Search This Blog

Sunday, April 18, 2021

KITUMBUA CHA KIHINDI - 1

  


IMEANDIKWA NA : KIZARO MWAKOBA

*********************************************************************************

Chombezo : Kitumbua Cha Kihindi

Sehemu Ya Kwanza (1)


Ilikuwa ni majira ya saa sita za mchana, joto likiwa kali kama ilivyo kawaida katika jiji la Dar Es Salaam. MAGOSHO kijana wa marehemu Mzee Machaku alikuwa jikoni akitayarisha chakula cha mchana kwenye nyumba ya mhindi NAKESHWAR alipokuwa akifanya kibarua cha kazi za ndani.

Bi. Fahreen ambaye alikuwa ni mke wa Nakeshiwar alifungua mlango wa jikoni taratiibu na kumkuta kijana akishughulika kazi zake za kila siku.

Bi. Fahreen alisimama mlangoni pale na kumtazama Magosho kwa jicho la tathmini na udadisi mkubwa. Aliweza kuona mgongo wa kijana yule uliokuwa umetuna kidogo pengine ni kutokana na mazoezi ya viungo ukiwa ndani ya fulana ya mikono mifupi iliyoacha misuli ya mikono yake iliyokuwa imejazia kiasi kuonekana na mwanamke yule. Bi Fahreen aliendelea kumchambua kijana yule kwa kumteremsha hadi miguuni na kuona misuli ya miguu ile ilivyosimama ipasavyo utafikiri mafungu ya magimbi.

Magosho alikuwa bize na kazi yake pasipo kufahamu kama nyuma yake kulikuwa na mtu akimchunguza.

Bi. Fahreen alimsogelea taratibu Magosho na kusimama nyuma yake. Alimeza funda kubwa la mate na kutoa pumzi ndefu. Umbile la kijana yule lilikuwa limevutia na kumkosha ndani ya mtima wake. Alitamani kupata japo nafasi ya kumkumbatia tu pengine nafsi yake ingeridhika.

Akanyanyua mkono wake wa kushoto na kuupeleka sehemu za kiunoni kwa Magosho taratibu huku akisita sita. Alihofia sana endapo kijana yule asingemuelewa angeiweka wapi sura yake. Hata hivyo alijipa moyo na peleka mkono wake kwenye kiuno kile. Alipomgusa tu Magosho alishituka kwa nguvu na kugeuka nyuma huku akitoa sauti ya mshituko.

“Hee! Kumbe veve iko oga sana?” alihoji Bi. Fahreen kwa rafudhi yake ya kihindi huku akijichekesha chekesha kinafki mbele ya kijana yule.

“Ah! Mama kumbe ni wewe!” alisema Magosho huku akishindwa kutafakari kitendo kile alichafanyiwa na bosi wake wa kike.

“Mimi iko toa dudu veve kwenye nguo yako. kwani Iko baya?” alihoji Bi. Fahreen akijibaraguza.

“Ahaa! Nashukuru mama hakuna ubaya” alijibu Magosho na kugeuka kuendelea na upishi.

Kitendo cha Magosho kuruka kama vile alikuwa amepigwa na shoti kilileta msisimko zaidi kwenye mwili wa Bi. Fahreen. Yani mwanamke yule alikuwa kama vile amepandwa na pepo gani sijui katika ubongo wake. Alikuwa hajielewi wala hajitambui kwa kila ambacho alikuwa anakifanya kwa wakati ule. Aliinua mkono wake na kuuweka kwenye bega la Magosho.

“Vipi Chakula bado iva?” akajifanya kuhoji huku mkono wake ukiwa bado kwenye bega la Magosho akimtekenya tekenya kwa vidole vyake.

“Namalizia mama” Magosho alijibu huku akihisi msisimko ndani ya mishipa yake ya damu. Alitamani kumwambia mke wa bosi wake atoe mkono kwasababu alikokuwa akielekea kulikuwa siko.

Mama yule wa kihindi aliendelea kuuchezesha mkono wake pale kwenye bega la watu bila huruma. Akapeleka mkono wake wa kulia kwenye kiuno cha kijana yule na kuendelea kufanya utundu wake.

Magosho ambaye alikuwa akikoroga jikoni alijikuta akishindwa kuendelea na kazi. Akainua macho juu kusikilizia hali fulani iliyosababishwa na vidole vya Bi.Fahreen kwenye kiuno chake. Alimgeukia mama yule na kumkuta amelegeza macho kama vile alikuwa amekunywa supu ya bamia.

Bi.Fahreen akatumia mikono yake kuvuta kichwa cha Magosho hadi usawa wa kifua chake. Ufupi wa Magosho ulipelekea nywele zake ndefu za kibantu kumchoma choma mama yule kwenye madafu yake mawili ya kifuani na kupelekea msisimko mkubwa.

Magosho alianza kupoteza uvumilivu na kuuma memo yake kwa nguvu huku amefumba macho na akisikilizia mapigo ya moyo wake yalivyokuwa yakienda mbio.

Baada ya mwanamke yule wa kihindi kuzidisha vituko, kijana Magosho akajikuta akizunguusha mikono yake na kuanza kuchezea furushi la mama wa wawatu ambalo lilikuwa likimfanya kuonekana tofauti na wahindi wengine. Kiukweli Bi. Fahreen alikuwa ameumbwa na kuumbika utafikiri mwanamke wa kibantu. Kuanzia juu alikuwa na umbo la kawaida lakini kuanzia chini ya kiuno chake chembamba kulikuwa na hipsi zilizotanuka kiasi cha kuwa na uwezo wa kutosha kubeba furushi kubwa lililokuwa nyuma.

Umbo lile adimu lilifanya mama yule kuonekana mnene kama ungemtazama kuanzia chini. Lakini pia ungemuona ni mwanamke mwembamba kama ungemtazama kuanzia juu na kuishia kitovuni. Jamani! Wacheni Mungu aitwe Mungu. Kuna watu wameumbwa nyie, Mnh!

*****

Magosho alikuwa ni mtoto wa mama Ashura ambaye alikuwa hohe hahe asiye na mbele wala nyuma. Mama huyo alikuwa akiwapenda sana watoto wake waliokuwa wawili tu kama mboni za macho yake. Halkadhalika Magosho na dada yake Ashura walikuwa wakimpenda sana mama yao kuliko kitu kingine chochote.

Asubuhi Magosho akiwa amelala juu ya kitanda cha teremka tukaze kilichokuwa kimepambwa kwa ukili chakavu ulioashiria kutengenezwa muda mrefu uliopita. Macho yake yalikuwa juu ya paaa lililo kuwa na tundu kubwa lililopitisha mwanga wa jua la asubuhi kwa kiasi fulani uliopelekea nuru kiasi ndani ya chumba kile kidogo kilichokuwa na kiza kutokana na na udogo wa madirisha yake.

Harufu mbaya iliyokuwa ikizalishwa na mfereji wa maji machafu uliopita usawa wa dirisha lake ilipenya ipasavyo kwenye tundu za pua yake na kusafiri hadi kwenye vifuko vya kuzalishia mate na kusababisha funda kubwa la mate kujaa mdomoni. Aliyatema chini na kuyafukia kwa mguu wake wa kushoto kwa urahisi kutokana na vumbi lililokuwa mle ndani ya chumba chake kilichokosa sakafu.

Sauti ya nzi mkubwa aliyekuwa na rangi ya kijani ambaye aliingilia kwa kupitia kwenye tundu la paa ilimgutusha. Nzi yule aliruka hapa na kutua pale mle chumbani. Magosho alijiinua kwa hasira na kuanza kumputa kwa kipande cha mti wa ufagio alichokitoa uvunguni.

Purukushani zile ziliendelea kwasababu kila alipojaribu kumpiga nzi yule aliruka na kwenda kutua sehemu nyingine. Alipotua juu ya mfuniko wa ndoo ya plastiki alimnyatia na kuinyanyua fimbo juu na kuitua kwanguvu juu ya ndoo ile iliyotoa sauti kubwa ‘Paaa’. Hata hivyo nzi aliruka na kutoka nje kupitia dirishani. Akamtazama kwa hasira na kutoa msonyo mrefu.

