo wa matofali uliochakaa, na lenyewe lilikuwa la kizamani, kuta nyeupe zilizogeuka kuwa nyeusi kwa mvua na hali ya hewa ndizo zilificha kila kilichomo humo ndani.

Shamba ni jina waliloipa nyumba hiyo wakiamini kwamba ila kinachopandwa humo ndani lazima kitoe matunda. Kwa jina la kitaaluma kabisa palijulikana kama Safe House, nyumba salama iliyoja usalama.

“Jasmini,” Madam S akaita.

“Yes Mom!”

“Nipe habari,”

“Nimekutana na Amata, nimemganga. Ila hapa kuna habari mpya…”

“Ipi?”

“Dkt. Mwakipesile wa MOI nimesafiri naye anaenda huko. Inaonekana ana mahusiano ya karibu na hawa watu. Amata anasema amempiga risasi James Msambamagoya…” akaeleza.

“What! Amemuua?” Madam S akashtuka.

“Sasa unashtuka nini, kwani si wanatakiwa wauawe,” Chiba akamuuliza.

“Muda wao bado kuna kitu tunakifanyia uchunguzi kikikamilika ndiyo tutatekeleza hukumu yao,” Madam akajibu.

“Na vipi kama wakitoroka usiku wa leo?” akamtupia swali.

“Labda kama wanaenda sayari nyingine…” Madam akajibu. Dakika hiyohiyo simu ikaita. Akaichukua na kuiweka sikioni.

“TSA 1 nakupata,” Madam D akaita.

“HOT, mpango wa kazi unatakiwa uanze mara moja, iwekwe doria kuzunguka Kisiwa cha Mafia, boti za kijeshi ikiwezekana, ndani ya saa sabini na mbili kuna nyambizi italeta mzigo mkubwa wa silaha na zitashukia hapa. Lakini inabidi tuhakikishe kuwa hakuna mtu anayetoka kwa njia ya maji kuelekea popote isipokuwa watalii peke yao,” Amata akaeleza.

“Na vipi umewaona?” akauliza HOT

“Nilikuwa kama Daudi kwenye pango la Sauli, nimekutana na Mtokambali nikamlaza usingizi, sikumfanya chochote. Nimepambana na Msambamagoya nimemuuza bega lake ijapokuwa naye amaenifanya kitu kibaya, hapa naumwa. Egra mke wa Dastan yupo kwenye lile jumba, amehifadhiwa, nimemuona kwa macho yangu,” akaeleza.

“Ok, sasa hivi natoa taarifa jeshi la maji kazi hiyo ianze,” HOT akaeleza.

“Naomba unitumie wadogo zangu wote pindi tu nitakapowahitaji. Kuanzia sasa nitakupigia simu kila baada ya dakika tisini. Ukiona kimya baada ya dakika hizo ujue niko matatani, ninahitaji uokozi,”

“Umesomeka!”

“Ova!”

* * *




Naomba unitumie wadogo zangu wote pindi tu nitakapowahitaji. Kuanzia sasa nitakupigia simu kila baada ya dakika tisini. Ukiona kimya baada ya dakika hizo ujue niko matatani, ninahitaji uokozi,”

“Umesomeka!”

“Ova!”

* * *

Kamanda Amata aliingia tena katika hoteli ile mchana wa saa saba, baada ya kupata chakula katika mgahawa uleule aliokula jana yake. Alizikwea ngazi paka mapokezi na kumkuta mwanadada yuleyule.

“Saa moja ijayo ninatoka, leo nafanya nusu siku,” yule binti akamwambia.

“Utanishtua,” Amata akamwambia na wakaachana.


Saa 12:37 mchana.

Kirongwe

Wakiwa wamelala huku na huko wakiongea mambo mawili matatu, Amata alisikia michakacho ya miguu ya mwanadamu. Harakaharaka kwa kusikiliza kwa umakini, akahesabu na kujua kuwa wapo watatu.

“Jovanina!” akamwita na kumpa ishara ya kunyamaza.

“Vipi?”

“Kuna watu nje ya mlango wako au sebuleni!”

