Search This Blog

Saturday, February 26, 2022

THAMANI YA FUKARA - 4

    

Simulizi : Thamani Ya Fukara

Sehemu Ya Nne (4)


"Kaa kimya mpumbafu wewe au umechoka kuongea na mama yako?"aliongea askari mmoja aliyekuwa zamu,

"Unaona mama hii kesi ya kutengeneza wala haina ukweli wowote lakini usiwaze sana mwishowe ukapata ugojwa wa moyo,siku zote damu ya mtu asiye na hatia huwa aiendi bure"aliongea Gabi kwa machungu akimtia moyo mama yake,

"Nami najua kuwa kinachoendelea hapa ni nguvu ya pesa lakini hatuna ujanja ngoja nikajaribu kama nitapata pesa niweze kuomba dhamana"aliongea mama yake Gabi huku akiagana na mwanaye kisha yeye akaenda mpaka nyumbani kwake,aliweka shamba lake lehani kwa ajili ya kutaka kuomba dhamana,

"Asipewe dhamana huyo sisi lengo letu tunataka afungwe jela"ilikuwa sauti ya mzee Herman baba yake Doris akimwambia mkuu wa kituo kwa njia ya simu.Mama yake Gabi alipofika mkuu wa kituo alikataa kabisa,

"Hatuwezi kumpa dhamana ilihali uchunguzi haujakamilika,mama subiri kama dhamana atapewa uchunguzi ukiwa tayari"aliongea mkuu wa kituo.

Siku ilikatika ikiwa Gabi hajaliona jua,kila alipokuwa anafikiria kesi ile ilivyotengenezwa alijawa na hasira na kuapa ndani ya moyo wake kuwa kama hatopelekwa jela basi lazima apambane kufa na kupona ili awe tajiri.Kawaida kwa mtuhumiwa huwa ni siku tatu za kukaa pale kituoni na siku ya nne hupelekwa mahakamani,kama ushahidi haujitosheleshi basi hurudishwa tena ndani kwa siku kumi na nne.Gabi alizidi kumuomba mungu asipelekwe mahakamani lakini kama wasemavyo wahenga kuwa dua la kuku huwa halimpati mwewe.Siku iliyofuata Gabi alipelekwa mahakama ya mwanzo na kupewa siku tatu ili kesi yake ipate kusikilizwa.

Huku kwa Layla anafunga safari kwenda kumtembelea Gabi lakini anapokea taarifa mbaya kuwa Gabi kapelekwa leo mahakamani na kesi yake itasikilizwa siku tatu mbeleni,mama yake Gabi alimwambia Layla huku machozi yalimtoka aliyafuta na kanga yake na kubaki kushika tama,

"Kwahiyo ndo hivyo mwanangu anapelekwa jela kwa kosa la kusingiziwa"aliongea mama Gabi huku kamasi zilizoambatana na machozi zikimtoka,Layla alimkumbatia kama kumfariji,

"Usijali mama hawezi kupelekwa jela nitapambana kufa na kupona"alisema Layla na kuondoka akionekana dhahiri kuwa mwenye hasira.




"Mama kama mnataka mwanenu nife basi huyo kijana mliyemshikilia ahukumiwe,na kama ataenda jela naapa mbele yako najiua, wazazi gani nyie mbona hamna huruma kisa mtu wa chini ndo mnamnyanyasa kiasi hiki?ahaa! hapana halitowezekana"aliongea Layla mara baada ya kufika nyumbani kwao na kumkuta mama yake,

"Tunafanya haya ili kukujengea wewe maisha ya badae,umekataa kwenda shule kisa huyo kinyago"aliongea mama yake Layla,lakini katu mwanaye hakukubaliana naye.Layla aliingia mpaka chumbani kwake na kuchukua hela kadhaa kisha akatoka ndani kwenda nje,

"Unasikia wewe hakikisha unaijua siku ya hiyo hukumu chukua hii hapa"yalikuwa maongezi ya Layla na mlinzi wa getini aliyeitwa mzee Singo

"Halafu nasikia kesi itasikilizwa ijumaa hivyo huenda hiyo ndo itakuwa siku ya hukumu"aliongea yule mlinzi wa geiti na kumfungua akili Layla aliyekuwa bado yuko kizani.Siku hiyo ilikuwa siku mbaya kwa Layla,mda wote alikuwa amekunja sura yake jambo lililomtia mama yake kumpoteza mwanae yule wa pekee.Layla aliingia chumbani kwake na kujifungia kwa ndani.Doris bado alikuwa hajapata taarifa ile lakini siku ile aliwasikia majirani zake wakiizungumzia ile habari,

"Kijana mdogo kama yule kupelekwa jela asee hii mbaya,yule mama yake sijui atakuwa kwenye hali gani ukizingatia ndo mwanaye anayemtegemea"

"Tuombe mungu lakini sina uhakika kama kweli Gabi ameweza kubebesha mimba,mbona alikuwa kijana mtulivu mno"

"Mmmmh hawa matajiri wanaweza kukufanya chochote wanachokitaka"yalikuwa maongezi ya majirani ambayo Doris aliyasikia,

"Mimba?inamaana Gabi amembesha Layla mimba?hapana sitaki kuamini"alijisemea Doris huku akienda mpaka kwa wale wanawake waliokuwa wanazungumzia ile habari,baada ya kuwadodosa kwa kina alitambua kuwa Gabi kasingiziwa na ni wazazi wake walioweza kufanya vile"moyoni aliumia lakini alimuogopa baba yake kumuulizia zile habari,

"Mama kwanini mkaka wawatu mmemfanya vile?"aliuliza Doris,

"Tunataka wewe usome,unafikiri haya maisha bila kusoma itakuwa vipi?