Sauti ya kicheko ilimgutusha na kumfanya kutupa macho mlangoni. Kumbe muda wote alipokuwa akifukuzana na nzi yule mdogowake Ashura alikuwa amesimama mlangoni akimtazama huku akicheka kwa kuziba mdomo kwa mikono. Tukio la kupiga kwenye ndoo kwa nguvu halafu akamkosa adui yake ndilo lilimfanya binti yule kuangua kicheko cha sauti. Ayubu alijikuta akifadhaika kwa kile alichokuwa akikifanya kuonekana na mtu mwingine.

"Unacheka nini?" Magosho alihoji.

"Hujui?" alihoji Ashura huku akiendelea kucheka.

"Dogo usinichanganye" Magosho alijifanya kukasirika.

"Dah! ila we mkali Broo. Yaani umempiga…..kahepa, ukampa tena…. kahepa, Ukavuta tena kwanguvu akakwepa, uka...." Ashura alikatishwa kauli yake na Magosho.

"Ashura ondoka" alisema Magosho kwa hasira.

"Dah! utadhania mchina vile jinsi ulivyokuwa ukipambana. Huuu haaa!...huuu!...haaa!" alisema Ashura huku akimuiga kaka yake alivyokuwa anampiga nzi.

"Ashura ntakutwanga ukaseme kwa mama yako" alisema Magosho huku akimsogelea mdogo wake Ashura taratibu.

"Thubutuuu! umemshindwa nzi utaniweza mie?" Ashura alizungumza kwa uchokozi huku akitabasamu kwa furaha. Alikunja ngumi na kumnyooshea kaka yake.

"Haya njoo sasa....njoo" alisema huku akirudi nyuma. Magosho akainua mti ule wa fagio na kutaka kumpiga nao. Ashura akatimua mbio kutoka nje huku akimcheka kaka yake.

Magosho alikuwa akipendana sana na dada yake Ashura ambaye alikuwa ni wa pekee. Ingawa walikuwa wamepishana sana kiumri lakini walikuwa wamezoea kutaniana na kufurahi kwa pamoja. Kutokana na sababu hiyo ndiyo maana Ashura hakuhofia kumtania kaka yake kwa kile kilichotokea. Pale Magosho alipochukua ufagio hakuwa na lengo la kumpiga mdogo wake bali alimtishia tu na alifahamu kuwa angekimbia.

Baada ya dakika kadhaa Magosho alitoka chumbani kwake na kumkuta mama yake pamoja na Ashura wakikaanga mihogo ya biashara.

"Wakuonja basi jamani" alisema Magosho kwa utani

"Lete hela hakuna cha bure hapa" alijibu Ashura huku akikata muhogo mbichi na kuumenya.

"Nawewe nini? Hebu kwenda huko" alisema Magosho huku akiinama na kuokota kipande cha muhogo kilichokwisha kaangwa.

"Chukua chai kabisa unywe" alisema mama Ashura huku akigeuza mihogo kwenye karai lililokuwa limeinjikwa jikoni.

"hapana mama nikinywa chai nitachelewa. Huu muhogo unatosha" alisema Magosho.

"Kwahiyo leo unakwenda kuhangaikia wapi?" Mama Ashura alihoji.

"Nakwenda mjini labda leo naweza kubahatika"

"Sawa ila uwe makini mwanangu" alisema mama Ashura kwa msisitizo.

"Sawa mama usijali" alijibu Magosho huku akivuta hatua kuondoka.

"Nzi huyo nyuma yako…" Ashura alipaza sauti kumtania kaka yake akimkumbushia tukio la kumpiga nzi chumbani kwake.

"We subiri nikirudi ndo utanitambua" alisema Magosho pasipo kugeuka nyuma na kutoweka machoni mwa Ashura na mama yake.

***

Safari ya Magosho ilikuwa ni ya mjini Kariakoo ingawa hakufahamu ni sehemu gani ambapo alilenga kufika. Lengo lake lilikuwa ni kwenda kutafuta ajira ili aweze kulea familia yake iliyokuwa na maisha magumu hasa baada ya kufariki kwa baba yao mpendwa mzee Machaku kwa ugonjwa wa malaria. Ingawa hawakuwa na maisha mazuri kipindi cha uhai wa baba yao huyo lakini kwa kiasi fulani maisha hayakuwa ya taabu kama wakati ule waliokuwa nao.

Magosho Alipofika mjini alianza kuzunguuka kwenye mitaa ya kariakoo. Alipinda kushoto na kukamata barabara ya vumbi. Alitembea kwa mwendo mrefu huku akisoma vibao vya mashirika mbalimbali barabarani. Mungu hamtupi mja wake, macho yake yalitua kwenye bango moja kubwa lililoandikwa kuwa walikuwa wanahitajika wafanyakazi hata kwa wale wasio kuwa na elimu kubwa yaani walioishia darasa la saba. Magosho akavuta pumzi na kuzitoa kwa nguvu akiwa haamini macho yake. Ajira zile zilikuwa zikitolewa kwenye kiwanda cha kusindika maplastiki.

Alifuata njia ambayo mshale uliokuwa umechorwa kwenye bango lile ulimuelekeza na kwenda kutokea nje ya jengo kubwa la ghorofa. Alipofika getini alimkuta mlinzi kama ilivyo mila na desturi ya makampuni mbalimbali.

“Habari yako afande” Magosho alianza na kumsalimia.

“Jambo ndugu” afande yule akasalimia badala ya kujibu salamu.

“Sijambo, nimeona tangazo la ajira. Sijui utaratibu upoje?” alihoji Magosho.

“Ahaa! Ni kweli. Sasa unatakiwa kusaini kwanza hapa. Gharama yake buku mbili” alisema afande yule huku akimfunulia daftari.

Magosho akakumbuka kuwa mfukoni mwake kulikuwa kumesalia shilingi elfu mbili tu. Inamaana kama angetoa buku mbili ile basi angerudi kwa miguu kwasababu angekosa hata nauli.

“Yaani broo hapa unaponiona nina buku tu mfukoni” Alisema Magosho kwa sauti ya kubembeleza.

“Sasa unadhani tutafanyaje?”

“Naomba nisaidie ndugu yangu”

“Siwezi, kama huna pesa we ondoka tu” alisema afande huku akifunga daftari lake.



“Ahaa! Ni kweli. Sasa unatakiwa kusaini kwanza hapa. Gharama yake buku mbili” alisema afande yule huku akimfunulia daftari.

Magosho akakumbuka kuwa mfukoni mwake kulikuwa kumesalia shilingi elfu mbili tu. Inamaana kama angetoa buku mbili ile basi angerudi kwa miguu kwasababu angekosa hata nauli.

“Yaani broo hapa unaponiona nina buku tu mfukoni” Alisema Magosho kwa sauti ya kubembeleza.

“Sasa unadhani tutafanyaje?”

“Naomba nisaidie ndugu yangu”

“Siwezi, kama huna pesa we ondoka tu” alisema afande huku akifunga daftari lake.


ENDELEA…2

Magosho akapata wazo la kuondoka halafu arejee baadaye akiwa na uamuzi sahihi. Alihofia kukurupukia maamuzi halafu baadae kuambulia majuto.

“Aroo we Mujamaa” Afande alimuita Magosho wakati alipokuwa akiondoka.

Magosho akageuka nyuma kumuangalia. Askari yule alimuoneshea ishara ya kumuita kwa kutumia kirungu chake. Magosho akarejea kwa mwendo wa kujivuta akiamini askari yule alikuwa akimsumbua bure.

“Lete hilo buku lako” alisema mgambo yule huku akifungua daftari amabalo mwanzo alilifunga baada ya kutajiwa shilingi elfu moja. Magosho alipotoa ile pesa alimkabidhi lakini mgambo yule alikataa kuipokea na kumwambia aiweke juu ya daftari.