Jovanina akataka kuteremka kitandani kuuelekea mlango, Amata akamzuia na kumrudisha kitandani. Akainuka yeye.

“Acha Spark, ngoja niwasikilize, watakuwa majirani hao, wasione mtu umeingia na mgeni, umbeya mtupu,”

“Jova’ usiende, hao si watu wema,” akamwambia. Hodi ya fujo ikabishwa mlangoni kwa kurudiarudia. Wakatazamana.

“Mi naogopa Spark,”

“Tulia!” Amata akamwambia na kuamka, akashuka kutoka kitandani na kuelekea sebuleni. Akashika ufunguo na kuuzungusha, akafungua mlango ule kwa ghafla, kabla hajafanya lolote alipokea pigo moja zito, palepale mbavuni. Akapoteza uelekeo na kuanguka juu ya meza, ikavunjika vipande.

Akiwa pale chini, akawaona wanaume watatu waliojazia vifua, weye sura mbaya zilizojaa ukatili wa kila aina. Wakamzunguka bila kusema neon, na yeye akabaki kuwatazama tu.

“Ndiyo ugonjwa wako, Malaya mkubwa we! Umekamatika,” mmoja waoa akaongea kwa sauti ya kukwaruza. Alikuwa mweusi, mrefu. Jovanina akatoka chumbani na kuja sebuleni, yule jamaa mrefu akamshika na kumkumbati, wakakumbatiana na kunyonyana ndimi zao. Amata aliuona usaliti huo kutoka pale chini alipolala, akafumba macho.

“Kwa heri Spark, kwa heri ya kuonana,” Jovanina akamuaga na kutoka nje akiwa amevali vazi la kupendeza. Wale jamaa wakaangua kicheko kinachouzi, Amata akameza mate tu asijue nini anaweza kufanya mbele ya njemba wale. Yule jamaa aliyemkubatia Jovanina akamkanyaga Amata kwa nguvu kwenye mbavu aliyoumia.

“Aaaaaaaiiggghhh mseng* wewe!” akatukana.

Wao wakaendelea kuangua kicheko tu huku yule mwenzao akiendelea kumkanyaga. Amata akaukamata mguu wa yule jamaa na kuuzungusha ghafla.

“Aaaaaaaaaa!” yule bwana akapiga kelele na kuuondosha mguu wake. Amata alijizungusha kama helikopta na kuwachota ngwala wawili wote wakaenda chini kama mizigo. Aliposimama akahisi kupigwa na kitu kizito kisogoni, akashindwa kustahamili, alipogeuka akashindiliwa Makonde mfululizo na kurudi sakafuni. Akajikuta anaishiwa nguvu na giza likimchukua, akajaribu kukodoa macho, wapi. Aliwaona watu watano watano ilihali walikuwa wawili tu. Akapoteza fahamu.

* * *

Mwanga mkali ukampiga usoni, akajitahidi kufumbua macho, hakufanikiwa.

“Zima!” akasikia sauti anayoifahamu. Sauti aliyoisikia mara chache wakati wa ujana wake. Akafumbua macho. Mbele yake palikuwa na watu watatu. Akashangaa, hakufungwa popote alikuwa chali sakafuni.

“Ujanja wako umefika mwisho, unajifanya mwandishi wa habari wewe kumbe ni jasusi siyo? Umekamatika,” Mtokambali akamwambia.

“Hapo ulipolala, ndipo alikaa Dastan Kihwelo, ndumi la kuwili, na akauawa ndani ya tindikali hii,” Big J akamwambia. Amata alimtazama mtu huyo anayeongea akiwa na bandeji kubwa begani mwake.

“Kumbe ile risasi ilikuingia eee?” akamuuliza. Big J akashikwa na hasira kali baada ya kugundua kuwa ni huyo aliye mbale yake ndiye aliyempiga risasi usiku uliopita. Akauma meno na kuinuka kitini. Kwa kutumia miguu yake, alimpiga Amata kwa mateke ya kutosha na kumwacha hoi. Mc Tee alikuwa akiangalia tu.

“Kwa hiyo ni wewe ndiye ulitufanyia vile usiku,” akamwambia.