"Sawa lakini sio kumuweka kwenye matitizo yule kaka,mmefanya makosa makubwa"aliongea Doris lakini mama yake hakumjibu zaidi aliendelea na shughuli zake.Doris hakuwa na ujanja tena kwani wazazi wake walikuwa wameamua tayari,

"Baba yako kalazimika kukununulia matokeo ili uweze kusoma lakini wewe hijiulizi tu unakaa ukiwa mujinga mjinga,na habari hizi usijaribu kumueleza baba yako shenzi kabisa anaweza kukutoa roho"aliongea mama yake Doris kwa ghadhabu.

***

Hadi siku nzima inapita Layla alikuwa bado amejifungia chumbani kwake,mama yake alijaribu kumuamsha ili angalau apate chakula cha usiku lakini Layla hakutaka kufungua mlango,

"Mme wangu tutampoteza mtoto tangu asubuhi amejifungia na hajala chochote"alisema mama yake Layla,

"Hana njaa siku zote ng'ombe mwenye kiu sio mpaka umuonyeshe maji,yule sio mtoto na kama anawaza yule kijana kuachiwa huru asahau kabisa"aliongea mzee Gozirbert kwa sauti maneno yale aliyasikia vyema Layla lakini alipanga kujifungia siku tatu mpaka siku ya Gabi kuhukumiwa na yeye aweze kufanya kile alichokuwa amekipanga.

Mama yake Gabi alikuwa mtu wa kulia mda wote lakini alijipa imani kuwa kisicho riziki huwa hakiliki,

"Mwanangu kama hana hatia najua mungu atampigania"alijisemea mama Gabi,alingoja siku ya hukumu iweze kuwadia.Ndugu wa Gabi hawakuwa na msaada wowote zaidi ya kumpa pole mama yake,hakuna aliyejitoa kumchangia licha ya kuwa na uwezo kifedha lakini kila mtu aliendelea na mambo yake.Hatimaye ilibaki siku moja,siku ile mama yake Gabi alimpelekea mwanaye chakula pale mahakamani,

"Mama vipi hakuna hata ndugu mmoja aliyekupa msaada?"aliuliza Gabi,

"Hayupo otoke wapi,kama unavyowajua wajomba zako walivyo na roho mbaya"aliongea mama yake Gabi,

"Wewe mama mda wa kuongea na mwanao umeisha"ilikuwa sauti ya askari.,waliagana kisha mama yake akaondoka,

"Usisahu kusali"ilikuwa sauti ya mama yake,Gabi aliitikia kwa kichwa.

Mda huo wote Layla alikuwa hajala kitu chochote jambo lililowapa hofu,

"Au kashajiua tayari?maana alisema atajiua"aliongea mama Layla,

"Haina jinsi hapa ni kuvunja kitasa"alisema mzee Gozirbert huku akimuita mlinzi wa geita na kuvunja kitasa mlango ukafunguka,walimkuta Layla akionekana kukauka midomo sababu ya njaa,

"Acha ujinga tafuta chakula ule"alisema baba yake,

"Siwezi kula kama hamjamuachia yule kijana asiye na hatia"aliongea Layla,

"Khaa,hadi mdomoni unatoa harufu hivi sasa kuhusu suala la yule kuachiwa huru sahau kabisa na chakula utakula"aliongea Mzee Gozirbert lakini Layla alikataa na kuendelea kulala hakujali njaa ya siku mbili aliyokuwa nayo,kweli ulikuwa upendo wa hali ya juu aliokuwa nao Layla,

"Muache atakula ngoja tuone akishahukumiwa yule kijana kama hatokula"aliongea mzee Gozirbert akimwambia mkewe.

***

Hatimaye siku ya hukumu iliwadia watu walijikusanya mahakamani pale kusikia kesi za ndugu zao,majira ya saa tatu hakimu alikaa kwenye kiti chake na kila mmoja aliyekuwa mahali pale alikaa kimya kusikiliza.Zilianza kesi za watu wengine,mnamo saa tano asubuhi Gabi alipandisha kizimbani na kesi yake ikasomwa,mashahidi walijitokeza akiwemo yule Daktari wa uongo,kwa upande wa Gabi hakukuwa na mashahidi wa kumtetea. Hakimu akajitosheleza na ushahidi ule alipandisha miwani yake ikamkaa vyema,

"Kutokana na ushahidi wa pande zote mbili kukamilika bwana Gabi unahukumiwa kwenda jela miaka thelathini pamoja na viboko kumi na tano kila siku asubuhi"aliongea hakimu huku akinyanyua kinyundo chake lakini kabla hajakigonga kupitisha hukumu ile mara ghafla ilisikika sauti,

"Kama mtamhukumu huyo kijana asiye na hatia basi namimi naukatisha uhai wangu mbele yenu"aliongea Layla huku akitoa kisu chake na kukiweka shingoni,Watu wote waligeuka shingo kumtazama aliyeongea maneno yale huku hakimu kile kinyundo akikiweka chini..