Kitendo kile kilimfanya Magosho kubaini kuwa kumbe mchango aliokuwa akiutaka askari yule ulikuwa ni kinyume na sheria. Ilimbidi atoe tu, sasa angefanya nini wakati yeye ndiye mwenye shida. Baada ya kutoa pesa alisaini kwenye daftari lile na kuelekea mapokezi.

Alipofika aliwakuta vijana wengine wamekaa kwenye foleni wakisubiri kufanyiwa usaili, na yeye akajiunga nao. Ulifika muda ambao aliitwa ndani kwenda kuonana na wahusika, yaani waajiri wenyewe. Alipoingia aliwakuta watu watatu wanaume wawili na mwanamke mmoja. Baada ya kuwasalimia walimuelekeza mahali pa kuketi.

“Karibu kijana” alisema mmoja wa wahusika wale.

“Asante sana” Magosho alijibu kwa unyenyekevu.

“Unatokea wapi?”

“Mbagala”

“Elimu yako?” mwanamke yule alihoji swali ambalo lilikuwa ni adui kwa Magosho. Hakupenda kulisikia katika masikio yake na ndilo lililomfanya kukosa ajira kwenye ofisi nyingi sana. Lakini hata kama alikuwa halipendi swali lile lakini ndio alikuwa amekwisha ulizwa hivyo hakuwa na namna zaidi ya kulijibu. Sasa shughuli ikaja ajibu nini? na kama angesema ameishia elimu ya msingi kungekuwepo na uwezekano wa kupoteza nafasi ingawa walikuwa wanaajiriwa hata wale wasio na elimu kubwa.

“Nimesoma hadi kidato cha nne” alijikuta akitamka.

“Umekuja na uthibitisho?” alihoji yule mama.

Siku ya kufa nyani miti yote hutereza, akashangaa sababu ya watu wale kumuuliza masuala ya elimu wakati kwenye matangazo yao wamesema wanawaajiri hata wale wasio na elimu. “Mnh hii sasa kali” akajisemea kimoyomoyo.

“Sikuja na uthibitisho wowote” akajikuta akiwajibu pasipo kujielewa.

“Ok usijali, hilo sio tatizo. Kama unahitaji ajira basi tutakuajiri” alidakia jamaa mmoja aliyekuwa pamoja na yule mama mle ndani.

“Labda tuambie kama kweli unahitaji kazi” alisema mtu mmoja.

“Nahitaji na ndiyomaana nipo hapa” Magosho akajibu kwa kujiamini.

“Sasa sisi tutajuaje kama kweli unahitaji ajira?” yule mwanamke akatupa swali.

“Kuja kwangu hapa inatosha ninyi muamini”

“Hilo halitoshi. Hebu thibitisha kauli yako”

“Amini nawaambia nahitaji kazi”

“Sikiliza kijana. Kwaufupi ni kwamba mkono mtupu haurambwi” alisema yule mama huku akijifanya yuko bize na kuandika andika vitu alivyokuwa anavifahamu yeye.

“Bado sijaelewa” Magosho alizungumza kwa mshangao.

“Kazi zipo kijana lakini kalamu ya kuandikia jina lako imekwisha wino” alisema mama yule huku akiendelea kuandika andika.

Magosho akatafakari kauli ile kwa umakini. Mtu anasema kalamu imekwisha wino inakuwaje anaendelea kuandika?.. Jibu alilolipata pale ni kwamba alikuwa anatakiwa kutoa chochote kitu. Wakati akiendelea kutafakari kauli ile sauti ya mwanaume ikamgutusha.

“Hata kama ukipata hamsini inaweza kutosha”

“Hamsini nini?” alihoji Magosho kwa mshangao.

“Alloo ajira hakuna naona unatuzunguusha” alisema jamaa kwa hasira.

“Ngoja kwanza Ngosha, Kijana nenda ukajipange halafu ukiwa tayari siku yoyote uje” yule jamaa mwingine alizungumza kwa sauti ya upole.

Kwakuwa Magosho alikwisha tambua ni kitu gani kilichokuwa kikitakiwa pale na hakuwa na uwezo wa kukipata alijiinua kwenye kiti na kutoka nje. Alikuwa amechoka kuliko maelezo. Hakuwa na namna zaidi ya kurejea nyumbani.

*****

Magosho alipofika nyumbani alikwenda moja kwa moja chumbani kwake pasipo kupitia kwa ndugu yake kumjulia hali. Akajitupa kitandani kwa nguvu kutokana na uchovu, kitanda nacho kikaitikia “Rabeka”. Kilikuwa kimevunjika kutokana na kushindwa kuhimili kile kishindo cha Magosho.

Ashura alishituka baada ya kusikia sauti ya kitu kikianguka chumbani kwa kaka yake. Alichokuwa akikifahamu yeye ni kwamba kaka yake huyo hakuwepo. Alifungua mlango na kuchungulia ndani. Alimkuta kaka yake amelala huku kitanda kikiwa kimevunjika.

“He kumbe umerudi?” alihoji Ashura kwa mshangao.

“Ndio nimeingia sasa hivi” alijibu Magosho huku akijizoa zoa kutoka pale chini.

“Kwahiyo ndio ukaamua kuvunja kitanda?”

“Ah! Nimechoka bwana”

“Sasa ukichoka ndio unavunja kitanda?”

“Bahati mbaya” Magosho alijibu kwa upole.

“Mavi yenyewe uharo halafu unayatia maji. Sasa utalala wapi?”

“Nitakitengeneza bwana!” Magosho alijibu kwa hasira kidogo, inaonekana hakupendezwa na maswali ya ndugu yake.

“Au ndio ulikuwa unapigana na yule nzi?” Ashura alihoji huku akicheka.

“Hebu ondoka Ashura, usinichanganye”

“Kweli nini! Mbona umekasirika?” Ashura alizidi kumtania kaka yake ambaye alikuwa ametawaliwa na uchovu pamoja pamoja na mawazo yaliyo changanyikana na hasira. Alichukua tena mti wa ufagio na kumkimbiza mdogo wake huku akimtishia kumtandika. Ashura akiwa mbele na yeye nyuma hadi kwa mama yao ambaye alikuwa amejipumzisha kwenye mkeka barazani.

“Mamaaa…mamaaa….mamaaa” Ashura alikuwa akikimbia huku akipiga kelele.

Mama Ashura alishituka kutoka usingizini. Masikini kumbe alikuwa hajisikii vizuri kiafya.

“ Mama mwanao nitampiga huyu” alisema Magosho huku akisogea hadi pale alipokuwa amelala mama yake.

“Vipi mama mbona umelala saa hizi unaumwa?” alihoji Magosho kwa sauti iliyojaa upendo na wasiwasi.

“Afadhali umerudi mwanangu” alisema mama Ashura kwa sauti ya chini.

“Una nini mama?”

“Vipi kwanza huko mjini, umefanikiwa?”

“Hakuna kitu mama, tatizo pesa. Kila mahali wanataka rushwa, yaani rushwa, rushwa inanuka” alisema Magosho kwa sauti kavu iliyokata tama

“Usikate tamaa mwanangu, mtafutaji hachoki” mama Ashura alizungumza kwa sauti ya chini isiyo ya kawaida.

“Vipi lakini mama unaonekana haupo sawa” alihoji Magosho.

“Nahisi kuumwa viungo vyote, Ila mgongo na kiuno ndio vinaniuma zaidi” alisema mama Ashura huku akijipepea kwa upande wa kitenge kutokana na joto la jijini Dar Es Salaam.

“Sasa umekunywa dawa?”

“Nimekunywa panadol, nenda kwa mama Mbingu akakupe mzizi wa muarobaini nije kuchemsha” alisema mama Ashura.

Wakati Magosho alipokwenda kuchukua dawa hiyo ya muarobaini huku nyuma hali ya mama Ashura ilibadilika na kuwa mbaya zaidi.

Ashura alimfuata kaka yake na kumfahamisha hali halisi. Magosho pamoja na mama Mbingu wakaongozana hadi kwa mama Ashura. Kwa kweli hali waliyoikuta pale haikuwa ya kuridhisha hata kidogo.