“Ndiyo ni mimi,” akajibu kijeuri. Kibwana akampiga teke lililotua usoni, nay eye mpigaji akayumba na kudakwa na wale vijana.

“Sasa nitakuhifadhi na usiku huu utakuwa ndiyo mwisho wako, mshenzi wewe!” Kibwana akongea kwa kufoka. Akawapa ishara wale vijana, nao wakamnyanyua.

“Si unapenda wanawake wewe! Sasa nitauona huo urijali wako, mpelekeni Cabin 4” akawaambia. Amata akaburuzwa kutoka pale stoo na kupitishwa mlango mwingine mpaka chumba hicho kilichojulikana kama Cabin 4, akatupiwa humo. Akapepesa macho na kukikumbuka kile chumba. Mbele yake aliona miguu ya mtu aliyesimama, akapandisha uso wake na kukutana macho na Egra. Macho yaliyojawa uchovu, mawazo, msongo na kukata tamaa.

Egra, akamsaidia Amata kuinuka na kumkalisha kwenye kiti, “we ni nani?” akamuuliza kwa sauti ya kinyonge, “mbona wamekupiga hivi?” akaongeza swali kabla hajajibiwa lingine.

Amata akamtazama mwanadada huyo kwa jozi la sekunde, akakumbuka usiku uliopita alimkuta kwenye chumba hichohicho.

“Pole!” Amata akasema.

“Asante! Lakini hujanambia wewe ni nani” akakumbusha swali lake.

“Naitwa Jaf… no Amata Ric au Kamanda Amata,” mbele ya mwanamke huyo akajikuta anashindwa kutumia uongo. Amdanganye nini? Hakuna.

“Umefikaje huku kuzimu?” Egra akauliza.

“Kuzimu wakati umenawiri?”

“Nimenawiri!” akajiangaliaangalia, “eti mimi nimenawiri…”

“Egra!” akamwita.

“Unanifahamu?”

“Ndiyo, nimekuja kukuchukua, kukurudisha nyumbani,” Amata akamwambia.

“Mimi mfungwa…” akaanza kulia. Amata akainuka kwa shida na kumkubatia.

She is so hot, mama yangu! Akajisemea. Akamketisha kitini. Egra hakukaa, akainuka na kwenda kwenye kona ya chumba hicho kulikuwa na kitambaa kilichofunika kitu. Akafunua. Msalaba.

Dastan Kihwelo! Akasoma. Akamtazama Egra.

“Mimi nafanya kazi aliyoiacha Dastan, marehemu mume wako,” akamwambia Egra.

“Kuingia kwenye hii ngome ya shetani ni rahisi lakini kutoka ningumu,” Egra akasema, “Mimi nilifikishwa hapa mwaka 1991, mume wangu alikufa kifo kibaya sana, walimyeyusha kwenye dawa… nimemuomboleza sana hata sasa. Nimekuwa mikifanywa mtumwa, mfungwa mara kadhaa nimelazimishwa kutumika kimapenzi. Nimepelekwa Muritius mara kadhaa kwa kazi hiyo. Sipendi lakini napewa vitisho…” Egra akazungumza kwa uchungu na kaunza kulia. Amata akainuka kitini akamkumbatia na kumuweka aketi, akapiga magoti mbele yake, “niangalie,” akamwambia.

“Nimefanya kazi kubwa sana kukutafuta mpaka nimekupata, nahitaji kukutoa hapa nikurudishe nyumbani. Unajua hapa upo wapi?” Amata akamuuliza.

“Sijui!”

“Mama yako anakusubiri, nilikutana naye juzi, bado anakulilia,”

“Nitafurahi kumuona tena, bado mzima?” akauliza.

Wakiwa katika mazungumzo hayo yaliyompa Egra matumaini, mlango ukagongwa kwa fujo, kilichofuata ilikuwa ni kufunguliwa kwa nguvu.

“Haya, umeshafaidi,” James Msambamagoya akazungumza kwa sauti yake ya kibabe. Wakamkamata Amata na kutoka naye mpaka kule chini stoo. Wakamtupa chini. Alipoinua macho yake akakutana uso kwa uso na Barbier.