Atafanya nini?ni upendo wa Aina gani huu?



"Samahani sana mtukufu hakimu,lakini huyu mtu mnayetaka kumpa hukumu hana hatia hii ni kesi imetengenezwa"aliongea Layla watu wote waligeuka kumtazama hata Gabi alipata nguvu tena baada ya kuona mtetezi wake amefika,Baba yake Layla alibaki kumtazama mwanaye alijua kama utafanyika uchunguzi wa kina basi anaweza kwenda jela alitoa simu ya kuinama chini ya meza akaandika message,

"Mzee mwenzangu maji yamezidi unga"ilikuwa message aliyoituma kwa mzee Herman ambayo ilimfikia hata na mwenyewe tumbo lilikuwa joto.

"Haya sawa unasema huyu kasingiziwa je una ushahidi gani juu ya haya unayoyasema?"aliuliza hakimu,ghafla Layla aliishiwa nguvu kabla hata hajazungumza chochote alidondoka chini, kutokana na njaa ya siku nne aliyokuwa nayo,kila mtu alisitaajabu tukio hilo haraka ililetwa gari na Layla akapakiwa ndani na kupelekwa kwenye kituo cha afya kilichokuwa jirani na eneo lile.Daktari wa pale alipomuangalia Layla aligundua kuwa ilikuwa njaa ya siku nne hivyo haraka alimuwekea mirija ya kupitisha chakula huku aliongezewa na maji mengi sana,

"Hivi kama mzazi unapata ujasiri gani wa kumuacha mwanao siku zote hizo akiwa hajala? wazazi mnawaua watoto wenu wenyewe halafu mnasingizia wachawi"aliongea Daktari.

***

Kule mahakamani kila mtu alikuwa kimya kwa mda huo walibaki kumtazama hakimu aliyeonekana kuandika kitu fulani,

"Hii kesi imehairishwa itasikilizwa tena tarehe kumi na saba ya mwezi ujao"aliongea yule hakimu na kufunga lile jalada kisha akaendelea na kesi zingine.Gabi alirudishwa tena selo huku mama yake akirudi nyumbani lakini moyoni mwake akitaraji ushindi,

"Najua mungu yuko nasi lazima atampigania mwanangu"alijisemea.

Huku mzee Herman alikuwa anaregeza tai yake iliyokuwa shingoni kutokana na jasho la hofu lililo mtiririka,

"Aseee mwenzangu hii kesi inaweza kutugeukia maana bila mwanao kuanguka chini tulikuwa tunaumbuka leo"alisema Herman,

"Hatuna jinsi hapa ni kwenda kufuta kesi kisha yule kijana aachiwe huru maana hatuna ujanja tena hapa tumechoma pesa za bure"aliongea mzee Gozirbert na moja kwa moja walianza mchakato wa kuifuta ile kesi kwa kutumia nguvu ya pesa.

Layla alirejewa na fahamu,lakini bado hakuwa na nguvu za kuzungumza chochote,mama yake aliyekuwa kando alibaki kumtazama mwanae,

"Yaani mnatumia pesa kuwakandamiza wanyonge?naomba mara moja yule kijana atolewe la sivyo najiua"aliongea Layla huku machozi yakimtoka,

"Ataachiwa tu kati ya leo au kesho"alimjibu mama yake.Layla aliposikia maneno ya mama yake alipata nguvu za kuamka na kuketi kitandani alipokuwa amelazwa,baada ya masaa matatu kupita waliruhusiwa na kurejea nyumbani ambapo walimkuta mzee Herman akiwa ndani na baba yake Layla wakionekana kujadiri jambo.Layla hakuongea chochote alipitiliza mpaka chumbani kwake ambako hakuaa sana kisha akarejea sebuleni,aliketi kwenye sofa iliyokuwa kando na alipokuwa amekaa mzee Herman,kimya kilitawala mahali hapo lakini kimya hicho kilivunjwa na Layla aliyeanza kwa kushusha pumzi,

"Nimerudi tena sasa twende mahakamani kumalizia ile kesi"aliongea Layla kwa kujiamini,hakuna aliyemjibu kwa uharaka,

"Hivi mbona umekuwa huna heshima siku hizi hujui mimi ni mzazi wako"aliongea baba yaka kwa hasira,

"Heshima nakuheshimu ila sio kwa hili unalotoka kulifanya tena nasema kuwa kesho yule kijana anatakiwa atolewe la sivyo narudi tena mahakamani muone kama hamjaumbuka"aliongea Layla kisha akatoka sebuleni pale na kwenda chumbani kwake akiwaacha wazee hao wakiangaliana.