“Nyie watoto mnahatari!... mama yenu anaumwa hivi mmemuweka tu ndani” alisema mama Mbingu kwa mshangao baada ya kuona hali ya mama mwenzie.

“Hali yake haikuwa hivi, amezidiwa sasahivi nilivyokuja kwako” aliizungumza Magosho.

“Haya tumpelekeni kwa Mzee Kutuzo haraka sana” alisema mama Mbingu na pasipo kuchelewa walimchukua na kumpeleka kwa mzee Kutuzo ambaye alikuwa ni mganga wa kienyeji.

*****

Baada ya kufika kwa mganga kwanza kabisa alitoa dawa kama huduma ya kwanza. Kwa kiasi fulani dawa ile aliyompa ilionekana kufanya kazi kwani mama Ashura alianza kupata ahuweni. Jambo ambalo lilileta matumaini kwa watoto wake pamoja na mama Mbingu.

Baada ya kutoa huduma ile mganga alianza mbwembwe zake za jadi na kupandisha maruhani. Lengo kubwa lilikuwa ni kutaka kuufanyia uchunguzi mwili wa mama Ashura ili apate matibabu yaliyo sahihi.

Jini alipanda na kuanza kuzungumza lugha ngeni kwenye masikio ya wateja wake. Aliendelea kutabana huku akiwa ameshikilia kipande cha kioo kilichokuwa kimefungwa fungwa vitambaa vilivyokuwa na rangi tatu, yaani nyeupe nyeusi na nyekundu. Mganga alikuwa akipiga mbweo mithili ya mtu aliyekuwa ameshiba sana. Watu wote walikuwa kimya wakimsikiliza mganga.

“Mgonjwa anaitwa nani” alihoji mganga Kutuzo.

“Mama Ashura” alijibu mama Mbingu.

“Jina lake la utotoni?”

“Mainaya” alijibu Magosho.

Mganga aliendelea kuzungumza maneno yake ya kiganga huku akitaja jina la Mainaya mara kwa mara. Baada ya sekunde kadhaa alitupa kile kioo na yeye akadondoka chini na kuanza kuunguruma kama mbwa.

Hali ile iliwashangaza sana wakina Magosho na wenzake. Hawakufahamu wafanye nini lakini mama mbingu ambaye alionekana kuwa mzoefu wa mambo yale akawaambia watulie.

Mganga alilala pale chini kwa dakika kadhaa halafu akainuka. Alichukua upembe mkumbwa wa mnyama uliokuwa umefungwa kitambaa cheusi na kuanza kumzunguushia nao mama Ashura. Alifanya zoezi lile mara kadhaa halafu akaokota kibuyu kilichokuwa na shanga kwenye shingo yake na kutoa dawa ambayo alimpaka mama Ashura usoni kisha akarudi kukaa kwenye kiti chake. Akaokota kile kioo chake na kukipiga piga kwa usinga wake mara kadhaa huku akikichungulia chungulia.

“Niseme nisiseme” alizungumza mganga yule kwa sauti nzito

“Sema mganga” alijibu mama Mbingu.

“Mainaya ametupiwa Jini ” alisema mganga huku akichungulia kioo chake.

“Mungu wangu!” alihamaki mama Mbingu.

“Jini?” Magosho akahoji kwa mshangao.

“Ndio tena Jini maiti” mganga alizidi kufafanua.

Magosho, Ashura pamoja na mama Mbingu wakawa wanatazamana wasijue cha kuzungumza. Mganga akavunja ukimya ule.

“Zaidi ya hayo Kuna vitu amelishwa ambavyo sio vizuri” mganga alizidi kuleta changamoto hasa kwa watoto wa mgonjwa.



“Kwahiyo itakuwaje mtaalamu?” Magosho akahoji.

“Tutaanza na kumtapisha hivyo vitu, halafu baadaye tutamtoa huyo jini maiti” alisema mganga kisha akachukua kikapu kilichokuwa na unga mweupe wa mahindi akakiweka pale karibu na mgonjwa. Akamgeukia Magosho na kumwambia achote kiasi fulani cha unga ule na kuuweka kwenye ungo ambao ulikuwa hauna kitu ndani yake. Magosho akafanya kama alivyokuwa ameagizwa na mganga yule. Na baada ya hapo mganga akamwambia Magosho achangue unga ule kuangalia kama kulikuwa na kitu ndani yake. Baada ya Magosho kufanya vile akabaini kuwa kwenye ungo ule hapakuwepo na kitu chochote zaidi ya ule unga aliouweka.

Mganga Kutuzo akachukua dawa kutoka kwenye kibuyu chake kikubwa na kuichanganya na ule unga, akachukua ungo mwingine na kumwambia Magosho afunike ule ungo uliokuwa na unga. Baada ya kitendo kile akachukua mapembe mawili ya mmnyama na kuyaweka juu ya ule ungo. Ukapita muda wa dakika kama tano ambazo mganga alizitumia kuzungumza maneno ya kiganga.

Magosho akaambiwa afunue ungo ule ili kutazama ndani yake kulikuwa na nini. Hakuna kilichoonekena zaidi ya ule unga. Mganga akamwambia Magosho achakue unga uliokuwemo kwenye ungo.

Loo! Magosho alishituka sana baada ya kugusa vitu fulani kwenye unga ule. Lilikuwa ni jambo la kushangaza sana. Vidole viwili vya mkono wa binadamu vilikuwa vimefungwa pamoja na sindano saba za kushonea nguo kwa mkono. Pia kulikuwa na nywele nyeupe ndefu, viwembe saba, kitovu cha mtoto mchanga, pamoja na hirizi ndogo iliyokuwa imefungwa kwa kitambaa cheusi. Vitu hivyo vyote vilikuwa vimefungwa pamoja. Vilikuwa vikitoa harufu mbaya sana.

“Vitu hivi ndivyo vilivyokuwa vinamletea maumivu makali ya mgongo na kuiuno” alisema mganga huku akivifungua vitu vile ambavyo yeye aliviita uchawi. Aliwahakikishia kuwa baada ya tiba ile mama yao asinge lalamika tena kuugua maradhi kama yale.

Mganga akaeleza kuwa sababu ya wachawi kumroga mama yule ni wivu kwasababu mama Ashura alikuwa ni mtu wa kujishughulisha na biashara za kukaanga mihogo na vitumbua, hivyo wakaona anapata sana ndiyomaana wakaamua kumkomesha. Akamalizia kwa kusema kuwa uchawi ule ulitokana na kushirikiana wanaume wawili na mwanamke mmoja.

“Nitawapa dawa ambazo mgonjwa wenu atazitumia, lakini ni lazima tumtoe jini aliyekuwa naye. Ni hatari sana.” Alisema mganga Kutuzo.

“Tawile mganga” mama Mbingu akajibu.

“Sasa ili kumtoa jini huyu kunatakiwa maji ya bahari lita tatu, shuka nyeupe mbili, kaniki tatu, na kitambaa chekundu mita tatu, mchele kilo saba, kisu ambacho hakijawahi kutumika, na mbuzi wawili yaani mweusi na mweupe.” Alimaliza mganga na kumuangalia Magosho ambaye alikuwa akiandika yale maada wakati anayataja.

Kiukweli gharama ya vitu vile ilimchosha Magosho na kupoteza matumaini ya kuvipata. Hata hivyo hakukata tamaa na kumaliza kuandika vitu vyote. Wakakubaliana na mganga kwamba wangerejea mara tu ya kupatikana vitu vile vilivyokuwa vikitakiwa.

*****

Kuugua kwa mama Ashura kulimuumiza sana Magosho kwasababu ni yeye aliyekuwa akitegemewa kwa kiasi kikubwa pale nyumbani. Hakuwa na namna nyingine zaidi ya kupambana kiume. Kwakuwa hali ya mama Ashura haikuwa nzuri ilibidi Ashura ajihusishe na shughuli za kibiashara. Yeye ndiye aliyekuwa akichoma vitumbua na kukaanga mihogo kwa ajili ya biashara. Hata hivyo biashara iliyumba kidogo kwasababu alitakiwa kumhudumia mama yake wakati huo huo..