Shetani! Akajisemea moyoni. Amata alijikuta anashikwa na hasira. Kumbe na mwanamke huyo vilevile.

“Lazima ufe mshenzi wewe, unaeharibu mipango ya watu,” Barbier akaongea kwa hasira na kumvamia Amata pale chini. Kwa wepesi Amata alijigeuza miguu yake ikachota mwanamke huyo na kumtupa kando. Akasimama wima, wale vijana wakamvamia lakini wakakutana na chuma cha reli. Konde la kwanza likampasua mdomo aliyekuwa mbele yake, akarudi nyuma. Alipokuja wa pili, akampiga karate matata kabisa na kumpepesua huku yule watatu akichezea kichapo ambacho hakukitegemea. Amata aliwatawanya kwa mapigo mfululizo na kufanikiwa kuwachanganya vibaya wale vijana. Barbier alijikusanya kutoka pale alipo tayari kwa pambano la mikono. Alikuwa na hasira na kiumbe huyo.

Akainuka kama mbogo, kwa mapigo ya kungfu akamtandika Amata kama sekunde kumi na tano hivi na kumwacha hajielewi.

“Nakuua!” akamwambia kwa hasira huku akiuma meno na kutoa kelele za kike. Kamanda Amata akaruka hewani na kumtandika teke la shavuni na kumvunja taya, Barbier alienda chini kama mzigo. Amata alipotua tu akakutana na ngumi nzito kutoka kwa mmoja wa wale vijana. Kabla hajakaa sawa akatandikwa na ubao wa mgongo, akawahi kugeuka na kuukamata ule ubao, akautumia kama wenzo na kujizungusha, miguu yake yote miwili ikamtandika huyo kijana, akarudi chini lakini yeye alisimama wima sakafuni. Alipotaka kugeuka akakutana na kabali nzito, ‘kabali namba sita’. Akampapasa mtu huyo aliyemkaba, alipomshika kiunoni akakutana na bastola, akaichomoa. Kosa. Risasi ya kwanza ikamchapa kijana aliyekuwa chini ikamtoa uhai. Barbier akasimama haraka akiwa na maumivu makali. Akapeleka mapigo kumshambulia Amata. Kamanda hakuwa na muda, alivuta kifyatulio na kuachia risasi moja iliyofumua kichwa cha mwanamke huyo na kumbwaga chini akiwa marehemu.

“Nisamehe!” yule aliyemkaba Amata alimwachia, akasimama kando mikono juu. Amata alikuwa akitweta, maana kupambana na watu hao wane ilikuwa shughuli kwelikweli.

“Niongoze walipo mabosi wako,”

“Sijui!” akajibu mkato. Risasi moja ikapiga mguu wa yule jamaa.

“Underground!” akapiga kelele.

“Onesha njia!” akamwambia. Yule kijana akiwa anatetemeka, akatembea kwa shida huku maumivu makali yakiutafuna mguu wake.

* * *

Usiku wa saa tano, chopa za jeshi zilikuwa zikirandaranda katika anga la kisiwa hicho, boti kadhaa ziendazo kasi zilikuwa majini zikitimua mbio kuelekea eneo hilo. Kutoka katika kituo cha jeshi la wanamaji Kigamboni, ishara ya kuwa kuna nyambizi kubwa iliyokuwa katika bahari ya Tanzaniaa ilionekana kupitiaa rada maalum iliyofungwa hapo. Coordinate zake zikasoma pasi na shaka na kuonesha wazi kuwa nyambizi hiyo ilikuwa karibu kabisa na Kisiwa cha Mafia.

“Inasoma karibu kabisa na Mafia upande wa Kaskazini Mashariki, ova!”

“Ground zero umesomeka ova!”

Mawasiliano kati ya wale wanaoongoza vyombo vile na wale waliokuwa katika kambi ya Kigamboni yalifanikisha kuonekana kwa chombo hicho kilichobeba silaha nzito na za kisasa.

“Pay attention lolote linaweza kutokea, ova!” kutoka chini wakatoa tahadhari.