"Ila ukiangalia yuko sahihi kabisa tulitaka kufanya unyama mbaya sana"aliongea mzee Herman,

"Ni kweli mzee mwenzangu hatuna budi kufanya jitihada za kumtoa yule kijana"aliongea baba yake Layla,alitoa simu yake na kuiweka sikioni kisha akafanya maongezi na askari mpango wa kufuta kesi ukawa umefanikiwa na Gabi akatoka selo akiwa amekonda sana kwa hizo siku alizokaa, Layla alimkumbatia kwa furaha na katafrija kadogo kalifanyika nyumbani kwao na Gabi.Mama yake Gabi alimshukuru Layla kwa ujasiri aliouonyesha mbele ya umati wa watu bila kuogopa chochote kile,,

"Badae mkikua muoane kabisa"aliongea mama yake Gabi kwa furaha.

Sasa zilipita siku kumi tangu Gabi aachiwe,bado mzee Gozirbert alikuwa akimtaka mwanaye Layla kwenda shule ambapo alipanga kumpeleka jijini Dar es salaam, lakini Layla hakuwa tayari kuondoka na kumuacha Gabi.

Kwingine nako Doris naye alikuwa bado anagoma kwenda shule alipopata taarifa kuwa Gabi kaachiwa, siku ile aliandaa zawadi ya kumpelekea Gabi ili ampongeze kwa ile misuko misuko,bado alikuwa na upendo mkubwa kwa Gabi licha ya kutoonesha jitihada zozote kama ilivyokuwa kwa Layla.

"Hapa ndo nimeweza kugundua tofauti ya kupenda na kutamani"alijisemea Gabi alipomfikiria Doris,

"Siwezi kuendelea kuwa naye wacha mipango ikikaa sawa nitamuoa tu Layla"alijisemea moyo wake ulimchukia Doris pamoja na ndugu zake ambao hawakuonyesha ushirikiano wowote.

Doris aliweza kukaribia nyumbani kwao na Gabi hakutaka kwenda mpaka pale hivyo alimuagiza mtoto aliyekuwa jirani,

"Nenda kamuite Gabi mwambie Doris anakuhitaji mara moja"aliongea Doris na yule mtoto bila kusita alitimua mbio kuelekea kwao na Gabi....





"Nenda kamuite Gabi mwambie Doris anakuhitaji mara moja"Doris alimuagiza yule mtoto ambaye hakuchelewa alitimua mbio haraka haraka na kuelekea ilipo nyumba ya akina Gabi,

"Kaka shikamoo"alisalimia yule mtoto,Gabi naye aliitikia salamu ile,

"Kuna dada mmoja anakuita sijui anaitwa ahaaa kasema nani sijuii eeh Doris,kasema uende mara moja"aliongea yule mtoto,Gabi alishtuka sana moyo wake ulisita lakini upande mwingine aliona bora aende akamsikilize,

"Kwanza pole sana kwa yaliyokutokea nimeshindwa kuonyesha jitihada na hii ni kutokana na wazazi wangu kunibana"aliongea Doris,Gabi alikubali kumsikiliza hasa baada ya kuona Doris amechomoa pesa nyingi na kumkabidhi.Waliongea mengi sana na maongezi yale yalipokwisha Gabi akaaga kwenda nyumbani wakipanga kuonana siku jumapili.Gabi alifika nyumbani na kuzihifadhi zile pesa,alianza kuzunguka ndani ya jiji la Arusha akiangalia sehemu ya kufanyia biashara.

***

Wazazi wake na Layla baada ya kuona hataki kwenda shule waliamua kutumia nguvu nyingi kumlazimisha Layla kwenda shule lakini kwake ilikuwa ngumu sana kuondoka kijijini pale kumuacha Gabi,

"Kama mko tayari labda na huyo kijana mmpeleke shule nitakayoenda kusoma mimi ili niwe naye karibu,vinginevyo mimi siko tayari"aliongea Layla bila kuwaogopa wazazi wake wake wale,

"Hayo majibu unamjibu nani?sasa narudia kusema kuwa utake usitake lazima uende shuleni"aliongea mzee Gozirbert baba yake Layla.

Maneno ya wazazi wake yalianza kumkera Layla hakuwa tayari kutengana na Gabi,usiku ule aliwaza akawazua jinsi ya kuweza kuishi na Gabi,

"Hakuna namna lazima nitoroke naye twende kuishi mbali na hapa"alijisemea Layla.Asubuhi ya siku ile alienda mpaka kwao na Gabi na kumkuta akiwa bado amelala,hakutaka kumwamsha alisubiri mpaka mama yake alipofungua mlango,

"Mbona asubuhi asubuhi kuna usalama kweli?"aliongea mama yake Gabi,

"Mama usalama upo wala hata usijali nimekuja kuwatembelea"aliongea Layla.Mama yake Gabi alimkaribisha ndani na Gabi naye aliweza kuamka,

"Nina maongezi nawewe hivyo naomba tutoke nje kidogo"aliongea Layla,

"Ahaah subiri basi walau nisafishe uso"aliongea Gabi.Layla alivuta subira mpaka pale Gabi alipomaliza,

"Eeh nambie sasa kwema huko"aliongea Gabi huku akijiweka sawa kwa ajili ya kumsikiliza Layla aliyeonekana kuwa na jambo la mhimu,