Magosho alikuwa akitoka na kwenda mjini kuhangaika kufanya vibarua na kupata visenti japo vichache lakini vilisaidia kuendesha maisha ya pale nyumbani kwao. Dawa alizokuwa akizitumia mama Ashura zilionekana kumsaidia kwa kiasi fulani.

Siku zilivyo sogea hali ya mama Ashura ilibadilika tena na kuwa mbaya zaidi. Hadi kufikia kipindi kile watoto wake hawakuwa wamepata fedha za kutosha kuweza kumtibia. Hapakuwepo na namna nyingine ya kufanya zaidi ya kuuza vitu vya ndani pamoja na nguo zao ili kuweza kupata pesa. Baada ya kuona wamepata pesa za kununulia vifaa vya matibabu wakampeleka mama yao kwa mganga Kutuzo.

Mganga alimtibia mama Ashura kwa takribani siku saba mfurulizo lakini hali ya mama yule haikutengemaa na badala yake ikazidi kuwa mbaya. Aliwapatia dawa za kunywa , kufukiza , na nyingine za kukoga. Hata hivyo hazikumsaidia na badala yake hali ya mgonjwa ikazidi kuwa mbaya.

“Kaka..” Ashura aliita huku akimnywesha uji mama yake.

“Naam” aliitikia Magosho

“Mimi naona tumpeleke mama hospitali”

“Unalosema ni lamsingi Ashura, lakini….”

“Lakini nini?”

“Hapana, nimekuelewa mdogo wangu” Magosho alijifanya hakuwa na kikwazo kumbe alitaka kusema hawakuwa na pesa. Akainamisha kichwa kwa sekunde kadhaa, alipoinuka akamwambia mdogo wake awe makini na mgonjwa yeye kuna mahali alikuwa anakwenda.

Baada ya dakika kama arobaini na tano hivi Magosho alirejea akiwa na kibajaji. Walimpakia mama yao na safari ya kuelekea hospitali ya Muhimbili ikaanza.

Kutokana na foleni walichukua takribani masaa mawili kufika hospitali. Hali ya mgonjwa bado haikuwa ya kuridhisha. Ashura alikuwa akitokwa na machozi muda wote. Magosho alijitahidi sana kujizuia kutoa machozi mbele ya dada yake ili asimkatishe tamaa. Mara kwa mara alikuwa akigeukia pembeni na kujifuta machozi.

Walipofika walimteremsha mgonjwa na kumpeleka mapokezi. Kulikuwa na idadi kubwa sana ya wagonjwa siku ile. Wagonjwa waliandikishwa lakini hawakuweza kutibiwa kutokana na mgomo wa madaktari hao uliokuwa ukiendelea nchini.

Kutokana na hali ile iliyokuwa imetawala pale hospitali ya Taifa ya Muhimbili Mama Ashura hakupata nafasi ya kutibiwa. Alikuwa ni miongoni mwa wananchi walioathirika kutokana na mgomo ule. Akiwa amepakatwa na Magosho huku akipumua kwa taabu akafumbua mdomo wake na kuzungumza.

“Magosho Baba….” Aliita mama Ashura

“Naam mama” Magosho aliitikia.

“Najua mnanipenda sana. Hata mimi nawapenda pia wanangu” alisema mama Ashura kwa taabu.

“Nikweli mama tunakupenda sana, na bado tunakuhitaji”

“Hamna sababu ya kuhangaika tena. Nirudisheni tu nyumbani”

“Hapana mama, ni lazima tuhakikishe unapona” alisema Magosho na kumeza funda la mate

“Naomba mpendane kama mimi ninavyowapenda wanangu” alisema mama Ashura kwa sauti ya chini iliyo toka kwa taabu.

“Sisi tunapendana mama na tunakupenda pia”

“Wewe Magosho ni mkubwa, mlee mdogo wako na usimtupe”

“Usiseme hivyo, mama”

“Ashura, mpende kaka yako na umheshimu sana, yeye ndiye baba yako ndiye mama yako aliyebaki” Mama Ashura alitoa maneno ambayo yalizidi kumtoa Ashura machozi. Hakuweza kuzungumza kitu zaidi ya kuumia ndani ya moyo wake. Akamshika mama yake mkono na kuuweka kifuani mwake.

“Kwanini unazungumza vitu vya ajabu mama?” Ashura alihoji huku machozi yakidondokea kwenye kiganja cha mkono wa mama yake.

“Mimi ngoja nipumzike wanangu” alisema mama Ashura na kufumba macho yake taratiibu. Viungo vyake vikapoteza joto la mwili na kukaribisha mzizimo. Shingo ikalegea zaidi na kichwa chake kuegemea tumboni kwa Magosho.

Kitendo kile kiliwashitua sana watoto wake hasa kutokana na maneno aliyokuwa akizungumza. Hawakuamini na wala hawakuwa tayari kukubaliana na ukweli wa hali halisi. Mama yao mpendwa alikuwa amekwisha iaga dunia akiwa mikononi mwao.

* * *

Maisha ya Magosho na mdogo wake yalizidi kuwa magumu kila kulipo kucha. Wote wawili walikuwa wakiishi kwenye chumba kimoja kwasababu nyumba yao walikuwa wameiuza ili wapate pesa za kumtibia mama yao. Pesa zote za mradi wa vitumbua na mihogo nazo walizitumia kule kwa mganga Kutuzo kumuagua mama yao jini maiti.

Mtu aliyekuwa akitegemewa na familia ile ya watu wawili alikuwa ni Magosho. Ilimbidi kufanya juu chini kuhakikisha mdogo wake anakula, anavaa, na kulala. Hakuwa tayari kumuona dada yake huyo mpendwa akilala na njaa kitu ambacho pengine kingesababisha kumkumbuka mama yao mara kwa mara.




Magosho alifanikiwa kupata pesa na kumpa mdogo wake kufungua mtaji mdogo wa kukaanga mihogo. Na yeye mwenyewe aliweza kupata mtaji wa kuuza maji ya pakti. Maji ambayo alikuwa akiyachota mtoni na kuyafunga kwenye vikaratasi vya nailoni baada ya kuyachemsha. Alipeleka kwenye jokofu la mtu ambalo alikuwa analipia kiasi fulani cha pesa. Kwa kiasi waliweza kuendesha maisha yao wenyewe.

Mungu hamtupi mja wake, Magosho alipata kibarua cha kufanya kazi za ndani maeneo ya Kariakoo nyumbani kwa mhindi mmoja aliyekuwa akijulikana kwa jila na NAKESHIWAR. Kitendo kile Magosho na mdogo wake walikiona kama vile ilikuwa ni bahati kubwa sana kwao. Hivyo Magosho akawa anatokatoka nyumbani asubuhi na kurejea jioni.

Maisha ya Magosho yalikuwa ni tofauti kabisa na yale ya awali alipofariki mama yao. Kutokana na mshahara ambao alikuwa akilipwa ingawa haukuwa mkubwa lakini aliweza kupanga chumba kingine karibu na nyumbani kwao ambacho aliishi mdogo wake. Pia aliweza kufufua mtaji wa kuchoma vitumbua na kukaanga mihogo ambao alikuwa akijishughulisha mama yao enzi za uhai wake.

* * *

Nakeshiwar alikuwa ni baba wa watoto wawili yaani RACHNA na VASHAL. Rachna alikuwa ni binti wa kwanza wa mzee Nakeshwar ambaye kwa wakati ule yeye alikuwa nchini India kimasomo. Kwahiyo nyumbani pale walikuwepo Nakeshiwar mkewake Bi.Fahreen, pamoja na kijana wao mdogo wa kiume ambaye ni Vashal.

Shughuli za Nakeshiwar zilikuwa ni za kusafiri mara kwa mara kibiashara. Hivyo mara nyingi nyumbani pale alikuwa akisalia Magosho na bosi wake wa kike Bi.Fahreen, na Vashal akitoka shule wanakuwa watatu.Wafanya kazi wengine walikuwa wakijishughulisha na kazi za nje zaidi, hivyo walihesabika kama vile hawakuwepo.