“Ground zero umesomeka ova,”

Chopa nne za jeshi zikakizunguka kisiwa kile kutoka pande zote, “msifanye chochote mpaka taarifa kutoka chini ova”.

“Roger! roger!”

Katika boti nyingine ya kisasa kabisa, Chiba, Scoba, Gina na Jasmini walikuwa wamekaribia sana katika kisiwa kile. Tayari kifaa cha Chiba kilishakuwa hewani na kukata mawasiliano ya simu pamoja na yale ya kamera za usalama kama usiku uliotangulia.

“Safari hii tufikishe jirani Zaidi,” Chiba akamwambia Scoba aliyekuwa akiongoza chombo hicho.

“Haina shida, utakalo lifanyike kaka,” akajibu na mara ghafla ile boti ikaayumba kushoto, kisha kulia na ukaa sawa tena.

“Scoba vipi?” Gina akauliza.

“Tunashambuliwa kutoka mbele,” akawaambia, “nimekwepa topido mbili hapo,” akaongezea.

“What?” Gina na Jasmine wakajikuta wakiuliza pamoja mara nyuma yao milipuko miwili ikatokea nyuma yao. Boti moja ya jeshi ikalipuka vibaya. Wakatazama nyuma, “wamechokoza nyuki,” Gina akasema.

“Tunashambuliwa, tunashambuliwa!!” kutoka katika helikopta wakatoa taarifa. Na wale wa kwenye boti nao wakaripoti kulipuliwa kwa boti moja. Vijana wa jeshi waliokuja kusaidia operesheni wakashikwa na gadhabu.

“TDO ipewe nafasi?” kutoka kwenye chopa moja wakauliza.

“Kuna mtu wetu muhimu ndani ya jengo, hold on men! Tunafungulia mamba wafanye kazi, ova!” kutoka kituo cha jeshi wakaruhusu askari walio katika boti wazuie mashambulizi. Ilikuwa bado mwendo mdogo sana kulifikia lile jumba la kifahari. Zile boti zikatawanyika, mbili upande huu na ile nyingine upande mwingine. Boti ya kina Chiba ikageuka na kurudi pale ilipolipuka ile ya jeshi ili kusaidia kama kuna majeruhi yeyote. Wakati Scoba akifanya hivyo. Gina alichumpa ndani ya maji na kuanza kuogelea kuelekea kwenye lile jumba halikuwa mbali sana na wala hakuna aliyemjali.

* * *



EP42


Zile boti zikatawanyika, mbili upande huu na ile nyingine upande mwingine. Boti ya kina Chiba ikageuka na kurudi pale ilipolipuka ile ya jeshi ili kusaidia kama kuna majeruhi yeyote. Wakati Scoba akifanya hivyo. Gina alichumpa ndani ya maji na kuanza kuogelea kuelekea kwenye lile jumba halikuwa mbali sana na wala hakuna aliyemjali.

* * *

Kutoka katika chumba cha chini kabisa, ndani ya jengo lile, Msambamagoya au Big J alimhifadhi Mtokambali kwa ajili ya usalama.

“Ukiona, dakika sitini sijarudi, unaweza kutoroka kwa kupitia njia hii, utatokea kwa Jovanina utajihifadhi hapo kwa muda,” akamwambia rais wake. McTee pamoja na kuwa aikuwa mwanajeshi zamani, alijikuta akitetemeka.

“Tumeshindwa kwa mara nyingine?” akamuuliza Big J.

“Hatuwezi kushindwa, we fanya nilivyokwambia. Ukifanikiwa kutoroka, kajifiche Mauritius na mimi nitaungana nawe huko,” Big J akatoka na kupanda ngazi kulekea juu. Alipojitokeza tu, akakuta hali mbaya, vijana wake aliokuwa akikaa nao kwa ajili ya usalama wote walikuwa sakafuni, damu ilitapakaa huku na kule. Akatazama eneo lile akasikitika. Alitamani awaite wote walio mafichoni waje, mapambano yaanzie hapo, lakini hakuna simu iliyokuwa inatoka. Big J akahisi kuchanganyikiwa, akaiendea ngazi inayopanda juu, akaanza kuikwe, alipokunja kona tu akakutana uso kwa uso na Amata.