"Unatambua fika kuwa wazazi wangu wananilazimisha kwenda shule sasa mimi siko tayari kukuacha wewe hapa, wazazi wangu hili neno wamelikazia sana kiasi kwamba nakosa amani huenda wakakufanyia jambo lingie tena baya hivyo basi nilikuwa na wazo litakaloweza kutunusuru,hakuna jinsi ni lazima tutoke hapa kijijini twende tukaishi mbali na hapa vinginevyo wanaweza hata kuua"aliongea Layla maneno yaliyokipa mtihani kichwa cha Gabi kuanza kufikiri,

"Hakuna cha kujiuliza sana hapo,nisingelikuwa mimi kukutetea sahivi ungelikuwa jela kwa kosa ambalo sio lako,je kama waliweza kukusingizia ile kesi je kukuua watashindwa?wale ni watu wenye hela wakikuua kesi wanaimaliza kimya kimya,niko hapa kutetea penzi lako nawaza kuacha utajiri wa wazazi wangu nakubali kwenda kuanzisha maisha upya na wewe sitajali maisha gani tutaishi hata tukilala nje sawa lakini sio kukuacha,bora kidogo cha halali kuliko kikubwa cha haramu ule ni utajiri wawazazi na sio wangu,fungua kichwa chako twende tukaanze maisha"aliongea Layla.Gabi alipotafakari sana kweli aliona maisha yake yako hatarini hakuna na cha kujiuliza zaidi ya kukubali.Walipanga siku mbili zijazo ndo waweze kusafiri,

"Sasa hapa tutaenda wapi?"aliuliza Gabi,

"Nadhani hakuna jiji lingine la kwenda tofauti na Dar es salaam jiji kubwa sana ambalo hata wakitutafuta itakuwa ni ngumu sana kuonekana,jiandae ila mama usimwambie kwanza tutaondoka kimya kimya"aliongea Layla na mara maongezi yao yalipoisha Layla alirudi nyumbani na kumuacha Gabi kwenye dimbwi la mawazo mazito.Kwanza kabisa alichimba shimo na kutoa pesa kidogo kisha zingine akazibakiza ili hata akifika huko maisha yakawa magumu arudi Kijijini akiwa na akiba atakayoiacha.Alifanya usafi wa nguo zake chache kisha akatulia na kuanza kuliwaza jiji la Dar es salaam ambalo mara nyingi alikuwa akilishuhudia kwenye magazeti na kwenye television.Pia alisikia kwa watu kuwa lile jiji linaongoza kwa utapeli lakini hilo halikumpa hofu.Hakuacha kuomba namba za jirani yake ili akienda Dar es salaam awe anawasiliana na mama yake.

Huku kwa Layla alihakikisha anaiba hela za wazazi wake na kuziweka sehemu salama ili siku ya kusafiri awe na pesa za kuanzia,alipohakikisha kila kitu kuwa sawa alitulia kusubiri siku yenyewe iweze kuwadia.Ikiwa imebaki sehemu moja Layla alienda tena nyumbani kwao na Gabi,

"Saa kumi kamili za usiku unatakiwa uwe tayari umeamka tukutane kwenye huu mti mkubwa hapa hakikisha unawahi ili kabla hakujapambazuka tayari tuwe nje ya Arusha"aliongea Layla huku akimkabidhi saa ndogo,Gabi alikubaliana naye kisha wakaagana kila mtu akingoja mda huo ufike.Usiku ule hakuna aliyepata usingizi si Layla wala Gabi,kila mtu aliendelea kuwaza jinsi itakavyokuwa wakifika jijini Dar es salaam.Wahenga walisema usiku wa deni haukawii kucha,kabla ya saa kumi Gabi alikuwa tayari yuko macho,alitoa saa yake iliyokuwa na uwezo wa kuwaka kwa mwanga mdogo na mara alipoiangalia aligundua kuwa ilikuwa saa tisa na dakika ishirini, hakutaka kulala tena aliamka kimya na kuchukua mfuko uliokuwa na nguo zake,alifungua mlango taratibu kisha akatoka nje na kuiangalia ile saa ilikuwa saa tisa na nusu,mama yake alikuwa usingizini hivyo hakuweza kusikia chochote.Majira yale yale Layla naye aliamka,kwakuwa alikuwa amepanga na mlinzi wa getini hivyo mlango aliukuta wazi.Alitembea hatua za kunyata mpaka pale walipokuwa wamekubaliana kukutana,wote walikumbatiana na kupeana baraka ili safari yao iwe ya amani isiwe na vikwazo vyovyote,walipanga kwenda na Basi la Arusha express lilikuwa linaanza safari saa kumi na moja.

Kipi kitatokea?safari yao itakuwa njema?