Siku moja jioni baada ya kumaliza kazi Magosho alikuwa akijiandaa kuondoka kurudi nyumbani. Ghafla akasikia sauti ya Bi. Fahreen ikimuita hatua chache kutokea pale alipokuwa.

“Gosoo” aliita Bi Fahree kwa lafudhi yake ya kihindi.

“Naam mama” Magosho aliitikia kwa heshima.

“Sasa veve nenda rudi, nenda rudi kila siku, hapana choka?”

“Nimesha zoea mama”

“Mimi taka veve kae hapa hapa, harafu ongezea sahara. Au nanaje veve?” alihoji bi Fahreen huku akiwa ameshika kiuno akimtazama Magosho.

Neno kuongezewa mshahara ndilo alilolisikia zaidi Magosho. Akavuta pumzi na kuzitoa kwa nguvu. Alikuwa akitamani sana bahati kama ile, na hatimaye aliiona ikimjia yenyewe. Akawaza kama yeye angeongezewa mshahara basi mdogo wake angeishi Maisha mazuri kidogo. Lakini kikwazo ni kwamba angewezaje kumuacha mdogowake na kuishi mbali naye?

“Sawa mama lakini nipe muda nifikirie” Magosho akajifanya kuomba muda.

“Hapana fikiria Goso, mimi ongeza mara mbili tena na tena” alisema Bi.Fahreen akizidi kuongeza dau kumshawishi Magosho kukubaliana na lile alilokuwa akilitaka yeye.

Magosho alikuwa tayari kufanya kama vile alivyokuwa anataka yule bosi wake mwanamke, tatizo ni kwamba hakuwa tayari kuishi mbali na mdogo wake kipenzi Ashura. Hata hivyo Magosho alipanga kwenda kuzungumza na dada yake kwanza, kama asingekubali basi asingemkubalia Bi.Fahreen.

* * *

Ilikuwa ni furaha kubwa kwa Ashura kusikia kuwa kaka yake alikuwa anatakiwa kuongezewa mshahara. Hakuwa na kipingamizi chochote juu ya uamuzi wa tajiri wa ndugu yake huyo wa kuhamia nyumbani kwa Nakeshiwar. Ashura alipiga magoti na kumshukuru muumba.

Magosho akahamia nyumbani kwa Muhindi huyo na kumuacha dada yake pale nyumbani pekeyake. Kwa kiasi fulani aliumia sana kuwa mbali na ndugu yake lakini hali ya maisha ilimsukuma kufanya vile.

Ilikuwa ni furaha kubwa sana kwa Bi.Fahreen kwa kitendo cha Magosho kukubali kuhamia nyumban pale. Alimhakikishia kumuongezea mshahara mara tatu ya ule aliokuwa akimpatia awali kama ambavyo alimuahidi.

Waswahili wanasema usilo lijua ni sawa na usiku wa giza. Uamuzi aliouchukua Bi.Fahreen ulikuwa na madhumuni yake ambayo aliyafahamu pekeyake.

Ilikuwa ni mchana wa majira ya saa saba. Baada ya kuandaa chakula Magosho alijiandaa tayari kwa kumfuata mtoto Shuleni. Ilikuwa ni kawaida yake kwenda shuleni kwa Vashal kumchukua kila ilipotimia mida ya kumaliza masomo. Kwakuwa Magosho hakuwa anajua kuendesha gari, dereva wa nyumbani pale alimsindikiza.

“Mama mimi namfuata Vashal” alisema Magosho.

“Ngoja tuongozane” alisema Bi.Fahreen huku akiingia chumbani kwake.

Baada ya dakika kadhaa mama wa kihindi alitoka akiwa amependeza. Kama kawaida yake alikuwa amejipulizia manukato ya mazuri nay a gharama kubwa. Kwakweli mama yule alikuwa amependeza sana, sijui enzi za usichana wake alikuwaje kwasababu hapo alipo alikuwa anavutia utadhania ni binti wa miaka ishirini na mbili hivi.

“Haya tende zetu Goso” alisema Bi.Fahreen na kutangulia mbele.

Magosho alimfuata nyuma mwanamke yule pasipo kuzungumza kitu. Walipofika nje walimkuta dereva amesimama pembeni ya gari akimsubiri Magosho wamfuate mtoto Vashal. Bi.Fahreen alinyoosha mkono wake kuchukua funguo za gari kutoka kwa dereva yule pasipo kuzungumza neon lolote. Dereva naye hakuwa mbishi kwa bosi wake akamkabidhi funguo za gari.

Mama aliingia na kugeuza mwenyewe gari. Alisimamisha karibu na miguu ya Magosho akimpa ishara ya kuingia. Magosho alitaka kuingia mlango wa nyuma lakini mama yule akamwambia akae mbele. Pasipo kipingamizi chochote Magosho akaingia kwenye gari lile na safari ya kuelekea shuleni ikaanza.

Kitu ambacho kilimshangaza Magosho ni pale mama yule alipoacha njia ya shuleni na kupita barabara iliyokuwa ikielekea sehemu nyingine tofauti. Alitamani kuhoji lakini akawaza pengine mke wa bosi wake alikuwa anapitia sehemu fulani. Safari ilikomea kwenye barabara ya vumbi mbali kabisa na makazi ya watu. Mama alisimamisha gari na kumgeukia Magosho.

“Vipi toto zuri, iko sikiaje kuwa na mimi hapa leo?” alizungumza mwanamke yule wa kihindi.

“Kawaida tu mama. Lakini tunatakiwa kumuwahi Vashal, si unajua mida hii ndio anatoka shuleni?” alisema Magosho kwa upole.

“Mimi iko tambua hiyo. Kwani Veve taki jua endesa gari?” alihoji Bi.Fahreen huku mkono wake mmoja ameupitisha kwenye mabega ya Magosho ambaye alikuwa ameketi kwa wasiwasi. Si unajua tena ukiwa na bosi wako lazima heshima zote zionekane hata kama ni za kinafki.

“Napenda sana mama” Magosho alijibu kwa furaha.

“Sasa mimi fundisa veve leo. Iko furahi?” alihoji Bi.Fahreen huku akimpapasa Magosho kwenye mabega yake.

“Nashukuru sana mama” alijibu Magosho kwa furaha na hamasa kubwa.

Ndugu msomaji unaweza ukafikiri ni zali lilikuwa limemdondokea Magosho lakini ni mipango tu ya Mungu.

“Haya kuje kae huku” alisema Bi.Fahreen akimtaka Magosho akae pale alipokuwa amekaa yeye. Magosho alitaka kuteremka ili kuzunguuka lakini mama yule akamzuia na kumwambia wapishane mle mle ndani ya gari.

Kwakuwa Magosho hakuwa na chochote alicho kifahamu alikubali kupishana na mke wa bosi wake mle mle ndani ya gari.

Bi. Fahreen akasogea kwa Magosho huku akiwa amekaa na kuegemea kiti cha gari na kumwambia apite juu yake. Magosho akasimama huku ameinama kidogo kujizuia kugonga juu ya gari na kutaka kumvuka mke wa bosi wake. Alipofika kati kati yaani akiwa amempa mgongo Bi. Fahreen akajikuta akivutwa chini. Akawa ameketi juu ya mapaja ya mama yule wa kihindi. Magosho alishituka sana na kuhisi amefanya kosa kubwa sana, hivyo alitaka kuinuka kwa haraka kabla mama yule hajakasirika.

“Oh! Pole sana Goso” alizungumza mama yule wa kihindi.

“Samahani mama” alisema Magosho huku akijiinua kwa tahadhari.

“Hapana jali. Ila ngoja sije umiza mimi” alisema Bi.Fahreen akimzuia Magosho kuinuka kutoka kwenye mapaja yake akidai kuwa angeweza kumuumiza.