Kitendo bila kuchelewa, Kamanda alimsukuma kwa nguvu yule jamaa aliyekuwa akimwongoza kwenda chini. Akampamia Big J. kabla hajafanya lolote akajikuta akipigwa guu la uso. Big J akaanguka chini mzima mzima. Akaivuta bunduki yake kubwa aliyokuwa kaipachika mgongoni. Amata akaruka upande wa pili na risasi zikatawanya kioo kikubwa cha dirisha. Big J akainuka haraka kumkabili mbaya wake. Bandeji yake bado ilikuwa begani na kidonda kilianza upya kutoa damu. Kamanda Amata naye akainuka haraka kujiweka sawa. Akainua chupa ya ua iliyokuwa kwenye kiukuta kidogo na kumrushia mbabe huyo. Hakuangaika kuikwepa, kwa kutumia bunduki ileile akaifumua ikiwa hewani, kisha akamlenga Amata tayari kummaliza.

“Huna ujanjaaaa!” akapiga kelele. Lakini ghafla, Amata akapigwa kikumbo kitakatifu na kuangukia upande mwingine huku risasi zikimiminika pale alipotoka. Gina akajiviringa chini na kumrushia Amata bastola iliyoshiba risasi. Hakufanya kosa, aliwahi kuinuka kiufundi kabisa lakini kabla hajafyatua, alijikuta kapata pigo moja zito lililoitoa bastola ile mkononi.

“Hukumu yako ni kifo,” Amata akamwambia.

“Ha ha haaaaaa hamna kitu, kifo utakishuhudia wewe,” Big J akatamba na kumwendea

Amata kwa kasi. TSA 1 naye akavuta hatua mbili ya tatu, akamkanyaga gotini na kujirusha tiki taka, goti la mguu wa pili likamtandika Big J kidevuni. Amata akatua sakafuni salama salimini kwa miguu miwili. Big J, pande la baba, liakaguna kwa maumivu. Likatema meno mawili.

“Na utaenda motoni kibogoyo…” Amata akamwambia. Gina aliinuka pale alipo, akajiweka sawa na kuingialia mtanange huo.

“Gina kaa pembeni, hii mechi nzito…” Amata akamwambia.

“Hakuna kitu kama hicho, huyu boya tu,” Gina akamtukana, akamsogelea Big J na kumvurumishia mapigo kadhaa ya karate lakini hakuna hata moja lililompata. Akabadilisha mtindo na kujiweka sawa kwa kung-fu, akapiga kata za kutosha za aina zote lakini bado hakuweza kumpata huyo jamaa hata kwa pigo moja. Mzunguko wa mwisho, alidakwa mkono. Big J akauzungusha na kusababisha hitilafu kwenye mifupa. Gina alipiga yowe la uchungu lililomfanya Amata kuhamaki. Akaiwahi bastola iliyokuwa chini lakini kabla hajafika akasikia kishindo kikubwa, akageuka na kushuhudia Gina akibamizika mlangoni na kuanguka hapo ndani. Amata alipokea konde zito, akayumba na kabla hajasimama akapata mateke kadhaa ya haraka haraka, akajaribu kuyakwepa na kujikuta keshafika ukutani. Akajaribu bahati yake, akajiangusha chini makusudi, akajiviringa na kuchukua kipande cha chupa kilichokua hapo chini. Akainuka, pigo lililofuata akalikinga kwa mkono ule wenye chupa, ikadidimia kwenye nyama ya mkono wa Big J. akavuta na kuchana sehemu kubwa ya nyama.

“Aaaaaaaaahhhhh!”

Amata akatumia nafasi hiyo akaruka na kumtadika kifuti cha paji la uso, Msambamagoya akahisi kuchanganyikiwa. Hajakaa zawa alichezea Makonde mazito ya chembe, akakohoa damu. Amata aligeuka mbogo, akaruka hewani na kumtandikaa mateke mawili maridadi kabisa, mwanaume akaenda chini kama mzigo.

“Ulihukumiwa kunyongwa, sasa natimiza hukumu hiyo…” akamwambia.