Saa kumi na nusu walikuwa wanafika stend kuu ya Arusha,walilikuta gari waliolitegemea likiwa bado halijaa,walipanda haraka na kukaa siti za mwishoni.Layla alijisikia faraja sana kuona yupo karibu na mtu aliyekuwa anamtafuta kwa kipindi kirefu sana alijisigeza karibu ili mwili wake ushikane na wa Gabi,

"Mpenzi tunaenda kuanza maisha upya huko hivyo hii pesa niliyokuja nayo hii hapa itunze"aliongea Layla na kufungua begi lake akazitoa zile pesa Gabi alizipokea na kuziunganisha na zakwake alizokuwa nazo,

"Tutafika tunafungua duka letu kubwa kama ni hela tayari tunayo ya kutosha"aliongea Gabi.Saa kumi na moja asubuhi Basi lilianza safari,

"Siamini kama ndo tunatoka kwenye jiji hili"aliongea Layla na kujilaza mapajani kwa Gabi,alifurahi sana,

"Kama ni penzi lake nitalifaidi mpaka nichoke"alijisemea Layla huku akijivuta zaidi ili hadi kifua chake kienee kwenye mapaja ya Gabi.Mwendo wa lile Basi ulikuwa mkali sana baridi ilitawala vyema ndani ya gari ile,njiani halikusimama na saa sita mchana lilikuwa linaingia Dar es salaam,abiria wote walikaa tayari huku walio kuwa na ndugu zao wakiwajulisha kuwa tayari wamefika,

"UBUNGO"Gabi alisoma bango lililokuwa kando ya barabara hapo aliweza kumuamsha Layla aliyekuwa amelala usingizi,

"Tayari tumefika mpenzi acha kulala"aliongea Gabi na mara moja Layla aliamka huku akiangaza macho yake kuishangaa stend ile ilivyojengeka vyema.Nyumbani kwao na Layla mzee Gozirbert pamoja na mkewe walichanganyikiwa sana,haikuwa kawaida kwa Layla kutoka bila kuaga,kilichowatia hofu zaidi ni pale walipoingia chumbani kwa Layla na kukuta baadhi ya nguo zake zikiwa hazipo,pembeni mwa kitanda waliona barua iliyokuwa na maneno machache aliyasoma mama yake Layla,

"Wazazi wengi mmeninyima furaha hivyo nimeamua niifate mimi mwenyewe mungu akipenda nitarudi wala msihangaike kunitafuta,kwaheri ni na pia nawapenda sana"maneno yale mama Layla aliyasoma kwa sauti,mawazo ya mzee Gozirbert alifikiri kuwa Layla atakuwa kwao na Gabi,hivyo akiwa mwenye hasira sana alienda mpaka nyumbani na kumkuta mama yake Gabi akiwa amejiianamia huku mkono wake ukiwa shavuni kuashiria majonzi,

"Mwanangu yuko wapi?"aliuliza mzee Gozirbert akiwa hata hajasalimia,

"Hata mimi mwenyewe sijui maana hata wa kwangu hayupo na haijulikani walikoenda"aliongea mama yake Gabi kwa wasiwasi mkubwa,

"Hujui? Sasa endelea kuwaficha utakiona cha moto"aliongea mzee Gozirbert na kutoa simu yake akaiweka sikioni,hazikupita hata dakika kumi Askari wawili walikuwa tayari wamefika na kumkamata mama yake Gabi hadi kituoni,lakini mama yake Gabi alikaa katu katu kuwa hajui chochote,taarifa zilikuja kuwa wamesafiri na Basi la Arusha express na haijulikani walikoenda, mawasiliano yalifanyika na dereva wa Basi lile kuwa wamewashusha stend ya Ubungo,picha ilipatikana ya Layla hivyo waliituma mpaka kwa Askari waliokuwa jijini Dar es salaam wakiambatanisha na maneno kuwa "ANATAFUTWA".Hivyo msako wa nguvu ulianza kwa Askari wa karibu na ile stend.

***

Layla na Gabi walibaki kushangaa,hawakujua pa kuanzia na pa kulala,

"Sasa tusipoangalia tunaweza kulala hapa"aliongea Gabi na mbele yao alikatiza kijana mmoja hivyo walimsimamisha,

"Kaka habari.."alisalimia Gabi,

"Salama kabisa nambie"alijibu yule kijana jina lake lilikuwa Abdul,

"Asee hapa naweza pata nyumba za kulala wageni?."

"Yeah,zipo nyingi tena sana ni wewe kusema Kama unataka za bei juu au bei ya chini kidogo",alijibu yule kijana,

"Nataka ya kawaida ili mradi niweze kulala kwa siku ya leo"aliongea Gabi,

"Okay kilete hicho kimada chako kisha tukodi bajaji itakayotupeleka mpaka sehemu husika"aliongea Abdul,Gabi alibaki kujiuliza neno "kimada"linamaana gani?hakupata jibu,alimfuata Layla aliyekuwa anashangaa ghorofa lililokuwa mkono wa kulia mwa ile stend.Bajaji ilisimamishwa na kuingia ndani akiwemo yule kijana,

"Tupeleke mawasiliano kwenye ile Gest ya MT"aliongea Abdul,ila alipoona pesa alizokuwa nazo Gabi alijisemea moyoni kuwa deni la kodi analodaiwa ataenda kulilipa kwa kuwa alipanga kuzitapeli zile pesa.

Hatimaye bajaji ilisimamishwa nje ya nyumba iliyokuwa na bango lililoandikwa mbele ya Ile nyumba"MT GEST HOUSE".