Mwanamke yule wa kihindi alipeleka mikono yake kwenye miguu ya kijana yule na kuanza kumpapasa taratiibu. Mapigo ya moyo wake yalikuwa yakimuenda mbio kiasi ambacho Magosho aliweza kuyasikia kupitia mgongo wake ambao ulikuwa umelala kifuani kwa mama yule. Chuchu zake ambazo zilikuwa zimetuna zilisababisha msisimko kwenye mishipa yake ya damu na kusafiri hadi ubongoni.

“Tar…Tara…Taratibu Goso sije umiza mimi bhanaa” Bi.Fahreen alizungumza kwa taabu na sauti akiwa ameibadilisha kwa kuitolea puani.

Magosho akazidi kuogopa na kuhisi alikuwa anamuumiza mke wa bosi wake. Yeye alihisi Sauti ile ya mama ilitokana na maumivu ya kukaliwa. Magosho akajitahidi hadi kujinasua kutoka kwenye mapaja ya Bi.Fahreen.

Mama yule alibaki amelegea kwenye kiti huku akihema juu juu kama vile alikuwa ametoka kukimbia mbio za olimpiki mita mia tano. Magosho akamtazama na kumuonea huruma mke wa bosi wake. Akaamini kwa asilimia miamoja kuwa kibarua chake kilikuwa njiani kuota nyasi.

“Samahani sana mama” Magosho alizungumza kwa unyenyekevu huku akiwa ameketi kwenye kiti cha jirani na kile alichokuwa amekikalia Bi. Fahreen.

Mama yule wa kihindi aligeuza shingo na kumtazama Magosho kwa jicho lililokuwa limelegea utafikiri alikuwa anataka kukata roho jambo ambalo lilizidi kumtisha Kijana wa watu. Kusema ukweli kilichomfanya kuwa na hali mbaya sio kwasababu heti alikuwa ameumizwa na Magosho, bali ni hisia zake za kimwili dhidi ya mtoto wa watu ndizo zilizokuwa zikimchanganya.

“Vipi mama mbona hivyo?” Magosho alihoji huku akisogelea kiti cha Bi.Fahreen. Pumzi yake ikamfikia mama yule wa kihindi na kuifanya hali ya mwanamke wawatu kuzidi kuwa mbaya.




Laiti Magosho angeujua ugonjwa wa Bi.Fahreen wala asingemkaribia. Kwasababu akiwa mbali mama yule alikuwa anapata ahuweni, lakini akimsogelea tu anakuwa hoi taabani bin mahututi.

Magosho akainua mikono yake na kumshika Bi.Fahreen kwenye mashavu kwa viganja vyake. Lengo lake lilikuwa ni kumjulia hali kutokana na kuonekana kuishiwa nguvu. Wakati akimchunguza mama yake yule ghafla alitereza na kudondokea kifuani kwa Bi.Fahreen. Kitu cha ajabu ni kwamba Bi.Fahreen ambaye alikuwa mgonjwa mahututi aliinua mikono yake ghafla na kumkumbatia Magosho halafu akawa anampapasa mgongoni huku akilalamika kimahaba.

“Goso don’t leave I feel good now” alizungumza mama yule kwa lungha ambayo ilikuwa ngeni masikioni mwa Magosho.

Magosho aliitoa mikono ya Bi.Fahreen na kujinasua haraka huku akitetemeka kwa woga na wasiwasi mkubwa uliokuwa umejaa hofu. Akahisi pengine mama yule angemfikiria vibaya, kumbe vibaya hivyo ndivyo alivyokuwa akivitaka mama wa watu wa kihindi.

“Gosooo I need your hug, come close please” (Nahitaji kukumbatiwa Magosho. Tafadhali njoo) Bi.Fahreen alilalamika kwa lugha ya kiingereza pasipo kufikiri kama mtu aliyekuwa akimsemesha alikuwa haelewi kitu. Ingawa alisoma hadi kidato cha nne lakini lugha ile ya ughaibuni ilimpiga chenga, na ndiyo sababu iliyopelekea kufeli mtihani wake wa mwisho na kuambulia sifuri.

“Don’t late Goso, just do quik” (Usichelewe Magosho, fanya haraka) Bi.Fahreen aliendelea kulalamika huku akiwa amejilaza kwenye kiti cha gari.

“Bahati mbaya mama nimetereza” alisema Magosho huku akitoka nje ya gari na kuzunguuka upande wa pili. Alifungua mlango na kusimama nje wakati mama yule akiwa ndani ya gari. Moyo wa Magosho ulikuwa umejawa na wasiwasi kwa hali ya juu. Alijiona ni mkosaji mbele ya mke wa bosi wake. Akawa ameinamisha kichwa chini akifikiria cha kufanya, wazo lililokuwa karibu ni kupiga simu kwa dereva wa nyumbani ikiwezekana akamchukua mke wa bosi wao na kumuwahisha hospitali.

Wakati Magosho akitaka kutoa simu na kumpigia dereva, mawazo ya mtoto Vashal yalimjia Bi.Fahreen. Alikurupuka kama vile mtu aliyekuwa kwenye usingizi mzito. Alikwenda haraka kwenye usukani na kuwasha gari. Tukio lile lilimshangaza sana Magosho. Imekuwaje mgonjwa aliyekuwa mahututi apone ghafla na kutaka kuendesha gari. Akahisi pengine malaria ilikuwa imempanda kichwani mama yule wa kihindi. Akawa amesimama pale pale nje akimtazama alichokuwa anataka kukifanya mke wa bosi wake.

“Tende veve” Bi.Fahreen alitoa sauti kavu baada ya kumuona Magosho ameduwaa nje ya gari.

“Mama unaumwa lakini utaendeshaje geari?” alizungumza Magosho kwa umakini mkubwa.

“Bana Goso, toto yangu iko pekeyake kule suleni” alizungumza mwanamke yule kwa msisitizo.

“Lakini…” Magosho alitaka kuzingumza kitu lakini mwanamke yule alimkatisha.

“Lakini nini bhana Goso veve, iko fanya jeuri sasa enh?” alizungumza mwanamke yule kwa ukali kidogo.

Magosho akaingia ndani ya gari pasipo kuzungumza neno lolote linguine huku akiwa na wasiwasi juu ya hali ya mama yule wa kihindi. Aliamini kwa asilimia zote kuwa mama yule alikuwa mgonjwa na asingeweza kujifanyisha kwasababu haikuwahi kutokea hata siku moja kufanya vitu kama vile

* * *

Zilikuwa zimepita wiki mbili tangu mzee Nakeshiwar aliporudi kutoka safarini Bangladesh kibiashara. Bi.Fahreen hakuwa anafurahishwa na uwepo wa mume wake nyumbani. Alikuwa hivyo kwasababu alimuona ni kikwazo kikubwa cha yeye kupata penzi la mfanya kazi wao ambaye alitokea kuukonga moyo wake.

Usiku Bi.Fahreena akiwa amelala na mume wake bwana Nakeshiwar alijiwa na mawazo juu ya kijana wao wa kazi. Alijitahidi kwa kadri ya uwezo wake kuweza kumtoa kwenye mawazo yake lakini alishindwa. Mume wake alikuwa kwenye usingizi mzito akikoroma. Laiti kama mawazo ya mtu yangekuwa yanapiga kelele sidhani kama Nakeshiwar siku ile angepata usingizi kutokana na mawazo aliyokuwa nayo mke wake.

Bi.Fahreen kila alipojaribu kufumba macho, sura ya Magosho ilimjia huku sura hiyo ikiwa imejawa na tabasamu la mapenzi. Kila alichofanya ili kupoteza hali ilikuwa vile vile. Akajishauri kuwa ni lazima aione sura ya Magosho usiku ule ili aweze kupata usingizi.

Mwanamke yule aliinua shingo yake na kumchungulia mume wake ambaye alionekana kuzama kwenye dimbwi la usingizi mzito. Baada ya kuhakikisha hilo Bi. Ahreen alifunua neti na kujichomoa mithili ya ndege aliyeekuwa anatoka kwenye kiota chake.