James hakukubali kufa kijinga, akainuka na kumuwahi Amata, akakosea padogo sana. TSA 1 kwa mikono yenye nguvu akaepa pigo la kifo la Big J, akafanya kama anampita hivi akaudaka ukosi wa shati la jamaa huyo akavuta kwa nguvu akakidaka kichwa, akamvuta chini wakaenda wote Amata akiwa katangulia. Alipofika chini akamgeua na kuikunja shingo yake vibaya. Mifupa ya shingo ya Big J ikaitika. Macho yakamtoka, miguu ikatapatapa, akakaata roho.

Amata hakuamini, akainuaka haraka na kumkimbilia Gina, akamuinua kutoka pale kwenye vipande vya mlango.

“Amekufa?” Gina akauliza.

“Tayari,”

“Nimeumia Amata,” akalalamika huku kajishika eneo la mbavu.

“Msiniue Tafadhali,” sauti ya kike ikasikika kutoka upande wa nyuma. Amata akagaeuka, na kugongana macho na mwanamke mweupe, mwarabu au chotara. Akamtazama kwa sekunde kadhaa. Hassna.

Akamshika mikono na kumkalisha chini, “Gina mlinde,” akatoa amri. Kisha akatoka pale na kushuka ngazi moja, Cabin 4, akavunja mlango na kumkuta Egra kajikunyata kwenye kona ya chumba akiwa kaukumbatia msalaba wa marehemu mumewe.

“Wakati wa kuondoka Egra,” akamwambia na kumshika mkono. Egra hakutaka kuuacha msalaba ule. Amata akaubeba na kuondoka nae mpaka alipo Gina, “mchukue huyo tuondoke,” akamwambia, nao wakatafuta njia ya kutoka nje.

Huko nje tayari wanajesshi walikuwa wameteremka kutoka kwenye boti na kulivamia lile jumba. Watalii ndani ya hoteli walitolewa nje wote na kuwekwa sehemu nyingine kabisa. Kizaazaa. Amata akiwa na Gina, Hassna na Egra walifanikiwa kutoka nje, wakapokelewa na vijana wa JW wenye silaha nzito.

“Kamanda Amata!” Amata akasikia akiitwa na mmoja wa wale vijana, akasimama na kumtazama. Hakumjua kutokana na jinsi alivyojiziba uso. Akajitoa ile barakoa.

“Joseph Rutashobya!” akamtambua. Joru akapiga saluti ya kukubali kwa mara nyingine kazi ya agent huyo wa siri wa serikali.

“Kazi nzuri Joru, hakikisha mmesafisha kila kitu huko ndani, ilakuna siri moja nakupa uifanyie kazi,”

“Yes Kamanda!”

“Katika kijiji cha Bweni kaskazini kabisa ya kisiwa hiki, kuna wanajeshi wetu waasi wamejificha walikuwa wakisubiri hizo silaha kuja kufanya mapinduzi… naomba muashughulikie kwa sharia zenu,”

“Umesomeka!”

“C4, C4,” Joru akaita kwenye redio yake.

“C4 anakusoma,”

“Uelekeo, upande wa kaskazini, kuna mifugo ipo malishoni, tukaichukue kwa njia yoyote tunayoweza,”

“Copy Sir!”

Chopa namba nne likateremka chini na vijana kama kumi walio kamili wakalikwea na kuondoka eneo lile.

Boti ya Scoba ilifika ukingoni kabisa mwa lile jumba, Egra, Hassna wakapakiwa. Gina na Amata wakafuatia. Chiba akateremsha kifaa chake na kukizima bila kurudisha mtandao eneo lile. Wakajifungia ndani. Amata akainua simu ya upepo wanayotumia mara nyingi kama ofisi.

“HOT, HOT,” akaita.

“TSA 1, nakupata,”

“Mission Clear, James Msambamagoya ametekelezewa hukumu yake. Mtokambali amefanikiwa kutoroka tena… tupo salama, tunarejea, ova” akampa taarifa fupi..

“Umesomeka… tukutane shamba operesheni nyingine TNS wameshaingia kazini, over and Out!”



MWISHO


1 comment:

BLOG