"Nitoe buku nne.."aliongea yule dereva bajaji,Gabi bila kuelewa chochote alizitoa zile pesa zilizokuwa kwenye mfuko wake wa nyuma,zilikuwa pesa nyingi na mara baada ya kumlipa yule wa bajaji yule kijana aliwaongoza mpaka ndani na kuhakikisha wamelipa chumba hivyo chumba walichoingia alikiona vyema na mara baada ya kujihakikishia hilo aliwaaga kisha akaondoka.Layla na Gabi waliingia mpaka ndani na kabla ya yote walielekea bafuni kuoga lakini Layla alikuwa na aibu kubwa hakuwa tayari kuoga mbele ya Gabi lakini Gabi alimsihi aondoe hofu.Zoezi hilo hakikudumu sana walitoka bafuni na kuagiza chakula,bado hawakujua kuwa wanatafutwa.Usiku wa siku ile kabla hawajalala walishauriana kuwa pale ndo mahali pazuri pa kuishi hivyo walimtafuta mwenye ile nyumba na kulipia miezi sita ya kukaa pale,

"Mpenzi leo naomba penzi lako"aliongea Layla kwa aibu,Gabi hakuwa na lakusema zaidi ya kumpa Layla alichokuwa anakitaka.Kila mtu aliporidhika na mwenzake walisogeleana na kuaanza kuutafuta usingizi wakipanga kesho yake kuanza kutafuta sehemu ya kufanyia kazi.

Majira ya saa sita usiku kukiwa kimya kweli ile nyumba waliyokuwa wamelala akina Layla na Gabi,yule kijana alifika kwenye dirisha la chumba walichokuwa wamelala,alitega sikio lake na kusikia wakikoroma.

**

Dawa aina ya CHLOROFORM,mara nyingi ilikuwa ikitumiwa na majambazi waliokuwa wanawateka watu,ilikuwa dawa yenye kumpa mtu usingizi wa masaa sita.Ndio dawa aliyokuwa nayo yule kijana aliipulizia vyumba vya jirani pia akapulizia kwenye kile chumba, baada ya kuhakikisha kuwa atafanya kazi yake bila mtu yeyote kuzinduka,ile dawa aliiamini kwa asilimia zote.Alianza kukata wavu zilozokuwa pale dirishani.Lengo lake lilikuwa ni kuziiba zile pesa alizoiona kwa Gabi.Layla na Gabi kila mmoja alikuwa kwenye usingizi mzito.

Atafanikiwa?je Kama atafanikiwa maisha gani watakayoishi Layla na Gabi??usikose sehemu ijayo.





Zoezi la kukata wavu lilidumau kwa takribani dakika kumi,mara baada ya kumaliza aliruka na kupanda pale dirishani kisha akadondokea ndani kwa kishindo, lakini hakuna aliyeweza kusikia kishindo kile.Alipekuwa kwenye suruali ya Gabi lakini hakukuta kitu chochote,aliendelea kupekua na kukuta fedha zilizokuwa kwenye droo iliyounganikana na kitanda,alizichukua na bila kuhesahu alizitia mfukoni kisha akatoka nje kupitia pale pale dirishani.Mara nyingi ndo zilikuwa kazi za yule kijana hasa kwenye ile nyumba ambayo madirisha yake hayakuwa na nondo,aliwaibia watu mbali mbali na mara nyingi alikuwa anakaa pale stendi kusubiri watu watakao kuja eneo lile wakiwa hawana ndugu,siku ile alichekelea moyoni alikuwa anadaiwa kodi hivyo siku ile alipata hela ya kulipa.

****

Majira ya saa nne asubuhi Layla alishtuka usingizi na kukuta ameloana kutokana na jasho lililokuwa mle ndani,alimwamsha Gabi na kuangalia saa iliyokuwa pale,

"Saa nne mmmh ulalaji gani huu"alisema Layla haikuwa kawaida yake kulala vile lakini Gabi alimwambia huenda ule ni uchovu wa safari,

"Mbona pesa sizioni hapa?"aliuliza Gabi kwashangao,

"Kwani uliziweka wapi"

"Si hapo juu ya droo au ulizihamisha?Gabi aliuliza lakini alipogeuza shingo yake kutazama dirishani alishangaa kuona kuwa uwazi huku wavu uliokuwa pale ukiwa umechanwa,

"Tumeibiwa tayari"aliongea Gabi Layla alibaki kutazam na kukumbuka maneno aliyowahi kuyasikia siku za nyuma kuwa mjini shule,

"Nini?Sasa kama wameiba hela zote tutaishije?"aliuliza Layla huku machozi yakianza kumtoka.Hata Gabi naye chozi lilimtoka,alibaki kutafakari maisha yatakuwa vipi jijini hapo ikiwa pesa waliyoitegemea kama mtaji imeibiwa tayari,walifarijiana kuwa huenda ni mungu kawaepushia jambo ndo maana karuhusu pesa zao kuibiwa.Layla alifungua begi lake na kukuta pesa iliyokuwemo ni elfu moja na mia mbili,