Alitembea kwa ncha ya vidole ili kuepuka mume wake asije akaamka kutoka usingizini. Ndugu msomaji hebu vuta picha mtu mzima akiwa ananyata kwa vidole kumtoroka mume wake. Sasa aliposhika kitasa tu cha mlango wa chumbani Mr. Nakeshiwar alishituka na kuanza kupapasa kitandani kwa lengo la kumkumbatia mke wake.

Mzee Nakeshwiwar alipopapasa mara kadhaa pasipo kumgusa mke wake, akabaini kuwa mke wake hakuwepo hivyo aliinuka ili kuhakikisha kwa macho yake. Alitupa macho mlangoni na kumuona mkewe amekamata kitasa cha mlango.

Lilikuwa ni jambo la kushangaza sana kwasababu chumba kile kilikuwa kimekamilika kwa kila kitu. Kulikuwa na choo na bafu chumbani mle. Sasa Bi.Fahreen amekutwa amekamata kitasa cha mlango anataka kutoka, Alikuwa anakwenda wapi? Mnh! Watu wana mambo jamani! Ngoja tuone pengine alikuwa anakwenda kufunga milango ya nje, au labda alikuwa anakwenda kufunga madirisha ya sitting room, ngoja tuone.

“Where are you going Darling?” (Unakwenda wapi mpenzi?) alihoji Mr. Nakeshiwar swali ambalo lilimfanya Bi.Fahreen kushituka kwa nguvu kwasababu hakuwa ametegemea kama mwanaume yule angeweza kuamka na kumsemesha.

“No my husband, I’m around” (Nipo mume wangu) alisema Bi.Fahreen. Alichofanya ni kutoa loki ya mlango ule na kuungua kisha akarudi kitandani huku akiwa na fundo la hasira kwenye moyo wake. Alijikuta akimchukia sana mwanaume yule kwa kitendo kile cha kuamka usingizini muda kama ule wa maangamizi. Yote hayo heti kwasababu ya mfanya kazi wao wa ndani. Mfanyakazi mwenyewe Magosho ambaye alikuwa hana lolote alilokuwa analijua juu ya yaliyomo moyoni mwa mama yule wa kihindi.

Bi.Fahreen aliporudi kitandani Mr. Nakeshiwar akamkumbatia ipasavyo mke wake. Ndio hivyo tena mtu chake, asiye na wake akumbatie mto. Kama mtu anataka kukumbatiwa au kukumbatia basi atafute wa kwake hakuna kuzengea zengea vya watu, tena Mungu na awalaani wale wote wanaozengea vya watu, Pumbavuu!

Kitendo kile cha Bwana Nakeshiwa kumkumbatia Bi. Fahreen, alikilaani sana mwanamke yule. Pumzi iliyokuwa ikitoka kwenye tundu za pua ya mume wake alihisi zikimletea joto kali lililomkera na kumsababishia kimuyemuye. Ni ajabu kwasababu siku zote mwanamke yule alikuwa akivutiwa sana na pumzi zile za mume wake. Ilikuwa akilala ni lazima wageuziane pua na mume wake ndipo apate usingizi vinginevyo angehangaita usiku kuha. Lakini siku ile ilikuwa kinyume nakwambia.

Baada ya dakika kadhaa Mr. Nakeshiwar alikuwa amekwisha pitiwa na usingizi. Mwanaume wa watu mwenyewe alikuwa hana tatizo katika suala la usingizi. Alikuwa akikoroma sana kiasi cha kuleta kero kwa mke wake. Siku zote ili Bi.Fahreen apate usingizi wa amani ilikuwa ni lazima asikie sauti ya mume wake ikikoroma. Lakini siku ile sauti ile ilikuwa ikimpigia kelele mama yule aliyekuwa amezama kwenye penzi la House boy wake kama vile alikuwa akisikia sauti ya mashine ya kukatia vyuma

Bi.Fahreen alihakikisha kuwa mzee yule wa kihindi alikuwa hajitambui, aliitoa mikono yake iliyokuwa imemkumbatia na kuiweka kitandani taratibu, kisha akalala kwa dakika kama mbili hivi ili kumsahaulisha mume wake kuwa alikuwa amemkumbatia. Kuna wanawake wabaya jamani yani wakiamua mambo yao wameamua hata ufanye nini hawazuiliki utafikiri majongoo. Sio wote lakini, wanawake wengine wanajielewa bwana.

Bi.Fahreen aliteremka kitandani na kuanza kunyata kama alivyofanya mwanzo, alifanikiwa kufungua mlango wa chumbani kwake na kutoka salama chumbani mle pasipo kumuamsha mume wake. Bi. Fahreen akaendelea kunyata hadi kwenye mlango wa Magosho na kusimama. Mapigo ya moyo wake yakaanza kwenda mbio. Aliinua mkono wake kutaka kushika kitasa cha mlango lakini moyo ulisita na kurudisha mkono chini. Akafanya zoezi lile mara kadhaa huku akijishauri aingie ama asiingie. Akapiga moyo konde na kuamua kufungua mlango ule.

Siku zote Magosho alizoea kufunga mlango wake kwa ndani kila alipolala, lakini siku hiyo alisahau kabisa kufunga mlango. Bi.Fahreen alipobaini kuwa mlango ulikuwa wazi akajikuta kijasho chembamba kikimtoka huku mapigo ya moyo wake yakiongezeka. Aliusukuma taratibu mlango ule na kuingiza kichwa kuchungulia ndani. Loo! Alijikuta akizidi kuchanganyikiwa baada ya kumuona mwanaume aliyekuwa akiutesa moyo wake akiwa kitandani huku amevaa boksa tu kutokana na hali ya hewa ya jijini Daressalaam.

“My God” alijikuta akitamka huku akiuma kucha ya kidole chake cha shahada mdomoni.

Masikini ya Mungu Magosho alikuwa amelala chali na mkono wake wa kushoto akiwa ameuchomeka kwenye nguo yake ya ndani na kukamata vyema mali zake. Kwa mara ya kwanza Bi.Fahreen aliweza kuliona tumbo la kijana yule likiwa wazi bila nguo. Lilikuwa limekaza tofauti na lile la mume wake ambalo halikuwa na mvuto hata kidogo, Bi.Fahreen aliweza kuiona misuli iliyokuwepo kwenye mapaja ya kijana yule ambaye alikuwa usingizini hasikii wala haoni.

Bi.Fahreen akaona hafaidi vizuri, akasogea hadi pale kitandani na kumuinamia Magosho. Hewa chafu iliyotoka kwenye mapafu ya Magosho ilipokelewa kwa furaha na kukaribishwa vyema kwenye pua za Bi.Fahreen.

Magosho alivuta pumzi kwa nguvu na kujinyoosha viungo vyake vya mwili na kuchomoa mkono wake kutoka kwenye hifadhi ya zana zake za kivita. Kisha akaendelea kuuchapa usingizi huku akiwa bado amelala chali. Kitendo cha kutoa mkono wake kiliweza kuruhusu umbo la silaha zake kuonekana kupitia kwenye kitambaa laini kilichotumika kuzisitiri.

Mwanamke yule akajikuta akitetemeka hasa baada ya kuona umbile la vile vitu vya watu ambavyo havikumhusu. Akameza funda kubwa la mate lililosababishwa na tamaa za kimwili. Kwa muda ule mama yule alikuwa amekwisha pagawa na alikuwa tayari kwa lolote ilimradi auridhishe moyo wake.

Bi.Fahreen aliuinua mkono wake wa kuume na kuutazama kwa sekunde chache halafu akawa anaupeleka taratiibu kushika ghala la watu bila ya ruhusa kutoka kwa mwenyewe. Wakati anatua mkono ule akashituliwa na sauti ya mlango wa chumbani kwake ukifunguliwa. Kitendo cha kushituka kilisababisha mkono wake kutua juu ya zana za Magosho kwa nguvu bila kutegemea na kusababisha kijana yule aamke kwa mshituko mkubwa.





“Shiiiiiiiii” Bi.Fahreen alimnyamazisha Magosho huku akiwa ameweka kidole mdomoni kumuashilia asipige kelele.


ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

BLOG