"Hatuwezi kufa njaa ilihali tunazo nguvu za kufanya kazi,hakuna namna kesho ni kuingia barabarani kuwa omba omba"aliongea Layla,ile elfu moja na mia mbili Gabi alitoka na kwenda kununua vitumbua kwenye mgahawa uliokuwa jirani na hapo lakini macho yake yaligongana na bango lilikuwa limebandikwa kwenye nguzo za umeme lilikuwa kubwa lakini alipolitazama vizuri aliiona picha ya Layla huku kwa chini yake kukiwa na maneno kuwa huyo mtu anatafutwa na jeshi la police.Alibaki kulikodolea macho huku moyoni akijisemea kuwa tayari wako hatarini,alinunua vitumbua na kurudi,alimkuta Layla akiwa kwenye hali ya majonzi,

"Asee tayari tupo kwenye hatari kubwa"aliongea Gabi kabla hata hajaketi,

"Hatari gani tena mbona unaniogopesha"aliuliza Layla kwa shauku,

"Picha yako imezagaa mitaani yaani unatafutwa na jeshi la police"Layla alishtuka sana kusikia maneno yale sasa aliiona hali ya hatari mbele yake,pia alijua kuwa kama yeye atakamatwa basi na Gabi atakuwa na kesi ya kuoa mwanafunzi jambo ambalo hakutaka litokee,

"Hakuna wa kukamatwa hapo'alisema Layla kwa kujiamini,

"Unamaana gani hii ni kesi tayari kama tukikamatwa"aliongea Gabi lakini Layla alimtaka wale vile vitumbua kwanza ili akili zifanye kazi vizuri,

"Nina wazo moja hapa ambalo litatusaidia"aliongea Layla, Gabi alikaa tayari kumsikiliza mara baada ya kuwa wameshiba,

"Usione watu waliochakaa hapa mjini ukasema ni machizi la hasha,hakuna chizi labda ni maisha yao kuwa magumu na usitegemee kwenda kuomba barabarani ukiwa umevalia nguo safi,jifanye chizi mwisho wa siku upate unachokitegemea,naomba tupumzike kwa siku ya leo kesho tutaamkia mzigoni"aliongea Layla kwa ujasiri,Gabi alijikuta akitoa tabasamu aliposikia maneno yake,

"Hakika wewe ni jasiri"aliongea Gabi na kumkumbatia Layla,siku ile walishinda ndani wakiongea maneno ya kutiana moyo.

Asubuhi ya siku ile waliamka asubuhi huku wakichana chana mavazi yao na kuyaloweka kwenye matope kisha kila mmoja alivaa na kubadili muonekano kabisa,walipokuwa tayari Gabi alitaka kuufungua mlango kutoka nje lakini Layla alimwambia bado asubiri,

"Layla alitoka nje na kwenda kuchota majivu kisha akayakoroga na kuanza kumpaka usoni Gabi naye alipoona vile alimpaka Layla hakuna mtu angeweza kuwagundua,

"Umeona sasa hii ndo maana harisi ya mjini shule,kuhusu kubadili mavazi tutakuwa tunayabadili usiku tukitoka kazini"aliongea Layla na kufungua mlango kisha wakatoka nje na kujifanya hawajuani hivyo kila mtu alielekea njia yake na kuhaidiana kukutana usiku,

"Usiende mbali usije kupotea kwenye hili jiji,kazi njema mpenzi"aliongea Layla na kila mmoja akielekea njia yake.Gabi alielekea Mawasiliano na kwenda mpaka stend ya Ubungo ndani,alizunguka sana siku ile hadi inafika jioni alikuwa na shilingi mia nane huku Layla akiwa amepata elfu moja na miatano.Wote walifurahi hivyo hiyo ndo ikawa kazi yao,kila walipokuwa wanataka kwenda kwenye ile kazi yao ilikuwa lazima wajipake majivu ili wasijulikane,mabango pia waliendelea kuyaona lakini kila mtu alikuwa anajifanya mwendawazimu huku mavazi yakiwa yametobo toboka,

"Mpenzi ujue hii kazi tukishaizoea lazima itatupa pesa nyingi mhimu kuweka akiba hata tukipata elfu moja lazima mia tano tuiweke kama akiba"aliongea Layla akiwa na Gabi wanakula mandazi na maji.Sasa walikuwa wenyeji tayari wa jiji hivyo walipanga kuanza kuzunguka sehemu nyingi huyu akienda Buguruni huyu anaenda mpaka Mbezi kwa usafiri wa kuunga unga.

***

Ilikuwa siku ya juma tatu siku hiyo hadi inafika saa mbili kamili usiku Layla alikuwa hajarejea nyumbani na haikuwa kawaida yake,Gabi aliingiwa na wasiwasi mkubwa hakujua pa kumpatia usiku ule.Aliwaza akawazua alikumbuka kuwa siku ile Layla alimuaga kuwa anaenda Mbezi na kabla ya saa kumi alisema atakuwa tayari asharejea lakini mpaka mda huo saa tatu usiku hakuwa amerudi.Kupitia sasa yake ndogo iliyokuwa mle ndani aliangalia nakukuta ni saa tatu dakika kumi na saba usiku lakini Layla alikuwa bado hajarudi...



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

BLOG